"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Thursday, March 28, 2019

MASWALI NA MAJIBU: SEHEMU YA 58


SWALI 1: Biblia inasema usiape kabisa, lakini ni kwanini watu wanaapa mahakani na katika kufunga ndoa?
JIBU: Ni vizuri kuelewa aina ya viapo mbalimbali vinavyozungumziwa katika biblia, ili usichanganyikiwe unapokutana na baadhi ya vifungu vinavyoonyesha wengine wakiapa lakini Biblia haiwahesabii kosa lolote kwa mfano pale mtume Paulo aliposema.

2Wakorintho 1: 23 "Lakini mimi NAMWITA MUNGU AWE SHAHIDI JUU YA ROHO YANGU, ya kwamba, kwa kuwahurumia sijafika Korintho".

Warumi 1: 9 "Kwa maana Mungu, nimwabuduye kwaroho yangu katika Injili ya Mwana wake, NI SHAHIDI wangu jinsi niwatajavyo pasipo kukoma",

Hivyo kwa maelezo mafupi Vipo viapo vya aina mbili..aina ya kwanza ni viapo vya uaminifu, mfano wa hivi ni maagano au nadhiri.. Kwamfano Nadhiri ni kiapo, kinachomfunga mtu kwa Mungu wake kwamba unakuta mtu anamwambia Mungu ukinitendea hivi nitakutendea hivi, au sitafanya kitu fulani kwa wakati fulani mpaka nimalize kutimiza kusudi fulani..Hivi vyote mbele za Mungu ni viapo, na mtu anafungwa katika hivyo mpaka avitimize, asipovitoa kwake mtu huyo inakuwa ni dhambi.

Hali kadhalika na pale wenzi wawili wanapofunga ndoa mbele za Mungu sawasawa na maagizo yake, moja kwa moja wanaingia katika viapo kwamba hakuna chochote kitakachowatenganisha mpaka kifo kitakapowakuta..Sasa iwe wamekiri hadharani au hawajakiri hadharani, wakishaingia kwenye ndoa tu, tayari maandiko yameshawafunga.

Hali kadhalika na mahakamani au katika mikataba ya kidunia: Ili mtu kujiridhisha na wewe uaminifu wako, huwa unaapishwa, kwamba unalolisema ni kweli, na kwamba utafanya sawasawa na mkataba au makubaliano mliyoingia..Sasa viapo kama hivyo vyote haviji kwa lengo la kujihesabia haki, au kujiona wewe uko sawa mbele za mtu, au kujifanya wewe ni mkamilifu hapana bali ni vya kuthibitishwa tu.

Lakini sasa vipo viapo ambavyo vinakuja nje ya utaratibu wa Mungu, kwa mfano mtu pale anaposema HAKI YA MUNGU vile!!, au naapa juu ya kaburi la babu yangu, au naapa kwa kichwa changu, au naapa juu ya kiti cha enzi cha Mungu, n.k…Unaona Vyote hivi ni viapo vinavyokuja kwa shinikizo fulani, au vinavyotokana na kiburi fulani, na mara nyingi viapo vya namna hii vinatoka katika kinywa cha mtu kwa makosa ya kushutumiwa, na si vinginevyo, hivyo watu wa namna hii mara nyingi hata bila kufikira anatoa maneno makuu kama hayo yaliyovuka mipaka, maneno ambayo hawezi hata kuyasimamia, kwamfano anaposema ninaapa kwa kichwa changu, utadhani kama yeye anajua hata hicho kichwa kiliundwaje undwaje, au mwingine anasema ninapa mbele ya kiti cha enzi cha Mungu utadhani yeye na Mungu ni mtu na mdogo wake, na hivyo ana uwezo sawa au unaokaribiana na Mungu n.k.

Viapo vya namna hii ndivyo Mungu kavikataa kwasababu vinatoka moja kwa moja kwa yule mwovu, Mungu hapendi watu wanaojikweza na wenye viburi..Hivyo mtu akijikuta katika hali kama hiyo ya kushutumiwa hapo maneno yake ndio yanapaswa yawe Ndio ndio, au Siyo siyo.. Basi,

Lakini ikiwa ni kama vitu kama nadhiri, au maagano,au mapatano ya ndoa, au mikataba, au mahakamani..Hayo hayaji kutokana na kushutumiwa au kiburi bali yanakuja kwa lengo la kujiridhisha, kukiri uaminifu wako tu, na si zaidi ya hapo, na hiyo huwa mtu hafikii hatua ya kujikweza au kujihesabia haki, au kujihalalishia mamlaka ya kutendewa alichosema kama imethibitika kuwa hajasimamia alichosema.


 SWALI 2: Mfalme Daudi aliwahesabu wana wa Yakobo apate kujua idadi yao kamili, 1mambo ya nyakati 21:7, jambo lililoonekana chukizo kwa bwana, mpaka kusababisha watu elfu sabini waangamie kwa tauni. SWALI. ni uovu gani hapo Daudi aliufanya ulete madhara hayo yote? au torati ilisemaje kuhusu watu kuhesabiwa?
JIBU: Hakukuwa na uovu wowote mkubwa kivile katika kuhesabu watu, japo Daudi alifahamu hakupaswa kufanya vile kwa wakati ule lakini yeye aliendelea kufanya ndio maana baadaye alikuja kujutia makosa yake, na kumwomba Mungu msamaha!.

Lakini sasa swali linabaki pale pale ni kwanini kwa kosa lake mwenyewe lisababishe zaidi ya watu ya elfu 70 kuangamia kwa tauni? Mpaka kufikia hatua Daudi mwenyewe kumlalamikia Mungu, na kumwambia kwanini unawaadhibu watu wengine wasio na hatia kwa kosa langu mwenywewe? Kwanini Mungu afanye vile? Kwanini awaadhibu na watu wasio na hatia kwa kosa la mwingine?...

Daudi hakufahamu sababu ya Mungu kufanya vile. Sasa ukisoma vizuri biblia, hiyo habari katika kitabu cha Samweli utaona jambo fulani pale la kuzingatia … Tusome

2 Samweli 24: 1 “TENA HASIRA YA BWANA IKAWAKA JUU YA ISRAELI, AKAMTIA DAUDI NIA JUU YAO, akisema, Nenda, ukawahesabu Israeli na Yuda. 2 Basi mfalme akamwambia Yoabu, jemadari wa jeshi la askari, waliokuwa pamoja naye, Zunguka sasa katikati ya kabila zote za Israeli, tangu Dani mpaka Beer-sheba, mkawahesabu watu, nipate kujua jumla ya hao watu”.

Unaona hapo ukisoma mstari wa kwanza utaona, kuna jambo wana wa Israeli walilifanya hapo kabla mpaka kupelekea hasira ya Mungu kuwaka juu yao..Kama ukisoma huko nyuma utagundua kuwa Mungu alikuwa hapendezwi na njia zao tangu siku nyingi, na ndio maana wakati mwingine alikuwa anawatia katika mikono ya wafilisti, na hapa pia vivyo hivyo, kuna mambo maovu walikuwa wanayafanya pengine kwa siri au hadharani (japo biblia haijaeleza hapo ni mambo gani) lakini ni dhahiri kuwa matendo yao yalimudhi Mungu sana, mambo kama kuabudu miungu migeni, rushwa, kudhulumu watu, mauaji yasioyo na hatia, kuhalifu sabato, kupitisha wana wao motoni, kuwaonea wajane na mayatima ni miongoni mwa vitu walivyokuwa wanavifanya wana wa Israeli kwa wakati ule..Hivyo Mungu akaamua kumtumia Daudi nia kama sababu ya kuwaadhibu makosa yao… Na ndio hapo tunakuja kuona Daudi anaingiliwa na shetani kufanya vile, kama tu vile Mungu alivyotaka kumwangamiza mfalme Ahabu akaruhusu Pepo la uongo likawavae wale manabii wake 400, kadhalika na Daudi naye aliingiwa na shetani kufanya mambo ambayo Mungu hakumwagiza , na baadaye tunaona tauni inakuja kuachiliwa juu ya Israeli ili Mungu kujilipizia kisasi juu yao wote waliomuudhi..

