"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Saturday, February 16, 2019

HUDUMA YA UPATANISHO.


2 Wakorintho 5: .17 “Hata imekuwa, mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya; ya kale yamepita tazama! Yamekuwa mapya.
18 Lakini vyote pia vyatokana na Mungu, ALIYETUPATANISHA sisi na nafsi yake kwa Kristo, naye alitupa huduma ya upatanisho;
19 yaani, Mungu alikuwa ndani ya Kristo, akiupatanisha ulimwengu na nafsi yake, asiwahesabie makosa yao; naye ametia ndani yetu neno la upatanisho.
20 Basi tu wajumbe kwa ajili ya Kristo, kana kwamba Mungu anasihi kwa vinywa vyetu; twawaomba ninyi kwa ajili ya Kristo mpatanishwe na Mungu.

Kuna sababu kadha wa kadha kwanini Yesu Kristo Bwana wetu, anajulikana kama Mwana wa Mungu, hiyo ni moja ya sifa yake kuu..Ingawa yeye alikuwa ni MUNGU katika mwili, lakini hilo halikuwa na umuhimu mkubwa sana kwetu kulifahamu , kuliko kumfahamu yeye kama mwana wa Mungu, ndio maana huoni mahali popote akitafuta kujionyesha yeye kuwa ni MUNGU. Hakutaka hilo, kwasababu hiyo sio sababu kubwa iliyomleta duniani, hakuja kutafuta kuabudiwa duniani…bali kutafuta kilichopotea. Kama ingekuwa amekuja kutafuta kuabudiwa kama Mungu, basi angekaa huko huko mbinguni kwenye utukufu wake angekuwa hana sababu ya kushuka huku duniani kwenye mavumbi..

Raisi anapokutana na familia yake cheo chake kinabadilika na kuwa Baba na MWANA-FAMILIA na sio raisi tena, hatamwadhibu mwanawe kwa kutumia vyombo vya dola, bali atatumia fimbo kama ikiwezekana, na Yesu Kristo alivyokuja duniani cheo chake cha kimungu kilibadilika na kuwa MWANA. Kwahiyo ilimpasa awe kama mwanadamu, ndio maana watu wasiomwelewa Bwana YESU wanapinga vikali kuwa yeye sio Mungu, Mungu gani anakufa? Analia? Anakula na kunya?...Ni kweli kwa kumchunguza tu pasipo kuwa na ufunuo wa utendaji wake kazi hutaweza kuona uungu wowote ndani yake. Lakini akikujalia kupata ufunuo utamwelewa vizuri yeye ni nani. ukisoma Wafilipi 2:5-8, pamoja na 1Wakorintho 2:6-8, na Tito 2:13 na Timotheo 3:16, Utapata  picha halisi ya kuwa yeye ni nani. Na kwamba alikuja katika SIRI KUU SANA, ijulikanayo kama Siri ya utauwa..Na biblia inasema siri hiyo haijulikani kwa kila mtu bali kwa wakamilifu tu peke yao ya kwamba Kristo YESU ni MUNGU.

Lakini Bwana Yesu alipokuja duniani alitamani sana sisi tumjue yeye kama Mwana wa Mungu kuliko kumjua yeye kama Mungu, ndio maana aliwauliza wakati Fulani wanafunzi wake..”watu husema ya kuwa mimi ni nani?” wakasema wengine Eliya, wengine Yohana mbatizaji, wengine Yeremia n.k akawauliza na wanafunzi wake, na ninyi mnasema ya kuwa mimi ni nani? “PETRO AKAJIBU WEWE NDIWE KRISTO, MWANA WA MUNGU ALIYE HAI.
Unaona?  Bwana Yesu alimsifia Petro kwa ule ufunuo alioupata wa kumtambua Kristo kama mwana wa Mungu..

“Yesu akajibu, akamwambia, HERI wewe Simoni Bar-yona; kwa kuwa mwili na damu havikukufunulia hili, bali Baba yangu aliye mbinguni” (Mathayo 16:16-19)
 Zingatia hilo neno “HERI” Ikiwa na maana kuwa amebarikiwa yeye alifahamuye hilo, unaweza ukajiuliza kwanini Bwana hakumrekebisha Petro na kumwambia hapana! Mimi si mwana wa Mungu, bali ni Mungu mwenyewe niliyekuja katika mwili. Unaona jambo ni lile lile, Yeye anataka tumwelewe ni kitu gani kilichomleta Duniani zaidi ya kuelewa ni kitu gani alichokiacha mbinguni.

