"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Saturday, February 24, 2018

DANIELI: Mlango wa 8

Jina la YESU KRISTO, BWANA wetu libarikiwe.

Karibu katika mwendelezo wa kitabu cha Danieli, Kama tulivyoona katika sura iliyotangulia Danieli akionyeshwa wale wanyama 4 waliotoka baharini, wa kwanza mwenye mfano wa simba, wa pili kama Dubu, watatu kama Chui na wanne alionekana kuwa mbali sana na wale wengine kwa muonekano wake ikiashiria utendaji wake ulikuwa ni wa tofauti, na tuliona wanyama wale waliwakilisha zile FALME 4 zitakazotawala mpaka mwisho wa Dunia, wa kwanza ukiwa ni Babeli, wapili, Umedi & uajemi, watatu Uyunani na wanne ambao ni wa mwisho ni RUMI.

Lakini tukiendelea na mlango huu wa 8, tunaona Danieli akionyeshwa maono mengine ya kipekee yanayohusiana na mambo yatakayokuja kutokea huko mbeleni kuhusiana na hizo falme kama Danieli 8:19 inavyosema.." Akaniambia, Tazama, nitakujulisha yatakayokuwa wakati wa mwisho wa ghadhabu; maana, ni ya wakati wa mwisho ulioamriwa. "

Tusome.
Danieli 8:1-4"
1 Katika mwaka wa tatu wa kumiliki kwake mfalme Belshaza maono yalinitokea mimi, naam, mimi Danieli, baada ya hayo yaliyonitokea hapo kwanza.
2 Nami naliona katika maono; ilitukia, nilipoona, nalikuwako huko Shushani ngomeni, katika wilaya ya Elamu; nikaona katika maono, nami nalikuwa karibu na mto Ulai.
3 Ndipo nikainua macho yangu nikaona, na tazama, mbele ya mto alisimama kondoo mume, mwenye pembe mbili; na pembe zile mbili zilikuwa ndefu; lakini moja ilikuwa ndefu kuliko ya pili, na ile iliyokuwa ndefu zaidi ilizuka mwisho.
4 Nikamwona huyo kondoo mume akisukuma upande wa magharibi, na upande wa kaskazini, na upande wa kusini; wala hakuna mnyama ye yote awezaye kusimama mbele yake, wala hakuna mnyama ye yote awezaye kupokonya mkononi mwake; lakini alitenda kama alivyopenda mwenyewe, akajitukuza nafsi yake.

Danieli katika maono haya alimwona kondoo mume mwenye pembe mbili, kumbuka ukiendelea mbele kwenye mstari wa 20 utaona tafsiri yake kuwa huyo kondoo anawakilisha ufalme wa UMEDI & UAJEMI,..
"20 Yule kondoo mume uliyemwona, mwenye pembe mbili, hizo ndizo wafalme wa Umedi na Uajemi. "

Na kama tunavyosoma hapo pembe moja ilikuwa ndefu kuliko nyingine na ndio iliyozuka mwishoni hii ikiwa na maana kuwa mfalme mmoja atakuwa na nguvu kuliko mwingine na huyu sio mwingine zaidi ya Koreshi mfalme wa UAJEMI ambaye tunaona alinyanyuka mwishoni baada ya Dario ambaye alikuwa ndugu yake mfalme wa Umedi kufa, Hivyo Ufalme wa Uajemi chini ya Koreshi uliimarika sana, mpaka ulipofikia wakati wa utawala wa Mfalme Ahasuero aliyemtwaa Esta kuwa malkia.

