"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Wednesday, June 5, 2019

MATUNDA YAPATANAYO NA TOBA!


Luka 3:7 ‘’Basi, aliwaambia makutano ya wale waliomwendea ili awabatize, Enyi wazao wa nyoka, ni nani aliyewaonya ninyi kuikimbia hasira itakayokuja?
8 Basi, TOENI MATUNDA YAPATANAYO NA TOBA; wala msianze kusema mioyoni mwenu, Tunaye baba, ndiye Ibrahimu; kwa maana nawaambia ya kwamba katika mawe haya Mungu aweza kumwinulia Ibrahimu Watoto.
9 Na sasa hivi shoka limekwisha kuwekwa penye mashina ya miti; basi kila mti usiozaa matunda mazuri hukatwa na kutupwa motoni’’.

Maneno hayo Yohana aliwaambia Wayahudi, ambao kwa kipindi kirefu walikuwa wanajua kuwa wao ndio Taifa teule la Mungu, uzao wa Ibrahimu wana wa Ahadi…Kwamba katika dunia nzima wao pekee ndio walioteuliwa na Mungu kuwa Taifa la Mungu…Na kweli ndivyo walivyokuwa kulingana na ahadi Mungu aliyomwahidia Ibrahimu. Na wapo baadhi waliokuwa wanaishi Maisha ya kumpendeza Mungu lakini wengi wao waliobweteka na kusema ‘sisi ni uzao wa Mungu hata tukifanya hiki au kile Mungu hatatutupa milele’ na hiyo ikawafanya  wawe wanaishi Maisha ya uvuguvugu.
Lakini hapa Yohana anatokea kutoka nyikani akiwaambia…. ‘enyi kizazi cha nyoka’…kumbuka wao wanajijua kuwa ni kizazi cha Ibrahimu, lakini Yohana anawaambia hapa ‘enyi kizazi cha nyoka’…Na wakati huo ilikuwa inajulikana na watu wote hata Yohana mwenyewe mbatizaji alikuwa anajua kuwa ‘ailaaniye Israeli amelaaniwa’…Kwasababu Mungu alimwambia Ibrahimu akulaaniye amelaaniwa, na akubarikiye amebarikiwa (Mwanzo 12:3)…Hivyo kuwaita ‘wana wa Israeli, uzao mteule wa Mungu kuwa ni uzao wa Nyoka ni kama kuilaani Israeli’.

Lakini Yohana hakuishia hapo, aliendelea kuwaambia…’msiseme mioyoni mwenu kuwa tunaye baba ndiye Ibrahimu.. kwa maana nawaambia ya kwamba katika mawe haya Mungu aweza kumwinulia Ibrahimu Watoto’’….
Yaani kwa lugha nyepesi hiyo sentensi ili ieleweke tunaweza kuiweka hivi; ‘Enyi wazao wa nyoka msijidhanie kuwa ni nyie tu ndio watu pekee wa Mungu na kwamba Mungu hawezi kuwa na watu wengine zaidi yenu…msifikiri hivyo hata kidogo…kwamaana hata kutoka kwenye vitu vinavyodharaulika visivyokuwa na uhai kama haya mawe Mungu anaweza kuwanyanyua watu wake wengine wa ahadi wanaompendeza’’.

Na kama ni msomaji mzuri wa Biblia utakuja kuona kuwa hayo mawe Yohana aliyokuwa anayazungumzia hapo ni sisi watu wa mataifa..Baada ya wayahudi (yaani waisraeli) kuikataa Neema iliyoletwa na Bwana wetu Yesu Kristo, Na kuyakataa maonyo haya ya Yohana Mbatizaji…Neema hiyo ilitoka kwao na kuhamia kwetu sisi watu wa mataifa…Sisi ndio hayo mawe tuliounuliwa kuwa Watoto wa Ibrahimu.

