"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Friday, March 30, 2018

TOKENI KWAKE ENYI WATU WANGU: Part 4


“HAKUNA KUZIMU sehemu ambayo roho za wenye dhambi zitateswa milele”, Papa Francis amenukuliwa akisema hayo Alhamisi katika mahojiano na gazeti la Italian Repubblica.

Papa aliongezea na kusema “Baada ya kifo, roho za watu watakaotubu zitasamehewa na kwenda mbinguni, lakini zile roho ambazo hazitatubu, haziwezi kusamehewa na hivyo zitapotezwa.”

Alimalizia na kusema “JEHANUM haipo, kilichopo ni nafsi za wenye dhambi kupotea milele.”

Mtu huyu mwenye mamilioni ya wafuasi leo hii katoa kauli asizoweza kuzithibitisha ndani ya maandiko matakatifu. Bwana Yesu alitoa mfano wa yule Tajiri na Lazaro kuthibitisha kuwa yapo mateso baada ya kufa, na kuzimu ipo yenye funza wasiokufa, na mateso yasiyoelezeka kwa wale wote waliokufa katika dhambi.

Lakini yeye (Papa) anasema mtu akifa anayo nafasi ya pili ya kutubu, hili limekuwa ni neno la faraja kwa wafuasi wake wengi, lakini hawajui nia ya shetani ni nini!! Nia yake ni watu waendelee kustarehe katika dhambi wakijua hata wakifa ipo nafasi ya pili! Lakini kumbuka Yule Tajiri wa Lazaro aliomba nafasi ya kwenda kuwahubiria tu ndugu zake akakosa sembuse kutubu!!!!!...Hakuna toba baada ya kufa, kitakachofuata ni HUKUMU.

Tokeni kwake enyi watu wangu……KUZIMU IPO! NI KITU HALISI KABISA USIDANGANYIKE.
 
 

JE! WEWE NI MBEGU HALISI?


Huu ni wakati wa kuwa makini sana juu ya hatma ya maisha yetu ya rohoni, kwasababu tusipokuwa makini katika nyakati hizi na kwa jinsi siku zinavyozidi kwenda tunaweza tukajikuta tunaangukia katika vifungo vya shetani pasipo hata kujijua.

Kumbuka shetani sasa hivi anatenda kazi ndani ya KANISA la Mungu, hawezi kutilia mkazo sana kwa watu wa nje walio waovu kwasababu hao ameshawapata siku nyingi..anakutafuta wewe unayejiita mkristo unayejiona umesimama. Na unadhani atakupatia wapi zaidi ya kanisani.? Huko ndiko kiti chake cha enzi alipokiamishia.

Bwana Yesu alizungumza hivi;

Mathayo 13:24-30

24 Akawatolea mfano mwingine, akisema, Ufalme wa mbinguni umefanana na mtu aliyepanda mbegu njema katika konde lake;
25 lakini watu walipolala, akaja adui yake akapanda magugu katikati ya ngano, akaenda zake.
26 Baadaye majani ya ngano yalipomea na kuzaa, yakaonekana na magugu.
27 Watumwa wa mwenye nyumba wakaenda wakamwambia, Bwana, hukupanda mbegu njema katika konde lako? Limepata wapi basi magugu?
28 Akawaambia, Adui ndiye aliyetenda hivi. Watumwa wakamwambia, Basi, wataka twende tukayakusanye?
29 Akasema, La; msije mkakusanya magugu, na kuzing'oa ngano pamoja nayo.
30 Viacheni vyote vikue hata wakati wa mavuno; na wakati wa mavuno nitawaambia wavunao, Yakusanyeni kwanza magugu, myafunge matita matita mkayachome; bali ngano ikusanyeni ghalani mwangu.

Kumbuka magugu na ngano ni vitu vinavyofanana sana, kwa kuviangalia huwezi ukavitofautisha mpaka vitakapokuwa vikubwa na kutoa mazao, Katika mfano huo tunafahamu kuwa aliyepanda hizo mbegu njema ni BWANA YESU na shamba lake ni KANISA. Tunaweza tukaona jinsi kanisa la kwanza lilivyokuwa safi, takatifu lisilojichanganya na mafundisho yoyote ya uongo au mapokeo yeyote ya kibinadamu, ni kanisa lililokuwa halina dosari,

Lakini baada ya shetani kuona hilo alianza kuja na mbinu za kuliharibu, hivyo aliiga njia ile ile ya kupanda mbegu kama vile Bwana alivyofanya. Ndipo akaanza kwanza kwa kupenyeza mafundisho ya uongo katikati ya kanisa la Mungu, kisha ile mbegu ya uongo ilipomea baadaye ikageuka na kuwa dini, na kukaa katikati ya kanisa la Mungu. Kuanzia hapo hizi mbegu mbili zikawa zipo pamoja zikishindana katika kanisani la Kristo.(Magugu na Ngano)

Mungu kwa kulifahamu hilo aliruhusu vyote vimee kwa pamoja mpaka wakati wa mavuno utakapowadia kwasababu kama tulivyoona magugu yakiwa machanga ni ngumu kuyatofautisha na ngano, yanafanana sana kwa tabia zao. Na Mungu aliposema yaache yakue pamoja ni kiashiria kuwa yote yapate mvua kutoka kwa Mungu.(Mathayo 5:45). Ikiwa na maana kuwa Mungu aliyaruhusu yafanikiwe katika njia zao kama vile tu zile mbegu njema zifanikiwavyo mpaka wakati wa mavuno utakapowadia. Yote yananyeshewa mvua, kumbuka hata manabii wa uongo wanatabiri kwa jina la Bwana na inatokea, wanaponya na kutoa pepo kwa jina la Yesu na yanawatii, lakini siku ile Bwana atawaambia siwajui nyinyi mtendao maovu. Kwasababu hawa walinyeshewa mvua moja na ngano halisi lakini ndani yao walikuwa ni magugu.

Hivyo Kanisa katoliki lilianza kujitokeza katika kanisa la Mungu kama GUGU la kwanza, enzi zile za kanisa la kwanza, lilianza na mafundisho tu (MBEGU), baadaye likaota mizizi na kujiundia dini inayofanana na ukristo katika kanisa, likazidi kusambaa katika shamba la Mungu na kusonga zile mbegu halisi za Mungu na ndio maana tunaona hili kanisa lilianza kuharibu mafundisho ya NENO LA MUNGU na kupachika mafundisho ya uongo na kama tunavyofahamu tabia halisi ya gugu ni kuharibu kile kilicho halisi, na ndio maana baadaye tunavyosoma katika historia liliuawa watakatifu wa Mungu zaidi ya milioni 68 waliojaribu kwenda kinyume na mafundisho yake ya uongo.