Na pia tunaona kondoo huyu akisukumu pande zote nne za nchi ikiashiria kuwa alifanikiwa kuteka sehemu kubwa ya dunia na mataifa makubwa, kuanzia India mpaka Ethiopia, jambo hili tunaweza tukalisoma katika kitabu cha Esta 1:1..." Zamani za Ahasuero; naye huyu Ahasuero alimiliki toka Bara Hindi mpaka Kushi, juu ya majimbo mia na ishirini na saba; "

Alionekana pia akijitukuza nafsi yake, ni dhahiri kuwa milki kubwa aliyokuwa nayo ni rahisi kujinyanyua moyo hivyo pengine alifikiri kuwa hakuna taifa lolote lingeweza kumwangusha. lakini kama tunavyoendelea
  
Mstari wa 5-8" unasema...

5 Nami nilipokuwa nikifikiri, tazama, BEBERU akatoka upande wa magharibi, juu ya uso wa dunia nzima, bila kuigusa nchi; na beberu yule alikuwa na pembe mashuhuri kati ya macho yake.
6 Naye akamwendea huyo kondoo mume mwenye pembe mbili, niliyemwona akisimama karibu na mto, akamshambulia kwa ghadhabu za nguvu zake.
7 Nikamwona akimkaribia kondoo mume, akamwonea hasira kali, akampiga kondoo mume, akazivunja pembe zake mbili; na huyo kondoo mume alikuwa hana nguvu kusimama mbele yake; bali akamwangusha chini, akamkanyaga-kanyaga; wala hapakuwapo awezaye kumwokoa kondoo mume katika mkono wake.
8 Na yule beberu akajitukuza sana; na alipokuwa na nguvu, pembe ile kubwa ilivunjika; na badala yake zikazuka pembe nne mashuhuri zilizoelekea pepo nne za mbinguni.

Vivyo hivyo ukienda mbele kusoma mstari wa 21-22 utaona tafsiri ya yule beberu kuwa ni Ufalme wa UYUNANI, ambao ndio ulioungusha ufalme wa Umedi na Uajemi,...{"21 Na yule beberu, mwenye manyoya mengi, ni mfalme wa Uyunani; na ile pembe kubwa iliyo kati ya macho yake ni mfalme wa kwanza.22 Tena katika habari ya pembe ile iliyovunjika, ambayo badala yake zilisimama pembe nne, falme nne zitasimama kutoka katika taifa lile, lakini si kwa nguvu kama zake. "}

Kumbuka kama tulivyosoma katika milango iliyopita, ufalme wa tatu uliokuja kutawala dunia ulikuwa ni UYUNANI na ndio unawakilishwa na yule chui mwenye vichwa 4 katika Danieli sura ya 7,

Hivyo Danieli anaonyeshwa tena jambo lile lile katika ono tofauti lakini kwa undani zaidi, na Beberu huyu anaonekana akija akiwa na PEMBE MOJA MASHUHURI katikati ya macho yake naye akaenda kumvamia yule kondoo mwenye pembe mbili na kumwangamiza kabisa.

"Alexanda Mkuu" ndio ile pembe mashuhuri iliyozuka, Historia inasema mtu huyu alifanikiwa kuteka falme nyingi kwa kipindi cha muda mfupi sana, ndani ya miaka 12 alikuwa ameshaitiisha sehemu kubwa ya dunia kuanzia makedonia, India, hadi Misri na ilipofika 331 KK aliidondosha ngome ya Umedi na Uajemi (ndio yule kondoo) na kuiangamiza kabisa.

Na kama tunavyosoma mstari wa 8, tunaona ile pembe ilipokuwa na nguvu ilivunjika ghafla, na badala yake zikazuka pembe nyingine 4 mashuhuri. Historia inaonyesha Alexandra Mkuu, ambaye ndio ile pembe, alikufa ghafla na ugonjwa akiwa bado kijana wa miaka 31, Hivyo baada ya kufa hakuonekana wa kumrithi, hivyo wale majenerali wake 36 waliokuwa chini yake walianza kuupigania ufalme, hakuonekana aliyekuwa na nguvu kama za Alexanda hivyo mwishoni walikuja kuishia wanne tu, na kuugawanya ufalme katika pande nne sawasawa na biblia ilivyotabiri. Na majenerali hao walikuwa ni:

1)Cassander - Alitawala pande za magharibi ambazo ni Makedonia na Ugiriki
2)Lysimachus -Alitawala pande za kaskazini ambazo ni Bulgaria na maeneo ya Asia ndogo
3)Ptolemy - Alitawala pande za kusini ambayo ni Misri
4)Seleucus - Alitawala pande za Mashariki ambazo zilikuwa Israeli, Syria na mashariki yake.

