"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Thursday, April 5, 2018

‘’MOTO HUFA KWA KUKOSA KUNI’’..NA NDIVYO ILIVYO KWA UASHERATI


Mungu kamuumba kila mwanadamu na maamuzi yake binafsi yasiyoweza kuingiliwa na kitu kingine chochote, Mungu kayaheshimu maamuzi hayo kiasi kwamba hata yeye mwenyewe hajajipa mamlaka ya kuyaingilia japokuwa anao uwezo huo, si zaidi shetani? hawezi kumwamulia mtu mambo!!. Ukiamua kuwa mlevi hakuna kitu chochote kitakachoweza kukuzuia, ukiamua kuwa mchawi hakuna yeyote atakayeweza kukuzuia..Vivyo hivyo ukiamua kuwa mtakatifu hakuna chochote kitakachoweza kukuzuia.

Jambo analolifanya Roho Mtakatifu ni kumshawishi au kumpa mtu kila sababu ya yeye kutokufanya maamuzi ya jambo fulani ovu, na mtu anapoamua kutii ndipo Roho anapozidi kuwa msaada mkubwa kwake katika kuenenda katika mwenendo mtakatifu.

Vivyo hivyo na shetani naye anachofanya sio kumlazimisha mtu kufanya maamuzi fulani bali anamshawishi kwa kumjengea mazingira yote ya yeye kuchukua uamuzi wa kufanya uovu, na mtu anapomtii ndipo shetani anapapata nafasi zaidi ya kummiliki na kumuharibu. Mwisho wa siku unasikia mtu ana pepo la usherati, halikumwingia hivi hivi ni yeye mwenyewe alifungua mlango mahali fulani na kuliruhusu.

Mtu anaamua kuwa mzinzi mara baada tu ya kuyatii mahubiri ya shetani katika akili yake. Fahamu tu biblia inasema 1Wakoritho 6: 18 “Ikimbieni zinaa. Kila dhambi aitendayo mwanadamu ni nje ya mwili wake; ila yeye afanyaye zinaa hutenda dhambi juu ya mwili wake mwenyewe.” Na pia inasema.. Mithali 6:32 “Mtu aziniye na mwanamke HANA AKILI KABISA; Afanya jambo litakalomwangamiza nafsi yake.” . Unaona hapo?? mwasherati wa aina yoyote ile yupo katika HATARI kubwa sana kuliko mtu mwingine yeyote.

Kwanini wengi leo wanashindwa na dhambi ya uasherati?

Ni Kwasababu ile ile, wanachukuliana na mahubiri ya shetani katika maisha yao. na kuyatii. Na Mahubiri hayo ni yapi?.

1)Kutazama Picha na Video za kizinzi (Pornography). Hii ni nyenzo kubwa sana shetani ameitumia kwa kizazi hiki kukiangamiza, Hii ni njia yenye ushawishi mkubwa kuliko zote, kiasi kwamba mtu akijiingiza huko uasherati hawezi akaukwepa kwa namna yoyote iwe ni ameshaingia kwenye ndoa au hajaingia, iwe ni kijana, au mzee haikwepeki, mtu huyo atabakia kuwa mwasherati au mzinzi daima. Na hapo shetani hajahusika kukufanya ukafanye uasherati hapana ni wewe mwenyewe kwa ufahamu wako kabisa na kwa miguu yako umeamua kuwa hivyo. Kama ingekuwa ni shetani kakuvaa ufanye hivyo, siku ile ya hukumu Mungu asingekuhukumu wewe angemuhukumu shetani.Lakini biblia inasema waasherati watahukumiwa… Na mtu anayetazama hivi vitu kama hatadondokea kwenye uasherati moja kwa moja basi ataishia kwenye masturbation ambayo nayo ni machukizo makubwa sana mbele za Mungu.

2) Njia ya pili ni ‘Mazungumzo mabaya’ ; Biblia inasema 1Wakoritho 15: 33 Msidanganyike; Mazungumzo mabaya huharibu tabia njema . " Haya ni mahubiri ambayo utakuta shetani anamuhubiria mtu pasipo hata yeye mwenyewe kujua, utakuta vijana au wazee kutwa kuchwa wanazungumza habari za wanawake, na wanawake vivyo hivyo utawakuta wana jadili habari za wanaume muda wote, lakini muda wa kutafakari mambo ya muhimu ya Mungu hakuna, sasa hapo watu kama hao ni rahisi sana kutawaliwa na roho za tamaa, kwasababu vichwa vyao wakati wote vimejazwa hayo mafundisho ya zinaa. Biblia inasema “hata uasherati usitamkwe kati yenu.”Utakuta kijana muda wote anaumalizia mtandaoni..ukitazama ni kitu gani anafanya, utagundua kuwa anachati katika magroup ambayo misingi yake ni uasherati, sasa kwa tabia hiyo haiwezekani wewe kuushinda uasherati hata uombeweje ni wewe tu kuamua kuacha hivyo vitu na kuanza kutii mahubiri ya Roho Mtakatifu ndani yako.

