"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Monday, November 19, 2018

NUHU WA SASA.

Mwanzo baada ya Adama na Hawa kuasi, Bwana aliwafukuza kutoka uweponi mwake, ndani ya ile bustani ya Mungu (Edeni)..Lakini tunaona baada tu ya kufukuzwa haikuishia hapo, bali tunaona pia ARDHI ililalaaniwa kwa ajili yao. Ikiwa na maana kuwa kila kinachopatikana kutoka ardhini, kitapatikana kwa tabu kuanzia huo wakati na kuendelea..Ilikuwa ni pigo kubwa kwasababu karibia kila kitu kinatoka ardhini, kwasababu hata mwanadamu mwenyewe anatoka ardhini, na ndio maana hata yeye anapatikana kwa uchungu, na kwasababu hiyo Bwana Mungu alimwambia mwanamke atazaa kwa uchungu..Na sio mwanadamu tu, bali hata wanyama na viumbe vyote hiyo laana iliwapata kwasababu nao pia wanatoka ardhini...Hivyo ile laana ya ardhi kulaaniwa NI PANA KIDOGO zaidi ya tunavyoielewa.

Lakini kama tukijifunza kitabu cha Mwanzo kwa undani zaidi, tutazidi kuona kuwa hiyo laana ya ardhi kulaaniwa haikuishia tu pale Adamu aliasi, bali utaona kuwa kwa jinsi muda ulivyokuwa unaenda na maasi yalivyokuwa yanazidi kuongezeka ile laana nayo ilikuwa inajiongeza.. Ndio maana utaona Kaini baada ya kumwua ndugu yake Habili, ile laana ya ardhi kulaaniwa iliongezwa kwake...

Mwanzo 4: 9 “Bwana akamwambia Kaini, Yuko wapi Habili ndugu yako? Akasema, Sijui, mimi ni mlinzi wa ndugu yangu?
10 Akasema, Umefanya nini? Sauti ya damu ya ndugu yako INANILILIA KUTOKA KATIKA ARDHI. 11 Basi sasa, UMELAANIWA WEWE KATIKA ARDHI, iliyofumbua kinywa chake ipokee damu ya ndugu yako kwa mkono wako;
12 UTAKAPOILIMA ARDHI haitakupa mazao yake; utakuwa mtoro na mtu asiye na kikao duniani.
13 Kaini akamwambia Bwana, Adhabu yangu imenikulia kubwa, haichukuliki.
14 Tazama, UMENIFUKUZA LEO KATIKA USO WA ARDHI, nitasitirika mbali na uso wako, nami nitakuwa mtoro na mtu asiye na kikao duniani; hata itakuwa kila anionaye ataniua.”

Unaona hapo? Baada ya laana ya kwanza Bwana Mungu aliyomlaani Adamu na uzao wake juu ya ardhi, tunaona Kaini anazidishiwa tena mara mbili baada ya kumwua ndugu yake..hivyo ni laana juu ya laana..

Kwahiyo hali hiyo ya laana kujiongeza juu ya laana iliendelea kwa miaka na miaka kutokana na maasi ya wanadamu...Mpaka ilipofika wakati karibia na gharika Bwana alipomchagua mtu ambaye kwa kupitia yeye ataisimamisha ile laana ya ARDHI KULAANIWA kila kukicha..Na ndio tunasoma Bwana alimnyanyua Nuhu kwa kizazi chake, Mtu mkamilifu na wa Haki, ambaye alipata sana Neema mbele ya Macho ya Mungu..kama tunavyosoma mtoto huyo alipozaliwa tu Baba yake kwa Imani akatoa unabii juu yake na kusema...
Mwanzo 5: 28 “Lameki akaishi miaka mia na themanini na miwili, akazaa mwana.
29 Akamwita jina lake Nuhu, akinena, HUYU NDIYE ATAKAYETUFARIJI KWA KAZI YETU NA KWA TAABU YA MIKONO YETU KATIKA NCHI ALIYOILAANI BWANA.
30 Lameki akaishi baada ya kumzaa Nuhu miaka mia na tisini na mitano, akazaa wana, waume na wake”.
Unaona, tangu Adamu mpaka Kuzaliwa kwa Nuhu, ni takribani zaidi ya miaka 1500 ilipita..kwahiyo kwa kipindi chote hicho matatizo yalikuwa makubwa sana duniani kwasababu ya Ardhi iliyolaaniwa na inayoendelea kulaaniwa kutokana na dhambi zilivyokuwa zinazidi kuongezeka..Kwahiyo Baba yake Nuhu, kabla hajafa alijua atazaliwa mwana ambaye kwa kupitia yeye hiyo laana itasimama na itakuwa faraja kwa vizazi vijavyo..
Na Nuhu alipokuwa mtu mzima, baada ya Baba yake kufa alianza kumtafuta Mungu na kwenda katika njia zake, na kutojichangamana na maasi ya ulimwengu..Na hivyo Bwana akapendezwa naye kuliko watu wote waliokuwa wanaishi duniani kwa wakati huo, kumbuka dunia ya wakati ule ilikuwa na watu wengi kama dunia ya sasa, lakini yeye akakubalika sana machoni pa Bwana.