Kumbuka hizi Pembe NNE ndio vile Vichwa vinne Danieli alivyoonyeshwa katika yule mnyama wa tatu, aliyefanana na CHUI katika Danieli sura ya 7.

Lakini tukiendelea kusoma kuanzia ule mstari wa 9 hadi wa 14 tunaona PEMBE nyingine NDOGO, ikizuka katikati ya moja ya zile pembe nne.

Tusome..
"9 Na katika moja ya pembe hizo ilitokea pembe ndogo, iliyokua sana, upande wa kusini, na upande wa magharibi, na upande wa nchi ya uzuri.
10 Nayo ikakua, kiasi cha kulifikilia jeshi la mbinguni; ikaangusha chini baadhi ya jeshi lile, na ya nyota, ikazikanyaga.
11 Naam, ikajitukuza hata juu yake aliye mkuu wa jeshi hilo, ikamwondolea sadaka ya kuteketezwa ya daima, na mahali pa patakatifu pake pakaangushwa chini.
12 Na jeshi likatolewa kwake pamoja na sadaka ya kuteketezwa ya daima, kwa sababu ya makosa; nayo ikaiangusha kweli hata chini; ikatenda ilivyopenda, na kufanikiwa.
13 Ndipo nikamsikia mtakatifu mmoja akinena, na mtakatifu mwingine akamwuliza huyo aliyenena, Haya maono katika habari ya sadaka ya kuteketezwa ya daima, na lile kosa lifanyalo ukiwa, yataendelea hata lini, kukanyagisha patakatifu na jeshi?
14 Akamwambia, Hata nyakati za jioni na asubuhi elfu mbili na mia tatu; ndipo patakatifu patakapotakaswa. "

PEMBE NDOGO

Hii Pembe ndogo iliyozuka kati ya zile nne, historia inaonyesha ni mtawala aliyezuka katika ufalme wa Seleucus mmoja wa wale watawala wanne ambaye alikuwa wa mashariki, na tunaona ilizidi kujiimarisha mpaka kufikia NCHI YA UZURI (AMBAYO NI ISRAELI), Na mtawala huyu si mwingine zaidi ya ANTIOKIA IV, EPIFANE. Aliyetawala kuanzia 175-164 KK ..alijiita EPIFANE, akiwa na maana kuwa yeye ni "MUNGU ALIYEDHIHIRIKA", huu ni mfano wa kile kile cheo cha mpinga-kristo atakayenyanyuka siku za mwisho. Kumbuka mambo yanayoandikwa, au yaliyotokea katika historia ni kivuli cha mambo yatakayokuja kutokea siku za mwisho.

Lakini tukisoma mstari wa 10 tunaona "Nayo ikakua{PEMBE}, kiasi cha kulifikilia jeshi la mbinguni; ikaangusha chini baadhi ya jeshi lile, na ya nyota, ikazikanyaga.

Kumbuka nyota za mbinguni zinafananishwa na makuhani wa Mungu, au viongozi wa watakatifu wa Mungu, ukisoma (Danieli 12:3., na ufunuo 2 & 3)utaona hilo jambo. Hivyo historia inaeleza huyu mtawala katili ANTIOKIA alishuka Yerusalemu na kuanza kuua wakuhani wa Mungu walokuwa wanahudumu katika nyumba ya Mungu na kuzuia watu wasitoe dhabihu katika nyumba ya Mungu( Hekaluni) na ndio maana ukisoma mstari wa 11 unasema " Naam, ikajitukuza{hiyo pembe} hata juu yake aliye mkuu wa jeshi hilo, IKAMWONDOLEA SADAKA YA KUTEKETEZWA YA DAIMA, na mahali pa patakatifu pake pakaangushwa chini".

