"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Wednesday, June 5, 2019

NINAJUA MAWAZO NIKUWAZIAYO:


Shalom mpendwa wa Bwana, karibu katika kuyafakari maandiko matakatifu, Na leo tutajifunza somo ambalo tunaweza kuliona nyuma wa wana wa Israeli kukaa Babeli miaka 70, Ni kwanini Mungu aliamua kuweka bayana kuwa watakaa utumwani miaka ile 70 , na kuwaambia kuwa wakifika kule kama ni kuzaa waendelee kuzaa watoto, wawaoze binti zao, wapende bustani, wajenge, n.k….yaani kwa ufupi tunaona Mungu hakuwa na haja ya Dua zao za kuomba warudishwe katika nchi ya Israeli kwa wakati ule, utaona hakuwashauri hata waishi kama wapitaji kule Babeli watakapofika, badala yake aliwaambia waendelee na shughuli zao za kawaida kama tu vile walivyokuwa wanaishi Israeli.. Ukisoma Yeremia 29 yote utaliona hilo.

Lakini ukweli ni kwamba hata ingekuwa ni wewe leo hii yamekukuta mambo kama hayo , mtu kaja kuiua familia yako yote, na ukoo wako wote halafu anakuchukua mateka kukupeleka nchi ya mbali na kukwambia baada ya miaka 70 nitakurudisha nchini mwako, kwahiyo ukifika kule wewe jenga, panda , uishi maisha ya furaha, JE! Ni kweli utakuwa na Furaha hiyo nchi ya ugenini unayoiendea ambayo huijui hata ikoje, wala hujui utakutana na watu wa aina gani huko?, Ni wazi kuwa Mawazo yako kila siku yatakuwa nyumbani,katika majozi ukitumaini siku yoyote utarudi lakini sio baada ya miaka 70.

Hiyo ndio hali iliyowakuta wana wa Israeli, Walipomkosea Mungu, kupita kiasi, mpaka Mungu kukata tamaa juu yao, Mungu alimruhusu Nebukadneza mfalme wa Babeli, aje kuwachukua utumwani, Hivyo lile kundi la kwanza lililoenda utumwani, lilipokuwa kule lilitamani sana lirudi nyumbani Israeli, mpaka kukatokea manabii wa uongo wakawa wanawadanganya kwa kuwafariji kuwa watakaa kule miaka 2 tu kisha Mungu atawarudisha nchi yao tena, lakini Mungu alizungumza nao kwa kinywa cha Nabii Yeremia na kuwaambia kuwa watakaa utumwani kwa muda wa miaka 70 mizima haitapungua wala haitaongezeka, na hivyo wasijitaabishe hata kidogo kufikiri hiyo itakuwa ni habari ya hivi karibuni, kikubwa tu waendelee kuoa, wapande na wajenge, wawatikie na mema hao maadui zao, siku zote watakazokuwa huko. na ndiyo tunasoma iliyompelekea hata Nabii Yeremia kupitia matatizo makubwa namna ile hata kufikia hatua ya kutaka kuuliwa na wayahudi, kwa taarifa mbaya alizokuwa anazileta, kwasababu Iko wazi kuwa hakuna mtu anayependa kufia utumwani,

Ni habari za kukatisha tamaa sana kwa namna moja au nyingine,wakikumbuka utumwa ule wa Misri jinsi walivyoteswa ndio wanaokwenda kukutana nao tena, kufanyishwa kazi ngumu,kutumikishwa, kuchapwa.Lakini tunasoma pamoja na hayo kuna maneno Mungu alizungumza nao kwa kinywa cha Yeremia..Na maneno yenyewe ndio haya:
Yeremia 29:11 “Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema Bwana, ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa ninyi tumaini siku zenu za mwisho”.

Wengi wetu tunasoma huu mstari lakini hatujui ni kwanini Mungu alizungumza maneno hayo…Maneno hayo Mungu aliwaambia wana wa Israeli wakati wanachukuliwa utumwani, Babeli.