Alifanyika kuwa MWANA WA MUNGU, ili kutuonyesha sisi NJIA ya jinsi mwana wa Mungu anavyotakiwa awe, ili siku atakapoondoka duniani, sisi tuliosalia kwa kuyaangalia maisha yake, tujifunze kwake, alikuja kutengeneza njia iliyoharibika..ili kwa kumtazama yeye tuyarekebishe maisha yetu. Ili yafanane na ya kwake ili nasi tuwe WANA WA MUNGU kweli kweli. Kama yeye alivyomtegemea Baba nasi tumtegemee Baba asilimia 100, kama yeye alivyokuwa mtakatifu hata akashuhudiwa mbinguni nasi tuwe hivyo hivyo, kama yeye alivyovumilia nasi tuvumilie majaribu, kama yeye alivyokuwa na upendo nasi tuwe na upendo.n.k Hizo ndio tabia za kuwa MWANA WA MUNGU. Sio kusema sisi ni wana wa Mungu lakini maisha yetu hata kidogo hayafanani na ya kwake, yeye ametupa kielelezo, kama yeye alivyofanya na kuishi na sisi pia tufanye na kuishi vilevile kama yeye..

Ni sawa na mwalimu aliyeona wanafunzi wake hawamwelewi akaamua kuvua cheo chake cha ualimu na kuvaa uniform za kiuanafunzi na kwenda kuketi pamoja na wanafunzi, na kujifanya yeye ni mwanafunzi na kusoma nao na kujiweka chini ya changamoto zote za kiuanafunzi ili tu kuwaonyesha njia bora ya kusoma inavyopaswa na kumwelewa mwalimu anapofundisha. Ndivyo na Bwana Yesu alivyofanya kuacha enzi na mamlaka kuja duniani. Ni kutuonyesha tu sisi njia!

Lakini tukiachana na hayo, tunaweza kujifunza pia sifa nyingine kuu ya KUWA MWANA WA MUNGU, Na sifa hiyo si nyingine zaidi ya UPATANISHO, Sifa hii ndio iliyobeba kiini cha somo letu leo…

Sasa sababu nyingine kubwa iliyomfanya Bwana Yesu kuwa mwana wa Mungu na si malaika ni KUTUPATANISHA SISI NA MUNGU. Kumbuka sisi tulikuwa tumepotea dhambini, na tulikuwa tayari wote ni wa kwenda kuzimu, hakuna hata mmoja wetu angepona hata Musa, hata Eliya, hata Yohana Mbatizaji hata Adamu mwenyewe wote walikuwa ni wakupotea…Lakini kwa kupitia damu ya Yesu Kristo, Mwana wa Mungu tumepatanishwa na Mungu. Tunakwenda mbinguni bure endapo tukimwamini yeye na kuyaishi maneno yake.

Hivyo basi ili na sisi tuwe wana wa Mungu ni lazima tuwe wapatanishi kama yeye. Utauliza? Na sisi kwahiyo inatupasa tumwage damu kama yeye?? Jibu! Damu ya Yesu inatosha!
ilishamwagika mara moja, lakini alitupa kielelezo kama yeye alivyotufanyia sisi na sisi tuyafanye kwa wengine, kwahiyo ndio wakati mwingine kama inabidi inatupasa na sisi kumwaga damu au kutoa uhai wetu kwaaajili ya wengine..maandiko yanasema hivyo katika kitabu cha 1 Yohana 3:16” Katika hili tumelifahamu pendo, kwa kuwa yeye aliutoa uhai wake kwa ajili yetu; imetupasa na sisi kuutoa uhai wetu kwa ajili ya hao ndugu” HUO NDIO UPATANISHO, Na kwa kufanya hivyo tutaonekana tumekuwa WANA WA MUNGU,kwa macho yakimbinguni, tutafananishwa na MWANA WA MUNGU,Yesu Kristo aliyetoa uhai wake kwa ajili yetu. Biblia inasema katika kitabu cha Mathayo..

Mathayo 5:9 “HERI WAPATANISHI; Maana hao WATAITWA WANA WA MUNGU”
Upatanishi unaozungumziwa hapo juu, sio kuwapatanisha watu wanaogombana au watu waliokosana hapana! Bali kujitoa kwa hali na mali kwa ajili ya kuwapatanisha watu na Mungu wao, KWA KUWAPELEKEA HABARI NJEMA za wokovu na hata kugharimika kufa, ilimradi tu umpatanishe mtu na Muumba wake, kama Bwana Yesu alivyofanya. Maandiko yanasema..