Hivyo kuanzia huo wakati wayahudi wote walikatazwa kufanya ibada yoyote katika nyumba ya Mungu, badala yake Antiokia akawalazimisha wayahudi wafuate tamaduni za kipagani za kigiriki badala ya sheria ya Musa.

Alizidi hata kufikia hatua ya kuiba vyombo vya hekaluni na kutengeneza madhabahu ya mungu wake wa kipagani-ZEU ndani ya HEKALU la Mungu, Hilo ni chukizo kubwa sana kwa Mungu na kwa Wayahudi, aliendelea kwa kuchinja vitu haramu kama nguruwe na kunyunyiza damu juu ya madhabahu ndani ya hekalu la Mungu. Na wayahudi walipojaribu kwenda kinyume naye juu ya kulichafua hekalu la Mungu aliwaua wengi kikatili na wengine kuwauza utumwani, alikataza wayahudi kutahiriwa, yeyote atakayekiuka adhabu yake ilikuwa ni kifo, wayahudi walilazimishwa kula nyama za nguruwe na kutolea dhabihu miungu migeni ya kigiriki mambo ambayo ni machukizo makubwa sana mbele za Mungu. Lakini kumbuka haya yote yaliwapata wayahudi kwasababu ya MAKOSA YAO, kama mstari wa 12 unavyoeleza...."12 Na jeshi likatolewa kwake pamoja na sadaka ya kuteketezwa ya daima, KWASABABU YA MAKOSA; nayo ikaiangusha kweli hata chini; ikatenda ilivyopenda, na kufanikiwa. "

Wayahudi walimsahau Mungu na kuacha kuzishika sheria zake hivyo Mungu akaruhusu kiongozi mbaya na mkatili kama huyu anyanyuke dhidi yao. Lakini baadaye Mungu alikuja kumuhukumu na kufa ghafla.

Kumbuka Antiokia ni kivuli cha mpinga-kristo atakayekuja, biblia inasema atajiinua nafsi yake na kutaka kuabudiwa kama Mungu tunasoma.1Wathesalonike 2:3 Mtu awaye yote asiwadanganye kwa njia yo yote; maana haiji, usipokuja kwanza ule ukengeufu; akafunuliwa yule mtu wa kuasi, mwana wa uharibifu; 4 yule mpingamizi, AJIINUAYE NAFSI YAKE JUU YA KILA KIITWACHO MUNGU, AMA ; hata yeye mwenyewe KUKETI KATIKA HEKALU LA MUNGU, akijionyesha nafsi yake kana kwamba yeye ndiye Mungu. "

Na kama vile Antiokia aliwalazimisha wayahudi waikane imani yao na kuabudu miungu ya kipagani, vivyo hivyo na mpinga-kristo (PAPA) atawalazimisha watu wa ulimwengu mzima kupokea dini yake inayotambulishwa na ile chapa, na yeyote atakayepinga adhabu yake itakuwa ni kifo cha mateso kama ilivyokuwa kwa Antiokia kumbuka wakati hayo yanatokea kanisa litakuwa limeshanyakuliwa.

Tukiendelea mstari wa 13-14 inasema..
"13 Ndipo nikamsikia mtakatifu mmoja akinena, na mtakatifu mwingine akamwuliza huyo aliyenena, Haya maono katika habari ya sadaka ya kuteketezwa ya daima, na lile kosa lifanyalo ukiwa, yataendelea hata lini, kukanyagisha patakatifu na jeshi? 14 Akamwambia, Hata nyakati za jioni na asubuhi ELFU MBILI NA MIA TATU (2300); ndipo patakatifu patakapotakaswa. "

Hizi siku 2300 ni sawa na miaka sita na theluthi moja hivi, ndipo uovu wote utaondolewa katika hekalu la Mungu, na Historia inaonyesha tangu kipindi Antiokia kuzuia sadaka za kuteketezwa mpaka siku ziliporejeshwa tena, ilikuwa ni siku 2300 kamili kama unabii ulivyotabiri.