Na lilipofikia kilele likazaa na magugu mengine mengi yanayofanana ni hilo, yakifanya kazi moja, kuiharibu mbegu halisi ya Mungu. Lakini biblia inasema wakati wa mwisho ambao ndio tuliopo sasa, yale magugu na ngano vitatenganishwa, yale magugu yataanza kwanza kwa kufungwa matita matita kwasababu yapo mengi,

JE! HAYA MATITA MATITA NI NINI?..Haya si mengine zaidi ya MADHEHEBU, na watakaoyafunga ni akina nani? Hawa Si wengine zaidi ya wanaojiita viongozi wa dini lakini ndani ni mitume wa uongo (2Wakoritho 11:13).

Mhubiri yoyote anayekupeleka kwenye dini yake zaidi ya kukupeleka kwa Kristo huyo ni mvunaji anayekufunga katika mojawapo ya tita la magugu. Kiongozi anayekufundisha mafundisho yasiyotokana na utakatifu, anakuambia tu! Mungu ni wa rehema, huku hana habari na mambo ya toba au kuhubiri utakatifu yeye anakazania mambo ya ulimwengu huu tu, ujue huyo ni mvunaji anayetaka kukufunga katika mojawapo ya tita la magugu lililoandaliwa kwa ajili ya kuchomwa moto.

Mhubiri anayekuhubira kutwa kuchwa mafanikio tu! Agusii hata siku moja hatma ya maisha yako ya rohoni, anayekuhubiria Kristo harudi leo wala kesho..mkimbie huyo ni mvunaji wa siku za mwisho kazi yake ni kuwafunga watu wa namna hiyo wasiotaka kujihusisha na mambo ya Mungu bali wajihusishao na mambo ya ulimwengu huu tu.

Ukiona kanisa linakuambia hakuna kuzimu na mateso yake, au halitaki kudumu katika NENO LA MUNGU peke yake,linakuongoza katika ibada za sanamu ambazo Mungu amezipinga vikali, kimbia haraka sana hilo ni TITA la kukusanya watu wa dizaini hiyo wasiotaka kudumu kutenda mapenzi ya Mungu..

2Wathesalonike 2:10 “na katika madanganyo yote ya udhalimu kwa hao wanaopotea; KWA SABABU HAWAKUKUBALI KUIPENDA ILE KWELI, WAPATE KUKOLEWA.
11 Kwa hiyo Mungu awaletea NGUVU YA UPOTEVU, WAUAMINI UONGO;
12 ili wahukumiwe wote ambao hawakuiamini kweli, bali walikuwa wakijifurahisha katika udhalimu.”

Na Kumbuka kila siku hawa wavunaji(Manabii wa uongo) na haya matita ya magugu yanazidi kuongezeka kuonyesha kuwa huu ni wakati wa mavuno wa siku za mwisho.
 

LAKINI NGANO HALISI NI IPI?

Ukisoma mfano huo kwa makini utaona kuwa NGANO HALISI haijakusanywa katika matita matita mengi kama magugu yalivyofanywa, bali Ngano imekusanywa pamoja mara moja tu na kupelekwa ghalani. Kuonyesha kuwa bibi-arusi wa Kristo hatakuwepo kati ya mojawapo ya hivyo vikundi, Bibi-arusi hana utambulisho wa kimadhehebu. Baada ya kukusanywa maramoja atapelekwa ghalani (mbinguni). Ndugu tunaishi katika wakati wa bibi-arusi wa Kristo kukusanywa kwa ajili ya unyakuo. Na anakusanyikia wapi?.

Bwana Yesu aliwaambia wanafunzi wake katika Mathayo 24: 23 “Wakati huo mtu akiwaambia, Tazama, Kristo yupo hapa, au yuko kule msisadiki.
24 Kwa maana watatokea makristo wa uongo, na manabii wa uongo, nao watatoa ishara kubwa na maajabu; wapate kuwapoteza, kama yamkini, hata walio wateule.
25 Tazama, nimekwisha kuwaonya mbele.
26 Basi wakiwaambia, Yuko jangwani, msitoke; yumo nyumbani, msisadiki.”

Hii Ikiwa na maana kuwa katika siku za mwisho watatokea mitume na manabii wengi wa uongo, na zitatokea dini nyingi na madhehebu mengi ya uongo, na kila moja likidai kuwa lenyewe lina Kristo, ili tu yapate kuwakufunga watu kwenye matita yao..lakini Bwana alisema yatakapowafuata na kuwaambia hivyo msisadiki?. Na ndipo wanafunzi wake wakamuuliza..kama hatutawasidiki hao basi tukusanyike wapi sasa? Jibu lake lilikuwa ni hili.

Luka 17: 37 “Wakajibu, wakamwuliza, WAPI, BWANA? Akawaambia, ULIPO MZOGA, NDIPO WATAKAPOKUTANIKA TAI.”

Mzoga ni NENO LA MUNGU, na TAI ni BIBI-ARUSI, Hivyo katika siku hizi za mwisho bibi-arusi safi wa Kristo hatakusanyika katika madhehebu na dini bali atakusanyika katika NENO LA MUNGU tu..yeye hatafungwa na dini bali atafungwa, ‘’na nini NENO linasema’’ Hicho tu. Hii ndio ndio nguvu Mungu aliyoiachia sasa hivi kwa bibi-arusi wake, kurudi katika imani ya Mitume, Biblia.

Hivyo ndugu jitathimini je! na wewe umefungwa kama magugu kwenye matita tayari kwa kuchomwa au unakusanywa ghalani mwa Mungu kwa NENO lake?. Kama umefungwa huko toka, sio kwa miguu bali kwa kugeuzwa moyo wako na kuligeukia NENO linachosema na sio mapokeo ya dhehebu. Kwasababu biblia inatuambia 1Petro 1:23 “Kwa kuwa mmezaliwa mara ya pili; si kwa mbegu iharibikayo, bali kwa ile isiyoharibika; KWA NENO LA MUNGU LENYE UZIMA, lidumulo hata milele.”

Hivyo Umeona hapo? Bibi-arusi amezaliwa kwa mbegu isiyoharibika KWA NENO LA MUNGU tu, na sio kitu kingine.
Ni maombi yangu kuwa utazaliwa mara ya pili kwa NENO LA MUNGU na kumtazama Kristo peke yake aliyekufia msalabani ili ufanyike kuwa ngano na sio gugu.

Ubarikiwe.

Thursday, March 29, 2018

YATAFUTE YALIYO JUU SIKU ZOTE.

Wakolosai 3:1 “Basi mkiwa mmefufuliwa pamoja na Kristo, YATAFUTENI YALIYO JUU KRISTO ALIKO, ameketi mkono wa kuume wa Mungu. 2 YAFIKIRINI YALIYO JUU, SIYO YALIYO KATIKA NCHI.”