2 Wakorintho 5: 17 “Hata imekuwa, mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya; ya kale yamepita tazama! Yamekuwa mapya.
18 Lakini vyote pia vyatokana na Mungu, aliyetupatanisha sisi na nafsi yake kwa Kristo, NAYE ALITUPA HUDUMA YA UPATANISHO;
19 yaani, Mungu alikuwa ndani ya Kristo, akiupatanisha ulimwengu na nafsi yake, asiwahesabie makosa yao; NAYE AMETIA NDANI YETU NENO LA UPATANISHO.
20 Basi tu wajumbe kwa ajili ya Kristo, KANA KWAMBA MUNGU ANASIHI KWA VINYWA VYETU; twawaomba ninyi kwa ajili ya KRISTO MPATANISHWE NA MUNGU.
 Umeona hapo? Ndugu…Kristo,Mwana wa Mungu alitupatanisha sisi na Mungu ndio maana akaitwa Mwana wa Mungu, kwasababu heri walio wapatanishi hao wataitwa wana wa Mungu, na sisi Bwana ametupa huduma ya upatanisho..Ndiyo haya maneno yanayosema nawe sasa,…kama maandiko yanavyosema hapo katika mstari wa 20 “KANA KWAMBA MUNGU ANASIHI KWA VINYWA VYETU; twawaomba ninyi kwa ajili ya KRISTO MPATANISHWE NA MUNGU.”



Biblia inakusihi ndugu unayesoma ujumbe huu ambaye hujawa kiumbe kipya bado, ambaye ni vuguvugu katika imani, ambaye bado unaupenda ulimwengu, ambaye bado hujaacha anasa, wala usengenyaji, wala ulevi, wala tamaa mbaya…inakuomba upatanishwe leo na Mungu.
Mgeukie yeye leo ukanywe maji ya uzima, kama Bwana mwenyewe alivyosema katika Ufunuo 22:17 “Naye mwenye kiu na aje; na yeye atakaye, na ayatwae maji ya uzima bure.”..Ni bure kabisa yanapatikana…Utafika wakati haya maji hutayapata bure wala kwa fedha, yatakuwa hayapo…Na unajua madhara ya kukosa maji ya uzima baada ya kifo??..ni mabaya sana usitamani uyakose huko.

Kama hujatubu dhambi zako, bado hujachelewa, mwambie Bwana akusamehe, mahali popote ulipo, jitenge peke yako kwa muda kisha tubu! Mwambie Bwana kuanzia leo unahitaji kuwa kiumbe kipya, unahitaji kupatanishwa naye, wewe mwenye dhambi na kama umemaanisha kufanya hivyo yeye “anakubali wakosa” atakusamehe na atakupa amani ya ajabu moyoni mwako, hiyo amani ndio uthibitisho wa kusamehewa dhambi zako, na bila kupoteza muda haraka sana nenda katafute ubatizo sahihi wa kimaandiko, wa maji mengi na kwa JINA LA YESU KRISTO(kulingana na Matendo 2:38) ili dhambi zako ziondoke kabisa kabisa, Baada ya kufanya hivyo Bwana Yesu Mwenyewe atakupa kipawa cha Roho wake Mtakatifu atakayekusaidia kushinda dhambi na kuilewa biblia vizuri..

Kwa kukamilisha hatua hizo utakuwa umezaliwa mara ya pili na kuwa kiumbe kipya…kama maandiko yalivyosema hapo juu..” MTU AKIWA NDANI YA KRISTO YA KALE YOTE YAMEPITA TAZAMA YAMEKUWA MAPYA”..Bwana mwenyewe atayafanya mapya maisha yako kwa kila NYANJA!
Mungu akubariki sana…Na kama tayari ulishakuwa ndani ya Kristo, yaani umeshazaliwa mara ya pili, Neno linasema TUMEPEWA HUDUMA YA UPATANISHO, hivyo ni wajibu wako pia kwenda KUWAPATANISHA WENGINE NA MUNGU WAO, yaani kwenda kuwaambia habari za Neema zilizopo ndani ya Yesu Kristo na Raha na Tumaini, na toba!. Huo ndio uthibitisho wa kuwa kweli umefanyika kuwa mwana wa Mungu, kumbuka Neno hili “heri wapatanishi maana hao wataitwa wana wa Mungu”.

Ubarikiwe sana.

Tafadhali “share” ujumbe huu kwa wengine,

No comments:

Post a Comment