Hivyo wakati mwingine hata sisi kama taifa au mtu binafsi, tunaweza kufanya makosa, na Mungu akakusudia kutuadhibu kwa kupitia viongozi wetu, na ndio hapo unaweza kushangaa viongozi wanaonyesha tabia za ajabu kwetu au kwako, anakuwa mkatili au dikteta,sisi tukidhani kuwa yule kiongozi ndio kakengeuka, lakini kumbe nyuma yake ni Mungu kasimama kumruhusu kwa makusudi kabisa mtu yule atumiwe na ibilisi ili au kutufundishwe sisi adabu. Mfano unaweza kuona Mfalme Nebkadneza alikuwa ni diktekta, aliteka mataifa yote ulimwenguni kwa nguvu na akayatawala kwa mabavu..na hata Taifa la Mungu Israeli liliwekwa chini wa utawala wa Nebkadneza lakini ukiisoma biblia kwa makini utaona kuwa Mungu ndiye aliyemtia Nebkadneza nia ya kwenda kuteka mataifa yote ulimwenguni pasipo hata yeye Nebkadneza kufahamu chochote…Na Mungu alifanya vile ili kujilipizia kisasi kwa mataifa yote yaliyomwacha ikiwemo na Taifa la Israeli watu wake.

Hivyo tunapaswa tuwe makini na njia zetu tumwombe Mungu kila siku..Ili wengine wasifanyike kuwa fimbo ya Mungu kutuadhibu sisi.
SWALI 3: Baba mmoja Ananisimulia akisema, "Mimi hapa huwa ninasikia watu wanaosema wanakuja kunikamata.akaniuliza je! Na wewe unawasikia? Nikamwambia hapana mimi siwaskii[saa hiyo ni yeye tu anawaskia]. Akanichukua akanishika mkono Akaniambia"Unaskia hiyo nyimbo yangu wanaimba?(Mimi siisikii yeye peke yake anasikia)"Nikamwambia hapana" ANAOGOPA SANA. Sasa Juzi juzi Usiku nikamkuta amesimama hapa nje nyumbani kwetu Akiwa ameshika panga mkononi mwake akaniambia "Unamsikia bibi mmoja kule ng'ambo anasema nimebaka mjukuu wake[Kwa bibi huyo ni mbali na hapa kwetu]?"Nikamwambia hapana.Akarudi nyumbani na panga lake.[Wakati huo anaongea yuko siriazi kabisa].Wakati mwingine ananiambia aliowaona watu wamesimama mlangoni kwake.

Sasa Swali:Ndugu kwa nyinyi Muonavyo Hicho ni kitu gani?? KARIBUNI___ [Nilijaribu kumueleza habari ya kumpa Bwana maisha akasema ATAPAMBANA KIJESHI[Nilijuwa anamaanisha kwa waganga],Lakini namuona sasa hawezi kupambana kijeshi alivyosema].Hali yake inazidi kuongezeka Ikifika mahali Si ajabu akawa kichaa kabisa.
JIBU: Shalom, Mambo yanayoendelea katika roho ni mengi, na shetani naye kila kukicha anaongeza mapana ya maarifa yake…mtu akizama katika maarifa ya shetani (mfano uchawi)..anakuwa anauwezo wa kufanya vitu ambavyo kwa namna ya kawaida haviwezekani kufanyika…sasa kwa mtu kama huyo aliyekuja kukusimulia kuwa anasikia sauti za nyimbo, na ana uwezo wa kusikia mtu akizungumza akiwa mbali, ni wazi kuwa kuna roho ipo ndani yake na hiyo ni roho ya yule adui.

Kwanini ni roho ya adui, na si ya Mungu? kwasababu matunda ya hiyo roho ni ya yule adui, kumpeleka kwenye uovu na kumweka katika vifungo vya uoga,wasiwasi na mkandamizo… Kwasababu matunda ya Roho Mtakatifu sio hayo…ingekuwa ni Roho Mtakatifu yupo ndani ya huyo mtu ungeona matunda ya Roho ndani yake kama yalivyoandikwa kwenye kitabu cha Wagalatia 5:22 “Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria.”

Umeona hapo? Roho Mtakatifu akiwa ndani ya mtu hivyo vitu hapo juu lazima vionekane, amani, furaha,upendo n.k…Lakini roho iliyopo ndani ya huyo mtu haijamsukuma kwenye upole, wala haimpeleki kwenye furaha, wala uvumilivu, wala amani…zaidi ya yote umempeleka kwenye hofu, mashaka na ghadhabu…hivyo hiyo ni moja kwa moja roho ya yule mwovu ipo ndani yake.

Sasa Roho Mtakatifu akiwa ndani ya mtu huwa ni lazima atoe na kipawa fulani juu ya huyo mtu, ndio hapo anawapa wengine vipawa vya unabii, wengine lugha, wengine miujiza,ishara,uchungaji, ualimu,uinjilisti n.k [kumbuka vipawa vya Roho ni tofauti na matunda ya Roho].

kadhalika na roho za mashetani ni hivyo hivyo, mtu akiwa na pepo fulani la utambuzi, ni lazima litampa uwezo fulani,(ni kama karama yake fulani hivi) watu wengine shetani anawapa uwezo wa kufanya utambuzi, wanakuwa na uwezo wa kutambua siri za watu, au kuona vitu vinavyoendelea sehemu nyingine mbali na mahali walipo, hata wakati mwingine wanakuwa na uwezo wa kusikia sauti na mazungumzo ya watu waliopo mbali kama huyo mzee, wengine wanakuwa na uwezo wa kufanya viishara ishara fulani (mazingaumbe mazingambwe) wengine wanakuwa hawana huo uwezo lakini wanakuwa wanauwezo mwingine mkubwa wa ushawishi…wanaweza kumshawishi mtu au jamii na wakafanikiwa kuleta vitu vyenye madhara kwa kutumia hivyo vipawa walivyonavyo vya nguvu za giza.

Kwahiyo kwa habari ya huyo mzee ni kwamba kafungwa na nguvu za giza, aidha kwa kujua au kwa kutokujua, na kwasababu hamjui Yesu Kristo, inawezekana yeye akajihisi anakipawa kutoka kwa Mungu cha uwezo wa kujua na kuwasikia maadui zake mahali walipo, lakini ni roho ya adui ipo ndani yake, pasipo yeye kujijua,hivyo nakushauri, tenga muda umhubirie injili, ili macho yake ya rohoni yafumbuke,umweleze uwezo uliopo katika Yesu Kristo, na tumaini lililopo ndani ya Yesu Kristo, na Bwana akimpa Neema ya kuamini injili na kuipokea, mwekee mikono na kumwombea kwa Jina la Yesu na hizo roho zitamwacha atakuwa huru kabisa. Na akizingatia kutubu kwa kuacha dhambi zake kabisa na kwenda kubatizwa katika ubatizo sahihi, basi Bwana atampa kipawa cha Roho wake Mtakatifu kwasababu yeye mwenyewe alisema ahadi hiyo ni kwa watu wote waliompokea..Na akiisha pokea Roho Mtakatifu basi yale matunda ya Roho yataambata naye..atapata amani isiyokuwa ya kawaida, furaha ya ajabu, upendo wa ajabu, uvumilivu usioelezeka, upendo usiokuwa na mipaka na fadhili nyingi.

Bwana akubariki

HADITHI ZA KIZEE.


Mtume Paulo anamwambia Timotheo “Bali hadithi za kizee, ZISIZOKUWA ZA DINI, uzikatae; nawe ujizoeze kupata utauwa.”( 1Timotheo 4.7).

