"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Wednesday, February 27, 2019

SIKU YA HASIRA YA BWANA.


Mtu ambaye ni mwepesi kuudhiwa, au mwepesi kulia, au mwepesi kukasirishwa basi mtu huyo mara nyingi anakuwa pia ni mwepesi kusahau makosa, au mwepesi kufurahi au mwepesi kucheka..Lakini mtu ambaye ni mzito kuudhika pale anapoudhiwa, au kukasirika au kulia au kuwaka hasira, basi mtu huyo vile vile mpaka afikie hatua ya kukasirishwa na baadhi ya mambo basi ujue kuwa itachukua muda sana kuituliza ghadhabu yake au hasira yake.

Tuchukulie tu mfano mtoto mdogo, kama ukimtazama kwa siku anaweza kulia hata mara tano au sita, utakuta kinachomliza ni vitu vidogo vidogo tu visivyo na maana, lakini mtu huyo huyo dakika chake mbeleni utakuta ameshasahau anacheza na wewe kana kwamba hujawahi kumuudhi kabisa..Lakini tuje kwa mtu mzima, anaweza asidondoshe chozi kwa hata kwa mamiaka, lakini siku ukimkuta analia basi ujue kuna jambo zito, tena zito sana tena sio jepesi hata kidogo, pengine utakuta ni msiba au kaumizwa sana,au kajeruhiwa sana, na hivyo mpaka hali hiyo imtokea ndani yake, basi haiwezi kuwa ni kitendo cha dakika chache kuondoka, pengine itamgharimu miezi au miaka ndipo iishe kabisa.

Hali kadhalika biblia imetuweka wazi kabisa, kuhusu hali ya Mungu wetu wa mbinguni tunaye mwabudu siku zote, yeye ni Mungu mvumilivu sana, ni mwingi wa rehema, ni mnyenyekevu, ni mwenye neema, ni mwingi wa huruma, haoni hasira haraka,..Na ni kweli ndivyo alivyo hata sisi wenyewe tunalishuhudia leo hilo pale tunapoona watu tunaona wanatembea barabarani uchi, watu wanamtukana Mungu hadharani lakini hasemi chochote, watu wanawachinja wenzao kama wanyama bila huruma na Mungu hafanyi lolote, watu wanawakata viungo watoto wadogo wasio na hatia wakiwa hai, na kuchukua viungo vya maalbino, wengine wanawachuna ngozi ili kwenda kuuza kwa waganga, mpaka tunajiuliza hivi Mungu hayaoni haya yote? Mbona hachukui hatua yoyote kali..Ingekuwa ni wewe au mimi ni Mungu ni wazi kuwa hakuna hata mmoja angesalia tungeshawateketeza wote.Lakini kwa Mungu haipo hivyo yeye alisema “..
 
Bwana si mwepesi wa hasira, (Nahumu 3:1)Ni mpole wa Hasira, mwingi wa rehema (Hesabu 14:8)
Pia Kutoka 34: 6 "…., Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli; 7 mwenye kuwaonea huruma watu elfu elfu, mwenye kusamehe uovu na makosa na dhambi;.."
Na pia Daudi anashuhudia hilo na kusema “Bwana ana fadhili, ni mwingi wa huruma, Si mwepesi wa hasira, ni mwingi wa rehema, Zaburi 145:8” Na  ukisoma pia Yona 4:2 na Nehemia 9:17..utathibitisha jambo hilo hilo.

Unaona hiyo ndio sifa yake kuu.. Lakini yeye kuonyesha rehema zake hata kwa waovu sio kwamba anapenda kuendelea kuwaona wanafanya mambo yao maovu, bali kinyume chake anataka wote wafikie toba, na ndio maana kila siku anawahubiria watubu, Lakini wasipotaka kutubu, kama tulivyoona kuwa mtu Yule ambaye si mwepesi kuudhika,ikifika siku ameudhika basi jua kuwa ghadhabu yake haiishi leo wala kesho, ndivyo ilivyo kwa Mungu ukali wa hasira yake hakuna atakayeweza kuuzima, si kwa toba wala kwa kulia siku ile itakapofika..

Watu wa kipindi cha Nuhu walipuuzia sana uvumilivu wa Mungu kwao, walihuburiwa injili kwa miaka mingi, lakini waliona mbona hakuna dalili yoyote ya kuadhibiwa, kama vile Mungu hayupo, Mungu hawezi kuangamiza dunia yote na watoto ndani yake,ndivyo walivyokuwa wanajifariji, Nuhu alionekana kama kichaa anacheza lakini siku ile walipoingia kwenye safina, ndipo waovu walipojua kweli hasira ya Mungu ni kali…watu 8 tu kati ya mabilioni ya watu waliokuwa wanaishi duniani ndio waliopona…Vivyo hivyo ilikuwa katika siku za Lutu, na ndivyo itakavyokuwa katika SIKU ILE YA HASIRA YA BWANA kama Bwana alivyoifananisha siku ile na hizo, ambayo hiyo ipo karibuni sana kutokea. Kutakuwa na kulia lakini Mungu hatasikia, kutakuwa na maombolezo lakini Mungu hataokoa, utasema ni wapi tena jambo hilo lilishawahi kutokea kwenye Maandiko,? Wakati wana wa Israeli walipoonywa kwa mamia ya miaka waache maovu na wamgeukie Mungu, lakini hawakutaka, Bwana aliwaonya waache maovu wasije wakapelekwa utumwani hawakusikia, wakatenda maovu mpaka ikafikia hatua ya Mungu kutokusamehe tena..kikombe cha ghadhabu ya Mungu kilikuwa kimejaa juu yao, ulinzi wa kiMungu ukaondoka juu yao, Nebukadneza akaja akawachinja watu mbele ya macho kama kuku, na waliosalia akawapeleka utumwani Babeli.. Tunasoma hayo katika.
 2 Nyakati 36: 11 “Sedekia alikuwa na umri wa miaka ishirini na mmoja, alipoanza kutawala; akatawala katika Yerusalemu miaka kumi na mmoja;
12 akafanya yaliyo mabaya machoni pa Bwana, Mungu wake; wala hakujinyenyekesha mbele ya Yeremia nabii aliponena kwa kinywa cha Bwana.
13 Tena akamwasi mfalme Nebukadreza, aliyemwapisha kwa Mungu; lakini akajifanyia shingo ngumu, akajitia moyo nguvu asimgeukie Bwana, Mungu wa Israeli.
14 Na zaidi ya hayo wakuu wote wa makuhani, na watu, wakakosa mno sawasawa na machukizo yote ya mataifa; wakainajisi nyumba ya Bwana aliyoitakasa katika Yerusalemu.
15 Naye Bwana, Mungu wa baba zao, akatuma kwao kwa mikono ya wajumbe wake, akiondoka mapema, na kutuma; kwa sababu aliwahurumia watu wake, na makao yake;
16 lakini waliwadhihaki wajumbe wa Mungu, na kuyadharau maneno yake, na kuwacheka manabii wake, hata ilipozidi ghadhabu ya Bwana juu ya watu wake, hata kusiwe na kuponya.
17 Kwa hiyo akaleta juu yao mfalme wa Wakaldayo, aliyewaua vijana wao kwa upanga nyumbani mwa patakatifu pao, asiwahurumie kijana wala mwanamwali, mzee wala mkongwe; akawatia wote mkononi mwake”.
Soma tena mstari wa 15 na wa 16…inasema.. “Bwana aliwatumia wajumbe wake, kwasababu aliwahurumia lakini wakawacheka na kuwadhihaki, hata ilipozidi ghadhabu HATA KUSIWE NA KUPONYA”..Unaona kuna hatua inafika kutakawa HAKUNA KUPONYWA TENA!! Yaliyotokea yametokea, hayawezi kubadilika tena wala kubadilishwa.