Hii ilitokea pale baadhi ya wayahudi kutokuvumiliana na vitendo vya Antiokia na kuamua kuasi kwa kuingia vitani hivyo wakanyanyuka wana wa Matthatias mmoja wao akiwa YUDA MAKABAYO, na kwenda porini kumpinga Antiokia siku zote za utawala wake, walifanikiwa kumshinda na kuichukua tena YERUSALEMU na KULIWEKA TENA WAKFU Hekalu la Mungu baada ya kuchafuliwa kwa muda mrefu, hivyo wakatimiza unabii wa siku 2300 hii ilikuwa ni mwaka 164 KK. Siku hiyo wayahudi wakaanza tena kutoa sadaka za kuteketezwa, Na ndipo ile sikukuu ya KUTABARUKU ilianzia hapo {KUTABARUKU ni kuweka wakfu} (Yohana 10:22).

Kumbuka ndugu Danieli alionyeshwa mambo hayo kwa ajili ya SIKU ZA MWISHO, kwa sehemu yametimia kama KIVULI TU, lakini matukio halisi yenyewe yatakuja katika vizazi hivi vya siku za mwisho siku mpinga-kristo atakaposimama na kuwakosesha watu wengi.

Hivyo ndugu biblia inasema 2Thesalonike 2:
7 Maana ILE SIRI YA KUASI HIVI SASA INATENDA KAZI; lakini yuko azuiaye sasa, hata atakapoondolewa.

Biblia inasema ni SIRI, hivyo inahitaji hekima kuigundua, utendaji kazi wake ni katika SIRI, na JINA lake pia lipo katika SIRI, BABELI MKUU MAMA WA MAKAHABA NA MACHUKIZO YA NCHI!(Ufunuo 17:5). ni roho ile ile iliyokuwa kwa Antiokia, ndio ipo mpaka sasa hivi, IBADA ZA SANAMU katika nyumba ya Mungu(KANISA), pombe kanisani, uasherati kanisani, ushoga kanisani, vimini kanisani, burudani kanisani, sanaa & siasa kanisani, mizaha kanisani, biashara kanisani n.k. haya yote ni machukizo kama aliyofanya Antiokia na Belshaza juu ya nyumba ya Mungu. Ni roho ile ile.

2Wakoritho 6:15 Tena pana ulinganifu gani kati ya Kristo na Beliari? Au yeye aaminiye ana sehemu gani pamoja na yeye asiyeamini?
16 Tena pana mapatano gani kati ya HEKALU LA MUNGU NA SANAMU? Kwa maana sisi tu hekalu la Mungu aliye hai; kama Mungu alivyosema, ya kwamba, Nitakaa ndani yao, na kati yao nitatembea, nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu.
17 Kwa hiyo, TOKENI KATI YAO, Mkatengwe nao, asema Bwana, Msiguse kitu kilicho kichafu, Nami nitawakaribisha.
18 Nitakuwa Baba kwenu, Nanyi mtakuwa kwangu wanangu wa kiume na wa kike, "

EPUKA ROHO YA UDHEHEBU NA DINI ZA UONGO MGEUKIE KRISTO AYASAFISHE MAISHA YAKO KWA NENO LAKE NA UZALIWE MARA YA PILI ILI UWE MTAKATIFU. Kwasababu biblia inasema pasipo huo UTAKATIFU hakuna mtu atakayemwona Mungu(Waebrania 12:14).

Mungu akubariki.

No comments:

Post a Comment