"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Thursday, July 19, 2018

MASWALI NA MAJIBU: SEHEMU YA 34


 SWALI 1; katika 1Yohana 5:6-9, (a) ningependa kujua kivipi Yesu alikuja kwa maji na damu?

(b)mashahidi watatu washuhudiao mbinguni wanatajwa, Neno ambaye ndiye Yesu bado ana nafasi ya mwana hata baada ya kutoka duniani?
(c)mashahidi wa duniani (roho,maji na damu) wanaotajwa ni kwa namna gani wanashuhudia? BARIKIWA SANA !

JIBU: A. Kwanza ni muhimu kufahamu wakati, Bwana Yesu alipokuwa pale Kalvari, baada ya kuchomwa mkuki ubavuni na yule Askari wa Kirumi, kulitoka MAJI NA DAMU, ikiashiria kuwa ndambi zetu, zinaoshwa kwa damu na kwa njia ya maji. Ikiwa na maana kuwa mtu ili apate ondoleo la dhambi zake ni lazima akabatizwe kwanza kwa kuzamishwa katika MAJI mengi kama ishara, na ndipo dhambi zake ziweze kusafishika kwa DAMU ya Yesu Kristo. Na ndio maana Bwana alisema aaminiye na kubatizwa ataokoka…

B.Na aliposema wapo watatu washuhudiao mbinguni na wapo watatu washuhudiao duniani, haikumaanisha kuwa kuna nafsi tatu za watu duniani na kuna nafsi tatu nyingine mbinguni. Hapana haimaanishi hivyo kwasababu maji yatashuhudiaje? Hayawezi kuongea wala kuhubiri injili, hivyo anaposema wapo watatu duniani yaani maji, damu na Roho anamaanisha zipo hatua tatu “mwanadamu kuzifuata ili kukamilika duniani” yaani mtu anapaswa aoshwe dhambi zake kwa kubatizwa katika MAJI, ili apate ondoleo la dhambi zake kwa DAMU ya Yesu na kupokea kipawa cha Roho Mtakatifu ambaye ndiye muhuri wa Mungu.Hatua hizi tatu ndizo zinazoshuhudia kwamba mwanadamu akizifuata hizo amekombolewa na kukamilishwa.

Matendo 2:38 “Petro akawaambia, Tubuni MKABATIZWE kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo, mpate ondoleo la dhambi zenu, nanyi mtapokea kipawa cha Roho Mtakatifu.”

C.Na aliposema wapo watatu mbinguni hakumaanisha tena kuna nafsi tatu mbinguni kila moja inajitegemea, hapana! Biblia ilimaanisha kuwa zipo hatua tatu mbinguni MUNGU MMOJA alizozitumia “kumkamilisha mwanadamu”, hatua ya kwanza alizungumza na wanadamu kama Baba(yaani MUNGU JUU YETU), hatua ya Pili alizungumza nasi kama NENO(MUNGU PAMOJA NASI,EMANUELI,) waebr 1:1-2 “Mungu, ambaye alisema zamani na baba zetu katika manabii kwa sehemu nyingi na kwa njia nyingi, mwisho wa siku hizi amesema na sisi katika MWANA, aliyemweka kuwa mrithi wa yote, tena kwa yeye aliufanya ulimwengu.” Hatua ya tatu kazungumza nasi kama ROHO MTAKATIFU(MUNGU NDANI YETU), katika Roho Mtakatifu ndio utimilifu wa Mungu kuzungumza katika ukaribu zaidi, yeye ndiye atufundishaye mioyoni mwetu na kututia katika kweli yote,

Yeremia 31: 1 Angalia, siku zinakuja, asema Bwana, nitakapofanya agano jipya na nyumba ya Israeli, na nyumba ya Yuda. 32 Si kwa mfano wa agano lile nililolifanya na baba zao, katika siku ile nilipowashika mkono, ili kuwatoa katika nchi ya Misri; ambalo agano langu hilo walilivunja, ingawa nalikuwa mume kwao, asema Bwana. 33 Bali agano hili ndilo nitakalofanya na nyumba ya Israeli, baada ya siku zile, asema Bwana; NITATIA SHERIA YANGU NDANI YAO, NA KATIKA MIOYO YAO; nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu. 34 WALA HAWATAMFUNDISHA KILA MTU JIRANI YAKE, NA KILA MTU NDUGU YAKE, WAKISEMA, MJUE BWANA; KWA MAANA WATANIJUA WOTE, tangu mtu aliye mdogo miongoni mwao hata aliye mkubwa miongoni mwao, asema Bwana; maana nitausamehe uovu wao, wala dhambi yao sitaikumbuka tena”.