SASA NI WAKATI GANI? NUHU ALIPOISIMAMISHA HIYO LAANA?.

Kwasababu tunaona Baba yake alishatabiri kuwa yeye ndiye atakayefariji uzao wao katika nchi aliyoilaani Bwana, hivyo ni lazima uje wakati ambapo Bwana ataisimamisha hiyo laana kupitia Nuhu. Na wakati huo sio mwingine zaidi ya WAKATI BAADA YA GHARIKA KUPITA..pale ambapo Nuhu alimtolea Bwana sadaka nzuri iliyompendeza na Bwana akaridhika na sadaka ile na KUAPA KUTOILAANI TENA NCHI kwa namna yoyote ile..Tunasoma hayo katika..
Mwanzo 8: 18 “Basi Nuhu akatoka, yeye, na wanawe, na mkewe, na wake za wanawe pamoja naye;
19 kila mnyama, na kila kitambaacho, na kila ndege, kila kinachokwenda juu ya nchi kwa kabila zao, wakatoka katika safina.
20 Nuhu akamjengea Bwana madhabahu; akatwaa katika kila mnyama aliye safi, na katika kila ndege aliye safi, akavitoa sadaka za kuteketezwa juu ya madhabahu.
21 Bwana akasikia harufu ya kumridhisha; Bwana akasema moyoni, SITAILAANI NCHI TENA BAADA YA HAYO KWA SABABU YA WANADAMU, MAANA MAWAZO YA MOYO WA MWANADAMU NI MABAYA TANGU UJANA WAKE; wala sitapiga tena baada ya hayo kila kilicho hai kama nilivyofanya. 22 Muda nchi idumupo, majira ya kupanda, na mavuno, wakati wa baridi na wakati wa hari, wakati wa kaskazi na wakati wa kusi, mchana na usiku, havitakoma”.
Unaona hapo? Bwana anasema “sitailaani tena nchi” na sio “sitamlaani tena mwanadamu” nchi na ardhi ni kitu kimoja. Kwahiyo baada ya Nuhu kumtolea Bwana sadaka iliyokubalika mbele zake, Bwana akaisimamisha na ile laana iliyokuwa inaendelea kujiongeza siku baada ya siku.

Mwanzo 9: 8 “Mungu akamwambia Nuhu, na wanawe pamoja naye, akisema, 9 Mimi, tazama, nalithibitisha agano langu nanyi; tena na uzao wenu baada yenu;
10 tena na kila kiumbe hai kilichoko pamoja nanyi, ndege, na mnyama wa kufugwa, na kila mnyama wa mwitu katika nchi pamoja nanyi; wote wanaotoka katika safina, hata kila kilicho hai katika nchi.
11 Na agano langu nitalithibitisha nanyi; WALA KILA CHENYE MWILI HAKITAFUTWA TENA KWA MAJI YA GHARIKA; WALA HAKUTAKUWA TENA GHARIKA, BAADA YA HAYO, KUIHARIBU NCHI.
12 Mungu akasema, Hii ndiyo ishara ya agano nifanyalo kati yangu na ninyi, na kila kiumbe hai kilichoko pamoja nanyi, kwa vizazi vyote hata milele;
13 Mimi nauweka upinde wangu winguni, nao utakuwa ni ishara ya agano kati yangu na nchi.
14 Hata itakuwa nikitanda mawingu juu ya nchi, upinde utaonekana winguni,
15 nami nitalikumbuka agano langu, lililoko kati yangu na ninyi, na kila kiumbe hai katika wote wenye mwili, wala maji hayatakuwa gharika tena kuwaharibu wote wenye mwili.
16 Basi huo upinde utakuwa winguni; nami nitauangalia nipate kulikumbuka agano la milele lililoko kati ya Mungu na kila kiumbe hai katika wote wenye mwili kilichoko katika nchi.
17 Mungu akamwambia Nuhu, Hii ndiyo ishara ya agano nililoliweka kati yangu na wote wenye mwili walioko katika nchi.”

