"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Monday, February 4, 2019

MASWALI NA MAJIBU: SEHEMU YA 54


 SWALI 1: Mimi ni askari magereza, na nimeamuriwa kumnyonga mfungwa aliyekuwa mwalifu kwa kosa la uuaji. Je! kufanya hivyo ninatenda dhambi?.

JIBU: Tunapaswa tufahamu vizuri utumishi wa Mungu jinsi ulivyogawanyika ili tusikose maarifa tukidhani ya kuwa Mungu anatenda kazi sehemu moja tu kanisa, mahali pengine hayupo, wala hajihusishi na mambo hayo. Tukisoma biblia tunaona Mungu anao watumishi wa aina mbili:

1) Watumishi wa ufalme wa mbinguni:

2) Watumishi wa kidunia:

Watumishi wa ufalme wa mbinguni: Ni wale wote wanaofanya kazi zihusuzo ufalme wa mbinguni tu, kuhakikisha habari njema zinawafikia watu wengi kwa njia ya injili, kulichunga kundi la Mungu wakati wote, kulihudumia kwa kila namna kupitia karama za Roho ambazo Mungu aliziachia katika kanisa..Na mfano wa watumishi hawa tunawajua ni wachungaji, waalimu, mitume, manabii, na wainjilisti, mashemasi, karama za maombezi, lugha, uponyaji, Neno la Hekima, Maarifa n.k..

Lakini Mfano wa watumishi wa kidunia, ni wale ambao wameamuriwa na Mungu kutimiza kusudi lake maalumu hapa duniani. Na mfano wa hao ni Serikali na taasisi zake zote zilizo chini yake.. Na Wengine mfano, ni mashirika mengine yote yasiyo ya Umma, yanayohusika na kutoa huduma za kijamii kwa watu. Hawa wote wanatimiza kusudi maalumu la Mungu lakini sio kusudi kamilifu lile ambalo alilitaka kila mmoja alifikie.

Hivyo Mungu huwa anatumia vyombo hivi vyote viwili kwa aidha kubariki, au kijilipizia kisasi, kwa walio waovu na walio wema. Sasa kama imetokea Mfano mtu anayo kiu ya kuijua haki, anapenda kutafuta kujua masuala ya Mungu kwa bidii hata kama yeye sio mkristo..Jambo Mungu analofanya ni kumsaidia kwa kumpelekea huyu mtu mtumishi wake wa ufalme wa mbinguni ili amfikishie huduma hiyo aliyokuwa anaihitaji mahali pale alipo. Mfano tunamwona Kornelio katika biblia, yeye hakuwahi hata siku moja kumfahamu YESU, lakini kwa jinsi alivyokuwa anabidii katika kumtafuta Mungu na kutenda haki na kutoa sadaka nyingi, basi Petro alitumwa kwake kwenda kumshuhudia habari njema za YESU KRISTO (Matendo 10),

Mfano wa mwingine kama huo tunaona kwa yule Mkushi aliyetoka Afrika kwenda kuhiji Yerusalemu, lakini alipokuwa njiana anarudi nchini kwake huku anasoma torati mahali palipoandikwa habari za YESU lakini katika fumbo. Mungu aliona kiu yake hivyo kutokana na bidii yake kwa Mungu ya kutaka kujua, basi Mungu akamtumia Mtumishi wake Filipo aende kumwelezea habari zile kwa ufasaha zaidi.

Vivyo hivyo mtoto wa Mungu anapomwomba Mungu ampe riziki za dunia, hawezi kwenda kumtafutia kazi kanisani kwasababu makanisa sio taasisi za kutengeneza fedha, au sio sehemu za biashara,Bwana Mungu atakachokifanya ni kuhakikisha anamtafutia nafasi nzuri katika taasisi Fulani husika, labda wizara Fulani ambapo pengine atamweka chini ya ma-manager Fulani wa serikali..ambao watamwajiri na kumpatia mshahara mzuri..sasa hao ma-manager ni watumishi wa Mungu kwa Yule mtoto wa Mungu anayetafuta riziki za kidunia.

Vivyo hivyo mtoto wa Mungu anapohitaji, maji safi au umeme mzuri, Bwana Mungu hawezi kumpelekea mchungaji au nabii kumpatia huduma hiyo, atampelekea watumishi wake wengine wanaohusika na mambo hayo kama tanesco na Idara ya Maji, watahakikisha wanamfikishia maji na umeme mpaka chumbani kwake anapolala.

