"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Thursday, February 8, 2018

DANIELI: Mlango wa 3

Jina la Bwana wetu na Mkuu wetu Yesu Kristo libarikiwe.
Karibu katika mwendelezo wa kitabu cha Danieli. Leo tukiutazama ule mlango wa tatu, Tunasoma baada ya Mfalme Nebukadreza kuota ile ndoto ya kwanza, inayohusu zile falme 4 zitakazotawala mpaka mwisho wa dunia,lakini hapa kwenye sura hii tunaona akitimiza maono yake kwa kunyanyua SANAMU kubwa ya dhahabu, na kulazimisha watu wa dunia yote waiabudu, Na mtu yeyote atayeonekana amekaidi adhabu yake ni kwenda kutupwa katika tanuru la Moto. Kama tunavyosoma.

Danieli 3:1-6" Nebukadreza, mfalme, alifanya sanamu ya dhahabu, ambayo urefu wake ulikuwa ni dhiraa sitini, na upana wake dhiraa sita; akaisimamisha katika uwanda wa Dura, katika wilaya ya Babeli.
2 Ndipo Nebukadreza akatuma watu kuwakusanya maamiri, na manaibu, na maliwali, na makadhi, na watunza hazina, na mawaziri, na mawakili, na wakuu wa wilaya zote, ili wahudhurie wakati wa kuizindua ile sanamu, mfalme Nebukadneza aliyoisimamisha.
3 Ndipo maamiri, na manaibu, na maliwali, na makadhi, na watunza hazina, na mawaziri, na mawakili, na wakuu wa wilaya zote, wakakusanyika ili kuizindua ile sanamu, mfalme Nebukadreza aliyoisimamisha; wakasimama mbele ya ile sanamu, mfalme Nebukadreza aliyoisimamisha.
4 Ndipo mpiga mbiu akapiga kelele akisema, Enyi watu wa kabila zote, na taifa, na lugha, mmeamriwa hivi,
5 wakati mtakapoisikia sauti ya panda, na filimbi, na kinubi, na zeze, na santuri, na zomari, na namna zote za ngoma, lazima kuanguka na kuiabudu sanamu ya dhahabu, mfalme Nebukadreza aliyoisimamisha.
6 Na kila mtu asiyeanguka na kuabudu atatupwa saa iyo hiyo katika tanuru ya moto uwakao.

Lakini pamoja na hayo walionekana watu baadhi waliokaidi amri ya mfalme nao ni Meshaki, Shedraka na Abednego. watu hawa tunasoma walikuwa ni wacha Mungu tangu awali, tunaona walikataa kula vyakula najisi vya mfalme, na hapa pia wanakataa kuabudu sanamu ambayo ni kinyume na sheria ya Mungu aliyowapa, kwa mkono wa Musa kule jangwani ikisema..
Kutoka 20:4 "Usijifanyie sanamu ya kuchonga, wala mfano wa kitu cho chote kilicho juu mbinguni, wala kilicho chini duniani, wala kilicho majini chini ya dunia.
5 Usivisujudie wala kuvitumikia; kwa kuwa mimi, Bwana, Mungu wako, ni Mungu mwenye wivu; nawapatiliza wana maovu ya baba zao, hata kizazi cha tatu na cha nne cha wanichukiao,
6 nami nawarehemu maelfu elfu wanipendao, na kuzishika amri zangu.
Hivyo Mfalme aliposikia habari yao alighadhibika na kuwatupa katika tanuru la Moto, lakini tunaona Bwana aliwaokoa na ukali wa moto ule.

Kumbuka Agano la kale ni kivuli cha Agano jipya,(wakolosai 2:17) yaliyotokea katika mwili agano la kale, yatakuja kutokea katika roho kwenye agano jipya, na ndio maana tunaona hapa inatajwa BABELI ya NJE, lakini tukisoma katika kitabu cha Ufunuo 17 &18 Tunaona inatajwa BABELI nyingine itakayokuja kunyanyuka nayo ni ya rohoni. Hivyo tabia inayojitokeza kwenye hiyo ya mwilini itafanana na hiyo ya rohoni.