Ndugu usidhani ukiachwa sasa kwenye UNYAKUO utakuwa na nafasi ya pili mbele za Mungu, kwamba utatubu na Mungu atakuhurumia, Fahamu nafasi ni moja tu nayo ni kwa Njia ya YESU KRISTO peke yake na sio kwa njia yako, ingekuwepo ipo nafasi nyingine, Yesu asingesema mtu haji kwa Baba isipokuwa kwa njia yangu mimi, badala yake angesema mtu haji kwa Baba isipokuwa kwa njia yangu au yako..Hautafika mbinguni ndugu kama chujio la UNYAKUO litakupita.. Na wote watakaobaki hakuta kuwa na lingine lililosalia kwao isipokuwa kukutana na ghadhabu ya hasira ya Mungu, na hiyo haina lengo lingine zaidi ya kuwaharibu watu wote waovu ambao, walikataa neema, walikataa kuishi maisha ambayo Mungu alikusudia kila mwanadamu ayaishi, ni mapigo ambayo hata mtu aombolezeje hawezi kusikiwa.

Kumbuka hiyo ni tofauti na dhiki ya mpinga-kristo, siku ya Bwana ni tofauti kabisa, ni wakati Mungu aliojitengea kujilipizia kisasi cha hasira yake. Usitamani uwepo huo wakati ukadhani kuwa utastahimili, au utaokoka..
Yoeli 2: kwa kuwa siku ya Bwana ni kuu, yenye kitisho sana; naye ni nani awezaye KUISTAHIMILI.
Bwana anasema tena Siku hiyo watu duniani wataadimika kuliko DHAHABU, kumbuka sio kama dhahabu, hapana! bali kuliko dhahabu…Tafakari hilo neno tunajua dhahabu ni jamii ya mawe, lakini upatikanaji wake sio wa kwenda tu nje na kuikota kama kokoto, ndivyo itakavyokuwa siku hiyo watu watakuwa wachache sana kama vile dhahabu ilivyoadimu, si ajabu hili taifa lote la Tanzania watasalia watu 2 au 3 tu au asisalie mtu kabisa…wakati wa gharika watu waliadimika kama dhahabu, alisalia Nuhu tu wanawe watatu na wake zao.

Isaya 13: 6 “Pigeni kelele za hofu; maana siku ya Bwana i karibu; itanyesha kama maangamizi yatokayo kwa Mwenyezi Mungu.
7 Kwa sababu hiyo mikono yote italegea, na moyo wa kila mtu utayeyuka.
8 Nao watafadhaika; watashikwa na utungu na maumivu; watakuwa na utungu kama mwanamke aliye karibu na kuzaa; watakodoleana macho; nyuso zao zitakuwa ni nyuso za moto.
9 Tazama, siku ya Bwana inakuja, SIKU KALI, YA HASIRA NA GHADHABU KUU, ili iifanye nchi kuwa ukiwa, na kuwaharibu watu wake, wenye dhambi, wasikae ndani yake.
10 Maana nyota za mbinguni na matangamano havitatoa nuru yake; jua litatiwa giza wakati wa kucha kwake, na mwezi utaacha nuru yake isiangaze.
11 Nami nitaadhibu ulimwengu kwa sababu ya ubaya wake, na wenye dhambi kwa sababu ya hatia yao; nami nitaikomesha fahari yao wenye kiburi; nami nitayaangusha chini majivuno yao walio wakali;
12 NITAFANYA WANADAMU KUADIMIKA KULIKO DHAHABU SAFI, na watu kuliko dhahabu ya Ofiri.
13 Kwa hiyo nitazitetemesha mbingu, na dunia itatikiswa itoke katika mahali pake, kwa sababu ya ghadhabu ya Bwana wa majeshi, na kwa sababu ya siku ya hasira yake kali.
Adhabu hiyo itakuwa ndani ya yale mapigo ya vitasa 7. (Yohana16 :1-21). Embu tazama kwa ufupi yatakayo tokea.

Ufunuo 16:1 “Nikasikia sauti kuu kutoka hekaluni, ikiwaambia wale malaika saba, Enendeni, mkavimimine vile vitasa saba vya ghadhabu ya Mungu juu ya nchi.
2 Akaenda huyo wa kwanza, akakimimina kitasa chake juu ya nchi; pakawa na jipu baya, bovu, juu ya wale watu wenye chapa ya huyo mnyama, na wale wenye kuisujudia sanamu yake.
3 Na huyo wa pili akakimimina kitasa chake juu ya bahari, ikawa damu kama damu ya mfu, na vitu vyote vyenye roho ya uhai katika bahari vikafa.
4 Na huyo wa tatu akakimimina kitasa chake juu ya mito na chemchemi za maji; zikawa damu.
5 Nami nikamsikia malaika wa maji akisema, Wewe u mwenye haki, uliyeko na uliyekuwako, Mtakatifu, kwa kuwa umehukumu hivi;
6 kwa kuwa walimwaga damu ya watakatifu na ya manabii, nawe umewapa damu wainywe; nao wamestahili.
7 Nikaisikia hiyo madhabahu ikisema, Naam, Bwana Mungu Mwenyezi, ni za kweli, na za haki, hukumu zako.
8 Na huyo wa nne akakimimina kitasa chake juu ya jua, nalo likapewa kuwaunguza wanadamu kwa moto.
9 Wanadamu wakaunguzwa maunguzo makubwa, nao wakalitukana jina la Mungu aliye na mamlaka juu yamapigo hayo; wala hawakutubu wala kumpa utukufu.1
10 Na huyo wa tano akakimimina kitasa chake juu ya kiti cha enzi cha yule mnyama; ufalme wake ukatiwa giza; wakatafuna ndimi zao kwa sababu ya maumivu,
11 wakamtukana Mungu wa mbingu kwa sababu ya maumivu yao, na kwa sababu ya majipu yao; wala hawakuyatubia matendo yao.
12 Na huyo wa sita akakimimina kitasa chake juu ya mto ule mkubwa Frati; maji yake yakakauka, ili njia itengenezwe kwa wafalme watokao katika maawio ya jua.
13 Nikaona roho tatu za uchafu zilizofanana na vyura, zikitoka katika kinywa cha yule joka, na katika kinywa cha yule mnyama, na katika kinywa cha yule nabii wa uongo.
14 Hizo ndizo roho za mashetani, zifanyazo ishara, zitokazo na kuwaendea wafalme wa ulimwengu wote kuwakusanya kwa vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi.
15 (Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake.)
16 Wakawakusanya hata mahali paitwapo kwa Kiebrania, Har-Magedoni.1
17 Na huyo wa saba akakimimina kitasa chake juu ya anga. Sauti kuu ikatoka katika hekalu, katika kile kiti cha enzi, ikisema, Imekwisha kuwa.
18 Pakawa na umeme na sauti na radi; na palikuwa na tetemeko la nchi kubwa, ambalo tangu wanadamu kuwako juu ya nchi hapakuwa namna ile, jinsi lilivyokuwa kubwa tetemeko hilo.
19 Na mji ule mkuu ukagawanyikana mafungu matatu, na miji ya mataifa ikaanguka; na Babeli ule mkuu ukakumbukwa mbele za Mungu, kupewa kikombe cha mvinyo ya ghadhabu ya hasira yake.
20 Kila kisiwa kikakimbia, wala milima haikuonekana tena.
21 Na mvua ya mawe kubwa sana, ya mawe mazito kama talanta, ikashuka kutoka mbinguni juu ya wanadamu. Wanadamu wakamtukana Mungu kwa sababu ya lile pigo la mvua ya mawe; kwa maana pigo lake ni kubwa mno.