Kwahiyo kwa hatua hizi tatu Mungu amezitumia kumkamilisha mwanadamu mbele zake….Tofauti na zile za kwanza(maji,damu, na Roho) ambazo ni mwanadamu anapaswa azifuate kukamilika mbele za Mungu, lakini hizi za mwisho(Baba, Neno na Roho) ni Mungu anazitumia kumkamilisha mwanadamu mbele zake.


SWALI 2: nitajuaje kama ndoto ni ya Mungu au ya shetani?

JIBU: Maarifa yanayohusiana na ndoto ni mapana kidogo, lakini kwa ufupi, zipo ndoto za aina tatu,

1) ndoto zinazotokana na shughuli (Mhubiri 5:3): hizi ndio mara nyingi zinamjia mtu, kwamfano mtu alikuwa anafanya shughuli fulani siku nzima na usiku anapolala bado anaota anaifanya ile shughuli au anaota mambo yanayoendana na jambo ambalo amekuwa akijishughulisha nalo mara kwa mara. Sasa Kutokana na shughuli ile kuchukua sehemu kubwa ya siku yake au maisha yake, inapelekea pia kuchukua nafasi kubwa katika ulimwengu wa ndoto zake. Ndoto hizi ni mwili ndio unaozitengeneza, hazitokani na Mungu wala shetani.

2) Ndoto zinazotokana na yule mwovu. Hizi zinatengenezwa na yule mwovu na kutumwa ndani ya mtu, Hizi ni ndoto zote zenye maudhui ya kumfanya mtu aikane au aiache IMANI, au zinampelekea mtu aende mbali na mpango wa Mungu, na huwa zinaambatana na ushawishi fulani mkubwa sana mara baada ya kuamka.

kwamfano mtu anaota kaachana na mume/mke wake na kupata mke/mume mwingine ambaye ni mzuri kuliko yule aliyekuwa naye, na anapoamka asubuhi anajikuta anaanza kuona kero ya kuishi na mke wake au mume wake kama ilivyokuwa hapo mwanzo. Au anashawishika kuamua kumwacha mumewe au mkewe.

Au mtu anaota mzazi wake mmoja ni mchawi na hamtakii mema, na ile ndoto inamtaka ajitenge na huyo mzazi, au amchukie awe naye mbali. Au mwingine anaota anafanya uzinzi/uasherati na mtu asiyemjua au anayemfahamu, na anajikuta akiamka asubuhi ile roho ya tamaa bado inakuwa ndani yake kwa nguvu zaidi, tofauti na alivyokuwa jana.

Au mtu anaota kapata utajiri kwa kumwibia mwajiri wake, au kwa kucheza kamari , na baada ya kuamka anajisikia msukumo ndani yake wa kwenda kufanya jambo lile na wakati mwingine mazingira aliyoyaona kwenye ndoto ndio hayo hayo anayaona akiwa nje ya ndoto kana kwamba ni unabii unatimia..

Au wakati mwingine mtu anaota ndoto ameenda kwa mganga, akafanikiwa na anapoamka anashawishika kufanya mambo yale, au mtu anajikuta anaota kuna sanamu mahali fulani au kuna mti mahali fulani umebeba mafanikio yake (pengine uani kwake) na kwenye ndoto anaona ameukata ule mti na mambo yote yakaharibika, na anapoamka anajikuta anaogopa kuukata ule mti akijua ndio mafanikio yake yapo pale.

Au wakati mwingine mtu anaota, ametenda dhambi na amejaribu kumwomba Mungu, na Mungu hataki kumsamehe, na anapoamka asubuhi anashawishika kuamini kuwa Mungu hataki kumsamehe na anamchukia.