Na kama Babeli ile ya kwanza ilivyounda sanamu na kulazimisha watu wa dunia nzima waiabudu na yeyote asiyeabudu atatupwa katika tanuru kali la moto vivyo hivyo na hii ya rohoni itaunda SANAMU yake na mtu yeyote atakayekaidi kuiabudu, adhabu yake itakuwa ni mateso ambayo biblia inasema hayajawahi kuwepo tangu dunia kuumbwa (DHIKI KUU)..Habari hii tunaweza kuisoma katika...
Ufunuo 13:15 Akapewa kutia pumzi katika ile SANAMU YA MNYAMA, hata ile sanamu ya mnyama inene, na kuwafanya hao WOTE WASIOISUJUDIA SANAMU YA MNYAMA WAUAWE.
16 Naye awafanya wote, wadogo kwa wakubwa, na matajiri kwa maskini, na walio huru kwa watumwa, watiwe chapa katika mkono wao wa kuume, au katika vipaji vya nyuso zao:
17 tena kwamba mtu awaye yote asiweze kununua wala kuuza, isipokuwa ana chapa ile, yaani, jina la mnyama yule, au hesabu ya jina lake.
18 Hapa ndipo penye hekima. Yeye aliye na akili, na aihesabu hesabu ya mnyama huyo; maana ni hesabu ya kibinadamu. Na hesabu yake ni mia sita, sitini na sita.

Kumbuka Mnyama huyu ni RUMI na dini yake ni KATOLIKI, ndio BABELI ya rohoni iliyopo sasa. Itafika kipindi itapata nguvu kwa kuunganisha DINI zote na Madhehebu yote ulimwenguni ili kuunda DINI moja (ambayo ndio SANAMU YA MNYAMA), ambayo pasipo hiyo hakuna mtu yeyote atakayeweza kuuza wala kununua wala kuajiriwa, na yeyote atakayeonekana hana chapa(utambulisho) wake, adhabu yake itakuwa ni mateso makali na vifo. Kama vile amri ya Mfalme ilivyokuwa kali juu ya akina Shedraka mpaka moto ukachochewa mara saba, ndivyo mateso yao yatakavyokuwa makali kwa wale wote watakaokataa kusujudia ile SANAMU ya Mnyama au kupokea CHAPA YAKE.


Kama ni mfuatiliaji mzuri wa Historia utaona mateso waliopitia wayahudi wakati wa utawala wa kimabavu wa Adolf Hitler, jinsi wayahudi walivyouawa kikatili kwenye magereza maalumu (CONCENTRATION CAMPS), walivuliwa nguo uchi wa mnyama na kuingizwa katika matanuru ya Gesi, wengine walikuwa wanapasuliwa wazima kama kuku kwa ajili ya uchunguzi wa kimaabara mifupa na msuli inachomolewa pasipo ganzi na kuwekwa kwa mwingine, 
wengine walitiliwa sumu machoni, wengine wanadondoshwa kwenye ndege maili nyingi kutoka hewani( zote hizi ni kwaajili ya utafiti wa kijeshi na kibaolojia), wengine wanafungiwa kwenye mashehena yenye kemikali kwa muda mrefu ili tu wafe taratibu kwa maumivu makali, wengine walikuwa wanaachwa kwenye barafu uchi, wengine wanafanyishwa kazi ngumu kwa muda mrefu bila chakula mpaka wafe, wengine wanaachwa na kiu kwa muda mrefu na kupewa maji ya chumvi tu kuchunguza kama mtu anaweza kuishi kwa maji ya chumvi kwa muda gani?, watoto wanafungwa na kugongwa nyundo kichwani kidogo kidogo kwa muda mrefu mpaka kufa, au ukichaa ili tu kuchunguzwa ni kwa muda gani mwanadamu anaweza akavumilia maumivu n.k. embu fikiria ni mateso ya aina gani hayo?, tazama picha hapo chini..


Kumbuka Adolf Hitler aliwafanyia hivyo kwasababu tu ni wayahudi, kwasababu wao ni taifa teule la Mungu, na si vingine, sasa hayo yote ni kivuli cha yatakayokuja huko mbeleni, huo ni mfano mdogo sana, Biblia inasema kutakuwepo na dhiki ambayo haijawahi kutokea na wala haitakuja kutokea tena baada ya hapo, Hivyo hawa wa mwisho watakuja kuuliwa kwasababu wanashikilia ushuhuda wa Kristo kwa kukataa kuisujudia SANAMU ya yule mnyama na kupokea chapa yake.
Ni mambo ya kutisha yanakuja huko mbele usitamani uwepo, anza kuweka sawa mambo yako yahusuyo wokovu leo kabla wakati haujaisha.