(Ikiwa utahitaji kufahamu kwa urefu juu ya vitasa 7 nitumie ujumbe inbox, nitukutumie uchambuzi wake wote.)…Sasa baada ya hayo mapigo kuisha kitakachofuata ni Hukumu kisha ziwa la moto.

Lakini hayo ni machache kati ya mengi yatakaowakuta wale wote ambao watakosa UNYAKUO sasa ambapo dalili zote zinaonyesha kuwa kizazi chetu hichi ndio kile Yesu alichokizungumzia kuwa hayo yote yatatimia..Ni saa gani hii tunaishi?..Kwanini huyathamini maisha yako ya milele?..Kwanini unaipuuzia hiyo neema iliyo juu yako? Unazini lakini Mungu hakusemeshi chochote, unatazama pornography kwa siri, lakini Mungu hakuadhibu kwa lolote, unafanya mambo machafu lakini Mungu kama vile hakuoni..sio kwamba anapendezwa na wewe au kwamba wewe ni mtu pekee sana kwake, na ndio maana hayakukuti mabaya sasa..

Lakini fahamu si mwepesi wa hasira ni Mwingi wa hasira..uvumilivu wake ndio unaokuvuta utubu..
2Petro 3:8 “Lakini, wapenzi, msilisahau neno hili, kwamba kwa Bwana siku moja ni kama miaka elfu, na miaka elfu ni kama siku moja.
9 Bwana hakawii kuitimiza ahadi yake, kama wengine wanavyokudhani kukawia, BALI HUVUMILIA KWENU, MAANA HAPENDI MTU YE YOTE APOTEE, BALI WOTE WAFIKILIE TOBA.
10 Lakini siku ya Bwana itakuja kama mwivi; katika siku hiyo mbingu zitatoweka kwa mshindo mkuu, na viumbe vya asili vitaunguzwa, na kufumuliwa, na nchi na kazi zilizomo ndani yake zitateketea.
11 Basi, kwa kuwa vitu hivi vyote vitafumuliwa hivyo, imewapasa ninyi kuwa watu wa tabia gani katika mwenendo mtakatifu na utauwa,”
Usipotubu leo upo wakati mbaya unakusubiria mbeleni usiokuwa na msamaha. Leo hii ukiwa tayari kuyakabidhi maisha yako kwa Bwana kwa kumaanisha kabisa, na sio nusu nusu, mguu mmoja huku na mwingine kule atakusamehe kabisa na kuyafuta makosa yako yote, kwasababu hicho ndicho anachokitafuta kwako.

Na ndio maana anasema:

Sefania 2: 3 “Mtafuteni Bwana, enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia, ninyi mliozitenda hukumu zake; itafuteni haki, utafuteni unyenyekevu; HUENDA MTAFICHWA KATIKA SIKU YA HASIRA YA BWANA”.

Uamuzi ni wako, lakini maombi yangu ni leo utubu ukabatizwe katika ubatizo sahihi wa maji mengi na kwa jina la YESU KRISTO kwa ajili ya ondoleo la dhambi zako.Kisha baada ya hapo utakuwa umezaliwa mara ya pili, kwa Roho Mtakatifu atakayeingia ndani yako”

SIRI YA MUNGU.


Shalom Mwana wa Mungu, karibu tujifunze biblia, chakula cha uzima, kitupacho afya rohoni, leo kwa Neema za Bwana tutajifunza kwa ufupi, juu ya SIRI YA MUNGU.
Biblia imetaja sehemu kadha wa kadha juu ya Siri ya Mungu, na leo tutajifunza hii siri ya Mungu ni ipi.
Warumi 16: 25 “Sasa na atukuzwe yeye awezaye kuwafanya imara, sawasawa na injili yangu na kwa kuhubiriwa kwake Yesu Kristo, sawasawa na ufunuo wa ile SIRI iliyositirika tangu zamani za milele”.
Unaona hapo, biblia imetaja kuwa ipo SIRI iliyokuwa imesitirika tangu zamani za milele.
Sasa kabla ya kwenda kujifunza hiyo siri ni ipi, ni vizuri kwanza tukaelewa neno SIRI lina maana gani kama lilivyotafsiriwa katika biblia yetu hii ya Kiswahili, Kumbuka lugha yetu ya Kiswahili haijajitosheleza kwa maneno mengi, kwamfano yapo maneno katika lugha ya kiingereza au kigiriki ambayo ukiyaleta katika lugha yetu ya Kiswahili yanakosa tafsiri. Na pia yapo maneno yetu ya lugha ya Kiswahili ambayo ukiyapeleka katika lugha ya kiingereza yanakosa tafsiri, kwa mfano neno “shikamoo” halina tafsiri kwa kiingereza. Lakini pia yapo maneno ya kiingereza yenye tafsiri zinazokaribiana sana hivyo yakiletwa katika lugha yetu ya Kiswahili yanatumia tafsiri moja, kwamfano neno la kingereza “mouse” na “rat” tafsiri yake kwa kiswahili ni moja tu ambayo ni panya, hali kadhalika maneno mengine kama “rabbit” na “hare” yote kwa Kiswahili tafsiri yake ni “sungura”

Lakini pia kuna maneno mawili ya kiingereza yenye maana zinazokaribiana sana lakini hayafanani..na maneno hayo ni “Secret” na “mystery”…yote tukiyaleta katika lugha yetu ya Kiswahili yana tafsiri moja yaani “SIRI” lakini yana maana mbili tofauti.
“Secret” ni neno la kiingereza lenye maana ya “kipande cha taarifa ambacho kinajulikana na mtu mmoja au zaidi ya mmoja, na kimehifadhiwa kisijulikane na watu wengine zaidi ya hao wanaokijua”…kwamfano wahalifu wawili wanapopanga njama ya kuvamia mafali fulani hiyo njama ni “siri”, au vikundi fulani vya upelelezi huwa vinafanya kazi zao katika siri, ikiwa na maana vina baadhi ya taarifa ambazo ni wao tu wanaozijua na hawampi mtu mwingine yeyote taarifa hizo, (wanafanya kazi zao katika siri).

