"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Monday, June 24, 2019

TAFUTA KUMJUA MUNGU ZAIDI YA SHETANI


Jina kuu la Bwana wetu Yesu Kristo libarikiwe.
Karibu tujifunze Neno la Mungu…Taa iongozayo miguu yetu na Mwanga wa njia zetu (Zab.119:105).

Karibia kila tukio linalotokea duniani baya au jema huwa linameruhusiwa na Mungu, hakuna kitu hata kimoja kinaweza kuendelea chini ya mbingu kama hakijaruhusiwa na Mamlaka iliyo kuu (yaani ya mbinguni). Utauliza hata zile ajali tunazoziona zimeruhusiwa zitokee?..jibu ni ndio…utauliza tena hata vifo vyote vya kikatili pamoja na shida na magonjwa ni Mungu kayaruhusu yatokee…jibu ni Ndio!...Mungu muumba wa Mbingu na nchi, aliyeumba vitu vyote vinavyoonekana na visivyoonekana dunia haijamshinda kiasi kwamba jambo Fulani linaweza kutokea pasipo ridhaa yake…Tukilifahamu vizuri jambo hili litatufanya tumtazame Mungu kwa jicho lingine.
Sasa kwanini anaruhusu vimbunga juu ya watu wasiomjua yeye…ni kwasababu ya maasi na maovu ya watu… na kwanini anaruhusu vimbunga juu ya watu wake wanaomjua yeye?…ni kwasababu ile ile kama alivyovileta kwa mtumishi wake Ayubu.

Siku zote shetani hawezi kujiamulia kufanya jambo lolote kabla halijamfikia kwanza Mungu, lipitishwe, Tunaweza kuona jambo hilo katika kitabu cha Ayubu.
Ayubu 1:7 ‘Bwana akamwuliza Shetani, Umetoka wapi wewe? Ndipo Shetani akamjibu Bwana, na kusema, Natoka katika kuzunguka-zunguka duniani, na katika kutembea huku na huku humo.
8 Kisha Bwana akamwuliza Shetani, Je! Umemwangalia huyo mtumishi wangu Ayubu? Kwa kuwa hapana mmoja aliye kama yeye duniani, mtu mkamilifu na mwelekevu, mwenye kumcha Mungu na kuepukana na uovu.
9 Ndipo Shetani akamjibu Bwana, na kusema, Je! Huyo Ayubu yuamcha Bwana bure?
10 Wewe hukumzingira kwa ukigo pande zote, pamoja na nyumba yake, na vitu vyote alivyo navyo? Kazi za mikono yake umezibarikia, nayo mali yake imeongezeka katika nchi.
11 Lakini nyosha mkono wako sasa, uyaguse hayo yote aliyo nayo, naye atakukufuru mbele za uso wako.
12 Bwana akamwambia Shetani, Tazama, yote aliyo nayo yamo katika uwezo wako; lakini usinyoshe mkono wako juu yake yeye mwenyewe. Basi Shetani akatoka mbele za uso wa Bwana’.
Unaona shetani hafanyi jambo lolote pasipo idhini ya Mungu..
Shetani anapompiga mtu kwa magonjwa na dhiki na tabu…cha kuangalia hapo sio kwenda kupambana na shetani..hapana! cha kufanya hapo ni kwenda kutafuta chanzo cha mambo hayo yote ni nini? Na ukishagundua kuwa ni Mungu karuhusu ndipo unapotakiwa kupoteza muda mwingi kumtafuta yeye kuliko kupambana na shetani…ili ujue sababu ya yeye kuyaruhusu hayo ni nini…kwasababu ukiacha kumwangalia Mungu na kupambana na shetani hutamweza hata kidogo…kwasababu yeye anafanya kazi kwa kibali maalumu kutoka juu na ana nguvu kuliko wewe..

Leo utaona mtu anaumwa na ugonjwa usiojulikana pengine kalogwa anatafuta kwenda kuombewa na kutafuta mchawi wake ni nani…anahangaika kwenda kukemea huo ugonjwa umtoke au huo uchawi umrudie mbaya wake na kupambana na shetani…lakini pasipo kujua kuwa mpaka ule ugonjwa umempata tayari Mungu mwenyewe alisharuhusu jambo hilo juu ya mwili wake…hivyo pa kwenda kutafuta suluhisho sio pengine zaidi ya kwa Mungu…

Ndio hapo itakubidi uende kwa Mungu kwa unnyenyekevu na magoti..Na kumwuliza Bwana sababu ya mambo haya yote ni nini? Ndipo Bwana atakufunulia…pengine Maisha yako si masafi mbele zake hivyo ameyaruhusu hayo shetani akupige ili wewe umrudie yeye na utakapotubu na kuyasafisha Maisha yako hilo tatizo linaondoka pasipo hata kuwekewa mkono na mtu yeyote…Au kama Maisha yako yapo sawa basi ameruhusu tu upitie hayo ili kukupeleka kwenye kiwango kingine cha kiroho kama alivyofanya kwa mtumishi wake Ayubu..nk zipo sababu nyingi.

Hebu fikiria endapo Ayubu angeacha kumfikiria Mungu na kuanza kukemea wachawi na mapepo yaliyowaua wanawe, au angeanza kutanga tanga huku na huko kusaka watumishi wamfanyie maombi ya kufunguliwa kwenye vifungo vya mikosi na laana na kupakwa mafuta angefikia wapi? Bila shaka angepoteza dira kabisa ya kujua sababu ya yeye kuyapitia hayo ni nini.
Kwahiyo kila kitu hata kama tunauhakika ni shetani katekeleza, tujue kuwa ni Mungu karuhusu shetani afanye hayo kwa namna ya kawaida hawezi kufanya kama kuna ulinzi wa kiMungu juu yako…Ukijifunza kufikiri hivyo hutakaa umwogope shetani kamwe! Wala hutakaa ujishughulishe kuijua elimu yake..utajikita katika kumjua Mungu Zaidi.

Tatizo la wakristo wengi wanaijua Zaidi elimu ya shetani Zaidi ya kumjua Mungu, mtu atakuelezea kwa mapana na marefu namna wachawi wanavyofanya kazi na namna wanavyologa na aina za majini na mapepo..na dawa za kienyeji, lakini mwambie akufafanulie hata mstari mmoja wa kwenye biblia kama anafahamu. Anamjua shetani Zaidi ya Mungu na hivyo linapotokea tatizo hawezi kujua chanzo chake.
Hivyo inatupasa tujizoeze kumtazama Mungu Zaidi badala ya shetani, biblia inasema Mjue sana Mungu ili upate kuwa na Amani, na sio tumjue sana shetani.

Bwana akubariki

No comments:

Post a Comment