"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Friday, November 30, 2018

MASWALI NA MAJIBU: SEHEMU YA 44

SWALI 1: Ni sahihi mtu kubatizwa kwenye maji ya KISIMANI?.

JIBU: Kwanza ni muhimu kufahamu maana ya hili neno UBATIZO.Hili ni neno la kiyunani lijulikanalo kama (BAPTIZO), lenye maana ya"KUZAMISHWA". Kwahiyo kama tafsiri ya jina lake ilivyo, mtu anapobatizwa ni lazima azamishwe mwili wake wote katika maji, Na kumbuka haisemi ni katika mto, bahari, ziwa, au kisima, n.k. La! Maagizo yametolewa ni kuzamishwa.

Kwahiyo Hakuna tatizo lolote mtu kubatizwa/kuzamishwa kisimani, ili mradi tu, maji yawe mengi ya kuweza kumzamisha mwili wake wote, hivyo iwe kwenye mto, kisima, chemchemu, pipa au baharini au kwenye dimbwi, popote pale la muhimu ni azamishwe mwili wote uzame usionekane na abatizwe kwa jina la Yesu Kristo. Ubatizo mwingine wowote tofauti na huo ni Batili. Hivyo Mtu huyo anapaswa akabatizwe tena.Kumbuka Nyakati za mtume Paulo kulikuwa na watu waliokuwa wanaujua ubatizo tu wa Yohana wa Toba, hawakuufahamu ubatizo uletao ondoleo la dhambi, Lakini Paulo alipowahubiria na kuamini wakabatizwa tena kwa ubatizo sahihi soma..

Matendo 19: 1 "Ikawa, Apolo alipokuwa Korintho, Paulo, akiisha kupita kati ya nchi za juu, akafika Efeso; akakutana na wanafunzi kadha wa kadha huko;
2 akawauliza, Je! Mlipokea Roho Mtakatifu mlipoamini? Wakamjibu, La, hata kusikia kwamba kuna Roho Mtakatifu hatukusikia.
3 Akawauliza, Basi mlibatizwa kwa ubatizo gani? Wakasema, Kwa ubatizo wa Yohana.
4 Paulo akasema, Yohana alibatiza kwa ubatizo wa toba, akiwaambia watu wamwamini yeye atakayekuja nyuma yake, yaani, Yesu.
5 Waliposikia haya WAKABATIZWA KWA JINA LA BWANA YESU.
6 Na Paulo, alipokwisha kuweka mikono yake juu yao, Roho Mtakatifu akaja juu yao; wakaanza kunena kwa lugha, na kutabiri.
7 Na jumla yao walipata wanaume kumi na wawili. "

Na wewe pia unaweza ukawa umebatizwa kwa ubatizo usio sahihi, hivyo usione aibu kwenda kubatizwa tena, ili kufanya imara wito wako na uteule wako.

Ni muhimu kufahamu kuwa hakuna ubatizo wa kunyinyuziwa kulingana na maandiko...Na ubatizo sahihi ni muhimu mno haupaswi kuupuziwa kwa namna yoyote ile. Kadhalika hakuna chuo chochote cha kupitia ndipo ukabatizwe, pale mtu tu anapoamini na kutubu kabisa kwa kumaanisha kuziacha dhambi zake moja kwa moja anapaswa aende akabatizwe kwa ajili ya ondoleo la dhambi zake na kupokea kipawa cha ROHO MTAKATIFU.

Matendo 2: 37 "Walipoyasikia haya wakachomwa mioyo yao, wakamwambia Petro na mitume wengine, Tutendeje, ndugu zetu?
38 Petro akawaambia, Tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo, mpate ondoleo la dhambi zenu, nanyi mtapokea kipawa cha Roho Mtakatifu".