Lakini tukirudi kwenye neno la pili la kiingereza linaloitwa “mystery” ambalo kwa Kiswahili limetafsiriwa hivyo hivyo “siri” lenyewe lina maana tofauti kidogo, neno hili mystery tafsiri yake halisi ni hii “ni taarifa ambazo hazijulikani na mtu hata mmoja, hazijulikani chanzo chake, wala sababu ya jambo hilo”..kwamfano mtu anapowasha taa na giza kuondoka, ulishawahi kujiuliza lile giza linakwenda wapi? Hakuna mtu anayejua, wala huwezi kupata jibu la hilo swali kwa mtu yeyote Yule, kwahiyo hiyo inajulikana kama mistery “Mystery”, ambapo kwa Kiswahili tunaweza kusema ni siri ya ndani sana isiyoweza kueleweka wala kuchunguzika.
Biblia inasema katika: 

Ayubu 38: 19“Iko wapi njia ya kuyafikia makao ya nuru? Na giza pia, mahali pake ni wapi? 20 Upate kuipeleka hata mpaka wake, Upate kuelewa na mapito ya kuiendea nyumba yake?”
 
Ayubu 38: 24 “Je! Nuru hutengwa kwa njia gani, Au upepo wa mashariki hutawanywaje juu ya nchi?”
 
Hizo zote ni mystery au siri za ndani zisizoelezeka. Hali kadhalika jinsi mtoto anavyoumbika katika tumbo la mwanamke, hakuna ajuaye ni nani alipeleka mifupa migumu kule, ni nani aliingiza nywele, n.k. vyote hivyo vinabakia katika siri kuu sana (Mysteries), zisizojulikana na kushangaza watu.

Sasa baada ya kuelewa hayo, tukirudi kwenye biblia kuna kitu kinachoitwa SIRI YA MUNGU, kama tulivyotangulia kusema…sasa hiyo siri inayozungumziwa hapo sio siri yenye tafsiri ile ya kwanza “secret” bali ni siri yenye tafsiri ile ya pili “mystery”, Kwahiyo siri ya Mungu haikuwa ni kipande cha taarifa fulani kilichojificha kilichojulikana na baadhi ya watu wachache tu, na kwamba kisingepaswa kijulikane na watu wengine, hapana badala yake bali siri ya Mungu ilikuwa ni taarifa au jambo ambalo lililokuwa halijulikani na mtu awaye yeyote Yule hata MALAIKA wa mbinguni, walikuwa hawalijui wala hawalielewi, hakuna taarifa zozote kuhusiana na hilo jambo, mtu anaweza akakisia tu lakini asiwe na taarifa zozote sahihi kuhusiana na hilo jambo, kama tu vile tusivyoelewa giza huwa linakwenda wapi pindi mwanga unapokuja, na linatokea wapi pindi mwanga unapoondoka..wala hakuna mtu yeyote anaweza kutupa majibu ya hayo maswali, kadhalika na siri ya Mungu ndio ilikuwa hivyo hivyo(ilikuwa ni mystery na sio secret).
 
Sasa hii SIRI ya ajabu ya Mungu ilikuwa ni ipi?

Mtume Paulo alitoa majibu ya swali hilo kwa uwezo wa Roho.

Wakolosai 1:26 “SIRI ile iliyofichwa tangu zamani zote na tangu vizazi vyote, bali sasa imefunuliwa kwa watakatifu wake; 27 ambao Mungu alipenda kuwajulisha jinsi ulivyo utajiri wa utukufu wa SIRI HII KATIKA MATAIFA, nao ni KRISTO NDANI YENU, TUMAINI LA UTUKUFU 28 ambaye sisi tunamhubiri habari zake tukimwonya kila mtu, na kumfundisha kila mtu katika hekima yote, tupate kumleta kila mtu mtimilifu katika Kristo”.

Unaona hapo, biblia inasema siri ambayo ilikuwa imefichwa tangu vizazi vyote, ikiwa na maana hakuna mtu aliyekuwa anaijua, lakini ilifunuliwa zamani za mitume, na siri hiyo haikuwa nyingine zaidi ya KRISTO YESU KUINGIA ndani yetu sisi watu wa MATAIFA. Haleluyaa!!

Tangu zamani yote, hakuna mtu angeweza kudhania kuwa sisi watu wa mataifa tungekuja siku moja kuwa wana wa Mungu, sisi tuliokuwa tunaitwa najisi, watu tuliokuwa mbali na Mungu, hakuna mtu angetegemea siku moja Wana wa Farao waliowatesa wana wa Israeli kwamba wangekuja kuitwa wana wa Mungu aliye juu, hakuna mtu angedhania kuwa wafilisti watu waliokuwa wanaitwa wasiotahiriwa kwamba siku moja watakuja kuitwa wana wa Mungu aliye juu, hakuna mtu angekuja kujua kuwa wamoabi waliowalaani wana wa Israeli wakati wanaelekea nchi ya ahadi, siku moja watakuja kuitwa wabarikiwa wateule wa Mungu aliye juu kwa kupitia Yesu Kristo, Ingekuwaje kuwaje kwanza ni sawasawa na sasahivi mtu akwambie kuna wakati utafika wachina wote wataitwa wamasai tena wamasai wa damu kabisa, ni jambo lisilosadikika. hakika hiyo ilikuwa ni siri ya ajabu ambayo isingeweza kudhaniwa na mtu yeyote, ni siri ambayo hata malaika walikuwa hawaijui. Lakini ilikuja kufunuliwa siku za mwisho.

Hakuna mtu angeweza kudhania kuwa MASIHI ambaye ametabiriwa kuja kuwaokoa wana wa Israeli peke yao, angekuja kwanza kuanza wokovu kwa watu wa mataifa, wanaoabudu sanamu, hakuna mtu au malaika angeweza kudhania kuwa siku moja Roho mwenyewe wa Mungu atakaa ndani ya watu wa mataifa. Hata malaika wa mbinguni hawakujua hiyo neema imetoka wapi, kama vile tusivyojua giza chanzo chake ni wapi, hiyo ni mystery.

