"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Tuesday, July 30, 2019

FAIDA ZA MAOMBI.


 
Maombi yamegawanyika katika sehemu kuu tatu 1) kushukuru 2) kuwasilisha mahitaji kwa mungu 3) Kutangaza.

1) MAOMBI YA SHUKRANI; Maombi haya ya shukrani ni Dhahiri na yanajulika na Wengi, kwamfano maombi ya kushukuru ni muhimu sana, na ni wajibu wa kila mtu, kuyafanya…Na haya yanahusisha kumshukuru Mungu kwa Uzima anaotupa, kumshukuru Mungu kwa afya anayotupa, ukizingatia wakati unapumua kuna wengine wapo ICU, wengine Mochwari n.k, pia maombi haya yanahusisha kumshukuru Mungu kwa mambo yote mabaya aliyokukingia katika wiki yote iliyoisha, mwezi wote uliopita na miaka yote iliyopita nyuma yako, njiani umepishana na mapepo mengi, shetani alikuwa amepanga mauti na ajali nyingi juu yako lakini Mungu kakuepusha nazo zote pasipo hata kukuambia, uthibitisho ni wewe kuimaliza wiki salama, na pia yanahusisha kumshukuru Mungu kwa riziki zote za kiduni anazotupatia, katika shughuli zetu na mapato yetu yote,..Kwahiyo maombi haya kwa ujumla yanahusisha kumshukuru Mungu kwa mambo yote anayoyafanya tunayoyaona na tusiyoyaona. Ni maombi yanayoonesha unyenyekevu wetu mbele za Mungu na kumwonesha Mungu wetu kuwa tunathamini na kuutambua na kuujali ulinzi wake na Fadhili zake juu yetu. Kwahiyo ni sehemu ya maombi ambayo ni muhimu sana.

2) Sehemu ya pili ya maombi ni ile ya KUWASILISHA MAHITAJI YETU MBELE ZA MUNGU. Hii inahusisha kumwendea Mungu kwa unyenyekevu kumwomba atufanyie au atupatie jambo Fulani katika Maisha yetu, Tunamwendea tukiamini kuwa yeye ndiye mpaji wetu (YEHOVA-YIRE). Tunamwomba azidi kutupa riziki zetu, azidi kuzifanikisha kazi zetu za mikono, azidi kutupa afya, azidi kutuepusha na yule mwovu na mipango yake yote, azidi kutupa Neema ya kumjua yeye Zaidi popote tuendapo atukutanishe na injili yake na kuitii, azidi kutupa mioyo ya nyama na si ya jiwe katika kutenda mapenzi yake, azidi kutupa hekima, tunamwomba Bwana azidi kutupa furaha, amani, upendo pamoja na kibali kila tuendapo, na kutufanikisha katika mambo yote katika masaa ya siku yaliyobakia, wiki na katika mwezi huu na unaokuja. Hapa tunamwomba Mungu atuepushe na kila jaribu lililopangwa na shetani kinyume chetu mbele yetu..Kama Bwana alivyosema mahali Fulani “Ombeni kwamba msiingie majaribuni. (Luka 22:40)”.

Ikiwa na maana kuwa usipoomba ni lazima utaingia majaribuni tu!..Wakina Petro usiku ule Bwana aliwaambia waamke kusali ili wasiingie majaribuni wakapuuza, wakalemewa na usingizi wakalala, masaa machache baadaye Petro alipojaribiwa na Ibilisi amkiri Yesu, alishindwa mwisho wake akamkana mara 3 lakini endapo angeomba usiku ule kama Bwana alivyomwambia na kuifunika siku yake wakati Ibilisi anamjaribu angeshinda lile jaribu, saa ile nguvu fulani ya ujasiri ingemshukia pale pale na angemkiri Bwana badala ya kumkana, au Mungu angemuepusha kabisa na jaribu hilo. Lakini kutokana na kwamba alikuwa hana hazina ya maombi ya kutosha, nguvu za roho zilikuwa chin alishindwa. Na aina zote za majaribu zinaweza kuzuiwa au kuepukwa kwa maombi… unapopita mahali na watu kukuudhi mpaka kukasirika na kugombana mpaka kutoa maneno machafu hilo ni majaribu ambalo ungeweza kulizuia kwa kuomba usiku mmoja kabla hujalala, au asubuhi kabla ya kuanza shughuli zako.

Kadhalika unapojikuta unafanya kitu kisichofaa ambacho hukutarajia au hukupanga kukifanya hilo nalo ni jaribu ambalo lingeweza kuzuiliwa kwa kuomba kabla ya kuianza siku..Na dhambi nyingine zote za bahati mbaya zinasababishwa na upungufu wa maombi. Inapotokea safari ya ghafla ambayo ni ya hasara na si ya faida hilo nalo ni jaribu ambalo endapo ungeomba lisingekukuta.nk n.K.