Ukipata muda pia pitia mistari hii ,( Matendo 8:16, 10:48)
SWALI 2: Asante mwalimu .lakini swali langu kuhusu ubatizo, kwa nini naona si sahihi kufanya ubatizo kwa maji ambayo yanasimama tu kama kisima, kidimbwi n.k maana maji yanayosimama inaashiria hayana uhai. Maji yanayoteremka kama mtoni ilivyo sahihi kimaandiko ama unasemaje unielimishe kidogo. Kwa kuongeze inadaiwa kwamba aina hizi za ubatizo inatokana kwa yule mpinga kristo . Kwa nini naonelea sharti ubatizo ni kwa maji inayoteremka?
JIBU: Ubarikiwe kwa swali lako, Kinachohitajika na cha muhimu ni maji mengi ya kumzamisha mtu, kwasababu maana yenyewe ya neno "ubatizo" ni "kuzamisha", na maji yote yana uhai, yawe yanatembea au yamesimama, na ndio maana maji yaliyosimama ukiyachukua na kuyamwagilia kwenye mmea wako unakua tu vizuri, haufi, maji yaliyosimama yana uhai sawa tu na maji yanayotembea. Kwahiyo ubatizo ni popote penye maji mengi. Ubarikiwe!



SWALI 3: Kuandika vi- notes ( kuhusu kitu ninachofundishwa kanisani au kujifunza biblia) sasa kitu kinachonishangaza sipati muda wa kuvipitia ? Sijui tatizo liko wapi ? Nisaidie hapo ndugu.
JIBU: Tatizo lipo kwako, unapaswa uonyeshe BIDII, kuyapitia yale unayofundishwa, kwa kujiundia wewe mwenyewe utaratibu wako binafsi, ambao utakuwezesha kupata muda wa kutosha wa utulivu kila siku kukaa chini na kuyapitia yale uliyofundishwa, vinginevyo utakuwa katika hatari ya adui kuyanyakuwa yale unayofundishwa kila siku, unafanana na ile mbegu iliyotupwa katika njia,(Marko 4:15) ambapo unalisikiaa lile Neno lakini hulitendi kazi hivyo adui adui anakuja na kulinyakua haraka…

Biblia inatuonya tuwe na bidii katika kusoma 1Timotheo 4:13 “Hata nitakapokuja, ufanye BIDII KATIKA KUSOMA…”.Unaona, hivyo tatizo kama la kwako sio la kuombewa, ni jambo la kurekebisha ratiba yako, na kutenga muda wako binafsi na Mungu wako kila siku. Upate kujifunza Neno la Mungu kwa bidii, na sio kwa ulegevu.
 

SWALI 4: Ndugu naomba unifungue akili kidogo juu ya hili? Katika wakorintho wa 1wakoritho5 :5. ' KUMTOLEA SHETANI MTU HUYO, ILI MWILI UADHIBIWE, ILI NA ROHO IOKOLEWE katika siku ya Bwana Yesu." .......ndugu zangu hapo pamenichanganya naomba mnisaidie ?.

JIBU: Shalom, Awali ya yote utaona kuwa waraka huo Mtume Paulo aliwaandikia watakatifu waliokuwa wanaishi Korintho, haukuandikwa kwa watu wote, hapana bali ni kwa “watakatifu tu”. Sasa adhabu za watakatifu zinatofautiana, zipo dhambi za mauti na zipo dhambi zisizo za mauti.

1Yohana 5:16 “Mtu akimwona ndugu yake anatenda dhambi isiyo ya mauti, ataomba, na Mungu atampa uzima kwa ajili ya hao watendao dhambi isiyo ya mauti. Iko dhambi iliyo ya mauti. Sisemi ya kwamba ataomba kwa ajili ya hiyo.
17 Kila lisilo la haki ni dhambi, na dhambi iko isiyo ya mauti.”

Hivyo dhambi zisizo za mauti ni dhambi ambazo mtu yeyote aliye mkristo akifanya anaweza akaomba au akaombewa na kusamehewa, lakini dhambi za mauti ni dhambi ambazo ukizifanya hata uombeweje au uombeje adhabu za mauti zipo pale pale.Ukitubu utasamehewa hapa duniani lakini adhabu ipo pale pale, Na moja ya dhambi hizo ndio mfano wa ile alioyoifanya Anania na Safira mke wake.