Kwahiyo YESU KRISTO, kuja kutuokoa sisi watu wa MATAIFA hiyo ndiyo ilikuwa SIRI YA MUNGU, iliyofichika tangu zamani za milele, hata Musa alikuwa hajui kwamba siku moja Uzao wa Farao utamwabudu Mungu wa Israeli kupitia Masihi, hata Eliya alikuwa hajui kwamba siku moja wale alioomba moto ushuke juu yao watoto wao watakuja kumjua Mungu wa kweli na kupata kibali mbele za Mungu, Hata Daudi hakujua kwamba wale aliokuwa anawaimbia maadui maadui siku moja watakuja kuwa marafiki wa karibu wa Mungu kupitia BWANA WA UTUKUFU YESU KRISTO.
Waefeso 3:1 “Kwa sababu hiyo mimi Paulo ni mfungwa wake Kristo Yesu kwa ajili yenu ninyi Mataifa;
2 ikiwa mmesikia habari ya uwakili wa neema ya Mungu niliyopewa kwa ajili yenu;
3 ya kwamba kwa kufunuliwa nalijulishwa SIRI HIYO, kama nilivyotangulia kuandika kwa maneno machache
4 Kwa hayo, myasomapo, mtaweza kuutambua ufahamu wangu katika SIRI YAKE KRISTO.
5 SIRI HIYO HAWAKUJULISHWA WANADAMU KATIKA VIZAZI VINGINE; kama walivyofunuliwa mitume wake watakatifu na manabii zamani hizi katika Roho;
6 YA KWAMBA MATAIFA NI WARITHI PAMOJA NASI WA URITHI MMOJA, na wa mwili mmoja, NA WASHIRIKI PAMOJA NASI WA AHADI YAKE ILIYO KATIKA KRISTO YESU KWA NJIA YA INJILI”
7 Injili hiyo ambayo nalifanywa mhudumu wake, kwa kadiri ya kipawa cha neema ya Mungu niliyopewa kwa kadiri ya utendaji wa uweza wake.
8 Mimi, niliye mdogo kuliko yeye aliye mdogo wa watakatifu wote, nalipewa neema hii ya kuwahubiri Mataifa utajiri wake Kristo usiopimika;
9 NA KUWAANGAZA WATU WOTE WAJUE HABARI ZA MADARAKA YA SIRI HIYO, ambayo tangu zamani zote ilisitirika katika Mungu aliyeviumba vitu vyote;
10 ili sasa, kwa njia ya kanisa, hekima ya Mungu iliyo ya namna nyingi ijulikane na falme na mamlaka katika ulimwengu wa roho;
11 kwa kadiri ya kusudi la milele alilolikusudia katika Kristo Yesu Bwana wetu”.
Mstari wa 9 unasema “NA KUWAANGAZA WATU WOTE WAJUE HABARI ZA MADARAKA YA SIRI HIYO”.
Ndugu unayesoma ujumbe huu, ukimjua Yesu Kristo, kwa mapana haya au zaidi ya haya, utaogopa!! Utajua ni jinsi gani hatukustahili lakini tumefanywa tustahili, utajua ni jinsi gani Neema ya Mungu inatisha,..kwasababu kama linafanyika jambo ambalo kwa namna ya kawaida haliwezekani, wala halielezeki, hiyo inatisha!! Hakuna mtu yeyote anayeweza kuelezea hii neema imetoka wapi? Kila mtu anashangaa hata malaika…iweje hawa watu wasiofaa wapokee kipawa cha neema kubwa namna hii? Manabii wa zamani na wenyewe walionjeshwa kidogo tu! Lakini bado hawakuielewa. Waliona tu lakini wasielewe chochote, pengine walidhani watu wa mataifa watakujua kumweshimu masihi tu, lakini sio kufanywa na wao warithi wa ahadi za Mungu.
 
Ndugu, usiudharau msalaba, Kristo amehubiriwa kwako mara ngapi?..utapataje kupona usipouthamini wokovu MKUU namna hii?? Waebrania 2:3…kumbuka maisha yako ni kitabu na matendo yako ni kalamu yenye wino, yanaandika matendo yako kila siku, kila mwezi na kila mwaka,. siku inapopita ni unaanza aya mpya, kila mwezi ni unafungua ukurasa mpya, na kila mwaka ni unaanza sura mpya ya kitabu chako,. Na kitabu chako unaanza kukiandika siku unapozaliwa…na kinaanza na JINA LAKO kwa nje, ndio maana baada ya kuzaliwa tu unapewa jina, na pengine umeshaandika nusu ya kitabu chako mpaka kufikia sasa, jitathmini katika hiyo nusu uliyoiandika umeandika ipasavyo?, siku ile ya mwisho kitabu chako kitafunguliwa tena maandiko yanasema hivyo na kitalinganishwa na kile kitabu cha uzima kama matendo yaliyoandikwa kwenye kitabu chako hayafanani na matendo ya kile kitabu cha Uzima, sehemu yako itakuwa ni katika lile ziwa la moto. Huko ndiko kukosekana jina lako katika kitabu cha uzima. Na kumbuka mbinguni hakuna makaratasi, hivyo kitabu cha uzima sio makaratasi yaliyoandikwa majina kama nakala za ankra, hapana bali na chenyewe ni maisha yaliyoandikwa, na cha kuogopesha ni kwamba hayo maisha sio mengine zaidi ya maisha ya watu yaliyoandikwa kwenye biblia, maisha ya mitume, maisha ya Yesu Kristo, maisha ya watakatifu wote, na Maneno yao waliyoyahubiri katika Roho, Ndio maana unaona biblia ni kitabu kilichojaa habari za maisha ya watakatifu, watu siku ya mwisho ndio watahukumiwa kulingana na hayo. Paulo anasema katika kitabu cha Warumi 2:16 “katika siku ile Mungu atakapozihukumu siri za wanadamu, sawasawa na injili yangu, kwa Kristo Yesu”

Ufunuo 20: 11Kisha nikaona kiti cha enzi, kikubwa, cheupe, na yeye aketiye juu yake; ambaye nchi na mbingu zikakimbia uso wake, na mahali pao hapakuonekana.
12 Nikawaona wafu, wakubwa kwa wadogo, wamesimama mbele ya hicho kiti cha enzi; NA VITABU VIKAFUNGULIWA; na kitabu kingine kikafunguliwa, AMBACHO NI CHA UZIMA; na hao wafu wakahukumiwa katika mambo hayo yaliyoandikwa katika vile vitabu, sawasawa na matendo yao……… 15 Na iwapo mtu ye yote hakuonekana ameandikwa katika kitabu cha uzima, alitupwa katika lile ziwa la moto”