Kwa kweli ni maneno ya faraja ambayo hata sisi mstari huu tunapenda kuutumia tunapopitia matatizo. Lakini habari yao inatufundisha nini?.Ndugu wana wa Israeli wanafananishwa na watoto wa Mungu sasa, yaani wale waliomwamini Kristo na baadaye wakarudi nyuma, wale walioujua ukweli wakaupinga..wale ambao Mungu amekuwa akiwaonya mara nyingi waache njia zao mbaya kwa mahubiri wanayosikia kila siku, lakini hawakusikia, mpaka imefikia hatua wamezama katika matatizo makubwa ambayo hawajui watatokaje, wengine wamezama kwenye uzinzi na sasa wamepata ukimwi, na leo hii kweli umetubu na kuacha uzinzi kabisa unataka Mungu akuponye, nataka nikuambie, kila mtu atavuna alichopanda, umemwomba Mungu akuponye lakini huoni mabadiliko yoyote, kesi yako wewe ni sawa na hii ya wana wa Israeli.

Hivyo nataka leo nikuambie kulingana na maandiko wala usihuzunike kujikuta umekaa katika hiyo hali kwa muda mrefu sana.. kama yalivyowakuta wana wa Israeli kwa makosa yao, ndivyo yalivyokukuta na wewe. Wao walikaa miaka 70 lakini siku moja walitoka….Na wewe usisahau Neno hili kuwa.. Mungu anayajua mawazo anayokuwazia wewe, ni mawazo ya amani wala sio mabaya kukupa tumaini siku zako za mwisho.

Umekuwa mwizi au mbakaji na sasa umefungwa, ni kweli umeshatubu kabisa kwa kudhamiria kuacha, umekuwa mtoto mzuri wa Mungu, huibi tena wala huna nia za Yule adui tena moyoni mwako…lakini unajiuliza ni kwanini mpaka sasa bado upo kifungoni Mungu hakutoi huko?, nataka nikuambie, kusamehewa ni kitu kingine, na kufutiwa adhabu ni jambo lingine, cha msingi ukijikuta katika hali kama hiyo, wewe kuwa tu mtulivu kuwa mtu mwema huko gerezani, mtumikie Mungu wako kwa uaminifu wote, ifanye kazi ya Mungu huko huko uliko, fanya shuhuli zote zinazokuja mbele yako, kana kwamba vile hutoki leo wala kesho, kwa kuwa Mungu anayajua mawazo anayokuwazia wewe ni kukupa tumaini katika siku zako za mwisho.

Sasa kumbuka wana wa Israeli walipofika Babeli japo walitubu na kulikuwa na watu wa Mungu wengi tu mfano wa Ezekieli, na akina Danieli, lakini hakuwaacha wateseke kama kwa utumwa ule wa Misri, aliwanyanyulia watu hodari na wenye hekima kama Danieli, Meshaki, Shedraki na Abednego, na kuwaweka katika jumba la kifalme mbele ya Nebukadreza, na kwa kupitia hao Mfalme aliwapa heshima wayahudi wote waliokuwa Babeli pamoja na Mungu wao , wamwabudu kwa uhuru na amani, waliishi kweli utumwani lakini hawakuwa kama watumwa muda wote waliokuwepo kule, ni kama vile Yusufu na ndugu zake, japo wote walikuwa utumwani lakini waliishi vizuri zaidi hata wa Wamisri waliokuwa kule ndivyo ilivyokuwa kwa wale waliokwenda Babeli.

Na baada ya ile miaka 70 ya adhabu kupita Mungu aliwafungulia mlango mkubwa wa kurudi katika nchi yao, lakini hawakurudi mikono mitupu walirudi pamoja na zawadi nyingi walizopewa kule Babeli, na hata wale waliosalia huko Babeli na kwenye nchi za mataifa kwa hiyari yao na wale ambao walikuwa wamesambaa duniani kote tunaona Mungu aliwanyanyulia tena watu kama Mordekai na Esta, kwenye viti vya enzi vya Uajemi, hawa nao waliwafanya wayahudi wapate heshima mara dufu duniani kote, waliogopeka na kuheshimiwa sana, japo walikuwa katika nchi za ugenini. Unaona jinsi mawazo ya Mungu yalivyokuwa mema juu yao mwisho wa siku, licha ya kutumikia adhabu lakini pia alipenyeza kusudi lake katika adhabu zao.