Kadhalika Mungu alitoa mamlaka kwa kanisa pia kutoa adhabu kama hizo, kwa makosa yale yaliyopitiliza, kwamfano juu ya habari hiyo utaona kuwa kulikuwa na watu wanajiita ni wakristo lakini wanafanya mambo ya aibu ambayo hata hayawezi kuonekana kwa watu wa mataifa wasiomjua Mungu, yaani mtu analala na mke wa baba yake na bado anajiita ni mkristo na anafanya ushirika na watakatifu, sasa watu wa  namna hiyo dhambi wazifanyazo adhabu yake ni mauti, na kanisa limepewa mamlaka ya kumtoa mtu huyo kwa shetani aadhibiwe, kusudi kwamba roho yake baadaye ije kupona, vinginevyo kama asipoadhibiwa hapa duniani, kwa uovu kama huo ni wa kuelekea moja kwa moja katika ziwa la moto..

Sasa akishakabidhishwa kwa shetani, jambo lolote linaweza kutokea juu yake, anaweza kutokewa na mambo ya ajabu, pengine hata ajali, ugonjwa, kifo cha ghafla n.k. lakini mwisho wa siku ni lazima afe. Hata atubu kwa namna gani hawezi kusamehewa hapa duniani. Hivyo sisi kama wakristo tunapaswa tuwe makini ni mambo tuyafanyayo tukijua kabisa sio kila dhambi tutapata rehema..nyingine zitatugharimu maisha yetu  hata kama tutatubu vipi kwa kumaanisha. Kwa urefu zaidi kuhusu dhambi ya mauti unaweza ukasoma kupitia link hii >>> dhambi ya mauti

Lakini pia ndugu ... Naomba unifungue akili kwa hili ... Mfano mko katika mazungumzo mazuri tu ghafla mwenzio akaanza KUMSENGENYA ndugu mwingine ? Sasa kwa upande wako unajua kwamba KUSENGENYA ni dhambi sasa utachukua maamuzi gani?

JIBU: Unayakatisha hayo mazungumzo na kuzungumza habari nyingine..usipoonyesha ushirikiano leo na kesho yule mtu atatambua kuwa wewe hupendi kuzungumza vibaya habari za watu wengine, hivyo siku nyingine hatakuja kukuletea habari hizo..Lakini kama utakuwa unakubaliana naye, na kuonyesha ushirikiano naye atakuona kuwa wewe ni mwenzake na hivyo kila siku utakuwa katika mazingira ya usengenyaji.

Kadhalika ni wajibu wako pia kujionyesha kuwa wewe ni mkristo. Watu wakishakufahamu kuwa wewe upo hivyo, wataogopa kukuletea habari za usengenyaji kwasababu watajua kuwa wewe huzipendi.

SWALI 5: Shalom ndugu nataka unisaidie katika hili kwa siku za hivi karibuni nimekuwa na changamoto mpya najikuta nawaka tamaa isiyo ya kawaida najikuta nina tamaa kali ya kutaka kuzini ila nachoshukuru kwa sasa naweza kujizuia hofu ni je?? haita ni shinda huko mbeleni..?
 
JIBU: Dalili  mojawapo inayoonyeshwa kuwa umezaliwa mara ya pili ni kutokushindwa na dhambi. Ukishaona mtu anasema kazaliwa mara ya pili halafu kaenda kuzini ni wazi kuwa bado hajazaliwa kwa Roho wa Mungu..

1Yohana 5:18 “Twajua ya kuwa kila mtu aliyezaliwa na Mungu HATENDI DHAMBI; bali yeye aliyezaliwa na Mungu HUJILINDA, wala yule mwovu hamgusi.”

Unaona hilo Neno HUJILINDA..Ikiwa na maana kuwa dalili zozote za kutenda dhambi  za makusudi  zinaponyemelea maisha yake hutafuta suluhisho haraka kabla ya kuingia katika mtego huo. Sasa kwa hali kama ya kwako, ni wazi kuwa nguvu zako za rohoni zimepungua. Na inawezekana ni moja ya mambo haya au yote..

     1)     Huombi
     2)     Hufungi
     3)     Hufanyi ushirika
     4)     Hutafakari Neno la Mungu.

Bwana Yesu aliwaambia wanafunzi wake, Mathayo 26:40 “Akawajia wale wanafunzi, akawakuta wamelala, akamwambia Petro, Je! Hamkuweza kukesha pamoja nami HATA SAA MOJA?
41 KESHENI, MWOMBE, MSIJE MKAINGIA MAJARIBUNI; roho i radhi, lakini mwili ni dhaifu.
Unaona, mtu anaingia majaribuni kama mtu sio mwombaji. Na kiwango cha chini tunapaswa tuombe kwa siku ni walau lisaa limoja..Hivyo kama wewe sio mwombaji tamaa zitakutawala tu, na pia utakosa raha ya wokovu wako. Maombi ni silaha moja kubwa sana, na shetani ndio anayopenda kuishambulia, kwasababu anajua akimtoa mtu katika mstari wa maombi ameshammaliza.