Hizi hadhithi za kizee ni zipi? (kwa kiingereza zinaitwa old wives’ tales). Ni Misemo na hadithi zilizotungwa na watu wa zamani, ambazo kwa kuzitazama kwa nje zinaonekana kama zina ukweli fulani ndani yake, lakini kimsingi hazina uhalisia wowote, ni hadithi za uongo. Karibu kila jamii zipo na naamini hata wewe ulishakutana nazo.

Kwa mfano embu jaribu kutafakari maneno haya ambayo pengine ulishawahi kuyasikia.

* Ukiwa unakojoa hakikisha unatema mate chini, vinginevyo mama yako atavimba matiti.

* Mtoto mchanga akiangalia kioo haoti meno,.
 
* Mtu akikuruka hutorefuka.

* Mtoto wa kike akikaa katikati ya mlango, hatoolewa
 
* Ukipita makaburini, ukanyoosha kidole chako kuelekea kule, king’ate mpaka kiume vinginevyo mama/baba yako atakufa.
 
* Binti akipika huku aimba, ataolewa mbali.
 
* Mwanaume asilie kwenye sufuria la sivyo siku ya ndoa yake mvua nzito itanyesha.
 
* Ukimuona albino usipojitemea mate kifuani mwako, basi wewe nawe utazaa albino. n.k N.K. zipo nyingi.
 
Sasa mambo haya, yameaminika kwa wengi, mpaka imefikia hatua licha tu ya kubakia kwenye jamii ya watu wasiomini (yaani watu wasio wakristo), sasa imefikia mpaka kwa watu wanaomfahamu Mungu, waliookoka . Siku moja nilisikia mtu mmoja anayejiita mtumishi wa Mungu kwenye Whatasapp, anaitwa Apostle Vincent Mkalla(samahani kwa kulitaja jina) akitoa ujumbe ambao umesambaa sana mitandaoni na unajulikana na wengi, katika ujumbe huo, alitoa habari ya mti mmoja ujulikanao kama mti MWAMVULI, akisema mti huu, ukiwa umepandwa nyumbani, basi fahamu kuwa utaleta mabalaa makubwa katika hiyo nyumba, anasema kwanza kabisa ukichunguza utaona kuwa baba ya nyumba hiyo lazima afe, pili, unaleta hali ngumu za kiuchumi katika familia, tatu unaleta magonjwa, na pia unasababisha familia kutawanyika, familia kuwa na madeni, pia watu wa nyumba hiyo wanajikuta wanapitia katika hali ya kulaumiwa pasipo kujua chanzo ni nini n.k.…na mambo mengine aliyoyasema pale kuhusiana na mti..
 
 
Lakini kilichonisikitisha zaidi wakati huo nilipokuwa ninasikiliza nilikuwa na mama mmoja, ambaye naye alikuwa anausikiliza kwa makini sana, kwa hofu akiamini kinachozungumzwa pengine ni kweli, na siku chache mbeleni nilikwenda nyumbani kwao, ambapo mti huo wenye kivuli ulikuwa umepandwa uwani, nikakutwa umekatwa, hali kadhalika niliporudi nyumbani kwetu kwa mama, nikakutwa umekatwa,maana hata nyumbani upo, na sehemu nyingine nyingi.. Kwa hofu kwamba madhara yatokanayo na mti huo waliosikia kutoka kwa mtumishi huyo wa Mungu yasiwakute.

Kaka/Dada hizi ni nyakati za mwisho na biblia inasema.. 1 Timotheo4 : 1-2”Basi Roho anena waziwazi ya kwamba nyakati za mwisho wenginewatajitenga na imani, wakisikiliza roho zidanganyazo, na mafundisho ya mashetani; 2 kwa unafiki wa watu wasemao uongo, wakichomwa moto dhamiri zao wenyewe;

Hizi ndizo siku hizo za mwisho, Na hizi ndio HADITHI ZA KIZEE ZISIZO ZA DINI Mtume Paulo anamwonya Timotheo ajiupushe nazo, ni mafundisho ya mashetani, hadithi ambazo zinafanya watu wapoteze shabaha ya kuujua uweza wa Mungu bila wao kujua wakidhani kuwa vitu vya asili vinaweza kuathiri hatma zao na sio mambo ya rohoni. Na hilo ndio linalowafanya wengi mpaka kufikia hatua ya kuabudu sanamu, kwasababu imani yao kidogo kidogo ilianza kuhamishwa kutoka kwa Mungu, na kuanza kuangalia mambo ya mwilini kama suluhisho la mambo yao na matatizo yao. Mwisho wa siku hata mtu akiwambiwa kaoteshe mkaratusi katikati ya shamba lako utapata hela atakwenda na kufanya hivyo kwasababu siku nyingi tayari alishahamishwa Imani yake kutoka katika Neno la Mungu na kuingizwa katika “Maashera” (ibada za masanamu), na pasipo yeye kufahamu hajui kuwa anamwabudu shetani mwenyewe..
 
Dada yangu tena sikumoja ananiambia ukiona mjusi au mende, kwenye nyumba hiyo ni ishara mbaya, ya kutokufanikiwa kiuchumi.

Siku nyingine nikakuta Ua moja ambalo sikujua maana yake, mpaka siku moja mama yangu mdogo ambaye amesema ameokoka aliponiambia ua lile, ni la Baraka linaeleza hali ya kiuchumi ya nyumba hiyo,likistawi basi uchumi unastawi, likisinyaa basi uchumi ni mdogo..Niliposikia vile nilisikitika sana rohoni.

Kumbukumbu 16:21 “Usipande mti uwao wote kuwa Ashera kwako kando ya madhabahu utakayofanya ya Bwana, Mungu wako”.

Sasa Yapo mambo mengi hatuwezi kuyasema yote hapa, yanafundishwa na baadhi ya watu wanaojiita ni watumishi wa Mungu na yanazidi kukithiri, na kusambaa, naamini hata na wewe ulishakutana yao.

Ndugu nataka nikuambie ukweli wa kibiblia hakuna ubaya wowote katika miti, ikiwa imepandwa kwa nia njema, hakuna ubaya wowote wa vyakula vya aina Fulani, ikiwa navyo vimepokelewa kwa shukrani kama biblia inavyosema, vyote vinatoka kwa Mungu, na vimeumbwa na Mungu..Kusema mti Fulani unasababisha kifo cha baba wa nyumba, jiulize ni nyumba ngapi duniani zimefiwa na wazazi wao,

Unaposema miti inasababisha hali mbaya kiuchumi ni familia ngapi duniani zinapitia matatizo ya kiuchumi?. Ndugu yangu, chanzo cha matatizo yote ni DHAMBI, na kutokumjua Kristo na uweza wake, lakini badala yake, wanafundisha chanzo cha mafarakano na magombano katika familia ni MITI, tangu lini mti ukimfarakanisha mtu na mtu?..Na mtu huyo anajiita ni mtumishi wa Mungu, na bado tena mkristo anamwamini mtu wa namna hiyo kisa tu katumia vipengele fulani vya maandiko kutibitisha uongo wake, na wengi wanamwamini, hujui kuwa hata shetani alitumia maandiko kuuthibitisha uongo wake kwa Yesu kule jangwani.

Hofu zimewakubwa watu wengi mpaka sasa, kila kitu wanachotokea hata kujikwaa kidogo tu anasema kalogwa, akipishana na paka, kuna mtu kamwendea kwa mganga, akipishana na mbwa mweusi usiku basi ni mchawi, sasa mbwa wa kweli atakuwa ni yupi? Kama kila mbwa ni mchawi, bundi wa kweli aliyeumbwa na Mungu atakuwa ni yupi kama wote ni wachawi, paka wa kweli aliye mweusi ambaye aliumbwa na Mungu atakuwa ni yupi kama kila paka mweusi ni mchawi,?...utasikia mwingine anakuambia jicho likicheza kidogo tu anasema kuna mtu anamsema, akipiga chafya kuna watu wanamtakia mabaya, huyo ni mkristo anazungumza maneno hayo. ..HADITHI ZA KIZEE zisizo na dini…

2Timotheo 4.3 “Maana utakuja wakati watakapoyakataa mafundisho yenye uzima; ila kwa kuzifuata nia zao wenyewe watajipatia waalimu makundi makundi, kwa kuwa wana masikio ya utafiti; 4 nao watajiepusha wasisikie yaliyo kweli, na kuzigeukia hadithi za uongo. 5 Bali wewe, uwe na kiasi katika mambo yote, vumilia mabaya, fanya kazi ya mhubiri wa Injili, timiliza huduma yako.”