Kama wasafiri hapa duniani, kila siku shabaha yetu inapasa iwe ni kufika mbinguni kwa gharama yoyote ile, Biblia imetuambia “tuyatafute” na “kuyatafakari” yaliyo juu, ikiwa na maana kuwa kwa bidii zote na nguvu zetu zote, tutafute kanuni za kutufanya sisi kuingia mbinguni, tumeambiwa tuutafute kama vile tunavyotafuta fedha au kama hazina iliyositirika (Mithali 2:4),

> Mambo ya ulimwengu huu yasiwe kikwazo cha wewe kuikosa mbingu, unapaswa utumie hekima popote ulipo usiwe na kisingizio kwamba kitu fulani kimekusonga usimtafute Mungu, kumbuka wapo katika dunia hii hii matajiri wakubwa kuliko wewe na bado wanayafikiria yaliyo juu, na maisha yao ni kama wasafiri tu hapa duniani, kama mfano wa akina Sulemani katika biblia, japo alikuwa ni tajiri lakini aliyatafakari sana yaliyo juu ,

> Wapo wenye vyeo vikubwa kuliko wewe katika kizazi hiki hiki unachoishi lakini fikra zao na mawazo yao yapo mbinguni, usiku na mchana wanamwomba Bwana ufalme wake uje!, mfano ni kama Danieli alivyokuwa katika biblia,japo alikuwa mwenye cheo kikubwa lakini kutwa mara tatu alikuwa akimwomba Mungu kuhusu hatma yake na watu wake.

> Vivyo hivyo wapo maskini kuliko wewe, hawana chakula wala nguo wala mahitaji yoyote lakini mawazo yao na fikra zao si katika mambo ya ulimwengu huu bali mbinguni, japo wanapitia magumu, wanaishi kama wasafiri tu hapa duniani…Wanaishi kama Lazaro wa kwenye biblia, ingawa alikuwa anakula makombo lakini hakutupa wokovu wake chini.

> Wapo wenye shida nyingi kuliko zako; wagonjwa, walemavu, hawana watoto, mayatima, lakini kwao hayo yote si kitu, mawazo yao na fikra zao zimeelekea juu mbinguni, siku kwa siku wakijihakiki maisha yao wasianguke, wakijiepusha na maovu wasije wakaikosa mbingu.

Na wewe je! UNAYATAFUTA YALIYO JUU! Au FIKRA ZAKO ZIMEELEKEA JUU MBINGUNI? Katika hali yoyote uliyopo?..Kumbuka vya duniani vinapita, hivyo visiwe sababu ya wewe kukusonga na kuikosa mbingu. Anza sasa kutamani kwenda mbinguni.
 
Tunaishi katika  muda wa nyongeza Bwana Yesu anakaribia kurudi.
 
Ubarikiwe.

Wednesday, March 28, 2018

USIMFANYIE JEURI ROHO WA NEEMA.


Kuna hatari kubwa sana kuidharau Neema ya Bwana YESU KRISTO, Katika agano la kale, kule jangwani Mungu alipokuwa anazungumza na wana wa Israeli katika mlima SINAI, Utukufu wa Mungu ulikuwa ni mkubwa kiasi kwamba hata watu wenyewe walikataa kuukaribia ule mlima kwa jinsi ulivyokuwa unatisha, kwa hofu na kwa kutetemeka walifikia hatua ya kumwambia Musa azungumze nao lakini sio Mungu. Mlima ule ulitisha sana hata kwa mnyama yoyote aliyeusogelea ilikuwa ni kifo.

Biblia inasema; katika Waebrania 12:18-25

18 Maana hamkufikilia mlima uwezao kuguswa, uliowaka moto, wala wingu jeusi, na giza, na tufani,
19 na mlio wa baragumu na sauti ya maneno; ambayo wale walioisikia walisihi wasiambiwe neno lo lote lingine;
20 maana hawakuweza kustahimili neno lile lililoamriwa, Hata mnyama akiugusa huo mlima atapigwa kwa mawe.
21 Na hayo yaliyoonekana jinsi yalivyokuwa ya kutisha, hata Musa akasema, Nimeshikwa na hofu na kutetemeka.
22 Bali ninyi mmeufikilia MLIMA SAYUNI, NA MJI WA MUNGU ALIYE HAI, Yerusalemu wa mbinguni, na majeshi ya malaika elfu nyingi,
23 mkutano mkuu na kanisa la wazaliwa wa kwanza walioandikwa mbinguni, na Mungu mwamuzi wa watu wote, na roho za watu wenye haki waliokamilika,
24 na Yesu mjumbe wa agano jipya, na damu ya kunyunyizwa, inenayo mema kuliko ile ya Habili.
25 Angalieni msimkatae yeye anenaye. Maana ikiwa hawakuokoka wale waliomkataa yeye aliyewaonya juu ya nchi, ZAIDI SANA HATUTAOKOKA SISI TUKIJIEPUSHA NA YEYE ATUONYAYE KUTOKA MBINGUNI;”.

Kama biblia inavyosema sisi tulio kwenye AGANO lililo bora la DAMU YA YESU KRISTO, tunaukaribia mlima wa mbinguni(SAYUNI YA MBINGUNI) mbali na wana wa Israeli wao waliukaribia mlima wa duniani(SINAI),.. Ni dhahiri kuwa wale walioukaribia mlima wa mbinguni, ambao maelfu ya malaika wamekusanyika ndio walio karibu zaidi na Mungu kuliko hao wengine.Hivyo hawa wa mbinguni ndio wanapaswa wawe na hofu kubwa zaidi na wawe makini zaidi, kwasababu wapo karibu na Mungu, hivyo kosa moja linaweza likakugharimu mauti ya kiroho.

Na ndio maana biblia inasema Wafilipi 2:12b-13 “ UTIMIZENI WOKOVU WENU WENYEWE KWA KUOGOPA NA KUTETEMEKA. 13 Kwa maana ndiye Mungu atendaye kazi ndani yenu, kutaka kwenu na kutenda kwenu, kwa kulitimiza kusudi lake jema.”

Hii tunayoiita NEEMA, ni kweli ni NEEMA lakini sio neema kwa wakati wote, Inapochezewa au kutupiliwa mbali inageuka kuwa laana mbaya kuliko zote. Biblia inasema hali ya mtu Yule aliyeidharau hali yake ya mwisho inakuwa mbaya kuliko ile ya kwanza.

2Petro 2:20 “Kwa maana wale waliokwisha kuyakimbia machafu ya dunia kwa kumjua Bwana na Mwokozi Yesu Kristo, kama wakinaswa tena na kushindwa, hali yao ya mwisho imekuwa mbaya kuliko ile ya kwanza.
21 Maana ingekuwa heri kwao kama wasingaliijua njia ya haki, kuliko kuijua, kisha kuiacha ile amri takatifu waliyopewa.
22 Lakini imetukia kwao sawasawa na ile mithali ya kweli, Mbwa ameyarudia matapiko yake mwenyewe, na nguruwe aliyeoshwa amerudi kugaa-gaa matopeni.”