Matendo 13:46 ’Paulo na Barnaba wakanena kwa ushujaa wakasema, Ilikuwa lazima neno la Mungu linenwe kwenu kwanza[yaani kwa waisraeli]; lakini kwa kuwa mnalisukumia mbali, na kujiona nafsi zenu kuwa hamkustahili uzima wa milele, angalieni, twawageukia Mataifa.
47 Kwa sababu ndivyo tulivyoamriwa na Bwana, Nimekuweka uwe nuru ya Mataifa, Upate kuwa wokovu hata mwisho wa dunia.
48 Mataifa waliposikia hayo wakafurahi, wakalitukuza neno la Bwana, nao waliokuwa wamekusudiwa uzima wa milele wakaamini’’.
Kwahiyo Kazi moja wapo Yohana Mbatizaji aliyokuja kuifanya ni ‘kuondoa mawazo potofu’ katikati ya wayahudi kuwa wao ni watu bora kuliko wote…Na kwamba Mungu hawezi kuwaacha kwa namna yoyote ile…Hivyo hata wakiendelea na Maisha yao machafu, Mungu atakuwa nao tu milele!! Kwasababu ni Waisraeli tu, Taifa la Mungu, uzao wa Ibrahimu…

Lakini Yohana akawaambia kwa uweza wa Roho, kuwa wasipozaa matunda yapatanayo na Toba zao…watakatwa (maana yake Mungu atawaacha na kuigeuzia Neema yake kwa watu wengine).Na wenyewe wataachwa ukiwa..Lakini hawakutaka kusikia na yakawakuta yaliyotabiriwa.

Kadhalika Neema imekuja kwetu sisi, Ujumbe ni ule ule kwetu pia..Tusijidhanie kuwa kwasababu Neema ipo, kwasababu tuna damu ya Yesu, na kwamba tunaweza kuomba toba wakati wowote na kupata msamaha..basi tukabweteka na kutokuzaa matunda yapatanayo na Toba! Na sisi pia tutakatwa na kutupwa motoni. Kama Mungu hakuwahurumia watu wake Israeli, unadhani sisi tutasalimikaje?

Warumi 11:19 “Basi utasema, Matawi yale yalikatwa kusudi ili nipandikizwe mimi.
20 Vema. Yalikatwa kwa kutokuamini kwao, na wewe wasimama kwa imani yako. Usijivune, bali uogope.
21 Kwa maana ikiwa Mungu hakuyaachia matawi ya asili, wala hatakuachia wewe."


SASA MATUNDA YAPATANAYO NA TOBA NI YAPI?.
Kumbuka hapa Yohana hakuwaambia wayahudi, watubui dhambi zao….hapana bali aliwaambia wazae matunda yapatanayo na toba zao…Ikiwa na maana kuwa Walishatubu! Lakini walikuwa hawazai matunda yapatanayo na toba zao….Siku zote baada ya toba..hatua inayofuata ni kutenda na kuishi kulingana na ulichokitubia…Kama Mtu alikuwa ni mwasherati anatubia kwanza uasherati wake, na akiisha kutubu anaizalia matunda ile Toba…Yaana anaanza kuishi Maisha ya usafi na anaacha uasherati kabisa, sio anatubu leo baada ya siku mbili anatenda tena ile dhambi, halafu anatubu tena na kufanya tena.. kama anacheza danadana..Hapana! hapo huzai matunda yoyote ndugu..Yohana alichowaambia kama sauti ya mtu aliaye nyikani ni kwamba ‘watu wazae matunda yapatanayo na Toba, au waishi Maisha yanayoendana na walichokitubia’…Hivyo ndicho alichokuwa anakisisitiza Yohana.

Watu wengi hawapendi kuambiwa ukweli lakini ukweli ni kwamba, Ukitubu halafu hujakusudia kuacha kile ulichokitubia..hapo ni unamkufuru Mungu!…Na unapokwenda kushiriki Meza ya Bwana, au kubatizwa na huku ndani ya moyo wake hujakusudia kuacha dhambi…ni bora usifanye hivyo tena, au usiende kubatizwa kabisa…kwasababu utakuwa unakwenda kujitafutia laana badala ya baraka.

Usijaribu kabisa kushiriki meza ya Bwana, kama hujakusudia kuacha dhambi zako, kama bado ni mwasherati, au mlevi, au mtazamaji wa pornography au mtukanaji.. kuna hatari kubwa sana…hata wakati mwingine ya kupoteza Maisha….Chagua kuwa baridi kabisa au moto ogopa uvuguvugu.