Timotheo kama mwalimu alionywa ajiuepushe na injili za namna hiyo, hali kadhalika azikatae, azikemee zisifundishwe katika kanisa la Mungu, na sisi leo tunazikemea na tunazikataa zisifundishwe kwa watu..Leo watu wengi wanafahamu zaidi habari za uchawi na ushirikina kuliko hata kumjua Mungu, shuhuda zilizojaa kwenye kichwa vya watu ni uchawi tu, kana kwamba huo ndio msingi wa kuwa mtu wa rohoni. Na hiyo inapelekea watu kuwa WAOGA kwa shetani, kwasababu mioyo yao imejazwa shuhuda za shetani zaidi kuliko Mungu, Mtu anaogopa hata kusalimia, au kumsaidia mtu asiyemjua kwa hofu tu ya uchawi, lakini haogopi maneno ya Mungu yanayomkataza yeye kwenda kutenda dhambi za makusudi. Na siku zinavyozidi kwenda hofu hii inazidi kuongezeka katikati ya watu..(hususani wanaojiita wakristo).

Hivyo hata ukiwaeleza nguvu zilizokatika Neno la Mungu, haziwasaidii sana, kwasababu mioyo yao haijajazwa na Neno la Mungu bali Neno la Shetani. Kwasababu biblia inasema Hazina yako iliyo ndipo utakapokuwepo na moyo wako. Na hivyo kila elimu inayokuja inawachukua..leo hata wakiambiwa wasipange mchicha kwenye nyumba zao zinawaletea umaskini watafanya hivyo, kesho wakiambiwa wasitumie mafuta ya nazi ya roho za majini watatatii, kesho kutwa wakiambiwa wakate kidole gumba kinawaletea mikosi na wakithibitishiwa na maandiko mawili matatu, watafuata..kwasababu ndani yao kumjua Mungu hakupo..Biblia inasema Tumjue sana Mungu ili tuwe na AMANI sio tumjue sana shetani ndio tuwe na Amani…Elimu ya shetani haileti amani bali hofu.

Mtu akija kukuambia leo, kuna bundi nimemwona batini kwako jana usiku, na ni mchawi…kitakachofuata hapo ni hofu, na wala si kitu kingine, utaanza kuiogopa hata nyumba yako unayoishi…

Lakini leo hii utakaposikia elimu iliyopo katika uweza wa Mungu…Kwamba Kristo alitwaa madhaifu yetu na yeye anatupenda kiasi cha kutuhurumia, na tena anatuambia tuutafute kwanza ufalme wake na haki yake, Hakuna hata unywele wetu mmoja utakaopotea, na zaidi ya yote anatuambia sisi tuliomwamini kuwa Baba yetu wa mbinguni anatujali sisi kuliko baba zetu wa kimwili..Mambo hayo ukiyajua yanakupa amani na furaha katika wokovu…na hayakufanyi kuwa mateka zaidi yanakufanya kuwa huru, elimu ya mashetani ndio inayokufanya kuwa mateka, na matunda ya roho ya shetani ndio haya..uwoga, hofu, mashaka, kukosa raha, uchungu, wasiwasi,visasi, wivu, hasira, chuki n.k mambo haya yote yanazalishwa na roho za mashetani kupitia elimu zake. Na shetani ndio anataka mambo hayo yawepo ndani ya mtu, ili apate nafasi ya kumkandamiza kimawazo na kiakili, Lakini Roho Mtakatifu ndani ya mtu, hayupo hivyo na wala matunda yake hayapo hivyo ….matunda ya Roho wa Mungu ndio haya..

Wagalatia 5: 22 “Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, 23 upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria”.

Hizi ni nyakati za hatari ndugu yangu, mafundisho kama hayo yatazidi kuongezeka, hayataishia kwenye miti, wanyama, na vyakula, yataendelea mpaka kwenye mwili wako, na maumbile yako..Hivyo usipokuwa makini kwa kutaka kukaa chini na kujifunza zaidi uweza wa Mungu katika Neno lake, KUMJUA SANA MWANA WA MUNGU (Waefeso 4:13)…badala yake unapenda kutafuta njia za mwilini kutatua matatizo yako nataka nikuambie ukweli wote, shetani atakutesa sana, utakosa raha ya kuishi hata kama unajiita umeokoka… na mwisho wa siku utachukuliwa na wimbi hilo na manabii, na waalimu wa uongo, ambao hao Injili ya kweli ya Kristo ipo mbali nao.

Sina muda wa kutosha ningekupa mifano kadha wa kadhaa ya hawa watumishi wa shetani ambao mimi binafsi nimewahi kukutana nao..ambao wengine wanatumia mifupa, na nywele, na biblia kuchukua watu mateka na sana sana wanawake kwasababu wao ndio sana sana wanahangaika huku na kule kutafuta mambo ya rohoni…Watumishi hawa ni ngumu sana kuwagundua kwasababu shetani kawanoa vya kutosha kama hujui maandiko wanakuchukua…na target yao kubwa ni wanawake…

1 Timetho 3:5 “…wenye mfano wa utauwa, lakini wakikana nguvu zake; hao nao ujiepushe nao. 
6 Kwa maana katika hao wamo wale wajiingizao katika nyumba za watu, na kuchukua mateka wanawake wajinga wenye mizigo ya dhambi, waliochukuliwa na tamaa za namna nyingi; 7wakijifunza siku zote, ila wasiweze kabisa kuufikia ujuzi wa kweli. 
8 Na kama vile Yane na Yambre walivyopingana na Musa, vivyo hivyo na hawa wanapingana na ile kweli; ni watu walioharibika akili zao, wamekataliwa kwa mambo ya imani”.

2 Petro 1.16 “Maana hatukufuata hadithi zilizotungwa kwa werevu, tulipowajulisha ninyi nguvu zake Bwana wetu Yesu Kristo na kuja kwake; bali tulikuwa tumeuona wenyewe ukuu wake”.

Kristo alipokuwa duniani hakutuelekeza katika miti, wala vyakula, wala wanyama, wala hakutuhubiria habari za washirikina na wachawi, badala yake alitumia muda mwingi kutufundisha jinsi ya kuwa na mahusiano ya karibu na Baba yetu wa mbinguni kama yeye alivyokuwa kwa baba yake..Na hilo ndio jambo la muhimu kwasababu ukishajua nafasi yako kwa Mungu wako basi hayo mambo mengine hayatakusumbua, hutakuwa na hofu, ya kifo, au matatizo, au shida, au chochote kile kwasababu baba yako atakuwa pamoja na wewe wakati wowote kukusaidia…hutakimbilia kwenda kuisingizia miti, na paka, na mbwa, na bundi, na mijusi, na popo, na fisi, kwa hali unayoipitia…Badala yake Mungu ndiye atakayekuwa jibu lako wakati wote.

