"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Monday, May 13, 2019

USILITAJE BURE JINA LA BWANA!


Kutoka 20:7 “Usilitaje bure jina la Bwana, Mungu wako, maana Bwana hatamhesabia kuwa hana hatia mtu alitajaye jina lake bure..”
Hii ni moja ya amri tulioizoea sana, Na tumekuwa tukidhani kulitaja jina la Mungu bure ni pale tu tunapo muhusisha na mambo yasiyo na maana, au pale tunapo apa, lakini hiyo ni sehemu mojawapo ya kulitaja bure jina la Mungu, ipo sehemu nyingine ambayo ni kuu zaidi, na inamuudhi Mungu sana, pengine na wewe ulishawahi kuifanya bila kujua na pengine ndio imekuwa kikwazo kikubwa cha mafanikio ya roho yako.

Pale unaposema leo nimeamua kuwa Mkristo nimeamua kumfuata Mungu kwa moyo wangu wote, pale unaposema maisha yangu ya kale basi, hapo ni sawa na umemwita Mungu aje kuyaongoza maisha yako kuanzia huo wakati na kuendelea, au kwa lugha ki-kibiblia tunasema umeliitia jina la Mungu lije kukuokoa, lakini pale unaposema Nimeokoka, mimi ni mkristo halafu, unaendelea kuyafanya yale yale uliyoyaacha kule nyuma, unaendelea kuiba,unazidi kuzini, unatazama pornography, unasengenya n.k. Hapo ni sawa kabisa na umemdhahaki Mungu kwamba ulimwita akuokoe na kumbe haupo tayari kuokolewa, Hapo umelitaja JINA LA MUNGU wako bure!.. Ni heri usingedhubutu kuujaribu wokovu kabisa maishani mwako ..

Ukisoma katika kitabu cha Mwanzo utaona watu walioanza kumtafuta Mungu, biblia imetafsiri kama “waliliita au wanalitaja Jina la Mungu”
Mwanzo 4: 25 “Adamu akamjua mke wake tena; akazaa mwana mwanamume, akamwita jina lake Sethi; maana alisema, Mungu ameniwekea uzao mwingine mahali pa Habili; kwa sababu Kaini alimwua. 26 Sethi naye akazaa mwana; akamwita jina lake Enoshi. HAPO NDIPO WATU WALIPOANZA KULIITIA JINA LA BWANA”.
Utaona pia katika maandiko BWANA akitangaza jina lake yeye mwenyewe…utaona halitaji jina lake kama YEHOVA, bali analitaja jina lake kama TABIA..Tunalisoma hilo katika kitabu cha Kutoka.
Kutoka 34: 5 “Bwana akashuka ndani ya lile wingu, akasimama pamoja naye huko, AKALITANGAZA JINA LA BWANA.
6 Bwana akapita mbele yake, AKATANGAZA, BWANA, BWANA, Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli;
7 mwenye kuwaonea huruma watu elfu elfu, mwenye kusamehe uovu na makosa na dhambi; WALA SI MWENYE KUMHESABIA MTU MWOVU KUWA HANA HATIA KAMWE; MWENYE KUWAPATILIZA WATOTO UOVU WA BABA ZAO, NA WANA WA WANA WAO PIA, HATA KIZAZI CHA TATU NA CHA NNE”.
Unaona mstari wa saba hapo?...tafsiri ya jina lake sio tu Mungu mwenye huruma bali pia ni MUNGU asiyeacha kumwesabia mtu mwovu kuwa hana makosa kamwe. Kwahiyo unapompokea Kristo maishani mwako halafu maisha yako yapo vilevile hayabadiliki…Hapo ni sawa na umelitaja jina Bwana Mungu wako Bure na atakuhesabia kuwa na hatia kwa hilo.

Embu tafakari mfano huu halafu wewe uhukumu, ni sawa na leo mtu ameagiza gari nje ya nchi labda tuseme Japan kwa makubaliano ya kuwa siku litakapofika ndipo atalilipa..Lakini siku linafika ili akabidhiwe gari lake afanye malipo biashara iishe, anageuka na kusema mimi sina haja na hilo gari kwanza nilikuwa ninawatania tu, labda siku nyingine nikiwa tayari.

Wewe unadhani, wale watu watamfanyaje?. Ni dhahiri kuwa hawawezi kumwacha hivi hivi waingie hasara kwa ajili ya uzembe wake, hivyo hapo kama hatatozwa faini, basi atafunguliwa mashtaka mahakani, na mwisho wa siku lazima atajikuta analipa mpaka senti ya mwisho kwa njia yoyote ile,…Na ndivyo ilivyo kwa Mungu, tunapolitaja jina lake, (JINA LA YESU ambalo hakuna jingine zaidi ya hilo ambalo litupasalo sisi kuokolewa kwalo. Matendo 4:12) lije lituokoe, tuonyeshe kweli kweli kutaka kuokolewa vinginevyo , Bwana hatutacha hivi hivi bila kutuhesabia kuwa wenye hatia..wakati mwingine mapigo au vifo vinatukuta kwa sababu hiyo.

Na ndio maana mtunzi wa Mithali alisema.. 30:8 “Uniondolee ubatili na uongo; Usinipe umaskini wala utajiri; Unilishe chakula kilicho kadiri yangu. 9 Nisije nikashiba nikakukana, Nikasema, Bwana ni nani? Wala nisiwe maskini sana NIKAIBA, NA KULITAJA BURE JINA LA MUNGU WANGU”.

Unaona huyu mtu alijua kabisa dhambi za wizi ni sawa na kulitaja jina la Mungu wake bure.

Na sisi pia kama tunalitaja jina la YESU mwokozi wetu kuwa ndio jina pekee lilnalotusababisha kuwa hivi tulivyo leo ndani ya wokovu basi na tuuweke ulimwengu mbali na sisi tumfuate Mungu wetu kweli kweli kwa kumaanisha..ili tujiepushe na laana, Kwasababu maandiko ndivyo yanavyotuonya.
1Timotheo 2:19 “..KILA ALITAJAYE JINA LA BWANA NA AUACHE OUVU”.

Jina la Kristo lisitamkwe kinywani mwako kama haupo tayari kuuacha ouvu..Na unaacha uovu kwa kutubu dhambi zako zote kwa kumaanisha kutokuzifanya tena, na kisha kubatizwa na kupokea kipawa cha Roho Mtakatifu.

Jina la mwokozi wetu YESU KRISTO na lihimidiwe daima..Amen.

No comments:

Post a Comment