Kwahiyo usiidharau sauti ya Mungu inapozungumza nawe moyoni, Bwana anataka kukupa uzima wa milele na kukuepusha na hukumu unayokuja, tumefunuliwa hii siri ya Mungu, ambao wakina Musa walitamani kuijua lakini hawakuijua, na manabii wengine wote vivyo hivyo, kwahiyo saa ya wokovu ni sasa, sio baadaye wala kesho, kama hujayakabidhi maisha yako kwa Bwana fanya hivyo leo, hata kama wewe ni muislamu au mbudha unasoma ujumbe huu, siku ile hutasema hukusikia, na kumpa Bwana maisha sio kumpa lisaa, au masaa au siku, hapana unampa maisha yako yote yaani kuanzia leo na kuendelea mpaka siku utakapoondoka duniani, unakusudia kuishi kwa kumfuata yeye, katika njia zake zote, unakusudia kuacha dhambi zote ulizokuwa unafanya kama uasherati, ulevi, anasa, usengenyaji, chuki, kutokusamehe, usagaji, utoaji mimba,ushoga, utazamaji pornography, masturbation, disco, uvaaji wa vimini na suruali, na upakaji wa makeup mpaka unatoka kwenye asili yako ya ubinadamu n.k .

Yeye anakubali wakosa na atakupa uwezo wa kushinda dhambi, , kwasababu kwa nguvu zako hutaweza kushinda dhambi hata kidogo....yeye ndiye atakuwezesha kwa namna ya ajabu utajikuta unashinda mambo hayo endapo utakubali kumfuata, wengine tulikuwa wabaya kuliko wewe lakini Bwana alitutengeneza, tulikuwa tunadhani ilikuwa haiwezekani kuishi bila kufanya hayo mambo, lakini tumeahakikisha maneno ya Mungu ni kweli kuwa ni rahisi na ni raha sana kuishi bila hayo mambo, na hatuna tena mizigo wa dhambi,na hakuna kiu tena hata kidogo ya hayo mambo, kama aliyafanya kwetu, atayafanya na kwako pia, isipokuwa Bwana anataka watu wanaomaanisha sio watu wanaositasita katika mawazo mawili, ukishakusudia kwa matendo kuacha hayo mambo haraka sana bila kupoteza muda nenda kabatizwe katika ubatizo sahihi kulingana na maandiko ambao ni wa kuzamishwa katika maji mengi na kwa Jina la Yesu Kristo kulingana na (Matendo 2:38), ili upate ondoleo la dhambi zako. Na baada ya hapo utakuwa milki halali ya Roho wa Mungu, utafanyika kuwa hekalu la Mungu kwa Roho atakayeingia ndani yako.
 
Na kama ulirudi nyuma, shetani anataka urudi zaidi ya hapo, nia yake ni akupeleke kwenye ziwa la Moto, hiyo ndiyo ndoto yake kubwa, sasa usikubali ndoto ya shetani itimie juu ya maisha yako, ziwa la moto aliandaliwa yeye na malaika zake..lakini anataka na wewe uende huko, hivyo mpinge na Bwana atakuwa upande wako.

Mungu akubariki sana.

MKUU WA GIZA.


Jina la Bwana wetu Yesu Kristo, libarikiwe sana. Karibu tujifunze Biblia, leo kwa Neema za Bwana tutajifuza juu ya Namna ya kutoka katika uvuguvugu wa kidunia.

Katika kitabu cha ufunuo sura ya pili na ya tatu tunasoma juu ya ufunuo wa yale makanisa saba, na kama tunavyojua makanisa yale yalikuwa ni makanisa halisi kabisa, yaliyozaliwa kutokana na Injili za Mitume hususani mtume Paulo aliyokuwa anaihubiri nyakati hizo, hata hivyo yalikuwa ni zaidi ya saba, lakini Roho aliyachagua hayo saba kwa kusudi maalum kuyafundisha makanisa ya siku za mwisho ambayo tunayoishi, utaona kulikuwa na makanisa mengine yaliyokuwa Korintho,Galatia, thesalonike,filipi nk lakini hayajatokea katika kitabu cha ufunuo isipokuwa yale saba tu..

Hivyo kama wewe ni mfuatiliaji mzuri wa vipindi vya kanisa utakuwa unajua kuwa, tayari kuna vipindi sita vimeshapita vya kanisa tangu Bwana Yesu Kristo aondoke, na sasa tupo katika kipindi cha kanisa la saba, na kanisa tulilopo ndilo la saba na la mwisho linalojulikana kama LAODIKIA. Kama hujafahamu kabisa jambo hili au ndio mara ya kwanza unalisikia basi katafute kujua kwasababu ni jambo linalojulikana na wasomaji wengi wa biblia, au nitumie ujumbe inbox nikutumie uchambuzi wa nyakati hizi saba za kanisa na wajumbe wake.
Sasa tabia ya hili kanisa la LAODIKIA ni kanisa vuguvugu, kama tunavyosoma katika kitabu cha Ufunuo wa Yohana mlango wa tatu.

Ufunuo 3: 14 “Na kwa malaika wa kanisa lililoko Laodikia andika; Haya ndiyo anenayo yeye aliye Amina, Shahidi aliye mwaminifu na wa kweli, mwanzo wa kuumba kwa Mungu.
15 Nayajua matendo yako, ya kuwa hu baridi wala hu moto; ingekuwa heri kama ungekuwa baridi au moto.
16 Basi, kwa sababu UNA UVUGUVUGU, wala hu baridi wala moto, nitakutapika utoke katika kinywa changu.
17 Kwa kuwa wasema, Mimi ni tajiri, nimejitajirisha, wala sina haja ya kitu; nawe hujui ya kuwa wewe u mnyonge, na mwenye mashaka, na maskini, na kipofu, na uchi.
18 Nakupa shauri, ununue kwangu dhahabu iliyosafishwa kwa moto, upate kuwa tajiri, na mavazi meupe upate kuvaa, aibu ya uchi wako isionekane, na dawa ya macho ya kujipaka macho yako, upate kuona.
19 Wote niwapendao mimi nawakemea, na kuwarudi; basi uwe na bidii, ukatubu.
20 Tazama, nasimama mlangoni, nabisha; mtu akiisikia sauti yangu, na kuufungua mlango, nitaingia kwake, nami nitakula pamoja naye, na yeye pamoja name”.
Kanisa hili la Laodikia lilianza mwaka 1906, na litaisha siku unyakuo utakapofika, sasa hili kanisa ndilo lililoonyesha tabia ya hatari kuliko makanisa mengine yote ya nyuma, kwasababu mbele za Bwana limepimwa na kuonekana kuwa ni vuguvugu, nusu Mungu, nusu shetani, ni kanisa Nafki, na ndio inayopelekea kuonekana kuwa ni kanisa lililoharibika kuliko makanisa yote.

