"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Thursday, May 17, 2018

KITABU CHA YUDA: SEHEMU YA 3

Jina la BWANA wetu na mwokozi wetu YESU KRISTO libarikiwe milele daima.
Karibu katika kujifunza maneno ya Mungu, leo tukiwa katika mwendelezo wa kitabu cha Yuda  tunapomalizia sehemu ile ya mwisho. Tunasoma.
Yuda 1: 14 "Na Henoko, mtu wa saba baada ya Adamu, alitoa maneno ya unabii juu ya hao, akisema, Angalia, Bwana alikuja na watakatifu wake, maelfu maelfu,
15 ili afanye hukumu juu ya watu wote, na kuwaadhibisha wote wasiomcha Mungu, kwa ajili ya kazi zao zote za upotevu walizozitenda bila kumcha Mungu, na kwa ajili ya maneno magumu yote ambayo hao wenye dhambi wasiomcha Mungu wameyanena juu yake.
16 Watu hawa ni wenye kunung'unika, wenye kulalamika, waendao kwa tamaa zao, na vinywa vyao vyanena maneno makuu mno ya kiburi, wakipendelea watu wenye cheo kwa ajili ya faida.
17 Bali ninyi, wapenzi, yakumbukeni maneno yaliyonenwa zamani na mitume wa Bwana wetu Yesu Kristo,
18 ya kwamba waliwaambia ya kuwa, Wakati wa mwisho watakuwako watu wenye kudhihaki, wakizifuata tamaa zao wenyewe za upotevu.
19 Watu hao ndio waletao matengano, watu wa dunia hii tu, wasio na Roho.
20 Bali ninyi, wapenzi, mkijijenga juu ya imani yenu iliyo takatifu sana, na kuomba katika Roho Mtakatifu,
21 jilindeni katika upendo wa Mungu, huku mkingojea rehema ya Bwana wetu Yesu Kristo, hata mpate uzima wa milele.
22 Wahurumieni wengine walio na shaka,
23 na wengine waokoeni kwa kuwanyakua katika moto; na wengine wahurumieni kwa hofu, mkilichukia hata vazi lililotiwa uchafu na mwili.
24 Yeye awezaye kuwalinda ninyi msijikwae, na kuwasimamisha mbele ya utukufu wake bila mawaa katika furaha kuu;
25 Yeye aliye Mungu pekee, Mwokozi wetu kwa Yesu Kristo Bwana wetu; utukufu una yeye, na ukuu, na uwezo, na nguvu, tangu milele, na sasa, na hata milele. Amina. "
Kama tulivyotangulia kusoma sehemu zilizopita tuliona watu wa aina TATU, mwovu aliowapandikiza katika kanisa la Mungu, waliofananishwa na nyota zipoteazo ambao weusi wa giza ndio akiba waliyowekewa milele, ambao wanafananishwa pia na miti ipukutishayo isiyo na matunda iliyokufa mara mbili, na visima visivyo na maji na miamba yenye hatari..wanafananishwa na magugu yaliyopandwa katikati ya ngano.
  Na maonyo haya kumbuka waliandikiwa watu ambao wapo katika safari ya Imani, wakafananishwa na wana wa Israeli walipokuwa safarini, Na kama tunavyosoma wengi wao hawakuweza kuishindania Imani yao na kuilinda Enzi yao wakaishia kuanguka kwa makosa mengi, ikapelekea kutokuiona ile nchi ya AHADI Mungu aliyowaahidia.
Na tuliona watu waliotumiwa na shetani kuwakosesha wana wa Israeli Jangwani, walikuwa ni KORA na BALAAMU. Hawa walikuwa ni manabii, Na ndio maana kitabu cha Yuda kimewataja watu 3, na mwingine alikuwa ni KAINI. Tukisoma mstari wa 11 unasema "Ole wao! Kwa sababu walikwenda katika njia ya Kaini, na kulifuata kosa la Balaamu pasipo kujizuia, kwa ajili ya ujira, nao wameangamia katika maasi ya Kora.
12 Watu hawa ni miamba yenye hatari katika karamu zenu za upendo walapo karamu pamoja nanyi, wakijilisha pasipo hofu; " .
Sasa huduma za watu hawa 3, ndizo zinazotenda kazi katika kanisa la Mungu leo, ili kuwapindua watu waliosimama katika Imani, na zinatenda kazi kwa udanganyifu wa hali ya juu kiasi kwamba ni ngumu kuzigundua. Katikati ya Huduma hizi ndipo kiti cha enzi cha shetani kilipo,(Ufunuo 2:13-14).
Wana wa Israeli walipokuwa kule jangwani wapo waliotii mafundisho ya Kora, ndio walioangamizwa naye, wapo pia waliousikiliza udanganyifu wa Balaamu nao pia wakaangamizwa, kadhalika katika kanisa wapo watakaopotea kwa kudanganywa na kwa kuyafuata mafundisho yatokayo kwa wachungaji wa uongo, mitume wa uongo, waalimu na manabii wa uongo, Huu ni wakati wa kuwa makini sana. Na utajuaje! kuwa hawa ni watumishi wa uongo? ni pale wanapoenda mbali na Neno, mfano wa Kora na Balaamu.

