"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Tuesday, November 27, 2018

UPENDO

Upendo ni kiini cha ukristo na pia ni KILELE CHA UKRISTO. Mungu hajaufunua Upendo kama moja ya tabia zake, kwa mfano hajasema mahali popote kuwa yeye ni mwenye upendo kama anavyosema juu ya tabia zake nyingine alizonazo, mfano Mungu muweza yote, au Mungu mwenye nguvu, Mungu wa rehema, au Mungu mwenye mamlaka n.k. hapana bali anapofikia kwenye suala la Upendo anasema “MIMI NI UPENDO”, yaani yeye kama alivyo ni UPENDO na si kama moja ya tabia zake..Hivyo hulifanya hili Neno upendo katika mtazamo wa rohoni kuwa na tafsiri pana zaidi kuliko sisi tunavyoweza kulichukulia.

1Yohana 4:16
“Nasi tumelifahamu pendo alilo nalo Mungu kwetu sisi, na kuliamini. MUNGU NI UPENDO, naye akaaye katika pendo, hukaa ndani ya Mungu, na Mungu hukaa ndani yake”.


Upendo ule unaozungumziwa kwenye biblia sio upendo wa kusema nakupenda kimdomo na wala si upendo wa kihisia bali ni upendo UNAOTENGENEZWA ndani ya moyo wa mtu, kwasababu chanzo chake si mwanadamu bali ni Mungu. Hivyo sio wa kutokea tu ndani ya siku moja, pale mtu anapozaliwa mara ya pili. Na ndio maana ukisoma katika kitabu cha 2Petro 1:1-10, utaona kuwa Upendo unachukua hatua ya mwisho kabisa baada ya mtu kupita hatua zote sita za kuelekea ukamilifu, upendo ndio unatokea mwishoni,

2 Petro 1: 5 “Naam, na kwa sababu iyo hiyo mkijitahidi sana kwa upande wenu, katika imani yenu tieni na WEMA, na katika wema wenu MAARIFA,
6 na katika maarifa yenu KIASI, na katika kiasi chenu SABURI, na katika saburi yenu UTAUWA,
7 na katika utauwa wenu UPENDANO WA NDUGU, na katika upendano wa ndugu, UPENDO.
8 Maana mambo hayo yakiwa kwenu na kujaa tele, yawafanya ninyi kuwa si wavivu wala si watu wasio na matunda, kwa kumjua Bwana wetu Yesu Kristo”
.


huwezi kurukia hatua ya mwisho ukasema kuwa unao upendo wakati hatua zile 6 bado hujazikamilisha ndani yako.Maana ile hatua ya mwisho ni Mungu mwenyewe. Hivyo ili kufikia hatua hiyo ya juu kabisa kileleni Mungu alipo, mahali ambapo utakuwa karibu sana na Mungu katika roho kuliko pengine popote ni hapo utakapoufikia Upendo wa Mungu ndani yako. Na hivyo ili kufika hapo inahitaji BIDII na si vinginevyo. Hiyo haiji kwa kuombewa wala kwa kuwekewa mikono. Biblia inasema ni kwa jitihada na bidii. Kama inavyosema:

1Petro 1: 1.22 “Mkiisha kujitakasa roho zenu kwa kuitii kweli, hata kuufikilia upendano wa ndugu usio na unafiki, basi JITAHIDINI kupendana kwa moyo.  Kwa kuwa mmezaliwa mara ya pili; si kwa mbegu iharibikayo, bali kwa ile isiyoharibika; kwa neno la Mungu lenye uzima, lidumulo hata milele”.


“Zaidi ya yote iweni na JUHUDI NYINGI katika kupendana; kwa sababu upendano husitiri wingi wa dhambi.” (1Petro 4:8).

Unaona biblia inasema pia katika:

1Yohana 4:20. “Mtu akisema, Nampenda Mungu, naye anamchukia ndugu yake, ni mwongo; kwa maana asiyempenda ndugu yake ambaye amemwona, hawezi kumpenda Mungu ambaye hakumwona. NA AMRI HII TUMEPEWA NA YEYE, ya kwamba yeye ampendaye Mungu, ampende na ndugu yake”.


Pamoja na hayo biblia inatuambia hata tukiwa na uwezo wa kuzungumza lugha za malaika hata tukiwa na imani timilifu ya kuweza kuhamisha milima, hata tukitoa mali zetu kuwapa maskini, hata tukitoa miili yetu iungue kwa moto lakini kama hatutakuwa na huo Upendo unaozungumziwa kwenye Neno la Mungu..hatuwezi kuwa kitu mbele za Mungu.