Lakini jambo lingine tunaweza kulisoma katika hii habari, Ni kwamba DANIELI haonekani kuwepo wakati sanamu ile inasimamishwa na watu walipolazimishwa kuiabudu. je! hii inafunua nini??.

Kama vile tulivyoona agano la Kale ni kivuli cha Agano jipya. Danieli ni mfano wa BIBI-ARUSI wa Kristo aliyekwisha jiweka tayari na kwenda kwenye UNYAKUO. Na ndio maana hatumwoni Danieli miongoni mwa wakina Shedraka, Meshaki na Abednego,.

Hivyo kabla ya hii DHIKI KUU kuanza kuna kundi dogo sana(BIBI-ARUSI wa KRISTO) watakuwa wameshanyakuliwa kwenye utukufu , watu hawa ni wale waliokuwa wamejiweka tayari, kwa UTAKATIFU, na Kudumu katia NENO na UFUNUO wa Roho Mtakatifu, ni watu walioshi kama vile wapitaji duniani wanaomngojea Bwana wao, Hawaabudu sanamu, sio walevi, sio wavutaji sigara, sio waenda disco na wasikilizaji wa miziki ya dunia hii, wasengenyaji, sio wezi wala walarushwa, sio wazinzi, sio watukanaji, n.k.


Kumbuka ndugu huyu mnyama anafanya kazi ndani ya DINI YA KATOLIKI, na atakayeisimamisha SANAMU yake atakuwa ni mpinga-kristo(katika kiti cha UPAPA)..na sanamu yake itakuwa ni "Muungano wa dini zote na madhehebu yote duniani (Ekumene)" .Na sanamu hii ilishaanza kuundwa tangu miaka ya 1900. kilichobaki ni "KUSIMAMISHWA TU" ili watu waiabudu.Na hivi karibuni itasimamishwa, lakini kinachohuzunisha zaidi ni watu wameshaanza kuiabudu hata kama haijasimamishwa, na ndio maana Bwana anasema tokeni kwake enyi watu wangu..(Ufunuo 18:4) kama hujafahamu ni jinsi gani chapa ya mnyama itatenda kazi fuatilia hii link...>>> 
https://wingulamashahidiwakristo.blogspot.com/2016/10/chapa-ya-mnyama.html

Unaweza ukaona ni jinsi gani siku zilivyokwisha, matunda ya nchi yamekwisha iva, Tunapoona vikundi vya kigaidi vinakirithiri, vikundi kama ISIS, Boko Haramu, Alshabaab, n.k. migogoro ya kidini kati ya taifa na taifa, Israeli na wapalestina, wabudha & waislamu, wakristo & waislamu n.k. yote haya yanazidi kumfungulia njia mpinga-kristo kuleta muafaka wa AMANI-FEKI, Juu ya masuala ya dini ambao wanasiasa wa dunia nzima wameshindwa kuyatatua. Kwa jinsi yanavyoendelea kuongezeka mpinga-kristo(PAPA wa wakati huo) atapewa nguvu na mataifa ya dunia yote, ndipo atakapoleta utaratibu mpya (NEW WORLD ORDER) ambao katika huo watu wote watalazimika kuufuata na mtu yeyote atakayekaidi, ni mateso yasiyoelezeka yatamkumba.


Hivyo NENO la Mungu linasema 1Wakorintho 7:29 Lakini, ndugu, nasema hivi, MUDA UBAKIO SIO MWINGI; basi tokea sasa wale walio na wake na wawe kama hawana;
30 na wale waliao kama hawalii; na wale wafurahio kama hawafurahi; na wale wanunuao, kama hawana kitu.
31 Na wale wautumiao ulimwengu huu, kama hawautumii sana; kwa maana mambo ya ulimwengu huu yanapita.

Tujiweka tayari kwasababu siku ya Bwana itakuja kama mwivi..1Thesalonike 5:1 Lakini, ndugu, kwa habari ya nyakati na majira, hamna haja niwaandikie.
2 Maana ninyi wenyewe mnajua yakini ya kuwa siku ya Bwana yaja kama vile mwivi ajavyo usiku.
3 Wakati wasemapo, KUNA AMANI NA SALAMA, ndipo uharibifu uwajiapo kwa ghafula, kama vile utungu umjiavyo mwenye mimba, wala hakika hawataokolewa.
4 Bali ninyi, ndugu, hammo gizani, hata siku ile iwapate kama mwivi. "

Uzidi kubarikiwa na BWANA YESU.

No comments:

Post a Comment