Hali Kadhalika pale mtu anapokuwa mwovu, anapotenda mabaya, anapomfanyia Mungu makosa kwa makusudi wapo vile vile watumishi Mungu aliowaandaa kwa ajili ya shughuli kama hizo ili kujilipizia kisasi kwake, na mojawapo wa hao watumishi wa Mungu ndio hivyo vyombo vya dola, mtu anapoua, unapoiba, unapobaka, unapokula rushwa,. Asidhani kuwa Mungu atasema naye kwa upole kama asemavyo naye kanisani, Na ndio hapo anakamatwa na kutiwa gerezani na wakati mwingine kuhukumiwa kunyongwa kama atakuwa anastahili adhabu hiyo,. Sasa Kwa namna ya kawaida unaweza kusema ni hawa watu wamemtendea hivyo, lakini kiuhalisia sio wao bali ni Mungu ndiye aliyemlipiza kisasa kwa makosa yake mwenyewe.

Na ndio maana biblia inasema: Warumi 13:1 “Kila mtu na aitii mamlaka iliyo kuu; kwa maana hakuna mamlaka isiyotoka kwa Mungu; na ile iliyopo umeamriwa na Mungu.
2 Hivyo amwasiye MWENYE MAMLAKA HUSHINDANA NA AGIZO LA MUNGU; NAO WASHINDANAO WATAJIPATIA HUKUMU.
3 Kwa maana watawalao hawatishi watu kwa sababu ya matendo mema, bali kwa sababu ya matendo mabaya. Basi, wataka usimwogope mwenye mamlaka? Fanya mema, nawe utapata sifa kwake;
4 kwa kuwa yeye ni mtumishi wa Mungu kwako kwa ajili ya mema. LAKINI UFANYAPO MABAYA, OGOPA; kwa maana hauchukui upanga bure; kwa kuwa ni mtumishi wa Mungu, amlipizaye kisasi mtenda mabaya kwa ajili ya ghadhabu.
5 Kwa hiyo ni lazima kutii, si kwa sababu ya ile ghadhabu tu, ila na kwa sababu ya dhamiri.
6 Kwa sababu hiyo tena mwalipa kodi; kwa kuwa wao ni wahudumu wa Mungu, wakidumu katika kazi iyo hiyo”.

Unaona hapo? Sasa tukirudi kwenye swali lililoulizwa linalosema: Mimi ni askari magereza, na nimeamuriwa kumnyonga mfungwa aliyekuwa mwalifu kwa kosa la uuaji. Je! kufanya hivyo ninatenda dhambi?.

Jibu ni kuwa “hutendi dhambi” . Kwani wewe umeamuriwa kutimiza wajibu wako, kwa kosa ambalo lilishaonekana limefanywa na mtu mwenyewe, mpaka kufikia hapo ni Mungu mwenyewe ameruhusu. kwasababu maagizo hayo hayajatoka kwako bali yametoka juu, lakini hutahesabiwa thawabu katika hilo mfano wa wale wanaomtumikia Mungu kwa habari ya kuokoa roho za watu na sio kuangamiza,..Na ndio maana ni vema pia kujua pale unapokuwa mkristo, ufahamu kazi unayotaka kuifanya ujue na majukumu yake yatakavyokuwa, Sio kila kazi itampa mkristo amani kuifanya, japo hata afanyapo hatahesabiwa makosa. Uamuzi ni wako binafsi.

Hivyo kabla hujaamua kujiingiza kwenye utumishi wowote piga kwanza faida zake na hasara zake. Je! Utumishi uufanyao ni ule utimizao mapenzi makamilifu ya Mungu au ni ule wa kisasi cha Mungu, kabla hujawa mwanajeshi jitafakari mara mbili mbili, kabla hujawa polisi jitafakari mara mbili mbili na daktari vivyo hivyo na kazi nyingine zote.

Ubarikiwe.
SWALI 2: Ni sahihi kutoka malali fulani na kwenda kutafuta huduma ya Uponyaji mahali pengine Mfano Kanisani kwako ikiwa umeomba sana na kuombewa bila kuona uponyaji, ni sahihi kwenda katika kanisa lingine kutafuta uponyaji?..