Pale unapojiita mkristo halafu bado unakwenda kwa waganga ili upate kitu Fulani, ukijifariji kwamba utatubu tu siku moja, kwasababu neema bado ipo!! Usidanganyike NEEMA haifanya kazi kwa namna hiyo shetani anataka ufikirie hivyo ili ukumbane na mauti ya kiroho kutoka kwa Mungu mwenyewe.

Unapojiita mkristo halafu bado ni mwasherati, mlevi, mwabudu sanamu, na huku unafahamu kabisa hayo uyafanyayo sio sawa, ukijifariji utatubu, kwasababu tunaishi chini ya NEEMA, biblia inasema ingekuwa heri kwako kama usingeijua ile haki, Ndugu utaangukia hukumu ya kifo cha kiroho,na ukishafikia hiyo hatua, ndio pale injili kwako inageuka kuwa upuuzi tu masikioni mwako au hadithi za kutunga, ROHO MTAKATIFU anakuacha na kuondoka, na ile hali ya kuugua ndani juu dhambi inaondoka kwako, kutenda dhambi kunageuka kuwa ni kitu cha kawaida, hapo hata uhubiriweje injili huwezi kugeuka unasubiria moto wa jehanum.

Shetani ndiyo agenda yake sasa hivi, kuwapofusha watu na hili Neno “tunaishi chini ya neema” na kusema Mungu ataturehemu tu! Hata tuwe watenda dhambi.. Kumbuka Neema ina pande mbili, kwa Yule anayeikubali ndio italeta manufaa chanya kwake, lakini kwa Yule anayeidharau na kuitupilia mbali inageuka kuwa LAANI kubwa mno.

Waebrania 10:26-29 “Maana, kama tukifanya dhambi kusudi baada ya kuupokea ujuzi wa ile kweli, HAIBAKI TENA DHABIHU KWA AJILI YA DHAMBI;
27 BALI KUNA KUITAZAMIA HUKUMU YENYE KUTISHA, NA UKALI WA MOTO ULIO TAYARI KUWALA WAO WAPINGAO.
28 Mtu aliyeidharau sheria ya Musa hufa pasipo huruma, kwa neno la mashahidi wawili au watatu.
29 Mwaonaje? Haikumpasa adhabu iliyo kubwa zaidi mtu yule aliyemkanyaga Mwana wa Mungu, na kuihesabu damu ya agano aliyotakaswa kwayo kuwa ni KITU OVYO, NA KUMFANYIA JEURI ROHO WA NEEMA?”.

Unaona hapo usitende dhambi za makusudi ukidhani neema itaendelea kudumu siku zote maishani mwako, Ndugu huu ni wakati wa kujitazama tena maisha yako ni wapi haujakaa sawa, unalega lega au vuguvugu. Fanya bidii usimame imara angali bado Roho wa NEEMA analia ndani yako uache dhambi, fanya hima usimfanyie jeuri kabla haujachelewa, kwa maana wakati wa wokovu uliokubaliwa ni sasa.

Tubu mgeukie Kristo aliye mkuu wa uzima wako, naye ni mwaminifu atakuosha na kukupa uzima wa milele.
 
Mungu akubariki.

WALIPO WAWILI AU WATATU KWA JINA LANGU

Naomba usome ushuhuda huu mfupi utakujenga,
 
 "Mimi na ndugu yangu tumekuwa na desturi ya muda mrefu kukaa pamoja na kushirikishana NENO LA MUNGU mara nyingi ili kuepuka usumbufu wa watu tumekuwa tukiondoka na kwenda mbali na makazi ya watu, sehemu zenye utulivu na kutumia muda mwingi kulitafakari NENO LA MUNGU, pamoja na kutiana moyo katika safari yetu ya Ukristo. Siku moja wakati tunatembea muda wa mchana kama saa 7 huku tunazungumza habari za Mungu na kutafakari ghafla mbele yetu njiani umbali si mrefu sana, tulioana punda watatu wamefungwa NIRA wanafuata njia, wakikokota kigari cha mzigo wa majani na nyuma kulikuwa na mtu mmoja aliyekuwa akiwaendesha hao punda, lakini jambo moja lilitushangaza kidogo ni kuona punda 3 wamefungwa nira huku wakikivuta kile kigari wakati mara nyingi inakuwa ni punda wawili tu!.

Hivyo tulipokaribia kuwasogelea ili tuone vizuri, Yule punda aliyekuwa katikakati yao alitoweka wakabaki punda wawili kama kawaida. Wakati tunalishangaa hilo tukio lilitokea wale punda walifika mahali wakakuta na mtaro, uliokuwa mgumu kidogo kuvuka kutokana na ule mzigo waliokuwa wanauvuta, hivyo Yule Bwana wao aliokuwa anawaongoza alipoona wamesimama aliwachapa kwa fimbo yake aliyokuwa nayo, lakini japo ule mzigo ulikuwa ni mkubwa kwa wao kuuvukisha katika ule mtaro mwishoni walifanikiwa kupandisha na kuendelea na safari.
Tulibaki tunajiuliza maswali ni kitu gani tumeona? Ni mazingaumbwe au nini?. Ndipo Mungu akutupa ufahamu saa ile ile ni kwamba Mungu alitufumbua macho tuone jambo linaloendelea katika roho kuhusu sisi,"


Biblia inasema Mathayo 18:20 “ Kwa kuwa walipo wawili watatu wamekusanyika kwa jina langu, nami nipo papo hapo katikati yao.”

Tafsiri ya lile ono ni kuwa wale punda wawili wanatuwakilisha sisi wawili mimi na ndugu yangu, Yule punda wa tatu aliyekuwa katikati na kisha baadaye akaja kutoweka alimwakilisha Bwana YESU.

Na ule mzigo wale punda waliokuwa wameubeba ni SHERIA ZAKE, hivyo tunapokuwa wawili au zaidi Mungu anatufunga Nira yake mwenyewe sisi kwa sisi, na yeye akiwa katikati yetu kutusaidia mzigo wake(sheria zake), hivyo sheria zake zinakuwa nyepesi kuzishika.

Bwana Yesu pia alitupeleka kwenye hili andiko Mathayo 11:28 “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha.
29 JITIENI NIRA YANGU, MJIFUNZE KWANGU; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu;
30 KWA MAANA NIRA YANGU NI LAINI, NA MZIGO WANGU NI MWEPESI.

Bwana alituonyesha kuwa anayo NIRA yake na MZIGO wake kwa watu wake, japo watu wa nje watauona kama ni mzigo mzito lakini Bwana akiwa katikati yetu unakuwa mwepesi kwasababu yeye anatusaidia, anakuwa anafanyika kama punda wa tatu katikati yetu.