Biblia inasema katika ule mstari wa 18 ".......Wakati wa mwisho watakuwako watu wenye kudhihaki, wakizifuata tamaa zao wenyewe za upotevu".
Jambo lingine  linalo tutambulisha kuwa tunaishi siku za mwisho, ni kutokea kwa watu wenye kudhihaki, na hawa hawatoki mbali! bali ni ndani ya kundi linalojiita kundi lililopo safarini, kumbuka waliomdhihaki Mungu ni Kora na wenzake baada ya kuona kuwa safari imekuwa ndefu, yenye shida, ambayo ingepasa ichukue wiki kadhaa tu kumaliza lakini imechukua miaka 40, wakaanza kudhihaki na kusema hiyo nchi tuliyoahidiwa mbona hatufiki hata sisi tunaweza tukajiongoza wenyewe??. Mfano huo huo wa baadhi ya watu wanaojiita wakristo, utasikia wanasema "Unakuja umekuwa YESU?"..."Yesu mbona haji?".n.k. na cha kusikitisha huyu ni mtu anayejiita mkristo ndio anafanya hivyo, hawaogopi hata kulitamka hilo jina lililo kuu, katika mambo yao ya kipumbavu. Moja kwa moja utafahamu watu  kama hao wameshaanguka katika maasi ya Kora, na wala hawapo katika Imani japo wanajiita wakristo.
Mtume Petro pia alisema.

2Petro 3:
"1 Wapenzi, waraka huu ndio wa pili niwaandikiao ninyi; katika zote mbili naziamsha nia zenu safi kwa kuwakumbusha,
2 mpate kuyakumbuka yale maneno yaliyonenwa zamani na manabii watakatifu, na ile amri ya Bwana na Mwokozi iliyoletwa na mitume wenu.
3 Mkijua kwanza neno hili ya kwamba katika siku za mwisho watakuja na dhihaka zao watu wenye kudhihaki, wafuatao tamaa zao wenyewe,
4 na kusema, Iko wapi ahadi ile ya kuja kwake? Kwa maana, tangu hapo babu zetu walipolala, vitu vyote vinakaa hali iyo hiyo, tangu mwanzo wa kuumbwa.
5 Maana hufumba macho yao wasione neno hili ya kuwa zilikuwako mbingu tangu zamani, na nchi pia, imefanyizwa kutoka katika maji, na ndani ya maji, kwa neno la Mungu;
6 kwa hayo dunia ile ya wakati ule iligharikishwa na maji, ikaangamia.
7 Lakini mbingu za sasa na nchi zimewekwa akiba kwa moto, kwa neno lilo hilo, zikilindwa hata siku ya hukumu, na ya kuangamia kwao wanadamu wasiomcha Mungu.
8 Lakini, wapenzi, msilisahau neno hili, kwamba kwa Bwana siku moja ni kama miaka elfu, na miaka elfu ni kama siku moja.
9 Bwana hakawii kuitimiza ahadi yake, kama wengine wanavyokudhani kukawia, bali huvumilia kwenu, maana hapendi mtu ye yote apotee, bali wote wafikilie toba.
10 Lakini siku ya Bwana itakuja kama mwivi; katika siku hiyo mbingu zitatoweka kwa mshindo mkuu, na viumbe vya asili vitaunguzwa, na kufumuliwa, na nchi na kazi zilizomo ndani yake zitateketea.
11 Basi, kwa kuwa vitu hivi vyote vitafumuliwa hivyo, imewapasa ninyi kuwa watu wa tabia gani katika mwenendo mtakatifu na utauwa,
12 mkitazamia hata ije siku ile ya Mungu, na kuihimiza; ambayo katika hiyo mbingu zitafumuliwa zikiungua, na viumbe vya asili vitateketea na kuyeyuka?
13 Lakini, kama ilivyo ahadi yake, mnatazamia mbingu mpya na nchi mpya, ambayo haki yakaa ndani yake.
14 Kwa hiyo, wapenzi, kwa kuwa mnatazamia mambo hayo, fanyeni bidii ili mwonekane katika amani kuwa hamna mawaa wala aibu mbele yake.
15 Nanyi uhesabuni uvumilivu wa Bwana wetu kuwa ni wokovu, kama vile na ndugu yetu mpenzi Paulo alivyowaandikia kwa hekima aliyopewa;"
Unaona hapo?. Uvumilivu wake Mungu ni kutuvuta sisi tutubu dhambi zetu, Lakini siku ya BWANA inakuja, inayotisha sana, kuwatekeza watu wote waasi, walioacha enzi yao. Wakati huo Bwana atakuja na watakatifu wake maelfu elfu, hao watakuwa ni wale waliokwisha nyakuliwa kabla, ndio watakaorudi na Bwana kuuhukumu ulimwengu wote, Kama HENOKO yule mtu wa 7 aliyenyakuliwa alivyoonyeshwa.(Ufunuo 19:11-20)