Sasa huu uvuguvugu unatoka wapi?..Huu uvuguvugu ni Pepo maalumu lililotoka kuzimu, na kutumwa duniani ili kufanya kazi maalumu ya ushawishi, na hili pepo halijatumwa kwa mtu mmoja hapana bali limetumwa kwa kizazi…Ni pepo lenye nguvu mara saba zaidi ya mapepo mengine yote..Ni pepo linalotenda kazi katika viwango vya juu kabisa vya utendaji kazi wa shetani, ambalo kazi yake hasaa ni kuwakosesha wanadamu wa kizazi cha siku za mwisho wamkosee Mungu wao, ili Mungu awakatae kabisa kabisa na kuwakana.

Sasa tujifunze kwa ufupi hili pepo linatendaje kazi, kabla ya kuja kuona madhara atakayoyapata mtu yule endapo hatalishinda..
Biblia inasema katika Waefeso 6: 11 
“Vaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kuzipinga hila za Shetani.
12 Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, JUU YA WAKUU WA GIZA hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho”.
Sasa Hawa wakuu wa giza wanaozungumziwa hapa wapo SABA, katika kila kanisa kulikuwa na mkuu mmoja, na katika hili kanisa la Laodikia yupo mmoja na ndiye mwenye nguvu kuliko wote. Na kama jina lake lilivyo “mkuu wa giza” anahakikisha kunakuwa na giza katika ulimwengu wa roho, anahakikisha hakuna nuru, na anahakikisha Nuru ya haki haiwazukii watu.

Na kauli mbiu yake aliyoipokea kutoka kwa shetani mkuu wake ni “KUHAKIKISHA WATU WOTE WANAKUWA VUGUVUGU DUNIANI”…kwahiyo anayo mapepo chini yake anayofanya nayo kazi kuhakikisha anatimiza lengo hilo. Kumbuka huyu mkuu wa anga, hatumshindi kwa kumkemea, hapana! Tutakuja kuona mbeleni namna ya kulishinda hili pepo.

Sasa anachokifanya ni kutumia nguvu za giza, na mapepo yake kuwafanya watu wawe vuguvugu, sio wanakuwa baridi wala moto! Hapana bali wanakuwa vuguvugu, hilo ndio lengo lake kubwa…Anahakikisha watu wamfahamu Mungu kidogo, na waufahamu uovu kidogo!..hataki kabisa mtu awe baridi hilo halitaki, anataka mtu awe hapo katikati..kwasababu anajua Mungu anamchukia mtu vuguvugu kuliko hata mtu yule aliye baridi..yaani kwa Mungu ni heri mtu awe mlevi na mwasherati moja kwa moja, kuliko mtu ambaye ni mwasherati kwa siri na bado anaenda kanisani au bado anasali..Huyo kwa Mungu anafananishwa na MATAPISHI!! Ni Bwana mwenyewe ndio alisema hivyo “ni heri ungekuwa moto au baridi kuliko kuwa vuguvugu”. Hivyo kule kuzimu katika vikao vyao ndio wameona wakifanikiwa kumfanya tu mtu awe vuguvugu, basi watakuwa wamemlaza kwa kila kitu.

Sasa hili pepo lenye nguvu mara saba kuliko mengine ndio lengo lake kubwa hilo!... wengi wanajua kuwa shetani mwanzoni alikuwa ni malaika mbinguni, lakini hawajui kuwa baada ya kulaaniwa hakunyanganywa nguvu zake na akili zake bali aliendelea kuwa nazo..Hivyo ni muhimu kujua kuwa yeye naye anatenda kazi kwa akili sana kiasi kwamba pasipo Roho wa Mungu, ni rahisi kuwadanganya hata yamkini walio wateule. Atahikikisha anatumia ushawishi mkubwa kumfanya mtu ajione yupo sawa na Mungu wakati bado ni mwasherati, mlevi, mla rushwa, anaishi na mwanamume au mwanamke ambaye hawajafunga ndoa, na bado mtu huyo ajione yupo sawa na Mungu n.k.

Huwa inauma sana unapokutana na mtu na unamwuliza umempa Bwana maisha yako na anakujibu NDIO, na unaendelea kumwuliza je! Bwana akija leo una uhakika wa kwenda naye mawinguni anakujibu NDIO nina uhakika kabisa, lakini ukija kumwangalia maisha yake utahuzunika kiasi cha kufa..

Kwamfano kuna mtu mmoja alinitumia ujumbe akaniambia mtumishi naomba uniombee kwasababu ni miaka mingi sasa sijapandishwa kazi, mimi ni kibarua tu,kazi yangu ni ya udereva, na bado ninafamilia, kwakweli alivyokuwa anaeleza alitilisha huruma sana huyu ndugu, nikamwuliza umempa Bwana maisha yako? akanijibu NDIO, nikazidi kumwuliza je! unauhakika Bwana leo akija utakwenda naye? Akajibu Ndio ninauhakika..Nikazidi kumwuliza tena je! una uhakika uovu wote haupo ndani ya maisha yako?.. namaanisha sio mlevi, sio mwasherati, hauna mwanamke unayetembea naye ambaye hamjaoana, sio mtukanaji, sio mla rushwa, sio mtazamaji wa pornography, sio mfanyaji masturbation n.k. akaniambia ndio hafanyi hayo yote!...na zaidi ya yote ameoa na ana mtoto, sasa lengo la kumwuliza vile sio kumweka kwenye mtego hapana! Bali kujua chanzo cha tatizo lake ili nijue namna ya kumsaidia kulingana na maandiko.

Baada ya kuniambia vile basi nikamwambia huna haja ya kuwa na hofu, wala usiogope! Maadamu upo katika mstari wa Bwana, Bwana hawezi kukutupa, Zidi kudumu katika haki subiri wakati wa Bwana, Bwana atakupatia kazi nzuri tu! mwamini yeye, akajibu amina!..Najua alitegemea nimwombee lakini sikufanya vile..

Baada ya siku kadhaa, nikaingia kwenye mitandao, nikakutana na post yake mahali.. “nguvu ziliniishia”…mambo anayo ya-post hata wasiomjua Mungu kabisa wanaona aibu kushiriki na wengine post hizo, ni picha chafu zisizoelezeka!!..Nilijihisi vibaya sana.

Nimekutana na watu wengi sana wa namna hiyo..wanahitaji Bwana awafanyie kitu fulani katika maisha yao, wanatamani wafanikiwe katika maisha, wawe matajiri, lakini hawajijui kuwa wao ni maskini wa roho, wanajiona kuwa ni matajiri wa roho kumbe ni maskini, wanajiona wapo sawa na Mungu kumbe hawamjui Mungu kabisa, ni lile lile pepo la Laodikia ndio lipo juu yao na ndilo linalowapusha wengi macho! Wasitambue ni hali gani mbaya ya kiroho waliyopo.