> Kuishi maisha ya kuukataa ulimwengu huo ni mzigo wa Kristo aliokutwisha, na ndio maana wengine watakushangaa unawezaje kuishi maisha ya kutokufanya uasherati.

> Kufanya kazi yoyote ya Mungu ni mzigo wa Kristo, lakini yeye anakupa wepesi hususani mnapokuwa wawili au zaidi na ndio maana kila mahali Bwana alikuwa akiwatuma wawili wawili kazini kuhubiri injili.

Hivyo ndugu, kuna umuhimu mkubwa kuwa na mwenzako au wenzako mnaofanana imani, kwasababu mnapokuwa wawili au watatu au zaidi kwa jina lake lile NENO lazima litimie, ATAKUWA KATIKATI YENU. Mnakuwa mmefungwa NIRA na Kristo pamoja, hivyo mtajikuta kiurahisi mnazitimiza sheria za Bwana bila ugumu wowote tofauti na unapokuwa mwenyewe.

Umuhimu wa kuwa na mwenzako au kukusanyika na wenzako ni uwepo wa kipekee unashuka mahali mlipo, vitu kama faraja, kutiana moyo, kulindana, kushirikishana, mafunuo n,k. vinatoka huko kiasi kwamba hata shetani inamuwia ugumu kupata nafasi ya kukujaribu kwasababu yupo ndugu yako pembeni anayekuchunga.

Ndio maana biblia inasema katika Mhubiri 4:9-12 “Afadhali kuwa wawili kuliko mmoja; Maana wapata ijara njema kwa kazi yao.
10 Kwa maana wakianguka, mmoja wao atamwinua mwenzake; lakini ole wake aliye peke yake aangukapo, wala hana mwingine wa kumwinua!
11 Tena, wawili wakilala pamoja, hapo watapata moto; lakini mmoja aliye peke yake tu awezaje kuona moto?
12 Hata ikiwa mtu aweza kumshinda yule aliye peke yake, wawili watampinga; wala kamba ya nyuzi tatu haikatiki upesi.”

Unaona hapo, kuna umuhimu wa kuwa karibu na ndugu anayeenda na wewe imani, Sisi baada ya Bwana kutufundisha hayo, tumekuwa tukikaa pamoja muda mrefu wakati mwingine kuanzia asubuhi mpaka jioni na tumekuwa tukimwona Mungu kwa namna ya kipekee isiyokuwa ya kawaida tofauti na pale mwanzo kila mtu alipokuwa kivyake.

Unawakumbuka wale watu wawili waliokuwa wanatoka Yerusalemu na kuelekea Emau, Njiani wakati wanazungumza habari za kufufuka kwake Yesu, Bwana mwenyewe aliwatokea na kuungana nao pasipo wao kujijua, baadaye kabisa mwishoni ndipo walipofunguliwa macho na kufahamu kuwa Yule alikuwa ni BWANA YESU mwenyewe(Luka 24).

Vivyo hivyo na wewe utakapojumuika na mwenzako au wenzako na kuanza kumzungumzia Bwana Lile Neno lake la ahadi lazima litimie. Na safari yako ya ukristo haitahitaji nguvu nyingi.
Natumai ushuhuda huu utakufanya uchukue uamuzi wa kujumuika na ndugu aliye  moja na wewe.

Bwana akubariki sana.

Monday, March 26, 2018

ZIKUMBUKE FADHILI ZA MUNGU


Ni rahisi KUANGUKA au KUPOA katika Imani kama hautajiwekea utaratibu wa Kujikumbusha matendo yote mema Mungu aliyokutendea nyuma katika maisha yako. Jambo lililowafanya Wana wa Israeli kule jangwani washindwe kusonga mbele na kukwazwa na mabaya, lilikuwa si lingine zaidi ya KUSAHAU fadhili za Mungu walizotendewa nyuma, kwamfano walipotoka Misri, na kukutana na kikwazo cha bahari, walianza kunung’unika wakasahau siku chache tu nyuma Mungu aliwapigania kwa mkono hodari dhidi ya maadui zao wamisri,

vivyo hivyo mara baada tu ya kufanyiwa muujiza mwingine wa bahari kupasuka walimshangilia Mungu kwa furaha na kumwimbia nyimbo za shangwe lakini baada ya siku tatu mbeleni, manung’uniko yakaanza tena pale walipokosa maji ya kunywa, tatizo lilikuwa ni moja tu! Walisahau wema wa Mungu waliotendewa siku chache nyuma, laiti wangetilia maanani mema yale na kukumbuka fadhili zote zile, wasingeshindwa kustahimili majaribu waliyokutana nayo. Na ndivyo ilivyoendelea kuwa katika safari yao yote, manung’uniko kila walipokutana na changamoto.

Na ndio sababu Mungu aliwakataza Israeli wote wasile WANYAMA WASIO CHEUA, kwa mfano nguruwe au farasi nk. Unajua ni kwa sababu gani??, kwasababu katika roho wanafunua kitu Fulani. Mnyama anayecheua ni mnyama ambaye akila chakula anao uwezo wa kukirudisha tena kinywani mwake na kukitafuna kisha akimeze tena, kwa mfano ng’ombe analo tumbo la akiba, akila baadaye anarudisha na kukitafuna tena. Hivyo wanyama wa namna hiyo hawakuwa najisi, kwa tabia hiyo tu. Ikifunua katika roho kuwa watu wote wasiokuwa na uwezo wa kuzikumbuka na kuzitafakari fadhili na sheria za Mungu ni NAJISI mbele zake. Watu wote wa Mungu wanapaswa wawe na uwezo wa kucheua, baada ya kusikia au kufanyiwa miujiza, sasa kinachofuata ni kuyarudisha tena katika akili na kuyatafakari hayo kila mara.

Yakobo 1: 22-25 “Lakini iweni watendaji wa neno, wala si wasikiaji tu, hali mkijidanganya nafsi zenu.
23 Kwa sababu mtu akiwa ni msikiaji wa neno tu, wala si mtendaji, mtu huyo ni kama mtu anayejiangalia uso wake katika kioo.
24 Maana hujiangalia, kisha huenda zake, mara akasahau jinsi alivyo.
25 Lakini aliyeitazama sheria kamilifu iliyo ya uhuru, na kukaa humo, ASIWE MSIKIAJI MSAHAULIFU, bali mtendaji wa kazi, huyo atakuwa heri katika kutenda kwake.”