Yakobo 4: 4.1 Vita vyatoka wapi, na mapigano yaliyoko kati yenu yatoka wapi? Si humu, katika tamaa zenu zifanyazo vita katika viungo vyenu?
2 Mwatamani, wala hamna kitu, mwaua na kuona wivu, wala hamwezi kupata. Mwafanya vita na kupigana, wala hamna kitu kwa kuwa HAMWOMBI! “

PILI, KUFUNGA: Kufunga kwa mkristo kuna umuhimu sana, kwanza, kunakusaidia kuutiisha mwili chini, na kuifanya roho yako kuja juu,..hivyo inakupa wepesi wa kusali na kuutawala mwili kirahisi. Na pia ukiwa ni mfungaji tamaa za mwili zinadidimia zenyewe ndani yako. 

TATU: kama sio mtu wa kujumuika na wengine kufanya ushirika, kuabudu na kumsifu Mungu. Hali mbaya za adui zitakusumbua kila siku. Jijengee tabia ya kuhudhuria ibadani, hata kama vingine havitakusaidia lakini ule ushirika u wa kumsifu na kumwabudu Mungu ni muhimu sana kwa mkristo yeyote aliyeokolewa.. Ni ahadi ya Mungu wanapojumuika wawili au watatu kwa jina lake, huwa anashuka katikati yao…Hivyo usipendelee sana kukaa mwenyewe kama upo mwenyewe..

NA LA MWISHO. NI UTAFAKARIJI WA NENO: Neno lenyewe linaweza kukupa nguvu, na maonyo juu ya maisha yako, na kukufariji. Kwa jinsi utakavyokuwa mtafakariji wa Neno zaidi ndivyo utakavyokuwa na uwezo wa kumshinda adui na njama zake, kwasababu mitego yote ya shetani na namna ya kuitatua ipo katika maandiko,Kwasababu huko huko katika kutafari Roho Mtakatifu ndipo anaposema na wewe.

Hivyo ukizingatia hayo, huwezi kuanguka leo na katika siku zinazokuja. Bwana akubariki sana.


BARUA INAYOSOMWA

2 Wakorintho 3:2 NINYI NDINYI BARUA YETU, iliyoandikwa mioyoni mwetu, INAJULIKANA NA KUSOMWA NA WATU WOTE;”
Maisha tunayoishi sisi ni BARUA ya Kristo, watu watutazamapo, wanapata ujumbe hata kabla ya sisi kuzungumza lolote,. Na matendo yetu ndiyo maandishi, na siku zetu ndizo kurasa, Tangu tulipompa Bwana maisha yetu, siku hiyo hiyo tunaanza kuandika kurasa njema za barua zetu.

Injili yenye matunda Kristo anayoyataka haihubiriwi kwa maneno matupu! Hapana bali inahubiriwa kwa matendo..Matendo yetu ndiyo yanayohubiri injili kuliko kingine chochote, Matendo yetu ndiyo yanayomtangaza Kristo kuliko kitu kingine chochote. Tunaweza tukawa na uwezo mzuri wa kuhubiri au kuongea lakini kama matendo yetu hayaendani na tunachokizungumza basi injili tunayoihubiri ni BURE!!.

Unaweza ukawa unahudhuria kanisani kila siku, unasaidia watu, lakini kama maisha yako ya siri ni machafu, kama maisha yako ya pembeni ni ya kiasherati, au ni mtazamaji wa pornography, au mfanyaji masturbation au mtukanaji, au mwizi, au mwuaji, au unacheza kamari, au mtu wa hasira usiyesamehe basi wewe ni barua yako ni mbaya, haijalishi unalitaja jina la Kristo mara ngapi..