3) Sehemu ya tatu na ya mwisho ya maombi ni maombi ya KUTANGAZA. Hii ni sehemu ya mwisho na ya muhimu sana kwa kila Mkristo kuifanya. Na faida yake kuu ya haya maombi ni ile ile ya KUTUEPUSHA NA MAJARIBU, Maombi haya ni maombi ya kimamlaka…Maombi haya na yale ya KUPELEKA MAHITAJI yanakazi moja tu nayo ni KUTUEPUSHA NA MAJARIBU.

Sasa kabla ya kuingia kujifunza juu ya jambo hili hebu kwanza tujifunze ulinzi wa kiMungu juu ya mtu aliyezaliwa mara ya pili.
Mtu anapozaliwa mara ya pili, na kuishi Maisha yanayompendeza Mungu asilimia zote, kunakuwa kuna ulinzi Fulani wa kiujumla ambao Mungu anauachilia juu yake, kiasi kwamba huyo mtu hata iweje hawezi kupotea, shetani hawezi kumtoa mkononi mwa Mungu, labda tu huyo mtu kwa hiyari yake mwenyewe aamue kujiuza kwa shetani, lakini kwa namna nyingine yoyote hawezi kutoka mikononi mwa Mungu, anakuwa analindwa kuanzia unywele wake mpaka unyayo wako, na anakuwa amevuka kutoka mautini kuingia uzimani, …Lakini pamoja na huo ulinzi wa kiujumla kuna sehemu ndogo sana ambayo Mungu kamwachia shetani aimiliki..na hiyo ni kutokana na kwamba bado tupo katika miili hii ya dhambi, sehemu yote ya ulinzi wa kiMungu tutakuja kuipata baada ya ukombozi wa miili yetu pale tutakapovaa miili mipya ya utukufu.

Ndio maana unaona sasa japokuwa umeokoka na unaishi Maisha ya kumpendeza Mungu kwa asilimia zote lakini bado utapitia wakati mwingine wa viudhaifu vya hapa na pale, utaumwa kichwa, utajisikia kichefuchefu, mafua yatakusumbua, wakati mwingine itakubidi umeze Panadol kupunguza maumivu au uende hospitali n.k. Sasa hiyo yote ni kuonesha kuwa Mungu hajaipa miili yetu hii asilimia 100 ulinzi…ingawa hivi viudhaifu haviwezi kutuathiri kiasi cha kututoa kwenye Imani, kwasababu Mungu hawezi kuruhusu tujaribiwe kupita tuwezavyo, alisema hivyo katika Neno lake.
1Wakoritho 10: 13 “Jaribu halikuwapata ninyi, isipokuwa lililo kawaida ya wanadamu; ila Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili”.
Kwahiyo haya majaribu madogo madogo ni lazima yaje! Na ni wazi kuwa yanaletwa na shetani kututesa tu! Na kutuhangaisha…Kwahiyo shetani anachokifanya ni kutumia hii nafasi aliyopewa ya sehemu ndogo ambayo Mungu kaiacha, kutujaribu…Na kwasababu anajua hawezi kumjaribu mwamini kwa asilimia zote, atahakikisha kuwa hiyo sehemu ndogo aliyopewa anaitumia ipasavyo.
Sasa swali? Anaitumiaje?

Anaitumia kwa KUTANGAZA, Anawatumia watu kutamka maneno Fulani Fulani juu yako, ambayo hayo yanaweza kutokea kama walivyozungumza, kwasababu Mungu alivyomuumba mwanadamu akizungumza kitu kwa Imani ni lazima kitokee hata kama mtu huyo sio mchawi. Ndio maana wazazi hata kama ni waabudu sanamu wanao uwezo wa kumbariki mtoto au kumlaani, na hizo baraka au laana zikampata huyo mtoto hivyo hivyo kama alivyozisema. Kwasababu hiyo basi shetani anaweza kutumia watu au wachawi au mapepo yake KUTANGAZA mambo Fulani mabaya juu ya mtu.