Kadhalika na kwa wakati tuliopo sasa, ili tusonge mbele au tuweze kusimama katika IMANI na kushinda wakati wa majaribu inatupasa tujiwekee utaratibu wa kutafakari na kujikumbusha kila siku mambo mema ambayo Mungu amewahi kututendea katika maisha yetu ya nyuma, Kwa mfano ulipowahi kupatwa na ugonjwa Fulani ambao ulikutesa sana na Bwana akakuponya, ni vizuri kujikumbushia jambo hilo kila siku, au ulimwomba Mungu jambo Fulani akakupa na kukufanikisha katika mambo yako na ukafahamu kabisa huyo ni Mungu aliyekutendea hivyo, unapaswa kulifikiria hilo kila siku usije ukasahau pale tatizo litakapokuja ili uweze kukabiliana nalo.

Kumbuka tena mahali Mungu alipokushindania ambapo unajua kabisa pasipo yeye usingeweza kufanikiwa, uwe unalitafakari hilo kila siku litakusaidia huko mbeleni ili umsimnung’unikie Mungu..Kuna hatari kubwa sana ya kuanguka kama hautajijingea huo utaratibu wa kukumbuka mambo uliyotendewa..Sisi wanadamu tuna tabia ya kusahau hivyo ili usisahau ni vizuri uwe unaandika chini kila wema Mungu anaokufanyia kila siku.Kwa kufanya hivyo ndivyo utakavyoweza kudumu katika IMANI siku zote. Na pia unaposoma Neno la Mungu jenga tabia ya kujikumbusha kila wakati ili usisahau mapenzi ya Mungu katika maisha yako.

Wakati mwingine unajikuta unadondoka katika dhambi za usengenyaji, kwasababu unasahau Neno la Mungu, linakuwa halijakaa kwa wingi ndani yako, unajikuta unashindwa kusamehe kwasababu huna tabia ya kutafakari kila siku NENO LA MUNGU, Unajikuta wewe ni mkristo lakini unazungumza maneno ya mizaha, kwasababu mistari inayohusiana na mambo kama hayo imefutika ndani ya moyo wako, huna jambo la kukukumbusha kila wakati.

Ni maombi yangu utaanza kujenga utaratibu kuanzia leo wa kurekodi mambo yote mazuri Mungu anayokutendea ili yawe akiba kwa wakati wa shida au majaribu mbeleni. Na pia utaanza kutafakari NENO la Mungu kila siku. Sulemani kwa hekima ya Roho alituandikia sisi tulio watoto wa Imani na kusema;

Mithali 7:2 “Mwanangu, yashike maneno yangu, Na kuziweka amri zangu akiba kwako.
2 Uzishike amri zangu ukaishi, NA SHERIA YANGU KAMA MBONI YA JICHO LAKO.
3 ZIFUNGE KATIKA VIDOLE VYAKO; ZIANDIKE JUU YA KIBAO CHA MOYO WAKO.”

Na Daudi alisema;

Zaburi 119: 97 “Sheria yako naipenda mno ajabu, NDIYO KUTAFAKARI KWANGU MCHANA KUTWA.
98 Maagizo yako hunitia hekima kuliko adui zangu, KWA MAANA NINAYO SIKU ZOTE.
99 Ninazo akili kuliko wakufunzi wangu wote, Maana shuhuda zako ndizo NIZIFIKIRIZO.
100 Ninao ufahamu kuliko wazee, Kwa kuwa nimeyashika mausia yako.”

Ubarikiwe na BWANA YESU.

ESTA: Mlango wa 1 & 2

MFALME wa WAFALME YESU KRISTO Bwana wetu, atukuzwe daima.

Karibu kwa neema za Mungu tujifunze kitabu cha Esta leo tukianza na ile sura ya 1 na ya 2.Ni vizuri ukiwa na biblia yako pembeni uipitie habari hii kwanza ndipo tuende pamoja. Kama tunavyofahamu Agano la Kale ni kivuli cha Agano jipya hivyo kila habari inayozungumzwa katika agano la kale, inafunua jambo fulani linaloendelea katika roho kwa wakati tunaoishi sasa.
Kitabu hiki kwa ufupi kinaelezea habari ya Mfalme Ahasuero wa Ufalme wa Umedi & Uajemi aliyekuwa tajiri sana na mwenye nguvu ni mfalme aliyetawala mataifa 127, biblia inasema kuanzia India mpaka taifa la Kushi (Ethiopia), kote huku alimiliki na kwa wakati ule alikuwa ni kama Mfalme wa dunia. Kwasababu Umedi na Uajemi ndio zilikuwa zinatawala dunia kwa wakati huo.


Hivyo ilifika wakati mfalme aliandaa sherehe kubwa sana kwa wakuu wake wote, pamoja na watu wote waliokuwapo katika mji wake (huko Shushani ngomeni), wakubwa kwa wadogo walihudhuria, watu walikula na kunywa jinsi wapendavyo, na kwa fahari yake aliamua kumwasilisha malkia aitwaye VASHTI, mbele za wakuu wote wauone uzuri wake, maana biblia inasema Vashti alikuwa ni mzuri sana wa uso, kwasababu hata tafsiri ya jina Vashti linamaanisha “mwanamke mzuri”.


Lakini mambo hayakuwa kama yalivyotarajiwa, Badala ya Vashti kumtii mume wake, na zaidi ya yote alikuwa ni MFALME, alikaidi amri ile kwa KIBURI cha Uzuri wake na kuamua kutokwenda, Jambo hili lilionekana kuwa ni aibu kubwa kwa Uajemi yote, kwasababu hakukuwa na desturi ya mwanamke kumvunjia heshima mfalme, Na tunasoma Vashti alikuja kuvuliwa umalkia wake na kutafutwa mwengine “ALIYE MWEMA KULIKO YEYE”.

Esta 1:19 “Basi mfalme akiona vema, na itoke kwake amri ya kifalme, nayo iandikwe katika sheria za Waajemi na Wamedi isitanguke, ya kwamba Vashti asifike tena mbele ya mfalme Ahasuero; na umalkia wake mfalme ampe mwingine aliye mwema kuliko yeye.”

Hivyo moja kwa moja, ikaanza kupangwa mipango ya kumtafuta malkia mwingine mahali pa Vashti, mbiu zikapigwa katika mataifa yote duniani (127) aliyokuwa anayamiliki, walikuja MABIKIRA vijana wengi na ESTA alikuwa mmoja wapo. Kumbuka wote hawa walitokea katika machimbuko tofauti tofauti, wengine katika familia za kitajiri, wengine katika koo za kifalme, wengine walikuwa mabinti za maakida, wengine familia za kisomi, wengine familia za mabinti warembo n.k. Kwahiyo walikusanyika wengi sana pengine mabinti 30,000 au zaidi.

Lakini tukiendelea kusoma habari tunaona kwamba kila mmoja alipewa uhuru wa kujipamba kwa jinsi atakavyo, apewe chakula atakacho, au lolote atakalolitaka apewe ili tu siku atakapopelekwa mbele ya mfalme isionekane kasoro yoyote kama walivyofanyiwa wakina Danieli, Shedraka, Meshaki na Abednego mbele ya mfalme Nebukadreza. Hivyo mabikira wote na Esta akiwa miongoni mwao waliwekwa chini ya msimamizi mmoja wa nyumba ya mfalme aliyeitwa “HEGAI”.