Maisha yetu yanapaswa yahubiri injili kwa watu wa nje kiasi kwamba mtu akikuona tu anajua moja kwa moja Yule ni Mkristo hata kabla hujazungumza lolote, akikuona juzi, jana na leo maisha yako ni yale yale masafi, hata kabla hajazungumza na wewe Neno moja anakiri moyoni kwamba wewe ni mwanafunzi wa Kristo.
 
Sio lazima tuonekane tumebeba biblia, au tumevaa kanzu, au tumevaa kama watu wa dini au tusikiwe tunaimba mapambio, au tuonekane tunaenda kanisani kila siku, au tusikiwe tukisali kila siku hapana! Hiyo ni vizuri lakini hata pasipo hayo mambo, pasipo watu kutusikia tukisali, au tukiimba, au tukienda kanisani n.k inapaswa wakituona tu, ndani ya muda mfupi wameshajua sisi ni watu wa namna gani, washajua kuwa sisi milki ya Yesu Kristo.

Unaweza usiwe unaongea kama watu wa kidini, lakini inapasa mtu akikutazama tu maisha yako, siku mbili tatu,lazima kuwe kuna kitu ndani yake kinamshuhudia kwamba wewe ni mwana wa Mungu. Kwa jinsi maisha yako yanavyoangaza Nuru, na kuonekana Barua inayosomeka vyema.

Mathayo 5:16 Vivyo hivyo nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona MATENDO YENU mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni...

Unaona? Kitu Bwana Yesu anachosema hapo ni kwamba nuru ya mtu inaangaza kwa matendo yake, na si kitu kingine na hichi ndicho watu wanachokitazama.

Hebu tujifunze kidogo Kitabu cha ESTA.

Esta alikuwa ni Myahudi lakini alizaliwa katika nchi ya Babeli, wakati wana wa Israeli wapo utumwani, hakuwahi kufika nchi yake Israeli.. aliishi na Kaka yake aliyeitwa Mordekai, baada ya wazazi wake kufa (ambapo Baba yake Esta alikuwa ni mjomba wake Mordekai). Walikuwa wanamcha Mungu yeye na Mordekai, lakini ilipofika wakati Mfalme wa Uajemi anatafuta malkia mwingine sehemu ya Malkia Vashti aliyemvunjia heshima Mfalme, Mordekai alimpandisha Esta kwenda kushindania hiyo nafasi ya umalkia miongoni mwa wanawali watakaochaguliwa na mfalme, Lakini jambo la kimiujiza ni kwamba Mordekai wala Esta hawakujitambulisha kuwa wao ni watu kutoka taifa gani wala Imani yao ni Imani gani...Na chakushangaza ni kwamba japo kuwa Esta hakuidhihirisha Imani yake mbele ya nyumba ya Mfalme wa Uajemi, lakini kwa matendo yake TAYARI WALE WALIOKUWA WANAWACHAGUA WANAWALI, WALISHAMSOMA ESTA NA KUGUNDUA KUWA NI MTU WA KIMUNGU, MWENYE TABIA NJEMA. Na kama ni msomaji wa Biblia utaona kuwa Ni Esta peke yake ndiye aliyepata kibali mbele ya Mfalme kuwa MALKIA kati ya wale wanawali wengine.


Sasa Ni nini tunachoweza kujifunza hapo?? Hata pasipo Kutaja DINI YAKO,WALA DHEHEBU LAKO, WALA IMANI YAKO, watu wanaweza kukusoma tu na kugundua wewe ni mtu wa namna gani? Watu wanaweza wakakusoma tu na kugundua Barua yako ni barua ya namna gani. Kwa mwenendo wako tu hata pasipo kusema BWANA ASIFIWE! au BWANA ATUKUZWE!
Sasa tukirudi kwenye kitabu cha Esta, tunaweza tukajifunza jambo lingine kubwa sana..

JE! Unajua kuwa kitabu cha ESTA ndio kitabu pekee cha Biblia ambacho kuanzia mwanzo wake hadi mwisho wake hakuna Neno “BWANA” wala neno “MUNGU”? Kama hujui hilo nenda kapitie tena biblia yako na utaligundua hilo. Sasa Jambo hilo linafunua nini? Japokuwa kitabu cha Esta hakijamtaja mahali popote Bwana wala neno Mungu halionekani, lakini tukisomapo kile kitabu tunamwona Mungu kwa sehemu kubwa sana na uwezo wake, na bila shaka watu wote tunafahamu kuwa ni kitabu takatifu cha Mungu...ikifunua jambo lile lile kwamba unaweza usionekane unalitaja jina la Bwana Mahali popote pale lakini watu WASOMAPO BARUA YAKO WANAMWONA MUNGU kwa kiwango kikubwa. Na hicho ndicho Mungu anachotaka. Simaanishi kuwa usilitaje jina la Bwana mahali popote hapana, ni wajibu wetu sote kufanya pia na hayo.