Hivi unajua kwamba wapagani wasiomjua Mungu, hawakuanza hivi hivi kuabudu miti na mawe?..unalijua hilo?..walianza kidogo kidogo kufikiri tatizo Fulani linasababishwa na miti Fulani au mawe Fulani, na walipoisafisha ile miti na yale mawe waliona kama matatizo yameondoka lakini walipoona kuwa kuna mengine ni sugu..waliona njia pekee ni kwenda kwa unyenyekevu chini ya hiyo miti..kuiomba kwa upole na utaratibu iwaondolee hayo matatizo na endapo hayo matatizo yataondoka basi wanaahidi kuifanyia jambo Fulani labda kuipa heshima Fulani..na kwasababu ni shetani yupo nyuma ya ule mti..anaondoa lile tatizo lao kwa muda na wale wanadhani ni mti umesikia maombi yao, hivyo wanaugeuza ule mti kuwa mungu wao..na shetani anatuma maroho yake kuwaingia wale watu wakati mwingine wanaanza kuota ndoto zinazoutukuza ule mti au wengine wanaona vitu vya ajabu kwenye ule mti n.k..lengo ni kutoa umakini wao kumhusu Mungu wa Mbinguni na kuwaleta kuamini miti na mawe kama miungu…Na haishii hapo akishajua watu wameuamini ule mti kupita kiasi..anawapa mpaka nafasi ya wao kuomba maombi yao au kupeleka mahitaji yao kwenye ule mti na akawafanyia…

Sasa roho hiyo hiyo ndio inayoingia kwa kasi katika kanisa katika siku hizi za mwisho, wengi wanaingizwa kwenye ibada za sanamu pasipo wao kujijua, shetani anahamisha umakini wa watu kumhusu Mungu wa Kweli wa Mbinguni na kuwatengenezea watu miungu ya kuiabudu, miti, mawe, sanamu n.k

Warumi 8: 35 “Ni nani atakayetutenga na upendo wa Kristo? Je! Ni dhiki au shida, au adha, au njaa, au uchi, au hatari, au upanga?........ 
38 Kwa maana nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo, 
39 wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu".

Ni matumaini yangu kuwa umepata kitu na utazidi kuchukua tahadhari juu ya hizi HADITHI ZA KIZEE, na kuanza kumtazama Mungu ili njia zetu ziwe zimenyooka siku zote.Na tuwe na Amani.

Ubarikiwe.

UFUFUO WA UZIMA NA WA HUKUMU.


Shalom, Mtu wa Mungu karibu tujifunze Injili, uweza wa Mungu uuletao wokovu, leo tutajifunza kwa ufupi juu ya NGUVU YA UFUFUO ILIYOPO NDANI YA YESU KRISTO. Katika kitabu cha Yohana tunasoma maneno yafuatayo aliyoyazungumza Bwana Yesu.

Yohana 5: 25 “Amin, amin, nawaambia, Saa inakuja,na sasa ipo, wafu watakapoisikia sauti ya Mwana wa Mungu, na wale waisikiao watakuwa hai.
26 Maana kama vile Baba alivyo na uzima nafsini mwake, vivyo hivyo alimpa na Mwana kuwa na uzima nafsini mwake.
27 NAYE AKAMPA AMRI YA KUFANYA HUKUMU KWA SABABU NI MWANA WA ADAMU.
28 Msistaajabie maneno hayo; kwa maana saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini WATAISIKIA SAUTI YAKE.
29 Nao watatoka; wale waliofanya MEMA KWA UFUFUO WA UZIMA, na wale WALIOTENDA MABAYA KWA UFUFUO WA HUKUMU”.

Katika mistari hiyo Biblia inasema Mwana kapewa amri na Baba ya kufanya hukumu na tena amepewa uwezo wa kufufua wafu kama vile Baba alivyo na uwezo wa kufufua wafu, tunayasoma hayo juu kidogo katika Yohana 5: 21 “Maana kama Baba awafufuavyo wafu na kuwahuisha, vivyo hivyo na MWANA AWAHUISHA WALE AWATAKAO”.

Kama wengi wetu tunavyofahamu kuwa kuna ufufuo utakaokuja baada ya maisha haya kuisha ambapo wale wote waliotenda haki watafufuliwa na kuurithi uzima wa milele, na wale wote waliotenda mabaya watafufuliwa kwaajili ya hukumu, na kila mmoja atahukumiwa kulingana na matendo yake na wale waovu watatupwa katika lile ziwa la moto, lenye moto usiozimika, waangamie milele.

Sasa jambo la kujiuliza hapa ni kwanini, Bwana Yesu awafufue wale waovu na kisha awahukumu na awatupe katika ziwa la moto…kwanini asingewaacha huko huko mautini, awahukumu huko huko na kuwatupa kwenye lile ziwa la moto wakiwa huko huko mautini, kuna umuhimu gani au haja gani ya wao kufufuliwa na tena wakati kuzimu wataenda tu??.
 
Kuna siri nzito sana hapo. Lakini kwa ufupi ni kwamba, siku ile ya hukumu watu wote waovu watavaa miili yao waliyokuwa nayo hapa duniani..yenye damu na mifupa na macho na moyo, na kusimama mbele za Bwana, na kisha kuongea naye ana kwa ana, kutoa hesabu kwa kila jambo na kila uovu waliokuwa wanaufanya, mbele ya kiti cha Hukumu…Jambo hilo halitafanyika mtu akiwa katika roho, hapana bali litafanyika mubashara kabisa katika mwili kama tulivyo hapa duniani…Na katika ziwa la moto mtu hatatupwa katika roho, bali atatupwa akiwa na mwili wake wa damu na nyama, na utaungua kule na ukiisha ndipo roho itaendelea nayo kuteseka milele kwenye huo moto milele.

Kwahiyo leo hatutaingia sana huko, lakini napenda tujifunze Nguvu ya ufufuo.
Ukiutafakari kwa makini mstari huo utakuja kugundua kuwa Kumbe Ufufuo sio tija. Kwasababu watu wote watafufuliwa, waovu na wema..kinachojalisha ni sababu ya kufufuliwa kwako. Kama mtu alikuwa mcha Mungu basi ufufuo kwake utakuwa wa maana, lakini kama alikuwa mwovu basi ufufuo kwake utakuwa ni laana.

Na ufufuo maana yake, ni “kukirudishia tena uhai au maisha kitu kile kilichokuwa kimekufa”..hiyo ndio maana ya ufufuo.
 
Sasa kuna ufufuo wa roho ambao unaendelea sasahivi, ambapo watu wote WANAISIKIA SAUTI YA MWANA WA ADAMU, na wanafufuka kutoka kwa wafu katika roho…Na sauti ya mwana wa Adamu ni Habari njema inayohubiriwa duniani kote leo, habari za msalaba na wokovu uliopo katika Kristo Yesu, sasa wapo ambao wanafufuka kwaajili ya uzima wa milele na wapo ambao wanafufuka kwaajili ya hukumu.

 
Wako ambao pindi tu wanapoisikia injili macho yao yanafumbuliwa (wanafufuka katika roho), hii inatokea pale ambapo wanachomwa dhamiri zao ndani ya mioyo yao, na kujijua kuwa njia zao sio sawa, hivyo kwa moyo mnyoofu wanaitii injili na kuokoka kikamilifu,wanaacha njia zao mbaya za kale, na kuzaliwa mara ya pili wakati huo huo na kuwa viumbe vipya.

Na wapo pia ambao wanapoisikia tu injili macho yao yanafunguka (wanafufuka) na kujua kabisa ndani ya mioyo yao Neno la Mungu ni kweli, na Roho Mtakatifu anawashuhudia kabisa kuwa Njia ya wokovu ni hii, na njia wanayoiendea wao sio sawa…Roho anawafufua katika roho zao, lakini kwasababu wanapenda giza kulika Nuru wanaikataa ile njia ya kweli,..na kwa makusudi, hawataki kugeuka na kutubu, wanaendelea na njia zao mbaya, hawa ndio wanaofufuliwa sasa kwa ajili ya hukumu. Wanayafumba macho yao kwa makusudi ingawa wamepewa neema ya kuona..Wanafahamu kabisa hata wakifa sasa hivi wanastahili Jeahanum ya Moto, lakini bado hawataki kutubu. Hawa wamefufuliwa kwa ajili ya Hukumu.

