"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Friday, May 17, 2019

NEHUSHTANI (NYOKA WA SHABA).


Musa alipewa maagizo na Mungu atengeneze nyoka wa shaba, amning’inize ili wale wote waliomuasi Bwana watakapomtazama nyoka Yule wapone saa ile ile.
Hesabu 21: 8 ‘’Bwana akamwambia Musa, Jifanyie nyoka ya shaba, ukaiweke juu ya mti, na itakuwa kila mtu aliyeumwa, aitazamapo ataishi. 9 Musa akafanya nyoka ya shaba, akaiweka juu ya mti, hata ikiwa nyoka amemwuma mtu, alipoitazama ile nyoka ya shaba, akaishi’’.
Lakini Mungu hakuwahi kuwaagiza Wana wa Israeli kuwa wakati wowote watakapokutana na madhara au matatizo basi wamsimamishe nyoka wa shaba wamtazame ili watapona, hakuwahi kufanya hivyo, lakini wana wa Israeli walitazama wakagandua SIRI ndani yake, wakasema ni lazima kutakuwa na uponyaji Fulani kwenye nyoka wa shaba kama sivyo Mungu asingemwagiza Musa kuiunda, hivyo ngoja tujijengee utaratibu wetu, wa kuifanyia ibada, na kumwomba Mungu kupitia ile naye Mungu atatusikia dua zetu..

Hivyo hilo jambo lilikuja kuendelea hivyo kwa mamia ya miaka mbeleni, mpaka likajengewa madhabahu kubwa na kuwa jambo maarufu sana Israeli, watu wakawa wanakwenda kuiinamia ile sanamu ya nyoka na kumwomba Mungu wa Israeli kupitia ile awaponye matatizo yao, wakaifukizia uvumba..

Hawakujua hilo lilikuwa ni chukizo kubwa sana kwa Mungu ndilo lililowapelekea hata kukumbana na matatizo yote yale ikiwemo kuchukuliwa utumwani tena.. Ndipo sasa baada ya miaka mingi sana kupita akatokea mfalme mmoja anayeitwa Hezekia yeye ndiye aliyefanikiwa kuliona hilo chukizo mara moja, Tusome:
2 WAFALME: 18:1 ‘’Ikawa katika mwaka wa tatu wa Hoshea, mwana wa Ela, mfalme wa Israeli, Hezekia, mwana wa Ahazi, mfalme wa Yuda, alianza kutawala.
2 Alikuwa na umri wa miaka ishirini na mitano alipoanza kutawala; akatawala miaka ishirini na kenda katika Yerusalemu; na jina la mama yake aliitwa Abiya, binti Zekaria.
3 Akafanya yaliyo mema machoni pa Bwana, mfano wa yote aliyoyafanya Daudi, baba yake.
4 Alipaondoa mahali pa juu, akazibomoa nguzo, akaikata hiyo Ashera; akaivunja vipande vipande ILE NYOKA YA SHABA ALIYOIFANYA MUSA; maana hata siku zile wana wa Israeli walikuwa wakiifukizia uvumba; naye akaiita jina lake NEHUSHTANI
5 Alimtumaini Bwana, Mungu wa Israeli; hata baada yake hapakuwa na mfano wake katika wafalme wote wa Yuda, wala katika hao waliomtangulia’’.

Embu jaribu kutafakari kwa utulivu uone kitu hapo! AGIZO lilikuwa ni la Mungu mwenyewe lakini sasa linageuka kuwa kitanzi na kikwazo kikubwa sana kwa watu…Tunaweza kuwalaumu wale tukasema walipungukiwa na akili lakini nataka nikuambie sisi wa kizazi hiki ndio tuliopungukiwa akili zaidi ya wale..Tutaona ni kwa namna gani tunafanya makubwa zaidi ya wao.

Mungu alimwagiza Musa achonge nyoka wa shaba kama ISHARA tu! ya kitu Fulani tu rohoni, nacho ndicho tunakuja kukiona sisi watu wa agano jipya, kuwa tendo lile Mungu aliliruhusu lifanyike vile kumfunua Bwana wetu Yesu Kristo atakapotundikwa msalabani kwamba kila mtu atakayemwamini aokolewe, hilo tunalithibitisha kwa maneno yake mwenyewe..
Yohana 3:14 ‘’Na kama vile Musa alivyomwinua yule nyoka jangwani, vivyohivyo Mwana wa Adamu hana budi kuinuliwa;15 ili kila mtu aaminiye awe na uzima wa milele katika yeye’’.
… lakini hakukuwa na kitu chochote cha maana ndani ya ile SHABA, uponyaji halisi haukuwa ndani ya shaba ile bali ulitoka kwa Mungu mwenyewe..matokeo yake watu wakaacha kumtazama Mungu ambaye ni mponyaji wao wakaigeukia shaba isiyoweza kusema, wala kunena, wala kuzungumza..