Ukiangalia hayo kwa ukaribu utaona upendo ni kitu cha utofauti na kile tunachokidhania Upendo wa Mungu ni jambo linalojengeka ndani ya mtu katika kipindi cha muda, hivyo inahitaji bidii ya kulipalilia ili liumbike, vinginevyo itakuwa ni ngumu kulifikia..Embu turudi pale kwenye 1Wakoritho 13 tuone biblia inasema nini juu ya Upendo mkamilifu..

“4 Upendo HUVUMILIA, HUFADHILI; UPENDO HAUHUSUDU; upendo HAUTAKABARI; HAUJIVUNI;
5 HAUKOSI KUWA NA ADABU; HAUTAFUTI MAMBO YAKE; HAUONI UCHUNGU; HAUHESABU MABAYA;
6 HAUFURAHII UDHALIMU, BALI HUFURAHI PAMOJA NA KWELI;
7 HUVUMILIA YOTE; HUAMINI YOTE; HUTUMAINI YOTE; HUSTAHIMILI YOTE.
8 Upendo HAUPUNGUI NENO WAKATI WO WOTE; bali ukiwapo unabii utabatilika; zikiwapo lugha, zitakoma; yakiwapo maarifa, yatabatilika”.


Unaona unaweza kutoa mali zako zote kuwapa maskini, lakini je! uvumilivu upo ndani yako?, Tumaini lipo ndani yako? kustahimili mabaya kwa ajili ya Kristo kupo ndani yako? Adabu njema ipo ndani yako? majivuno yameondoka ndani yako?. Kuamini yote unayoambiwa na Mungu kupo ndani yako,? Unaweza ukasaidia maskini sana lakini je! Uchungu upo ndani yako? Unaweza ukawa na karama ya kunena kwa lugha na kuona maono, na kutabiri, lakini je! Unahesabu mabaya kwa ndugu yako n.k??.

Sasa hivi vyote vikiungana na kuonekana ndani ya mtu ndio Neno Upendo wa Mungu linaumbika. Lakini huwezi kusema wewe hauhusudu kama hutaonyesha bidii ya kutokufanya hivyo..kama wewe ni wa kukaa kuwazungumzia vibaya wengine, na bado ni mkristo, hata kama utakuwa una karama kubwa kiasi gani basi mbele za Mungu wewe si kitu ndivyo biblia inavyosema. Kama hutaonyesha bidii katika uvumilivu kwenye mambo yote kwanza kwa ajili ya imani yako na kwa ajili ya kudhulumiwa au kuonewa huwezi kusema upendo wa Mungu upo ndani yako.

Hivyo ni wajibu wetu sisi sote (mimi na wewe), kuonyesha bidii kuutafuta upendo kwasababu ndio kifungo cha ukamilifu, ndio kilele cha ukristo wetu. Na hii inakuja Kwa kuvitunza kwa bidii hivyo vigezo vilivyotelewa hapo juu, mpaka kufikia hatua ya vyenyewe kujengeka ndani yetu na kuwa ni TABIA yetu. Sasa tukishafikia hatua hiyo biblia inasema hapo sisi ni watu wakamilifu sana.

Wakolosai 3:14 “Zaidi ya hayo yote jivikeni upendo, ndio kifungo cha ukamilifu”.


Tunapaswa tuyatawale maisha yetu kwa kanuni za Neno la Mungu, kwa bidii, kuonyesha zile tabia zinazoambatana na Upendo wake. Kila siku tukiyarekebisha maisha yetu, na kutengeneza upya pale tulipojikwaa jana, ikiwa tulishindwa kuwavumilia ndugu zetu au marafiki zetu kwa mabaya waliyotutenda na kukataa kuwasamehe, ni wakati wa kujirekebisha, kufanya bidii kusamehe, ikiwa tulikuwa tunatafuta mambo yetu wenyewe, tunapaswa tufanye bidii kubadilika, ikiwa tulikuwa hatufadhili tunapaswa pia tufanye bidii kufadhili, na kuwa na adabu ili tuonekane kuwa ni watoto wa Mungu. Na kufikia hatua ya kupendana sisi kwa sisi pasipo unafki,

1Yohana 4: 12 “Hakuna mtu aliyemwona Mungu wakati wo wote.


Tukipendana, Mungu hukaa ndani yetu, NA PENDO LAKE LIMEKAMILIKA NDANI YETU”.

Hivyo sisi sote tuzidi kuonyesha bidii katika kupendana mpaka tumfikie Bwana mwenyewe ambaye ni UPENDO.Kama Bwana wetu Yesu alivyofikia.

Ubarikiwe sana.

No comments:

Post a Comment