JIBU: Shalom! Mtu anayefanya hivyo anaonyesha wazi kuwa yeye ni mchanga wa kiroho au hana imani kwa Mungu anayemwabudu..

Na Kundi la watu wa namna hii mfano wao ulishazungumziwa katika biblia. Tunaona wakati fulani wanafunzi wa Yesu wakiwa katika huduma yao waliyopewa na Bwana ya kuzunguka katika vijiji na miji kuhubiri habari za njema za ufalme na kutoa pepo, na kuponya magonjwa na kufufua wafu, n.k.,tunaona walifanikiwa kufanya hivyo kwa mafanikio makubwa sana, mpaka kufikia hatua wanamrudia Bwana wakishangalia kwa shangwe wakisema Bwana tazama PEPO wanatutii kwa jina lako!!..

lakini tunasoma haikuwa hivyo wakati wote, kuna kipindi walipita sehemu fulani na kukutana na mtu mmoja mwenye shida sana, mtu huyo alikuwa na kijana wake ambaye alisumbuliwa na mapepo kwa muda mrefu sana , hivyo yule baba wa mtoto alipowaona mitume aliwauliza kama wanaweza kumtoa pepo. Na wanafunzi wa Yesu bila kutuliza akili zao kwanza wao wakaanza tu kushindana na lile pepo kama walivyokuwa wanafanya kwa mapepo mengine, hivyo walifanya hivyo kwa muda mrefu pasipo kufanikiwa, inawezekana walijiuliza ee! Leo imekuwaje mbona , mbona pepo hili sugu? Haiwezekani halitaki kutoka, wakati tumeshakutana na makubwa zaidi ya hili na yametoka..hili kwanini linatusumbua.. tuendelee kupambana nalo, hivyo waliendelea kutoa jasho muda mrefu huku baba mzazi wa mtoto anawaangalia tu!…Mitume hawakujua kuwa kumbe kulikuwa na tatizo pia upande wa pili wa yule aliyemleta, wao hawakulitambua hilo…

Lakini wao waliendelea kushindana nalo kutwa nzima wasiweze kulitoa, mpaka baadaye Bwana alipokuwa anashuka mlimani na kuwakuta wale watu wamekusanyika wengi, na kuwauliza kitu gani kinaendelea..ndipo yule mtu mwenye mtoto aliyekuwa na pepo akawaacha mitume pale, hawana nguvu ya kutosha ya kutoa pepo, na kurukia kwa Bwana YESU,…sasa angalia kwa makini haya maneno mtu huyu aliyomwambia Bwana…. Alisema hivi “UKIWEZA neno lo lote, utuhurumie, na kutusaidia.”..Unaona hapo? Hilo neno UKIWEZA Kauli yake hiyo ilithibitisha mtu huyu alikuwa ni wa kubahatisha, bahatisha, aamini kama mtu fulani anaweza kumsaidia,alikuwa haamini hata mitume wa Bwana wangekuwa na uwezo ule wa kutoa pepo, kauli ile inathibitisha yupo tayari hata kumpeleka mtoto wake kwa mtu mwingine ikiwa mtu huyo pia atashindwa kumponya...na ndio maana kila mtu aliyekutana naye kumwomba msaada alimwambia UKIWEZA!..UKIWEZA!..hata alipofika kwa BWANA alimwona tu kama mtu wa kawaida na kumwambia maneno hayo hayo UKIWEZA!..Ndipo Bwana akamkea saa ile ile na kumwambia ati nini? UKIWEZA?.

Embu Tusome kidogo.