Leo hii tunajua ni kweli Mungu alimwagiza Elisha achukue CHUMVI na kuitia katika chemchemi ya maji iliyokuwa inazaa mapooza..Na baadaye maji yale yakawa matamu,.Lakini kumbuka sio chumvi iliyotibu maji bali ni Mungu ndiye aliyefanya vile, lakini ni kwanini leo hii tunaihusisha chumvi na mambo ya ibada ikiwa hatujaongozwa kuitumia?.Nasi tunasema vile vile kama wana wa Israeli, Mungu kaweka uponyaji wa kiungu ndani ya chumvi,..tunasema kuna nguvu fulani ndani ya chumvi kama sivyo kwanini Mungu alimwagiza Elisha aiweke katika maji?...Tunamtia Mungu wivu pasipo sisi kujijua..

Halikadhalika tunayapa MAJI heshima, na kusema maji yana nguvu ya kusafisha mtu ndani yake, na kumtakasa, Tunamweka nyuma Mungu tunayapa maji heshima, ndugu Huko ni sawa kuiabudu sanamu ya Shaba.

Vivyo hivyo na vitu vingine vyote, tunasema UDONGO unabeba uhai, kwahiyo tukiumwaga kwenye biashara zetu, utazifufua, huku tukishikilia kile Bwana Yesu alichokifanya alipotengeneza TOPE ardhini na kumpaka Yule kipofu machoni, na macho yake kufumbuka, tunasema kama udongo usingekuwa na uponyaji Fulani Yesu asingeagizwa kutengeneza tope na kumpa kipofu..na kibaya zaidi mpaka tumeshavipa majina kama VITENDEA KAZI VYA KIROHO.

Tunahusisha MISALABA katika Ibada zetu. Kama unapenda msalaba wako kwanini usiunig’inize nyumbani kwako kama kumbukumbu lako la Bwana kukufia msalabani, lakini ni kwanini unakwenda kuuinamia, kuomba kupitia huo, unadhani unampa Mungu heshima hujui kuwa ni ASHERA hilo umeiweka moyoni mwako.

Na mambo mengine mengi, tunayafanya hatujui kuwa ndivyo tunavyomtia Mungu wivu. Fumbua macho yako, utoke kwenye uchanga wa kiroho, ikiwa Mungu amekuongoza kutumia mojawapo ya vitu hivyo kama ishara ya kitu Mungu anachokifanya rohoni ni sawa, kama amekuongoza kutumia maji tumia, amekuongoza kutumia mafuta tumia, na uthibitisho wa kuwa umeongozwa na Mungu kufanya hivyo, ni kwamba hakitakuwa unakirudia rudia,….Elisha halikuwa hatumii chumvi kila tatizo linalokuja mbele yake…Wala sio kila mgonjwa aliyekuja mbele yake alikuwa anamwambia akaoge mto Yordani mara saba. Alikuwa anafanya vile pale alipokuwa anaongozwa tu! Na sisi tunapaswa tuwe hivyo hivyo.

lakini kama tunageuza Imani yetu kutoka katika nguvu ya uweza wa DAMU YA YESU inayoweza kufuta na kuondoa kila kitu na kuvipa vitu hivyo visivyo na uhai heshima Fulani ya kiroho kwamba vina nguvu Fulani au uwezo Fulani wa wa kusababisha mambo, basi tujue moja kwa moja tunamfanyia ibada shetani. Na Mungu anachukizwa nazo kupindukia kwa namna ile ile anavyochukizwa na waabudu baali na Jua.

Na madhara yake ni kwamba, Mungu atatupiga kwa kukosa kwetu maarifa, wakati mwingine badala ya tatizo kuisha ndivyo litakavyoongezeka, kwasababu biblia inasema ni heri ungekutana na ghadhabu ya Mungu kuliko WIVU wake, na ibada zote za sanamu zinaleta wivu mbele za Mungu.
Mithali 27:4 ‘Ghadhabu ni kali, na hasira ni gharika; Lakini ni nani awezaye kusimama mbele ya WIVU’.
Wimbo uliobora 8: 6“………….wivu ni mkali kama ahera. Mwako wake ni mwako wa moto, Na miali yake ni miali ya Yahu.”
Huu ni wakati wa kutubu(yaani kugeuka), na kumwabudu yeye katika Roho na Kweli.

Jina la Bwana wetu Yesu Kristo lihimidiwe milele na milele. Amin.

 Bwana akubariki.

No comments:

Post a Comment