3) Mavazi: Vimini, suruali, kaptura, nguo zinazobana na zinazoonyesha vifua na migongo wazi kwa wanawake n.k., hivi vyote ni vichecheo vya uasherati, mavazi hayo yalibuniwa kwa kazi hizo, kuwavuta wazinzi wasogee karibu na wewe, hivyo mtu anayejiita mkristo na kuanza kuzivaa moja kwa moja anakaribisha uwepo wa uzinzi ndani yake.

4) Mziki na filamu za kidunia: Kusikiliza miziki ya kidunia hii pamoja na filamu za kimapenzi ni kichecheo kikubwa cha kubebwa na roho hizi, asilimia 99 ya miziki yote ya kidunia zina mahudhui ya kiasherati ndani yake unategemea vipi uepukane na tabia hizo?. Na ndio maana utakuta mtu analalamika hawezi kuacha kuwa mzinzi/mwasherati wakati muda wote anaumalizia kwenye vitabu, filamu na tamthilia za kimapenzi. Viache hivi vitu kwanza na ndipo utakapoanza kuona wepesi.

Na mambo hayo yakishakaa ndani yako sana, sasa yanakuwa yakijirudia rudia yenyewe tu kwenye akili yako, mpaka inakuwa ngumu kuyakwepa kwasababu ndio yaliyoujaza moyo wako,
Hivyo ndugu ukitaka kuushinda uasherati usitafute kuombewa, dawa ipo ndani yako mwenyewe kwanza ni kuchukua uamuzi wa kukataa kutii mahubiri yote ya shetani, na kuanza kumtii Roho Mtakatifu anapougua ndani ya moyo wako, ukifahamu kuwa mtu atendaye mambo hayo mwisho wake ni kuzimu… kwa kufanya hivyo utampa Roho Wa Mungu nafasi ya kukutengeneza up mpaka mwisho wa siku unajikuta ile tamaa imezikwa kabisa, na kuweza kuishi maisha pasipo kutamani uasherati kabisa..Hivyo kataa hayo mahubiri yote ya shetani anayokuletea kupitia mtandao,(Pornography) na picha za uchafu, kwa kupitia kuchat katika mambo yasiyofaa, kwa kupitia mazungumzo mabovu, na kampani zisizo za ki-Mungu, kwa kupitia filamu, vitabu, tamthilia na miziki ya kidunia pamoja na mavazi ya kikahaba, Anza kukaa mbali kwanza na hivyo vitu vyote, na ndipo utakapoanza kuitawala mapenzi yako.

Na pia mawazo machafu yanapokujia kichwani kwako ni kuyakataa kwa kutafakari NENO LA MUNGU badala yake, ukizingatia hayo kidogo kidogo Roho Mtakatifu anaanza kuyazika ndani yako, mpaka kufikia hatua ya kutoweka kabisa na kuwa na uwezo wa kujitawala. Kwasababu biblia inasema
(Mithali 26: 20a, “MOTO HUFA KWA KUKOSA KUNI”)….Hivyo uasherati pia hufa kwa kukosa vichochezi. Unapojitenga na vichocheo vyote hivyo hata ile tamaa ya kufanya uasherati inakuwa haipo. Roho Mtakatifu anaizika mpaka inafikia hatua watu watakushangaa unawezaje kuishi muda wote huo pasipo kuwa mwasherati?.

Lakini kama hutaki kuweka chini hivyo vitendea kazi vya uasherati kamwe hutaweza kumshinda shetani.Kwasababu biblia pia inasema WAASHERATI WOTE sehemu yao ni katika lile ziwa la Moto(Ufunuo 21:8)..Hivyo ndugu iogope hukumu ya Mungu, anza kubadilika sasa kimbia uasherati. Mwili wako ni Hekalu la Roho Mtakatifu, na mtu auharibuye Mungu kasema atamuharibu mtu huyo.

Ubarikiwe.

No comments:

Post a Comment