Kwahiyo ndugu unayesoma ujumbe huu, usifurahie tu Roho wa Mungu anapokushuhudia ndani yako kuwa KRISTO ndiye njia ya kweli na uzima, huo ni ufufuo tu! Ambao hata waovu wanapewa…hata waovu katika nyakati hizi za mwisho wanapewa neema hiyo mioyoni mwao kujua kuwa Kristo ni njia ya kweli na uzima, na kwamba hakuna uzima wowote nje yake yeye.. Hiyo ni neema ya ufufuo ambayo watu wote wanapewa waovu na wema..Lakini swali ni je! Unafufuliwa kwa sababu gani?.

Kama unaisikia injili kila siku inayokuambia ulevi, uasherati, utukanaji, rushwa,uvaaji mbaya ni dhambi, mustarbation, usagaji, na pornography…na ndani ya moyo wako unajua kabisa ni kweli ni dhambi kufanya mambo hayo..fahamu tu! Ufufuo uliopewa ni wa hukumu na sio wa uzima wa milele, haijalishi unayajua maandiko kiasi gani, au umezungumza na malaika kiasi gani,au umemwelewa Kristo kiasi gani, au umeponywa na Yesu kiasi gani,

Mtume Paulo kwa uwezo wa Roho aliandika habari za watu hawa wafanyao dhambi kwa makusudi huku wakijua kabisa wanayoyatenda sio sawa…Wameisikia injili (wakapata ufufuo katika roho zao)..lakini ufufuo wao ukawa ni wa mauti.

Warumi 1: 18 “Kwa maana ghadhabu ya Mungu imedhihirishwa kutoka mbinguni juu ya uasi wote na uovu wa wanadamu waipingao kweli kwa uovu.
19 Kwa kuwa mambo ya Mungu yanayojulikana yamekuwa dhahiri ndani yao, KWA MAANA MUNGU ALIWADHIHIRISHIA.
20 Kwa sababu mambo yake yasiyoonekana tangu kuumbwa ulimwengu yanaonekana, na kufahamika kwa kazi zake; yaani, uweza wake wa milele na Uungu wake; HATA WASIWE NA UDHURU
21 kwa sababu, walipomjua Mungu hawakumtukuza kama ndiye Mungu wala kumshukuru; bali walipotea katika uzushi wao, na mioyo yao yenye ujinga ikatiwa giza.
22 Wakijinena kuwa wenye hekima walipumbazika;
23 wakaubadili utukufu wa Mungu asiye na uharibifu kwa mfano wa sura ya binadamu aliye na uharibifu, na ya ndege, na ya wanyama, na ya vitambaavyo.
24 Kwa ajili ya hayo Mungu aliwaacha katika tamaa za mioyo yao, waufuate uchafu, hata wakavunjiana heshima miili yao.
25 Kwa maana waliibadili kweli ya Mungu kuwa uongo, wakakisujudia kiumbe na kukiabudu badala ya Muumba anayehimidiwa milele. Amina.
26 Hivyo Mungu aliwaacha wafuate tamaa zao za aibu, hata wanawake wakabadili matumizi ya asili kwa matumizi yasiyo ya asili;
27 wanaume nao vivyo hivyo waliyaacha matumizi ya mke, ya asili, wakawakiana tamaa, wanaume wakiyatenda yasiyopasa, wakapata nafsini mwao malipo ya upotevu wao yaliyo haki yao.
28 Na kama walivyokataa kuwa na Mungu katika fahamu zao, Mungu aliwaacha wafuate akili zao zisizofaa, wayafanye yasiyowapasa.
29 Wamejawa na udhalimu wa kila namna, uovu na tamaa na ubaya; wamejawa na husuda, na uuaji, na fitina, na hadaa; watu wa nia mbaya, wenye kusengenya,
30 wenye kusingizia, wenye kumchukia Mungu, wenye jeuri, wenye kutakabari, wenye majivuno, wenye kutunga mabaya, wasiowatii wazazi wao,
31 wasio na ufahamu, wenye kuvunjamaagano, wasiopenda jamaa zao, wasio na rehema;
32 ambao wakijua sana hukumu ya haki ya Mungu, ya kwamba wayatendao hayo wamestahili mauti, wanatenda hayo, wala si hivyo tu, bali wanakubaliana nao wayatendao”.
Unaona Biblia inasema..”kwa maana walipomjua Mungu hawakumtukuza” na inasema “Mungu aliwadhihirishia ndani yao”..ikiwa na maana kuwa watu hawa, nuru ya haki iliwazukia ndani yao, au kwa lugha nyepesi tunaweza kusema ufufuo ulipita ndani ya roho zao, wakaiona kweli na kuiamini lakini walipoiamini hawakuifuata!..Hilo ndio jambo la kuogopesha, mtu anauona ukweli lakini haufuati…Nimewahi kuona madaktari bingwa ambao wanajua elimu yote ya biolojia ya ini na figo, na ni washauri wazuri wa kushauri watu wasitumie pombe na sigara kwani ni hatari kwa afya zao, lakini wao ndio watumiaji wakubwa wa mambo hayo, na wanakufa kwa magonjwa hayo hayo…Na ukiwauliza kwanini wanafanya hivyo na hali wanajua kwa kina na mapana madhara ya hivyo vitu katika mwili, zaidi hata ya watu wengine wanavyojua…wanakujibu basi tu! Nimeamua na nimependa kufanya hivyo, na atazidi kukuambia yupo tayari kufa na wala haogopi.

Sasa watu wa namna hii pia wapo katika Kanisa la Kristo, wanajua kabisa uzinzi ni dhambi, kwamba waasherati wote sehemu yao ni katika lile ziwa la moto, na wengine wamepewa maono na ndoto za jehanamu wameonyeshwa mahali wanawake wanaovaa vimini na suruali walipo lakini hao hao utawakuta wanaendelea kufanya hivyo bila uoga wowote. Ni kwasababu gani wanafanya hivyo? Ni kwasababu wapo katika ufufuo wa hukumu. Mpaka unaweza ukasema kwanini Mungu awafunulie mioyo yao waiamini injili halafu na bado wasiifuate si ni bora asingewapa kabisa neema hiyo..kuliko kuwapa halafu wasiifuate?..Jibu ni rahisi… “kila mtu lazima aisikie sauti ya mwana wa Adamu na kutoka kaburini aliko”.

Kadhalika pia usifurahie kwasababu kazi yako iliyokuwa imekufa ikafufuliwa tena, kwasababu huo unaweza ukawa ni ufufuo wa mauti kwako, furahia kazi yako kufufuka kwa ajili ya ufufuo wa uzima..

Unapokwenda kuombewa kazi yako au afya yako na kupona, na kisha maisha yako hayageuki hata kidogo, zaidi ya yote ndio unakuwa mbaya kuliko ulivyokuwa hapo kwanza, hujisikii vibaya kuendelea na uasherati wako, wala kiburi chako, nataka nikuambie hiyo ni dalili moja wapo ya kazi yako kufufuliwa kwa ajili ya hukumu yako mwenyewe,..hiyo kazi yako yako itakuwa kitanzi kwako cha kukuua na hatimaye kukupeleka katika ziwa la moto…Biblia inasema “…Na kufanikiwa kwao wapumbavu kutawaangamiza Mithali 1:32”.

Kwahiyo furahia pale kazi yako inapofufuka na kustawi na inazidi kukufanya kuwa mtakatifu na mkamilifu mbele za Mungu, mali zako zinapoongezeka ndipo na kiwango chako cha usafi kinavyozidi kupaa..hapo kazi yako itakuwa imefufuliwa kwa ufufuo wa uzima. Haitakupeleka jehanamu.

Bwana akubariki sana, kama hujampa Yesu Kristo maisha yako…usikawie kawie, kama amezungumza nawe moyoni mwako zaidi ya mara moja na kukushuhudia kuwa njia unayoiendea sio sawa, na wewe mwenyewe umehakikisha jambo hilo moyoni mwako, usijaribu kwenda kutatufa visababu vya kujihalalishia njia zako. Mtii leo, yeye anawakubali wakosaji, na anasamehe dhambi, akikusamehe amekusamehe kweli kweli hana visababu sababu vidogo vidogo vya kukushitaki tena au kukulaumu..Unakuwa mpya kabisa mbele zako.

