"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Friday, May 25, 2018

MASWALI NA MAJIBU: SEHEMU YA 22


SWALI: Ubarikiwe mtumishi ila naomba unifafanulie maana ya huu mstari 1Timotheo 2:12 “Simpi mwanamke ruhusa ya kufundisha, wala kumtawala mwanamume, bali awe katika utulivu.”. Na pia Biblia inamaana gani iliposema  katika zaburi 68:11 “Wanawake watangazao habari ni jeshi kubwa;”?


JIBU: Ubarikiwe dada yangu... jambo la kwanza ni vizuri tufahamu kuwa Mungu hana upendeleo katika utendaji kazi wake, na watu wote kwake ni sawa. Lakini Mungu wetu ni wa utaratibu, na huo utaratibu kauweka katikati ya viumbe vyake vyote, je! si zaidi sana katika kanisa lake TAKATIFU?.. Embu wazia hili;

 Mfano Raisi anatoa agizo leo kwamba kila mwananchi popote alipo anatakiwa kuilinda nchi yake kwa gharama yoyote ile.. Sasa Swali ni je! Watu wote watoke waende kuwa makomandoo porini kuilinda mipaka na kushika mitutu? kwasababu tu wao ndio wana jukumu la juu zaidi la kulilinda taifa?. Jibu ni hapana..ni dhahiri kuwa wengine watakuwa wanajeshi, wengine maaskari, wengine wapelelezi, wengine usalama, wengine watoa taarifa mbaya (wananchi wa kawaida) n.k. lakini hawa wote kwa pamoja tunaona wanafanya kazi ya ulinzi wa taifa isipokuwa ni katika vitengo tofauti tofauti, na pia kuna vitengo ambavyo vitawahusu wanaume tu kwa mfano ukomandoo na vitengo vingine vitawahusu wanawake tu na vingine vitawahusu wote kwa pamoja, hivyo mgawanyo wa majukumu ni ili kazi ya ulinzi wa taifa iende kwa ufasaha zaidi, hilo tu. 

Kadhilika na katika Kazi ya Mungu pia..Bwana aliposema Enendeni ulimwenguni kote mkahubiri injili kwa kila kiumbe....hakumaanisha kwamba watu wote tukawe mitume au waalimu...Hapana sio wote wenye hicho kipawa cha kwenda kuzunguka huku na huko kuhubiri, wengine watakuwa manabii, wengine wainjilisti, wengine mashemasi, wengine watakuwa na karama za kukirimu, uponyaji, miujiza n.k. Lakini wote kwa pamoja wanafanya kazi ya kuhubiri habari njema za ufalme. Kadhalika Mungu alitenga pia kazi za wanawake na za wanaume. Na nyingine zinafanywa na jinsia zote. 

Dada zangu biblia inaposema "wanawake watangazao habari ni jeshi kubwa", hakumaanisha moja kwa moja wanawake wote wakawe mitume au waalimu wa biblia...Unapaswa ufahamu unatakiwa utangaze habari kwa njia gani na kwa nafasi  ipi uliyowekewa, vinginevyo utakosa shabaha, na kuona kama biblia inajichanganya!!!...Maagizo yaliwekwa katika kanisa..Kwamba wanaume ndio wasalishe kila mahali...wala wanawake hawana ruhusa ya kufundisha kanisani (mahali penye mkusanyiko wa wanaume na wanawake)...Na sababu zilishawekwa pale unaweza ukazisoma mwenyewe(1 Timotheo 2:12) ndio maana hukuna mtume yoyote wa Bwana Yesu aliyekuwa mwanamke, sio kwamba wanawake wa kipindi kile walikuwa ni wadhaifu sana walau aonekane hata mmoja!..Hapana. Hivyo ni vitengo vilivyowekwa na Bwana kwa wanaume tu.

Lakini mwanamke hakatazwi kuhubiri injili mbele ya wanawake wenzake, lakini sio mbele ya kanisa. Anaweza akawafundisha watoto, na kufanya kazi nyingine za kanisani, kama maombezi, karama za uponyaji, karama za kinabii, karama za kutafsiri lugha, n.k. pia kusambaza kazi za Mungu kwa njia mbalimbali. kama vipeperushi, cd, makala, biblia n.k. lakini sio kusimama moja kwa moja na kuhubiri kanisani au kuwa mwalimu au mtume au mchungaji hizo ni kazi za wanaume kulingana na maandiko...Hivyo mwanamke akizingatia hayo atakuwa amehubiri injili moja tu na wale wengine tena na kama akiwa mwaminifu thawabu yake itakuwa kubwa kuliko hata wanaume wanaohubiria maelfu katika madhabahu...

Mtume Paulo alifunuliwa jambo hilo na Bwana mwenyewe, sio kwa akili zake, na wala haikuwahusu wakorintho peke yao  bali watu wote wa vizazi vyote, Alisisitiza  kwamba hayo ni maagizo ya Bwana, akaonya pia “lakini mtu akitaka kuwa mjinga na awe mjinga 1wakorintho 14:34-40”
Mbarikiwe sana.


SWALI 2: Napatikana Morogoro Tanzania, swali langu, je!, kanisa ni nini? Na linapatikana kwenye maandiko?