1 Wakoritho 11:22 ‘ Maana kila mwulapo mkate huu na kukinywea kikombe hiki, mwaitangaza mauti ya Bwana hata ajapo.
27 Basi kila aulaye mkate huo, au kukinywea kikombe hicho cha Bwana isivyostahili, atakuwa amejipatia hatia ya mwili na damu ya Bwana.
28 Lakini mtu ajihoji mwenyewe, na hivyo aule mkate, na kukinywea kikombe.
29 Maana alaye na kunywa, hula na kunywa hukumu ya nafsi yake, kwa kutokuupambanua ule mwili.
30 Kwa sababu hiyo wako wengi kwenu walio hawawezi na dhaifu, na watu kadha wa kadha wamelala.
31 Lakini kama tungejipambanua nafsi zetu, tusingehukumiwa."

Wala usijihusishe na maagizo yoyote ya Bwana Yesu kama kuhubiri, kubatiza, kubatizwa, kushiriki kwenye vikundi vya maombi ya ndani, kutawadha au kutawadhwa miguu n.k kama hujakusudia kuacha dhambi….sisemi kutubu peke yake!! Bali Nazungumzia KUACHA! Au kwa lugha ya kibiblia KUZAA MATUNDA YAPATANAYO NA TOBA YAKO! Kama Yohana alivyozungumza kwa uweza wa Roho.

Je! Unazaa hayo matunda leo?...Tangu usikie kuwa uasherati ni dhambi, umetubu mara ngapi dhambi hiyo lakini bado unaendelea kuifanya?..tangu usikie kuwa ulevi, utazamaji wa pornography, utukanaji, ulaji rushwa, usengenyaji, wizi, usagaji, ushoga, uchawi, ulawiti, ufanyaji masturbation ni dhambi lakini bado unaendelea kufanya?...Yohana aliwaita watu hao kuwa ni KIZAZI CHA NYOKA! Ingawa wao walijiona kuwa ni uzao wa Ibrahimu..Bwana Yesu aliwaita kuwa ni kizazi cha Nyoka ingawa walijitetea kwake kuwa ni uzao wa Ibrahimu…Wao walijihesabia haki lakini mbele za Mungu walionekana wamestahili kwenda jehanamu ya moto.

Ndugu unapoambiwa ukweli sio kwamba unahukumiwa..Yohana alipowaita wayahudi uzao wa nyoka sio kwamba aliwalaani au kuwahukumu…hapana alijua kabisa lile andiko linalosema (amlaaniye Israeli naye amelaaniwa) bali aliwaambia ukweli kwa lengo la wao kutubu kutubu sio kwa lengo la kuwashutumu au kuwahukumu….kwasababu ndivyo walivyokuwa wanaonekana mbele za Mungu…Kadhalika leo unapousikia ukweli usikimbilie kufikiria kuwa unahukumiwa …bali ufikirie kugeuza njia zako na kufurahia umeambiwa ukweli.
Biblia inatuonya tuzae matunda yapatanayo na Toba! Hilo ndio Neno la Leo.

Ikiwa hujampa Bwana Maisha yako, hujachelewa kabisa…ingawa umechelewa!! Hivi sasa bado unyakuo hujapita, lakini kipindi sio wakati mrefu kuanzia sasa utatokea, na mambo mabaya yataikumba dunia nzima… hivyo hapo ulipo tenga dakika chache, peke yako tubu dhambi zako zote na kisha baada ya kutubu dhamiria kuacha yote uliyoyatubia…unakuwa hufanyi tena hizo dhambi hata iweje..unaziacha kuanzia leo na kuendelea! shetani asikudanganye kuwa huwezi…unaweza! Hivyo kusudia kuzaa matunda yapatanayo na ulichokitubia..Na baada ya hapo nenda katafute ubatizo sahihi wa kuzamishwa katika maji mengi na kwa jina la BWANA YESU KRISTO (Matendo 2:38) kwaajili ya ondoleo la dhambi zako. Na Bwana mwenyewe atafanya yaliyosalia..kukupa wewe Roho Wake Mtakatifu atakayekusaidia kushinda dhambi, na kuyaelewa maandiko, na kukulinda mpaka siku ya unyakuo itakapofika ili uwende naye mawinguni.

Bwana akubariki sana kwa kudhamiria kwako kumfuata Mungu.
www.wingulamashahidi.org

No comments:

Post a Comment