Au ndoto nyingine mtu anaota amekufa baada ya kujaribu kuwa mkristo au kumpa Kristo maisha yake. N,k…Sasa ndoto zote kama hizi zinatoka kwa yule mwovu kwasababu zina maudhui ya kumlazimisha mtu asilitii Neno la Mungu au aende kinyume na maagizo ya Mungu, zinampeleka mtu katika kutenda dhambi zaidi kuliko kumfanya kuwa mtakatifu, nyingine zinamfanya mtu awe mwoga zaidi na kumchukia Mungu kuliko kumpenda! N.k

Namna ya kuzidhibiti hizi ndoto ni kuamua kuishi maisha masafi yampendezayo Mungu na kujifunza kwa kina Neno la Mungu ili shetani anapoleta mawimbi yake kama bahari uwe na uwezo wa kuyadhibiti, Kadhalika na kudumu katika maombi. kwamfano mtu anayeoota kafanya kosa na hasamehewi, hiyo ni mishale ya shetani kutaka kukuvunja moyo usitake kuendelea kumtafuta Mungu, kwahiyo kama Neno halipo ndani yako linalosema “1Yohana 1: 9 “Tukiziungama dhambi zetu, Yeye ni mwaminifu na wa haki hata atuondolee dhambi zetu, na kutusafisha na udhalimu wote. ” hutaweza kumshinda shetani.

Au ndoto inapokuja umegombana na mke wako na umeachana naye na kupata mwingine bora kuliko huyo, utajua imetoka kwa yule mwovu kwasababu Neno la Mungu limekaa ndani yako linalosema “Luka 16:18 18 Kila amwachaye mkewe na kumwoa mke mwingine azini; naye amwoaye yeye aliyeachwa na mumewe azini. ” Hivyo unajua ni ndoto iliyotoka kwa yule mwovu kukutaka wewe kutoka nje ya kusudi la Mungu na kutenda dhambi.

Au unapoota umebeti na umekuwa tajiri ghafla, utajua kabisa ni ndoto kutoka kwa yule mwovu kwasababu Neno la Mungu limekaa ndani yako linalosema “11 Mali iliyopatikana kwa haraka itapunguka; Bali yeye achumaye kidogo kidogo atazidishiwa. (Mithali 13:11)” Kwahiyo utajua ni yule mwovu anataka kukupeleka kwenye kazi iliyolaaniwa.

Kadhalika na ndoto nyingine zote zinazofanana na hizo utazipima kwa Neno la Mungu tu! na utaweza kuzishinda na kuzifahamu kama Neno la Mungu linakaa ndani yako. Na pia kusali kabla ya kulala ni muhimu sana..Hiyo itasaidia kufunga mipenyo yote ya yule mwovu anayoweza kuitumia kukujaribu katika ndoto.

3)Aina ya tatu ya ndoto ni ndoto zinazotoka kwa Mungu. Hizi ni zile zinazomjia mtu kutoka kwa Mungu kwa maudhui ya kumwonya mtu au kumuimarisha katika imani, na hizi haziwi kwa wingi kama zile zinazotokana na shughuli nyingi.
Mfano wa ndoto hizi ni pale mtu anapoota kakutana na mtu/muhubiri kamshuhudia na kumwonya juu ya maisha yake maovu na anapoamka asubuhi anajikuta anahukumiwa na maisha ya dhambi anayoishi na kushawishika kutubu.
Na mfano mwingine wa hizi ndoto ni pale mtu anaota unyakuo umepita na kaachwa, na anapoamka asubuhi anashawishika kujikagua maisha yake, nyingine mtu anaota kafa na kaenda kuzimu na anapoamka asubuhi anagundua ilikuwa ni ndoto tu.

Nyingine ni zile mtu anaota kafanyiwa jambo baya sana la kumuumiza, na anapaamka asubuhi anajikuta yeye ndiye kamtendea mtu hilo jambo, hivyo anashawishika kujirekebisha na kutubu,

Nyingine unakuta mtu anaota kabeti, au kaenda kwa waganga, au kufanya uasherati, au kaiba, au kamtukana mtu, au kachukua mke au mume wa mtu, au kamsengenya mtu, au kaua na baada ya kufanya hivyo mambo yake yote yakaharibika, akajikuta kafilisika, au kafungwa, au kahukumiwa kufa, na anapoamka asubuhi anashawishika kutokufanya moja wapo ya mambo hayo ili yasimpate hayo mabaya. Hizo ni ndoto kutoka kwa Mungu, zinalenga kumuonya mtu

Na nyingine unakuta mtu anaota yupo shuleni anasoma, na kumbe alishamaliza muda mrefu sana, na anajiona anapambana kusoma na bado anafeli, ndoto ya namna hii unajua kabisa ni kutoka kwa Mungu kwasababu inayokuonyesha aina ya maisha unayoishi kwamba mwendo wako ni wa taratibu katika kumtafuta Mungu na bado upo nyuma ya wakati.