Mungu Hataki tuwe kama wanafki kama mafarisayo, ambao kwa nje, tunaonekana ni wakidini lakini kwa ndani ni wachafu. Malkia Esta hakubeba Torati na kuingia nayo kwa Mfalme ndipo akubalike, hakujidhihirisha kwamba yeye ni Myahudi, mwana wa Ibrahimu, na kwamba anamwabudu Mungu wa aliyeziumba Mbingu na nchi..hakufanya hayo yote, yeye aliingia tu mbele ya mfalme na barua ya maisha yake, na utii wake, unyenyekevu wake, upole wake, usikivu wake, na utulivu wake, na tabia yake njema, aliingia na tabia yake ya kuwa na kiasi, ya mtu asiye na majivuno, asiye na kiburi, asiyekuwa na tamaa, aliingia na tabia yake ya kuridhika, na kutotamani mambo makubwa, aliingia na tabia yake ya kutokusengenya, ya kutokuwa mwashetati, hiyo ndiyo iliyomfanya apendwe na Mfalme, hiyo ndiyo iliyomfanya akubalike..Hiyo ndiyo iliyomfanya Barua yake isomeke vyema mbele za Mfalme, na Ufalme wa Uajemi wote, na hiyo ndiyo iliyomfanya KITABU CHAKE JAPOKUWA HAKINA JINA LA BWANA MAHALI POPOTE LAKINI KIMEINGIA KATI YA VITABU 66 VYA BIBLIA.

Kaka/Dada uliye mkristo usomaye ujumbe huu, ifanye barua yako isomeke vyema, kusudi kwamba watu wakishauona mwenendo wako, roho zao zipate kuponywa. Mwenendo tu wa mtu ni nguvu tosha ya kumgeuza mtu kama vile Neno linavyoweza kumgeuza mtu. Wakati mwingine ndoa yako inamatatizo na umehangaika huku na kule, umefunga na kusali, lakini bado mume wako anazidi kuwa mwovu, anazidi kuwa mlevi, mke wako hana nidhamu, hamchi Mungu, watoto wako ni watukutu hawataki kukutii, wazazi wako ni waashirikina, wanagombana, wametengana..Na wewe ni mkristo umejaribu kuomba, hata wakati mwingine kuwashuhudia lakini bado hakuna mabadiliko..Tatizo linaweza kuwepo katika mwenendo wako, wanapokutazama hawaoni kitu cha kuwavutia kuwa kama wewe. Lakini ikiwa mwenendo wako utaubalishwa na kuishi maisha ya nidhamu na utakatifu na kumcha Mungu, basi fahamu kuwa hiyo ni injili tosha ya kuwafanya wao wabadilike. Embu soma vifungu hivi vinavyosema juu ya familia.
1Petro 3:1 “Kadhalika ninyi wake, watiini waume zenu; kusudi, ikiwa wako wasioliamini Neno, wavutwe kwa mwenendo wa wake zao, pasipo lile Neno;
2 wakiutazama mwenendo wenu safi, na wa hofu.”
Unaona hapo? Hivyo ndugu ikiwa bado hujamkabidhi Bwana Yesu maisha yako, mpe leo, Tubu mgeukie kwasababu yeye ndiye Njia ya kufika mbinguni, hakuna mwingine, njia nyingine za kidini, kidhehebu, mtu binafsi, n.k zote zinaishia mautini..Yesu ndiye mwokozi, Siku tunazoishi ni siku za Mwisho, zilizotabiriwa. Na Neema inakaribia kurudi Israeli, na Kristo kulichukua kanisa lake, je! umo miongoni mwa watakaoenda na Bwana??
Neema ya Bwana wetu Yesu Kristo izidi kuwa nawe!!

Tafadhali “share” kwa wengine,
Mungu akubariki.