Lakini tunaona kuwa japokuwa Bwana aliisimamisha ile laana bado kulikuwa na matatizo madogo madogo yaliyoendelea kutokea.. kulikuwepo bado na vipindi vya njaa duniani ingawa mvua bado zilikuwa zinanyesha kwa misimu, bado vilikuwepo vipindi vya matetemeko, vipindi vya taabu, nyakati za kula kwa jasho n.k Hivyo kwa lugha nyingine ni kwamba Nuhu alisimamisha laana isiendelee lakini hakuiondoa laana kabisa.

Agano Mungu aliloingia na Nuhu, halikutosha kuondoa LAANA YOTE MUNGU aliyoilaani ARDHI, lilikuwa ni agano la kuleta UNAFUU tu wa maisha juu ya wanadamu.
Hivyo ni lazima aje mwingine mfano wa Nuhu ambaye sio tu kuisimamisha laana bali KUIONDOA KABISA LAANA ISIWEPO, dunia irudi katika hali yake ya kwanza, kusiwepo na tabu tena, kusiwepo na kula kwa jasho tena, zisiwepo shida tena n.k Na huyu si mwingine zaidi ya YESU KRISTO.

Na kama tunavyoona ili kwamba Bwana aibariki tena ardhi kama alivyofanya kwa Nuhu, ni lazima gharika ipite Kwanza kuiharibu dunia yote, kisha ndio ije ile baraka na kabla hajaiharibu dunia kwa gharika, alimuhifadhi kwanza Nuhu na wanawe ndani ya safina.

Vivyo hivyo katika siku hizi za mwisho wakati BWANA MUNGU anataka kwenda kuifuta kabisa laana ya DUNIA, ARDHI ILIYOLAANIWA. Bwana Mungu alimnyanyua YESU KRISTO kwa mfano wa Nuhu, ili kwa kupitia yeye Bwana ayarejeshe mambo yote yaliyoharibika, arejeshe dunia iwe kama Edeni, aiondoe laana yote ambayo haikumalizika kuondolewa na Nuhu.
Na ni lazima gharika kwanza ije ili kuondoa waovu wote, ulimwenguni ndipo mambo yote yafanywe kuwa mapya..Hivyo kabla ya Yesu Kristo kuja duniani kurejesha mambo yote, siku zake zitafananishwa kama siku za Nuhu, ataijenga safina ambayo ni NENO LAKE, na kuwaingiza watu wake humo, na kisha kuihukumu dunia kwa moto kama Nuhu alivyoihukumu kwa gharika.

Waebrania 11: 7 “Kwa imani Nuhu akiisha kuonywa na Mungu katika habari za mambo yasiyoonekana bado, kwa jinsi alivyomcha Mungu, aliunda safina, apate kuokoa nyumba yake. Na hivyo AKAUHUKUMU MAKOSA ULIMWENGU, akawa mrithi wa haki ipatikanayo kwa imani.”

Kwahiyo Yesu Kristo ndiye mhukumu wa ulimwengu na mrithi, ATAKAYETUFARIJI SISI KATIKA ARDHI HII ILIYOLAANIWA NA BWANA, na faraja hiyo haitakuja sasa, bali baada ya ulimwengu huu kuteketezwa, ndipo hapo dunia itarejeshwa na kuwa kama paradiso ya kwanza. Katika utawala wa miaka 1000 na katika umilele.

Ndugu yangu unayesoma haya. Hii dunia haiwezi kufanywa upya kabla maangamizi hayajaja, hii dunia haina muda mrefu kama wengi wanavyodhani, Kristo mfano wa Nuhu anawaingiza wanawe sasa kwenye safina yake aliyoitengeneza yeye mwenyewe (NENO LAKE) na akisha maliza kuwaingiza wote mlango wa neema unafungwa, na kisha ghadhabu ya Mungu kumwagwa ulimwenguni kote. Na anasema kama ilivyokuwa katika siku za Nuhu ndivyo itakavyokuwa katika siku za kuja kwake mwana wa Adamu, siku za Nuhu watu walikuwa wanakula na kunywa,(anasa), walikuwa wanaoa na kuoana (ndoa za jinsia moja),walikuwa waasherati kama leo, wanaojipenda wenyewe, watu wa fashion, wanawake na wanaume wasiovaa mavazi ya kujisitiri, walikuwepo watu wa dhihaka, wauaji, wasengenyaji, wasiosamehe, wala rushwa, wacheza dansi n.k Ndio hao hao wapo sasa..Tusiangukie katika hilo kundi ndugu yangu. Bwana alimfunulia Mtume Petro mambo hayo yatakayotokea siku hizi za mwisho na kusema..