Hivyo na wewe ambaye ulimkosea Mungu na sasa umekutana na mabaya, mpaka sasa upo shimoni, na kwa bahati nzuri ulitubu dhambi zako, na uliziacha kabisa, ni wazi kuwa Mungu alikusamehe siku ile ile ulipogeuza Nia yako na njia zako.., lakini bado unaona hujatoka katika hilo shimo ulilozama, iadha la magonjwa, au vifungo, au shida, au taabu, nataka nikuambie usivunjike moyo, endelea kumtumikia Mungu katika hali uliyopo, haijalishi itakuchukua wiki, au mwezi au miaka mpaka kufunguliwa kabisa, lakini wewe endelea kumtumikia katika hali uliyopo na yeye atakubariki atakuongeza atakufundisha , atakuzidisha huko ulipo, na wakati wake ukifika atakufungua moja kwa moja..shetani asikudanganye kuwa Mungu amekuacha, au anakuchukia. Kutumikia adhabu haimaanishi kuwa Mungu hakupendi..

Isaya 44: 21 “Kumbuka haya, Ee Yakobo; nawe Israeli, maana wewe u mtumishi wangu; nimekuumba; u mtumishi wangu; Ee Israeli, hutasahauliwa na mimi”.

Mithali 4 11 “Mwanangu, usidharau kuadhibiwa na Bwana, Wala usione ni taabu kurudiwa naye”.

Na pia kama hujatubu dhambi zako ukihofia kwamba Mungu hatakusamehe…Hiyo ni sauti ya Ibilisi inazungumza na wewe..inayotaka kukupeleka ukajinyonge kama Yuda! Mungu anataka utubu akusamehe dhambi zako zote bure kwasababu yeye ni mwenye rehema…Anataka utubu ukiwa kwenye hayo hayo madeni ya kupindukia, anataka utubu katika hali hiyo hiyo ya magonjwa na vifungo, katika hali hiyo hiyo ya ushirikina na uchawi uliyopo, katika hali hiyo hiyo ya uuaji na utapeli uliyopo, katika hali hiyo hiyo ya ukahaba na usagaji.Tubu leo naye atakusamehe! Na kukubadilisha kwa maana anakuwazia mawazo mema sana huko mbeleni, kukupa wewe tumaini.

Mwisho kabisa nataka umalizie kwa kuyatafakari maneno haya:
Zaburi 103: 11 “Maana mbingu zilivyoinuka juu ya nchi, Kadiri ile ile rehema zake ni kuu kwa wamchao.
12 Kama mashariki ilivyo mbali na magharibi, Ndivyo alivyoweka dhambi zetu mbali nasi.
13 Kama vile baba awahurumiavyo watoto wake, Ndivyo Bwana anavyowahurumia wamchao.
14 Kwa maana Yeye anatujua umbo letu, Na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi.
15 Mwanadamu siku zake zi kama majani; Kama ua la kondeni ndivyo asitawivyo.
16 Maana upepo hupita juu yake, kumbe haliko! Na mahali pake hapatalijua tena.
17 Bali fadhili za Bwana zina wamchao Tangu milele hata milele, Na haki yake ina wana wa wana;
18 Maana, wale walishikao agano lake, Na kuyakumbuka maagizo yake ili wayafanye''.
Ubarikiwe.

Tafadhali “share” ujumbe huu kwa wengine na utakuwa umefanya kazi ya kuipelekea injili mbele.

Kwa mafundisho mengine mengi pia unaweza kutembelea website yetu (www wingulamashahidi org)

No comments:

Post a Comment