Nikakutana na dada mwingine nikamwuliza umempa Bwana maisha yako, akajibu ndio nampenda sana, nikamwuliza unamfahamu mtu fulani (nilimtaja tu mhubiri fulani maarufu wa zamani)..akajibu ndio namjua, nikamwuliza ulimsikia wapi..akanitajia nilimsoma kwenye agano la kale!..nikamwambia mbona huyo hayupo kwenye agano la kale,..akaniambiaa aah samahani nilimsoma kwenye agano jipya! Nikwambia hayupo hata kwenye agano jipya, akaniambia yupo wapi?, nikamwambi ni muhubiri tu aliyewahi kutokea miaka hamsini iliyopita nyuma..Huyu pia sikumwuliza kwa nia ya kumtega bali nilikuwa nataka nimfundishe kitu,…lakini tayari yeye alikuwa anajiona anajua kila kitu hana haja ya kitu kingine, baada ya muda mfupi nilijaribu kumpeleka kwenye maandiko nimfundishe, akakwazika akaondoka.

Nikakutana na mwingine tena, …nikamwuliza dada umempa Bwana Yesu maisha yako akanijibu ndio nimempa, ndio mwokozi wangu na ninampenda sana, nikamwambia akija leo una uhakika wa kwenda naye, akanijibu kabisa asilimia 100, nikamwuliza unamjua aliyeandika kitabu cha mhubiri? Akasema hamjui, nikamwuliza aliyendika kitabu cha wimbo uliobora je! akasema pia simjui, nikamwambia kama kweli unampenda Bwana ingekupasa kuyajua haya yote na zaidi ya haya, ila sikulaumu!..nikataka kujaribu kumfundisha msingi wa imani ya kikristo kwanza ndipo tuendelee mbele..hakutaka kuendelea kuongea akakatisha mazungumzo na kuondoka.

Hilo ndio tatizo la watu wengi katika kizazi chetu hichi cha Laodikia, Tunamwomba Mungu utajiri, na wakati ndani ya mioyo yetu ni Adui yetu, tangu lini mtu akaenda kumwomba adui yake gari, au mali au fedha?? Je! Atampa? Sharti apatane naye kwanza ndipo hayo yote apewe…Wengi leo wanapenda kwenda kumwomba Mungu mali wakati ndani ya mioyo yao wamekorofishana naye, ni matapishi mbele za Mungu, wapo mbali naye, ndani ya mioyo yao kuna kila aina ya uchafu..uasherati, ulevi, rushwa, anasa, mizaha, usengenyaji, pornography, punyeto n.k Biblia inasema ..” 
Mathayo 23:25 Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnasafisha nje ya kikombe na chano, na ndani yake vimejaa unyang'anyi na kutokuwa na kiasi. 26 Ewe Farisayo kipofu, safisha kwanza ndani ya kikombe, ili nje yake nayo ipate kuwa safi.”
Ni lile lile pepo la LAODIKIA linalotenda tenda kazi katika siku hizi za mwisho, kuwafanya watu wajione kuwa wana kila kitu katika roho, wakati ni maskini wa roho..
Bwana Yesu anasema maneno haya… “Nayajua matendo yako, ya kuwa hu baridi wala hu moto; ingekuwa heri kama ungekuwa baridi au moto.
16 Basi, kwa sababu una uvuguvugu, wala hu baridi wala moto, nitakutapika utoke katika kinywa changu.
17 Kwa kuwa wasema, Mimi ni tajiri, nimejitajirisha, wala sina haja ya kitu; nawe hujui ya kuwa wewe u mnyonge, na mwenye mashaka, na maskini, na kipofu, na uchi”.

Ndugu unayesoma ujumbe huu, kamwe usiruhusu hii roho ya uvuguvugu, kila siku yachunguze maisha yako, shetani yupo kazini, kuhakikisha kuwa unakuwa hapo katikati, si moto wala si baridi…Na kama maandiko yalivyotangulia kusema, Ni heri uwe baridi kabisa…ni heri ukawe mwasherati na useme hujaokoka, ni heri uwe mvaaji vimini na mpakaji lipstick na wanja na useme hujaokoka, ni heri uwe unaenda disco kila siku au unaishi na mwanamke/mwanamume ambaye hamjaoana na useme sijaokoka na wala simjui Mungu, wewe adhabu yako siku ile haitakuwa kubwa, kuliko useme mimi nimeokoka na unampenda Bwana wakati bado unavaa vimini, tena bila aibu unauonyesha maungo yako wazi kwenye mitandao, bado unapaka wanja mfano wa Yezebeli na lipstick kiasi kwamba tofauti yako na mwanamziki maarufu wa kidunia hapa nchi hakuna. Unamdhihaki Mungu. Wewe mbele za Mbele za Mungu ni matapishi na kinyaa.

Ni heri ukatubu sasa, na kukusudia kuacha hayo mambo, usiruhusu fikra zako zipotoshwe na mkuu wa ulimwengu huu(shetani) kwa kupitia wakuu wake wa anga..
Waefeso 2: 1 “Nanyi mlikuwa wafu kwa sababu ya makosa na dhambi zenu;
2 ambazo mliziendea zamani kwa kuifuata kawaida ya ulimwengu huu, NA KWA KUMFUATA MFALME WA UWEZO WA ANGA, ROHO YULE ATENDAYE KAZI SASA KATIKA WANA WA KUASI;
3 ambao zamani, sisi sote nasi tulienenda kati yao, katika tamaa za miili yetu, tulipoyatimiza mapenzi ya mwili na ya nia, tukawa kwa tabia yetu watoto wa hasira kama na hao wengine.
4 Lakini Mungu, kwa kuwa ni mwingi wa rehema, kwa mapenzi yake makuu aliyotupenda;”
Unaona? Bwana anaweza kukugeuza ukikusudia kumfuata kweli kweli, unachopaswa kufanya ni kutubu kwa kudhamiria kabisa kuacha dhambi, na kufanya maamuzi ya kutokuwa vuguvugu tena!! Hiyo ndio njia pekee ya kulishinda hili PEPO (MKUU WA ANGA) wa Laodikia…Ni kufanya maamuzi thabiti kwamba kuanzia leo mimi na dhambi basiii….lipstick basi, vimini basi, ulevi basi, uasherati basi, rushwa basi, anasa basi, marafiki wabaya basi, pornography basi,..Huo ndio ushauri wa Bwana alioutoa kwa kanisa la Laodikia…anasimama mlangoni na kubisha, hataingia mpaka wewe umefungua mlango, hatavunja mlango wa moyo wako na kuingia kwa nguvu, anasubiri wewe ufanye maamuzi ya kuacha dhambi, ndipo aingie. Na baada ya hapo fanya hima ukabatizwe katika ubatizo sahihi wa maji mengi na kwa jina la Yesu Kristo. Usishirikiane kabisa na MKUU WA GIZA HILI, na Bwana mwenyewe atachukua nafasi ya kuhakikisha haujikwai.

Mungu akubariki. Tafadhali "share" ujumbe kwa wengine.