Kwahiyo kwa ufupi ndoto zote zinazotokana na Mungu utazijua pia kama Neno la Mungu linalo kaa ndani yako, ndoto yoyote inayokupeleka kumtafuta Mungu zaidi, kutubu, au kukuonya tabia uliyonayo ambayo sio nzuri unajua kabisa ndoto hiyo inatoka kwa Mungu. Lakini kama umeota na ukaona baada ya kuamka inakufanya utende dhambi, au uichukie imani au ujitenge na kweli basi hiyo utajua moja kwa moja ni ya shetani.

Ayubu 33:14

"Kwa kuwa Mungu hunena mara moja, Naam, hata mara ya pili, ajapokuwa mtu hajali.
15 Katika ndoto, katika maono ya usiku, Usingizi mzito uwajiliapo watu, Katika usingizi kitandani;
16 Ndipo huyafunua masikio ya watu, Na kuyatia muhuri mafundisho yao,
17 Ili amwondoe mtu katika makusudio yake, Na kumfichia mtu kiburi;
18 Yeye huizuia nafsi yake isiende shimoni, Na uhai wake usiangamie kwa upanga.
19 Yeye hutiwa adabu kwa maumivu kitandani mwake, Na kwa mashindano yaendeleayo daima mifupani mwake;


 SWALI 3: Tunasoma baada ya Majusi kushika njia mpaka kwa Mfalme(Yesu) walianguka 1.WAKAMSUJUDIA--nao walipokwisha kufungua 2.HAZINA--zao wakamtolea3.TUNU--;4.DHAHABU-- 5.UVUMBA--na 6.MANEMANE. Naomba kufahamu hivyo vitu ambavyo hao mamajusi walimfanyia na kumtolea mfalme Yesu viliashiria ndugu zangu?.

JIBU: Mathayo 2: 10 Nao walipoiona ile nyota, walifurahi furaha kubwa mno.
11 Wakaingia nyumbani, wakamwona mtoto pamoja na Mariamu mamaye, wakaanguka wakamsujudia; nao walipokwisha kufungua hazina zao, wakamtolea tunu; DHAHABU na UVUMBA, na MANEMANE.

Ukisoma hapo utaona zile zawadi wale mamajusi walizozipeleka ni tatu tu na sio nne au tano. hazina ndio hizo tunu zenyewe, na tunu ndio zile tatu yaani (dhahabu, uvumba na manemane)…..

Sasa hizi zawadi tatu kila moja ilikuwa na maana yake kubwa, Tukianza na dhahabu, wale mamajusi walifahamu kuwa aliyezaliwa ni mfalme na anastahili heshima ya kifalme na kitu chenye thamani kubwa kuliko vyote ambacho angestahili kupewa mfalme ni dhahabu, kwasababu dhahabu inaweza kubadilishwa na kuwa hata fedha na kutumiwa kwa matumizi mengine yeyote..kwahiyo hii zawadi ya dhahabu ilikuwa ni zawadi yenye manufaa kimaisha, tofauti na hizo zawadi mbili nyingine zilizobakia zenyewe zilikuwa na manufaa ya kiujumbe zaidi kuliko kimatumizi..

Kwa mfano zawadi ya UVUMBA. Kwa kawaida uvumba sio zawadi tunaweza tukasema uzito wa kumfaa mtu kwa wakati wote, ni zawadi isiyokuwa na thamani kubwa sana,hivyo hatuwezi kivile kuiweka katika makundi ya zawadi kama zawadi , tuchukulie kwamfano Mtu kasafiri kutoka mbali tuseme Marekani halafu anakuletea zawadi ya msalaba au ufunguo..Kwa namna ya kawaida wewe unayoipokea huwezi kwenda kuiuza au kuitumia kwa matumizi yako yoyote, zaidi sana utafahamu moja kwa moja kuwa ni zawadi iliyobeba ujumbe Fulani wa ndani zaidi ya kinachoonekana,

Mfano mwingine tunafahamu pale binti anapoagwa baada ya kuposwa na kwenda kuolewa huwa kuna baadhi ya zawadi zinaambatanishwa naye kutoka kwa watu wa nyumbani kwake, licha ya kupewa vitu vya ndani na mali..lakini kuna mambo madogo madogo utakuta anakabidhiwa pia na hayo ndio yana ujumbe mzito kuliko hata vile vitu vya thamani alivyopewa, kwamfano utakuta anapewa ufagio, au ungo,..Ikiwa na maana kuwa mwanamke anapaswa awe Msafi na awe anazingatia Mapishi n.k...