2 Petro 3: 2-12
1 Wapenzi, waraka huu ndio wa pili niwaandikiao ninyi; katika zote mbili naziamsha nia zenu safi kwa kuwakumbusha,
2 mpate kuyakumbuka yale maneno yaliyonenwa zamani na manabii watakatifu, na ile amri ya Bwana na Mwokozi iliyoletwa na mitume wenu.
3 Mkijua kwanza neno hili ya kwamba katika siku za mwisho watakuja na dhihaka zao watu wenye kudhihaki, wafuatao tamaa zao wenyewe,
4 NA KUSEMA, IKO WAPI AHADI ILE YA KUJA KWAKE? KWA MAANA, TANGU HAPO BABU ZETU WALIPOLALA, VITU VYOTE VINAKAA HALI IYO HIYO, TANGU MWANZO WA KUUMBWA.
5 Maana hufumba macho yao wasione neno hili ya kuwa zilikuwako mbingu tangu zamani, na nchi pia, imefanyizwa kutoka katika maji, na ndani ya maji, kwa neno la Mungu;
6 kwa hayo dunia ile ya wakati ule iligharikishwa na maji, ikaangamia.
7 Lakini mbingu za sasa na nchi zimewekwa akiba kwa moto, kwa neno lilo hilo, zikilindwa hata siku ya hukumu, na ya kuangamia kwao wanadamu wasiomcha Mungu.
8 Lakini, wapenzi, msilisahau neno hili, kwamba KWA BWANA SIKU MOJA NI KAMA MIAKA ELFU, NA MIAKA ELFU NI KAMA SIKU MOJA.
9 BWANA HAKAWII KUITIMIZA AHADI YAKE, KAMA WENGINE WANAVYOKUDHANI KUKAWIA, BALI HUVUMILIA KWENU, MAANA HAPENDI MTU YE YOTE APOTEE, BALI WOTE WAFIKILIE TOBA.
10 Lakini siku ya Bwana itakuja kama mwivi; katika siku hiyo mbingu zitatoweka kwa mshindo mkuu, na viumbe vya asili vitaunguzwa, na kufumuliwa, na nchi na kazi zilizomo ndani yake zitateketea.
11 Basi, kwa kuwa vitu hivi vyote vitafumuliwa hivyo, imewapasa ninyi kuwa watu wa tabia gani katika mwenendo mtakatifu na utauwa,
12 mkitazamia hata ije siku ile ya Mungu, na kuihimiza; ambayo katika hiyo mbingu zitafumuliwa zikiungua, na viumbe vya asili vitateketea na kuyeyuka? “

Unaona hapo juu anavyosema? “BWANA HAKAWII KUITIMIZA AHADI YAKE, KAMA WENGINE WANAVYOKUDHANI KUKAWIA, BALI HUVUMILIA KWENU, MAANA HAPENDI MTU YE YOTE APOTEE, BALI WOTE WAFIKILIE TOBA.”

Anakuvumilia leo ili utubu, ili utubie uasherati wako, ili utubie usengenyaji wako, ili utubie uvaaji wako mbaya, ili utubie dansi zako unazoenda kucheza kila siku, ili utubie kutokusamehe kwako, ili utubie kula kwako rushwa, ili utubie hasira zako zinazowaka pasipo sababu, anataka kukuingiza kwenye safina yake katika dakika hizi za mwisho za majeruhi. Na kutubu sio tu kuomba msamaha, hapana bali maana yake ni KUGEUKA NA KUACHA UNAYOYAFANYA. Na baada tu ya kuamua kwa dhati kugeuka, hatua inayofuata ni ubatizo wa maji mengi, na kwa jina lake YESU (Matendo 2:38).

Hivyo Mgeukie leo YESU. Kwasababu yeye ndiye Mungu aliyemchagua na kumtia mafuta kwa UKOMBOZI, hakuna mwingine zaidi yake, kila kitu kimewekwa chini yake, na yeye ndiye atakayeihukumu hii dunia mfano wa Huhu. Ili ayafanye mambo yote kuwa mapya baada yake, ili siku ile ATUFARIJI tukafurahi naye katika mbingu mpya na chini mpya ambayo itashuka hapa duniani, mahali ambapo tutakuwa na raha milele, mahali ambapo kutakuwa hakuna magonjwa wala njaa, wala shida, wala mauti,wala dhiki, wala maadui..Mahali ambapo tutafutwa machozi yetu na tutakula mema yote ya nchi Bwana aliyotuandalia zaidi hata ya ilivyokuwa pale Edeni.

Bwana akubariki sana.

Tafadhali washirikishe na wengine mambo haya, na Bwana atakubariki.

No comments:

Post a Comment