Marko 9: 17 “Mtu mmoja katika mkutano akamjibu, Mwalimu, nimemleta mwanangu kwako, ana pepo bubu;
18 na kila ampagaapo, humbwaga chini, naye hutoka povu na kusaga meno na kukonda; nikasema na wanafunzi wako wamtoe pepo, wasiweze.
19 Akawajibu, akasema, Enyi kizazi kisichoamini, nikae nanyi hata lini? Nichukuliane nanyi hata lini? Mleteni kwangu.
20 Wakamleta kwake; hata alipomwona, mara yule pepo alimtia kifafa; naye akaanguka chini, akagaa-gaa, akitokwa na povu.
21 Akamwuliza babaye, Amepatwa na haya tangu lini? Akasema, Tangu utoto.
22 Na mara nyingi amemtupa katika moto, na katika maji, amwangamize; lakini ukiweza neno lo lote, utuhurumie, na kutusaidia.
23 Yesu akamwambia, Ukiweza! Yote yawezekana kwake aaminiye.
24 Mara babaye yule kijana akapaza sauti, akasema, NAAMINI, nisaidie kutokuamini kwangu.
25 Naye Yesu akiona ya kuwa mkutano unakusanyika mbio, akamkemea yule pepo mchafu, akamwambia, Ewe pepo bubu na kiziwi, mimi nakuamuru, mtoke huyu, wala usimwingie tena.
26 Akalia, akamtia kifafa sana, akamtoka; naye akawa kama amekufa; hata wengi wakasema, Amekufa.
27 Lakini Yesu akamshika mkono akamwinua naye akasimama”.

Umeona hapo kwenye mashaka ya kwamba UTAWEZA! ndipo palikuwa na shida na ndio hilo lililomfanya asipokee uponyaji wa mtoto wake kwa wakati husika…Bwana aliliona tatizo lilipokuwa na ndipo akamkea saa ile ile,..Unaniambia mimi UKIWEZA kama ulivyowaambia wale?..Kwangu mimi hakuna hiyo kauli..Hamkuweza kumtoa yule pepo kwa kwa fikra yako hiyo..UKIWEZA..Sasa ukiendelea pale Unaona pindi tu yule mtu alipoirekebisha kauli yake na fikra zake mbovu nakusema NAAMINI,basi yule pepo alitoka kiurahisi baada ya kukemewa kidogo tu! na Bwana.

Leo hii watu wanakwenda katika madhabahu yoyote ya Mungu, huku vichwani mwao wanadukuduku ATAWEZA kweli huyu?,.Kanisa hili LITAWEZA KWELI kumponya mtoto wangu?, Huduma hii itaweza kweli kuliondoa tatizo langu? Ikishindikana hapa nitakwenda kwa mtumishi yule, kwa mchungaji yule, ngoja nijaribu tu!..Badala amwangalie Kristo aliyekwenda kumfuata huko amsaidie anaanza kuwapima wanadamu kana kwamba wao ndio watakaomtolea matatizo.

Na ndio maana mwisho wa siku wanakimbia huku na kule, na wakiona hakuna suluhisho wanarudi kwa waganga wao waliowaacha huko nyuma. Ndugu ili uweze kulitatua tatizo hilo, ni vema ufahamu je! huo uponyaji unautarajia kutoka kwa nani? Ikiwa ni kwa Yesu basi hutatangatanga kwenda huku na kule..Utabaki kumwangali Bwana Yesu (Mponyaji mwenyewe) Baki pale pale ulipo mtazame yeye na yeye mwenyewe kama alivyokuahidi atakuponya na uache kupima viwango vya neema kati ya watu wa Mungu, Ukidhani tatizo lipo kwa watumishi hujui kuwa kumbe lipo katika fikra zako….Ndio maana Sehemu nyingie Bwana alikuwa anawaambia wale aliokuwa anawaponya “imani yako imekuponya”..Na ndio maana wengi wenye fikra hizo huwa hawapokei uponyaji wao kwa wakati, utakuta mtu hata asiyemjua Mungu leo hii tu kapokea uponyaji wake, kwasababu fikra zake zote zipo katika kupokea uponyaji wake na si katika watu, lakini huyu ambaye amekuwa katika wokovu muda mwingi aliyezunguka huku na kule hajaambulia chochote .

Kadhalika ukiwa na imani kwa Mungu wako ya kutosha hauhitaji kwenda kwa mtu yeyote kukuombea. Kwasababu Kristo tayari yupo ndani yako, na yupo na wewe kila siku. Unapomwomba anakusikia hapo ulipo..Haimfurahishi Kristo kumtegemea mtu wa tatu kukuhudumia angali uwezo huo wa kukutana naye unao.

Rekebisha, mahusiano yako na Kristo sasa, Acha kuwaangalia wanadamu, dumu katika Neno lake, hilo ndilo suluhisho.

Ubarikiwe.

No comments:

Post a Comment