Hivyo hivyo na wale mamajusi walipata ufunuo wa wanayemfauata ni nani, na ndio maana walikwenda na dhahabau lakini wakaongezea kubeba na Uvumba juu yake?..

Sasa Kumbuka katika hekalu la Mungu, uvumba ulikuwa unavukizwa tu na makuhani baada ya sadaka kutolewa sasa ile damu ilichukuliwa na kupelekwa katika madhabahu ya dhahabu iliyokuwa kule patakatifu, na hapo ndipo uvumba ulikochomwa kujaza ile nyumba ya Mungu harufu nzuri ya manukato na utukufu, na kumbuka kazi hiyo aliifanya kuhani mkuu peke yake. Hii ikifunua kuwa Huyu aliyezaliwa Yesu Kristo, licha tu ya kuwa mfalme atakuja kuwa KUHANI pia, kwasababu kila kuhani lazima awe na uvumba mkononi mwake wa kuvukiza mbele za Mungu…Na Yesu Kristo ndiye kuhani mkuu wetu. Haleluya.

Waebrania 4: 14 “Basi, iwapo tunaye kuhani mkuu aliyeingia katika mbingu, Yesu, Mwana wa Mungu, na tuyashike sana maungamo yetu.
15 Kwa kuwa hamna kuhani mkuu asiyeweza kuchukuana nasi katika mambo yetu ya udhaifu; bali yeye alijaribiwa sawasawa na sisi katika mambo yote, bila kufanya dhambi.
16 Basi na tukikaribie kiti cha neema kwa ujasiri, ili tupewe rehema, na kupata neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji”.

Kwahiyo wale Mamajusi walipata ufunuo huo kuwa Yule atakuja kuwa kuhani mkuu pia..Jambo ambalo wengi wa waliokuwa pale hawakulifahamu hilo, mpaka alipokuja kupaa mbinguni, mitume ndio wakamwandikia habari zake.

Kadhalika MANEMANE, ni zao lililotoka katika miti likiwa na maana ya “Uchungu”, manemane ilitumika kutengenezea dawa, Hivyo zawadi kama ile isingeweza kuonekana inafaa sana kwa mazingira kama yale ya furaha ya kuzaliwa Mfalme duniani, lakini walifanya vile kwasababu ilikuwa inabeba ujumbe mwingine wa ndani zaidi..Kama tafsiri ya jina lake lilivyo ilifunulia kuwa mtoto aliyezaliwa licha ya kuwa mfalme atapitia mateso na uchungu mwingi, na hilo lilikuja kujidhirisha alipoteswa na kusulibiwa kwa ajili yetu… Wakati akiwa katika safari yake ya kwenda msalabani wale askari walimchanganyia mvinyo na manemane na kumnyeshwa, lakini Bwana aliitema kwa jinsi ilivyokuwa chungu,(Soma Marko 5:23)..Gharama Bwana aliyoilipa kwa ajili ya dhambi zetu ni kubwa sana, mfalme kufa na kuteswa msalabani kwa ajili ya mtu mwenye dhambi asiyestahili kwa chochote, hakika ni jambo la neema sana.

Hivyo wale mamajusi Mungu aliwapa kuona mbali zaidi ya zile hazina walizozipeleka. Kama mamajusi ambao hawakuwa wayahudi walisafiri kutoka nchi za mbali kwa muda wa miaka miwili, ili tu kumwona mfalme YESU akiwa mchanga, tutapataje kupona sisi tulioshuhudia matendo yake makuu ya neema kuu namna hii ambayo kila siku yanatuita tutubu dhambi?. Tutapate kupona tukidharau leo!
Ubarikiwe!!

No comments:

Post a Comment