Waefeso 5.14 “Hivyo husema, Amka, wewe usinziaye, Ufufuke katika wafu, Na Kristo atakuangaza.”

kwahiyo Hapo ulipo tubu, dhamiria kuacha dhambi zote ulizokuwa unazifanya nyuma, Fufuka sasa katika ufufuo wa Uzima katika jina La Yesu, na sio ufufuo wa Mauti, mfanye Bwana kuwa tumaini lako kuanzia leo na kuendelea.. Na baada ya kutubu katafute ubatizo kwani ni wa umuhimu sana kukamilisha wokovu wako na ni maagizo ya Bwana mwenyewe aliyoyatoa kwamba ni lazima kila mtu aliyempokea yeye akabatizwe, na ubatizo sahihi ni wa kuzamishwa katika maji mengi na kwa jina la Yesu Kristo kulingana na Matendo 2:38, na Bwana mwenyewe atakupa kipawa cha Roho wake mtakatifu atakayekusaidia kushinda dhambi na kukuongoza katika kuijua kweli yote ya maandiko.

Bwana akubariki.

MADARAKA YA WAKATI MKAMILIFU.


Shalom mtu wa Mungu, ni kwa rehema za Bwana tumeiona siku ya leo, hivyo hatuna budi kumshukuru sote pamoja kwa mema anayotutendea na pia kushiriki katika kujifunza maagizo yake kila iitwapo leo. Hivyo nakukaribisha tutafakari kwa ufupi juu ya haya “madaraka ya wakati mkamilifu” yanayozungumiwa kwenye maandiko, tutayaona ni yapi, na yatakuja wakati gani?.
Biblia inasema.
Waefeso 1:9 “akiisha kutujulisha siri ya mapenzi yake, sawasawa na uradhi wake, alioukusudia katika yeye huyo.
10 Yaani, KULETA MADARAKA YA WAKATI MKAMILIFU atavijumlisha vitu vyote katika Kristo, vitu VYA MBINGUNI na vitu VYA DUNIANI pia. Naam, katika yeye huyo;
11 na ndani yake sisi nasi tulifanywa urithi, huku tukichaguliwa tangu awali sawasawa na kusudi lake yeye, ambaye hufanya mambo yote kwa shauri la mapenzi yake.”
Sasa Kama ukisoma huo mstari wa 10 kwenye tafsiri nyingine za biblia kwa lugha iliyo nyepesi unaweza kusomeka hivi,
“Wakati mkamilifu utakapofika, basi vitu vyote ya mbinguni na duniani vitajumuishwa pamoja kwa yeye huyo..Au wakati uliokusudiwa (wa Mwisho) basi mambo yote ya mbinguni na ya duniani yataletwa pamoja katika yeye huyo (KRISTO YESU)..
Ndugu tukimjua Kristo, na ukuu wake na uweza wake, basi hatutaishi maisha ya kutokujali tu, tukiwa hapa duniani, hatutauchukulia ukristo wetu kama kitambulisho cha dini tu kama wengine wanavyofanya badala yake tutaishi kwa mitume wa zamani walivyoishi,..Leo Tunaishi maisha ya uvuguvugu na machafu kila siku na huku bado tunajiita ni wakristo, ni kwasababu tumekosa ufunuo wa kumjua Yesu Kristo ni nani katika maisha yetu, tumekosa shabaha ya kufahamu ni mambo gani na gani yalimfanya Yesu kuja duniani, tunadhani alikuja kufa tu msalabani halafu basi, na sasa ameketi mkono wa kuume wa Mungu mbinguni akisubiria kurudi tena kuja kunyakua watu wake….Hatujui mengine zaidi ya hayo.

Hiyo ndio sababu inayotufanya tunaishi maisha ya kuukinai wokovu, tunaposoma habari za watu ambao walijitoa maisha yao, watu ambao hawakupenda maisha yao hata kufa kwa ajili ya Bwana, tukisoma habari ya Ibrahimu ambaye japo Mungu alimpa kila kitu lakini aliishi kama mpitaji hapa duniani kukaa kwenye mahema, akiutazamia mji wenye misingi (YERUSALEMU MPYA),sio hii ya sasa inayoharibika,(Waebrania 11:8)…watu ambao Mungu aliwapa kila kitu lakini hawakupumbazwa na vitu walivyopewa, macho yao wakati wote yalielekea juu, mfano wa Ibrahimu na Ayubu…Sio kana kwamba walikuwa hawajipendi hapana bali waliona mbele, walipokea ufunuo wa mambo yanakuja na hivyo wakaanza kujijengea misingi mizuri kuanzia hapa duniani ili wakifika kule, iwe heri kwao. Lakini sisi tunaona wokovu ni kama kitu-baki, ni kitu tu cha ziada, na sio kila kitu katika maisha yetu.

Hatujui kuwa Kristo sasa yupo katika hatua za mwisho kabisa za kutimiliza mambo yake yote, na yeye mwenyewe hakutuficha siku anakwenda kwa Baba alisema, “ninakwenda kuwaandalia makao”,

Sasa ni vizuri kufahamu kuwa Kristo alipokuwepo duniani alikuja kufanya upatanisho wa kitu vikuu vitatu.

1) UPATANISHO KATI YA SISI KWA SISI

2) UPATANISHO KATI YA SISI NA MUNGU

3) UPATANISHO KATI YA MBINGU NA DUNIA.

Kristo alikuja kutupatanisha sisi kwa sisi, kumbuka hapo mwanzo wayahudi (yaani Waisraeli) walikuwa hawachangamani na mataifa kabisa, Israeli limekuwa likijulikana ni Taifa teule la Mungu, Mungu alilolibariki kupitia Ibrahimu. Ilikuwa hakuna namna yoyote ile sisi watu wa mataifa tungeweza kumfikia Mungu, lakini kwa kupitia Bwana Yesu, sisi ambao tumezaliwa mara ya pili ni mamoja sawa na wayahudi, mbele za Mungu hakuna aliye juu ya mwenzake, bali wote tunakubaliwa sawa kwa kupitia damu ya Kristo. Hiyo ni nafasi kubwa sana ya upendeleo..Jaribu kufikiria taabu walizozipata wengine kwa muda mrefu sisi tunakuja kuzila kiuwepesi namna hiyo. Ni neema kubwa sana. Jambo hilo unaweza kulipata katika kitabu cha Waefeso..

Waefeso 2: 11 “Kwa ajili ya hayo kumbukeni ya kwamba zamani ninyi, mlio watu wa Mataifa kwa jinsi ya mwili, mnaoitwa Wasiotahiriwa na wale wanaoitwa Waliotahiriwa, yaani, tohara ya mwilini iliyofanyika kwa mikono;
12 kwamba zamani zile mlikuwa hamna Kristo, mmefarakana na jamii ya Israeli, wageni wasio wa maagano ya ahadi ile. Mlikuwa hamna tumaini, hamna Mungu duniani.
13 Lakini sasa, KATIKA KRISTO YESU, ninyi mliokuwa mbali hapo kwanza mmekuwa karibu kwa damu yake Kristo.
14 Kwa maana yeye ndiye amani yetu, ALIYETUFANYA SISI SOTE TULIOKUWA WAWILI KUWA MMOJA; AKAKIBOMOA KIAMBAZA CHA KATI KILICHOTUTENGA.
15 Naye akiisha kuuondoa ule uadui kwa mwili wake; ndiyo sheria ya amri zilizo katika maagizo; ili afanye hao wawili kuwa mtu mpya mmoja ndani ya nafsi yake; akafanya amani.
16 AKAWAPATANISHA WOTE WAWILI NA MUNGU KATIKA MWILI MMOJA, KWA NJIA YA MSALABA, AKIISHA KUUFISHA ULE UADUI KWA HUO MSALABA.
17 Akaja akahubiri amani kwenu ninyi mliokuwa mbali, na amani kwao wale waliokuwa karibu.
18 Kwa maana kwa yeye sisi sote tumepata njia ya kumkaribia Baba katika Roho mmoja.
19 Basi tangu sasa ninyi si wageni wala wapitaji, bali ninyi ni wenyeji pamoja na watakatifu, watu wa nyumbani mwake Mungu”.