Kazi ya huyu HEGAI ilikuwa ni kuhakikisha kuwa anawahudumia na kuwapa mahitaji yao kwa jinsi watakavyo. Tukisoma;

Esta 2:1-4 1 Baada ya hayo, hasira yake mfalme Ahasuero ilipotulia, alimkumbuka Vashti, na vile alivyotenda, na yale yaliyoamriwa juu yake.
2 Basi watumishi wa mfalme waliomhudumu walimwambia, Mfalme na atafutiwe mabikira vijana wazuri;
3 naye mfalme aweke wasimamizi katika majimbo yote ya ufalme wake, ili wakusanye pamoja mabikira vijana wazuri wote waende Shushani ngomeni, kwenye nyumba ya wanawake mikononi mwa HEGAI, MSIMAMIZI-WA-NYUMBA WA MFALME, mwenye kuwalinda wanawake; tena wapewe VIFAA VYA UTAKASO.
4 Naye yule msichana atakayempendeza mfalme na awe malkia badala ya Vashti. Neno hilo likampendeza mfalme, naye akafanya hivyo.”


LAKINI NI SIRI IPI ILIYOMFANYA ESTA AKUBALIKE KULIKO MABIKIRA WENGINE?.

Biblia haimtaji Esta kama alikuwa ni mwanamke mzuri kuliko wote waliohudhuria, hapana biblia inasema alikuwa na Uso mwema tu, wala hakutokea katika familia ya kitajiri kama wenzake, wala hakuwa na elimu kama wale wengine pengine ingekuwa chachu ya kumfanya mfalme avutiwe naye lakini vyote hivyo hakuwa navyo. Bali kuna jambo lingine liliomfanya mfalme avutiwe naye. Na hili tunalipata kwa HEGAI, YULE MSIMAMIZI WA NYUMBA YA MFALME na MORDEKAI mjomba yake.

Wakati wengine wakimwendea Hagai na kumlazimisha awape vitu wanavyotaka wao ili wamwendee mfalme, Esta hakuwa hivyo, bali alijinyenyekeza kwa Hegai, Huku akishikilia maagizo aliyopewa na mjomba wake Mordekai kuwa ASIJIONYESHE KABILA LAKE HUKO AENDAKO, hivyo kwa jambo hilo tu ilimpelekea Hegai avutiwe naye sana kwasababu hakupeleka sifa yoyote imuhusuyo yeye mbele zake, na kwa kuwa Hegai alikuwa ni msimamizi wa nyumba ya mfalme, kwa uzoefu wa miaka mingi aliokuwa nao kule alitambua mfalme huwa anapenda msichana wa tabia gani au huwa hapendi msichana wa tabia gani, kwasababu yeye ndiye aliyekuwa msimamizi wa Vashti kabla hajawa malkia. Kwahiyo alitambua tabia ya mfalme kuwa anapenda mwanamke katika mwonekano upi, na katika tabia ipi. Na siri hiyo HEGAI alimfunulia Esta peke yake.Akamtenga Esta na wale wengine na kumpa matunzo ya kipekee kwa msaada wa vijakazi wengine saba.

Esta 2:8-9 “Basi ikawa, wakati iliposikiwa amri ya mfalme na mbiu yake, wasichana wengi wakakusanyika huko Shushani ngomeni mikononi mwa Hegai; Esta naye aliingizwa katika nyumba ya mfalme, mikononi mwa Hegai mwenye kuwalinda wanawake.
9 Yule mwanamwali akampendeza, akapokea fadhili kwake; naye akampa upesi vifaa vya utakaso, pamoja na posho zake, na vijakazi saba walio haki yake, wa nyumbani mwa mfalme. Pia akamhamisha yeye na vijakazi wake akawaweka mahali pazuri katika nyumba ya wanawake.
10  Walakini Esta hakudhihirisha kabila yake wala jamaa yake, kwa maana ndivyo alivyomwagiza Mordekai asiwadhihirishe.”

Kwahiyo baada ya ule muda wa utakaso kuisha ambao ulikuwa ni miezi 12 tu, Esta na wenzake waliingizwa mbele za mfalme kila mmoja akijionyesha ujuzi wake na uzuri wake, na utashi wake, kila mmoja kwa namna yake, pengine wengine walionyesha familia za kitajiri walizotokea, wengine tamaduni zao za kujua kucheza vizuri na urembo wao, wengine pamoja na uzuri wao juu ya hilo walionyesha elimu zao kubwa mbele ya mfalme, pengine wengine walionyesha kuwa wametoka kabila moja na mfalme, hivyo wangestahili, na mambo kadha wa kadha.

Lakini tukirudi kwa Esta yeye hakuonyesha chochote, isipokuwa vile tu alivyopewa na Hegai aende navyo mbele za mfalme. Na badala yake hakuonekana aliyekuwa mfano wa Esta mbele ya mfalme.

JE! BIBI-ARUSI WA KRISTO ANAPATIKANAJE?

Tunaposoma habari hii tunajifunza kwa Bwana Yesu jinsi alivyoanza kumtafuta BIBI-ARUSI wake bikira safi tangu vizazi vya kale hadi sasa, Kwahiyo mambo haya tafsiri yake kwa kanisa ni;

>Mfalme Ahasuero anamwakilisha BWANA YESU, 
>malkia VASHTI ambaye baadaye alikuja kutolewa katika Umalkia wake anawakilisha taifa la ISRAELI, 
>ESTA anamwakilisha BIBI-ARUSI wa kweli aliyekubaliwa na Kristo, 
> Wale mabikira wengine ; Wanawakilisha MADHEHEBU.
>Hegai na Mordekai wanawakilisha NENO LA MUNGU na Roho Mtakatifu.
Israeli kama taifa teule la Mungu, lilifananishwa na mke wa Mungu(Yeremia 3:14), na ndivyo lilivyokuwa kwa miaka yote, Lakini Mfalme wake (YESU KRISTO) alipokuja ili afanye nao karamu, walimkataa kwa kiburi na zaidi ya yote wakamzalilisha pale kalvari mbele ya dunia yote ni mfano tu wa Vashti alivyomwaibisha mfalme Ahasuero mbele ya dunia yote. Japo Bwana Yesu alikuja kwa upole kwa mke wake Israeli wao walimkataa na kumpinga, Na ndio maana tunaona Bwana Yesu aliwaambia Ee Yerusalemu, Yerusalem “Ni mara ngapi nimetaka kuwakusanya pamoja watoto wako, kama vile kuku avikusanyavyo pamoja vifaranga vyake chini ya mabawa yake, lakini hamkutaka!”