JIBU: Ndio linapatikana kwenye maandiko, Maana halisi ya neno KANISA sio jengo...bali maana ya kanisa ni "WALIOITWA". Hivyo kanisa ni mkusanyiko wa watu walioitwa.
Lakini Swali ni je! Wameitwa kutoka wapi?..jibu: wameitwa kutoka katika vifungo vya dhambi, na kamba za yule mwovu, na kuingizwa katika neema ipatikanayo kwa  damu ya BWANA YESU KRISTO katika ulimwengu wa Roho. Mfano wana wa Israeli walipoitwa kutoka Misri waliitwa Kanisa.

 kwahiyo watu wote Bwana Yesu aliowaita na kuwafanya kuwa wake HAO NDIO  KANISA la Mungu, na aliongezea kuwapa vipawa kila mmoja (yaani karama za rohoni) kwa jinsi alivyopenda yeye..wengine aliwafanya kuwa MITUME,wengine MANABII wengine WAINJILISTI wengine WAALIMU, WACHUNGAJI n.k kwa pamoja wanashirikiana kuunda familia moja ya Roho (familia hii kwa lugha nyingine inaitwa mwili wa Kristo)...ukisoma efeso 4 utaona jambo hilo


Mlango 4 1 Kwa hiyo nawasihi, mimi niliye mfungwa katika Bwana, mwenende kama inavyoustahili WITO WENU MLIOITWA; 2 kwa unyenyekevu wote na upole, kwa uvumilivu, mkichukuliana katika upendo; 3 na kujitahidi kuuhifadhi umoja wa Roho katika kifungo cha amani. 4 MWILI MMOJA, na Roho mmoja, kama na mlivyoitwa katika tumaini moja la wito wenu. 5 Bwana mmoja, imani moja, ubatizo mmoja. 6 Mungu mmoja, naye ni Baba wa wote, aliye juu ya yote na katika yote na ndani ya yote. 7 Lakini kila mmoja wetu alipewa neema kwa kadiri ya kipimo cha kipawa chake Kristo. 8 Hivyo husema, Alipopaa juu aliteka mateka, AKAWAPA WANADAMU VIPAWA. 9 Basi neno hilo, Alipaa, maana yake nini kama siyo kusema kwamba yeye naye alishuka mpaka pande zilizo chini za nchi? 10 Naye aliyeshuka ndiye yeye aliyepaa juu sana kupita mbingu zote, ili avijaze vitu vyote. 11 Naye alitoa wengine kuwa mitume, na wengine kuwa MANABII; na wengine kuwa WAINJILISTI na wengine kuwa WACHUNGAJI na WAALIMU; 12 kwa kusudi la kuwakamilisha watakatifu, hata kazi ya huduma itendeke, hata mwili wa Kristo ujengwe; 13 hata na sisi sote tutakapoufikia umoja wa imani na kumfahamu sana Mwana wa Mungu, hata kuwa mtu mkamilifu, hata kufika kwenye cheo cha kimo cha utimilifu wa Kristo; 14 ili tusiwe tena watoto wachanga, tukitupwa huku na huku, na kuchukuliwa na kila upepo wa elimu, kwa hila ya watu, kwa ujanja, tukizifuata njia za udanganyifu. 15 Lakini tuishike kweli katika upendo na kukua hata tumfikie yeye katika yote, yeye aliye kichwa, Kristo. 16 Katika yeye mwili wote ukiungamanishwa na kushikanishwa kwa msaada wa kila kiungo, kwa kadiri ya utendaji wa kila sehemu moja moja, huukuza mwili upate kujijenga wenyewe katika upendo".


SWALI 3: Kule kwenye utawala wa miaka 1,000 wakati BWANA WETU YESU KRISTO akiwa MFALME wa Wafalme tutamuona kwa macho?Ama uwepo wake tu watosha kumtambulisha?.Kama sasa hatumuoni kwa macho lakini niBWANA&MFALME wetu.ndugu itakuwaje wakati huo wa huo utawala?



JIBU: Siku ile BWANA YESU atakapokuja na watakatifu wake, atakuwa dhahiri kabisa tutamwona uso kwa uso....na atatawala kama Mfalme wa dunia nzima, tutamshika tutaongea naye, tutamuuliza na maswali yote ambayo kwasasa hatuna nayo majibu..atayajibu yote...na tutambusu na kumkumbatia pia Bwana wetu kama nafasi  ikipatikana....Kiufupi sisi na yeye tutakuwa kama mtu na kaka yake isipokuwa ni Mungu wetu..


1Yohana 3: 2 “Wapenzi, sasa tu wana wa Mungu, wala haijadhihirika bado tutakavyokuwa; lakini twajua ya kuwa atakapodhihirishwa, tutafanana naye; kwa maana tutamwona kama alivyo. 3 Na kila mwenye matumaini haya katika yeye hujitakasa, kama yeye alivyo mtakatifu”.
 Ubarikiwe.
Ukiwa na maswali yahusuyo biblia na utapenda kupewa ufafanuzi. Tutumie kwa kupitia hii Email: watakatifuwasikuzamwisho@gmail.com.  Au uliandike kwenye sehemu ya ::"comment"..na utajibiwa ndani ya muda mfupi.

No comments:

Post a Comment