Hali kadhalika Kwa kumwamini tu Yesu na uweza katika damu yake, basi moja kwa moja tunakuwa tumepatanishwa na Mungu na hivyo tunakuwa na uwezo wa kupakaribia patakatifu pa patakatifu mahali Mungu alipo juu sana, na kuzungumza naye uso kwa uso katika roho, na kupokea rehema itokayo kwake. mambo ambayo hapo mwanzoni hayakuwepo, ilikuwa ni kuhani mkuu tu, alipelekea maombi yake katika maskani iliyofanywa na wanadamu huku chini mfano wa ile ya mbinguni, kisha Kerubi wa Mungu pale chini ndiye aliyekuwa anayachukua hayo maombi na kuyasogeza mbele ya kiti cha enzi cha Mungu huko juu mbinguni, lakini sasa kwa kupitia damu ya Yesu, sisi wenyewe tuingia moja kwa moja mbinguni kwa damu ya Yesu, na kupeleka haja zetu na majibu ya maombi yetu, sawa tu na makerubi na malaika wa Mungu walio mbinguni, sisi na wao hatuna tofauti yoyote, mbele za Mungu tukiwa ndani ya Kristo ni kitu kimoja.

2 Wakorintho 5: 17 “Hata imekuwa, mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya; ya kale yamepita tazama! Yamekuwa mapya.
18 Lakini vyote pia vyatokana na Mungu, ALIYETUPATANISHA SISI NA NAFSI YAKE KWA KRISTO, NAYE ALITUPA HUDUMA YA UPATANISHO;
19 yaani, Mungu alikuwa ndani ya Kristo, akiupatanisha ulimwengu na nafsi yake, asiwahesabie makosa yao; naye ametia ndani yetu neno la upatanisho”.

Na Jambo lingine la mwisho Kristo aliloleta NI KUIJUMUISHA MBINGU NA NCHI KUWA KITU KIMOJA..vitu vya mbinguni na vitu vya dunia, Sasa Hakuna yoyote ambaye angeweza kufanya jambo hili, inahitaji nguvu ya ajabu inayovuka viwango vya fikra za kibinadamu, inahitaji iwe muumba kufanya shughuli hii..
 
Wakolosai .1:9 “Kwa kuwa katika yeye ilipendeza utimilifu wote ukae; 20 na kwa yeye kuvipatanisha vitu vyote na nafsi yake akiisha kufanya amani kwa damu ya msalaba wake; KWA YEYE, IKIWA NI VITU VILIVYO JUU YA NCHI, AU VILIVYO MBINGUNI”.

Sasa jambo hilo ndilo linalokuja kutokea katika WAKATI MKAMILIFU ULIOKUSUDIWA, Yesu aliposema naenda kuwaandalia makao, ili nilipo mimi na nyinyi muwepo, na makao hayo yamegawanyika katika sehemu tatu, ya kwanza ni makao ya roho zetu ambayo hata sasa sisi tuliopokea Roho Mtakatifu tupo ndani yake, Waefeso 2: 6 “Akatufufua pamoja naye, akatuketisha pamoja naye katika ulimwengu wa roho, katika Kristo Yesu;

Na makao ya pili ni MIILI MIPYA ambayo tutaipokea tukifika mbinguni miili isiyoharibika, na makao ya tatu ndio hiyo NCHI MPYA NA MBINGU MPYA…Ambayo hiyo sasa itashuka kutoka mbinguni na kutua hapa duniani…Itashuka Hapa hapa duniani hatutaishi mbinguni milele, makao yetu yatakuwa ni hapa maandiko yanasema hivyo.

Na ndio hapo hilo neno linalosema “atavijumlisha vitu vyote katika Kristo, vitu vya mbinguni na vitu vya duniani pia.” Ndipo litakapotimia,

Ndugu yangu Kristo anayo nafasi kubwa sana maishani mwetu, kwanza kati yetu sisi wanadamu, pili kati yetu sisi na Mungu na tatu kati ya makao yetu ya sasa na ya yale ya baadaye..Embu jaribu kufikiria, ikiwa leo hii hutaweza kuzishiriki Baraka za Ibrahimu tu ambazo Mungu alimwahidia yeye na uzao wake (Wayahudi) kuwa watakuja kuirithi nchi, japo kweli walikuwa vile lakini bado hawakuweza kumkaribia Mungu, sasa wewe ambaye sasa ni mtu wa mataifa na bado huna habari na Kristo siku ile utaonekania wapi?..Itawezekanikaje kumfikia Mungu, au utamshawishi vipi Mungu hata akusikie maombi yako sasa wewe ambaye unasua sua katika mawazo mawili.

Hujapatanishwa, na Wayahudi, hujapatanishwa na Mungu, bado hujapatanishwa na hayo makao mapya yanayokuja huko mbeleni, unatagemea vipi, Mbingu utaiona ndugu?. Matumaini yako ni nini?, tegemeo lako lipo kwa nani?...
 
Muda umekaribia wa madaraka ya wakati mkamilifu kuanza, Kristo kuvileta vitu vyote pamoja, chini ya mikono ya MUNGU..lakini wale wote wanaopinga, biblia inasema kitakachosalia kwao ni kuangamizwa milele.

Yesu yupo mlangoni ndugu yangu, fanya uamuzi sasa, wakati ndio huu, pokea kuponi yako sasa ya kuwa na uhakika wa maisha baada ya kufa, ulimwengu huu unaousumbukia unakuahidia nini miaka yako 100 mbeleni kama sio ukomo wa mauti?. Kwanini usikubali NEEMA HII YA UPATANISHO inayokuja kwako bure, ingekuwa ni wanadamu ungejaza fomu ngapi ili ukubaliwe tu uwe raia wa taifa fulani?, ungejaza fomu ngapi ili ukubaliwe kuwa mrithi wa taifa fulani?, ungejaza form ngapi ili ufikie tu kigezo cha kumfika raisi wa taifa fulani?. Lakini kwa Mungu haipo hivyo, vyote hivyo ni bure, na vinapatikana hata hapo ulipo sasa hivi.

Chukua maamuzi sasa, kabla ya mlango wa neema kufungwa. Unachopaswa kufanya hapo ulipo ni kutubu kabisa dhambi zako kwa kukusudia kuziacha,..unakusudia kuacha ulevi, anasa, wizi, uasherati uongo, uvaaji usio na maadili, na kila aina ya uchafu, Kisha hatua inayofuata ni kwenda kubatizwa, hakikisha unabatizwa katika ubatizo ulio sahihi wa kimaandiko, yaani ni ule wa kuzamishwa katika maji mengi, na kwa jina la YESU KRISTO, (zingatie hilo uwe ni kwa jina la YESU) sawasawa na maandiko (Matendo 2:38, 8:16, 10:48, 19:5), ili upate ondoleo la dhambi zako. Na baada ya hapo Mungu mwenyewe atakupa kipawa cha Roho Mtakatifu, atakayekusaidia kushinda dhambi na kukuongoza katika kuijua kweli yote ya maandiko Yohana 16:13.

Na kuanzia hapo utakuwa na nafasi ya kuwa mshirika wa mambo yote ya kimbinguni Mungu aliokusudia kuwafunulia watoto wake.

1Wakorintho 2:9 “lakini, kama ilivyoandikwa, Mambo ambayo jicho halikuyaona wala sikio halikuyasikia, (Wala hayakuingia katika moyo wa mwanadamu,) Mambo ambayo Mungu aliwaandalia wampendao.”

Ni maombi yangu utafanya hivyo sasa.
 
Tafadhali “SHIRIKI” ujumbe huu na wengine.Bwana akubariki sana.