Mathayo 23:38 “Angalieni, nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.
39 Kwa maana nawaambia, Hamtaniona kamwe tangu sasa, hata mtakaposema, Amebarikiwa ajaye kwa jina la Bwana.”

Unaona hapo baada ya wayahudi kumkataa aliye mfalme wao na mume wao, walikuja kukatwa(Warumi 11) na kutolewa katika nafasi yao ya umalkia, na ndipo Mungu akaanza kutafuta malkia mwingine mahali pake, Ndipo NEEMA ikatugeukia sisi mataifa, akitafuta BIBI-ARUSI safi atakayekaa mahali pa Israeli.


Na kama vile tunavyoona walijihudhurisha mabinti wengi mbele za mfalme kutoka maeneo mbali mbali duniani kote. Hawa mabinti si wengine zaidi ya madhehebu mbalimbali na kila moja linajiona kuwa limestahili kuwa bibi-arusi wa BWANA YESU zaidi ya lenzake. Huoni leo hii Kanisa Katoliki linajiona kanisa pekee mama ambalo Mungu amelipokea?, walutheri nao vivyo hivyo, Waanglikana wanajiona wao ndio wapo sawa, wasabato nao vivyo hivyo wao ndio kanisa litakalokwenda kumlaki Bwana mawinguni, mashahidi wa Yehova nao vivyo hivyo, wapentekoste nao wanajiona kuwa wamestahili kuwa bibi-arusi wa KRISTO, na madhehebu mengine yote yanafanya ivyo hivyo..kumbuka leo hii duniani kuna madhehebu ya kikristo zaidi ya 40,000 na yote wanadai kuwa yapo sahihi zaidi ya mengine?. Lakini tujiulize je! Wote hawa watakuwa bibi-arusi wa Kristo??.
Jibu ni hapana bibi-arusi ni mmoja tu na ni ESTA basi. Yule tu atakayekidhi vigezo vya mfalme ndiye atakayekuwa malkia.


JE! ESTA NI MFANO WA DHEHEBU GANI SASA HIVI?

Tabia ya kwanza ya Esta aliyoonywa na Mordekai mjomba yake(aliye mfano wa Roho Mtakatifu) ni “KUTOKUFUNUA KABILA YAKE” mahali aendapo . Hiyo ni sifa iliyomfanya Esta apate kibali kwanza kwa HEGAI na kisha kwa Mfalme. Ukitaka kufahamu kwamba jambo la kujisifia, au kueleza chimbuko lako lilikuwa ni harufu mbaya mbele za mfalme, utaona kuwa japo Esta alikuwa ni malkia kwa muda mrefu mfalme alioishi naye hakuwahi hata siku moja kumuuliza Esta yeye ni kabila gani au jamaa zake ni nani?, au watu wake ni watu na namna gani!!, mpaka baadaye sana matatizo yalipotokea, hii ilionyesha kuwa mfalme alikuwa havutiwi na chimbuko la mtu unapokuja mbele zake, Yeye alimtaka Esta kama Esta tu katika unyenyekevu wake wote yeye kama alivyo, bila kujihesabia haki mbele zake. Na ndivyo Kristo anavyotaka watu wamwendee mbele zake.


Na jambo lingine lililomfanya Esta akubalike mbele za mfalme ni kumsikiliza HEGAI, ambaye ni Mfano wa mitume na manabii (yaani NENO LA MUNGU), Esta alipata ujuzi wa taratibu za kumwendea mfalme tofauti na wale mabinti wengine kwa kudumu katika maagizo ya HEGAI.

Na sasa hivi maana ya “KUFUNUA KABILA NI NINI?”. Pale unapomwendea Kristo na desturi za kimadhehebu; Ukatoliki, ulutheri, usabato, uanglikana, u-JW,n.k. pale unapoulizwa je! Wewe Ni MKRISTO? unasema mimi ni mlutheri, au mimi ni mbranhamite au mimi ni mpentekoste n.k...mpaka hapo hizo ni hatua za awali za wewe kutokidhi vigezo vya wewe kutokuwa bibi-arusi wa Kristo. Kwasababu pale utakapokwenda kukutana na HEGAI wako(yaani NENO LA MUNGU), na kuambiwa vitu visivyoendana na dhehebu lako.. utaishia kupinga na kujikuta unamfuata Bwana Yesu kwa desturi zako mwenyewe na sio desturi zilizopo katika NENO LAKE.

Hivyo ndugu ili uwe bibi-arusi aliyekubaliwa jambo la kwanza ondoa udhehebu ndani ya fikra zako, toka kwenye kamba za kidini na za kimadhehebu, halafu mfuate yeye kama ulivyo, unaona mafarisayo walimfuata Yesu na madhehebu yao wakaishia kukatwa, vivyo hivyo ukishilia dhehebu na kumfuata YESU utakatwa kama wao. Mgeukie HEGAI wako yaani INJILI YA MITUME NA MANABII.. BIBLIA TAKATIFU.. mfuate MFALME YESU KWA NJIA HIYO ndipo utakapomwona.


Biblia inasema Tokeni kwake enyi watu wangu..kumbuka udhehebu ni chapa ya mnyama, alama hii ukiikumbatia itakusabibishia usimuone Bwana siku ile ya unyakuo itakapofika..bibi-arusi wa kweli wa Kristo ni mnyenyekevu aliyekaa chini ya uongozi wa Roho Mtakatifu peke yake na kudumu katika kile NENO LINACHOSEMA na SIO KILE KANISA LINACHOSEMA.

Neno la Mungu linaposema “mwanamke avae mavazi ya kujisitiri(1Timotheo 2:9)” na wewe unasema haijalishi dhehebu letu halihimizi hivyo, ni sawa na kukataa maagizo ya Hegai na bado unataka uwe bibi-arusi hiyo haiwezekani..pia NENO linaposema “usijifanyie sanamu za kuchonga na kuziabudu (kutoka 20)” na wewe anaenda kuchukua sanamu ya mtakatifu Fulani na kuiabudu na kusema dhehebu letu linatufundisha hivyo..Na bado unasubiri siku ile uchaguliwe na Bwana uende mbinguni…Nataka nikuambie ndugu yangu siku ile utaikosa licha ya juhudi zako zote za kujionyesha kukubaliwa siku ile utalia na kuomboleza kama wale wanawali wapumbavu wa kwenye Mathayo 25 walivyokuwa. Kwasababu tu ya kuyadharau maagizo ya HEGAI (NENO LA MUNGU).

Hivyo maombi ni Bwana akupe kuliona hilo, na kuwa Bibi-arusi safi aliyestahili kwenda katika KARAMU YA MWANA-KONDOO. Mfuate Bwana kama ulivyo bila kuwa na utambulisho wowote unaokufuata hapo nyuma.

Mungu akubariki. Usikose mwendelezo huu wa Kitabu cha Esta sura zinazofuata.

Shalom.