Yuda 1:14 "Na Henoko, mtu wa saba baada ya Adamu, alitoa maneno ya unabii juu ya hao, akisema, Angalia, Bwana alikuja na watakatifu wake, maelfu maelfu,
15 ili afanye hukumu juu ya watu wote, na kuwaadhibisha wote wasiomcha Mungu, kwa ajili ya kazi zao zote za upotevu walizozitenda bila kumcha Mungu, na kwa ajili ya maneno magumu yote ambayo hao wenye dhambi wasiomcha Mungu wameyanena juu yake."
Ndugu huu ni wakati wa kufanya wito wako, na uteule wako imara(2Petro 1:10), angali upo safarini, Sio wakati wa kutanga tanga huku na kule, kila wimbi la mafundisho unapokea..Unaweza ukaona mafundisho fulani ni mazuri yanavutia na kukupa faraja, lakini hujui kidogo kidogo yanakutoa katika njia ya IMANI,..Hapo mwanzoni ulikuwa unasali, ulikuwa unafunga, ulikuwa unawasaidia watu, ulikuwa mnyenyekevu,ulikuwa na huruma, ulikuwa unaogopa hata kuvaa mavazi ya aibu na kutembea nayo barabarani, ulikuwa ukisikia Neno la Mungu tu, unatetemeka lakini baada ya kufika sehemu fulani! na kusikia mahubiri fulani tu! kutoka kwa watumishi fulani, kuanzia hapo  hayo  mambo yote yakafa kabisa,Yesu kwako amekuwa kama kitu cha ziada, hana sehemu kubwa katika maisha yako kama zamani, hata ule uwepo wa ki-Mungu uliokuwa unausikia kwanza umetoweka, hamu ya kutamani mambo ya mbinguni imekufa. fahamu tu hapo umeiacha imani waliyokabidhiwa watakatifu mara moja tu! geuka haraka. kwasababu hapo ulipo ndipo penye kiti cha enzi cha shetani alipo Balaamu na Kora. Hivyo ondoka haraka sana, Rudi katika imani,..Ishindanie hiyo kwasababu shetani ndiyo anayoiwinda.
Tafuta uhusiano wako binafsi na Mungu, kwa kudumu katika maonyo ya biblia, Na BWANA ni mwaminifu safari aliyeianzisha mioyoni mwetu ataitimiliza..kama alivyosema.
Yuda 1: 24 Yeye awezaye kuwalinda ninyi msijikwae, na kuwasimamisha mbele ya utukufu wake bila mawaa katika furaha kuu;
25 Yeye aliye MUNGU PEKEE, MWOKOZI WETU, KWA YESU KRISTO BWANA WETU; UTUKUFU UNA YEYE, NA UKUU, NA UWEZO, NA NGUVU,TANGU MILELE, NA SASA, NA HATA MILELE. AMINA.
Mungu akubariki sana.
Unaweza pia uka-Share kwa wengine, ili nao pia wanufaike, na Mungu atakubariki.

No comments:

Post a Comment