Kumbuka tena kwa msisitizo..kama umezaliwa mara ya pili na kuishi Maisha yampendezayo, haijalishi ni mambo gani makubwa watayatangaza juu yako, hayatatimia yote kwasababu kuna asilimia kubwa ya ulinzi wa kiMungu kwenye Maisha yako, lakini pia yapo baadhi madogo madogo yanayoweza kutimia na hiyo ni kwasababu hatujapewa dhamana wa ulinzi wa miili hii asilimia zote kama tulivyotangulia kusema..(huu ni msingi mkubwa ambao unahitaji kuelewa) Na sio kwamba Mungu kashindwa kutufunika asilimia zote, hapana ni kwasababu tu ndivyo imempendeza iwe hivyo…kwamba tujue kwamba bado tupo duniani?, tujue kuwa sisi bado ni wadhaifu mbele zake, na tujifunze kumtegemea yeye na kumwomba ulinzi…na pia tujue kuwa vita bado vinaendelea…mpaka siku tutakapovaa ile ya utukufu, ndipo vita vitaisha.
2Wakorintho 1:8 “Maana ndugu, hatupendi, msijue habari ya dhiki ile iliyotupata katika Asia, ya kwamba tulilemewa mno kuliko nguvu zetu, hata tukakata tamaa ya kuishi.
9 Naam, sisi wenyewe tulikuwa na hukumu ya mauti katika nafsi zetu ili tusijitumainie nafsi zetu, bali tumtumaini Mungu, awafufuaye wafu,
10 aliyetuokoa sisi katika mauti kuu namna ile; tena atatuokoa; ambaye tumemtumaini kwamba atazidi kutuokoa;”
Sasa ili kupunguza nguvu za shetani kwa majaribu yake anayoyatumia kwa NJIA YA KUTANGAZA…Na sisi tulioamini tuna wajibu huo huo, wa kuingia kwenye maombi ya kuzipunguza hizo nguvu ndogo ndogo za shetani zinazofanya kazi kwenye Maisha yetu…Na maombi hayo hatuyafanyi kwa kupeleka mahitaji mbele za Mungu, bali kwa KUTANGAZA kama yeye anavyotangaza..Ndio hapo sasa Kila siku kabla ya kuianza siku unatamka baraka katika siku hiyo, unalaani na kufuta kila kazi zote za Adui zilizopangwa katika siku hiyo kwa jina la YESU, Unalaani vidhiki na vijaribu vidogo vidogo vilivyopangwa na shetani…Na unatamka kwa maneno yanayosikika kabisa, kwasababu maneno yanaumba, kwa Mungu aliiumba dunia kwa Neno, Unatamka kwa kutangaza kuziharibu nguvu zote na kufuta maneno yote yaliyozungumzwa na watu, wachawi, au mapepo katika siku nzima…unalaani nguvu zote za giza zilizoachiwa siku hiyo zitakazokufanya uikane Imani, au upate hasara ya jambo Fulani, au zitakazokufanya ulumbane au ugombane na watu, unalaani kwa kinywa chako kila nguvu zote za giza zilizoachiwa na yule adui kukufanya usipate muda wa kusoma Neno,na kila ratiba isiyoeleweka iliyopangwa kuzimu kinyume chako na ndugu zako…Unahikikisha unagusa kila kipengele katika Maisha yako, afya yako,familia yako, kazi yako na Imani yako. Usiache kitu!, kwasababu na yule adui anajua anaomlango mdogo juu ya Maisha yako hivyo anakaza kuutumia vizuri.
Mithali 18:21 “Mauti na uzima huwa katika uwezo wa ulimi; Na wao waupendao watakula matunda yake.”
Kwa kufanya hivyo utakuwa umeharibu mipango yote midogo midogo ambayo shetani alikuwa amepanga kukusumbua katika siku hiyo na wiki hiyo. Na hivyo utakuwa umejiongezea Ulinzi wa kiMungu kwa asilimia nyingine kadhaa mbele. Kama alikuwa akuletee viugomvi, viugonjwa, unashangaa siku inaisha bila hivyo vitu, kama alikuwa amekusudia kukuletea vitabu vya hapa na pale visivyoeleweka vinatoweka.

Nakumbuka mwanzoni mwanzoni nampa Bwana Maisha, nilikuwa napitia changamoto nyingi sana na nilikuwa sijui chanzo chake ni nini?..lakini baada ya kujifunza somo la maombi, niliona mabadiliko makubwa sana…

Kwa hiyo ni maombi ya Muhimu sana na kila Mwamini anatakiwa aombe. Na ni moja ya silaha 6 tulizopewa katika biblia..
Waefeso 6: 11 “Vaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kuzipinga hila za Shetani.
12 Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho.
13 Kwa sababu hiyo twaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kushindana siku ya uovu, na mkiisha kuyatimiza yote, kusimama.
14 Basi simameni, hali mmejifunga kweli viunoni, na kuvaa dirii ya haki kifuani,
15 na kufungiwa miguu utayari tupatao kwa Injili ya amani;
16 zaidi ya yote mkiitwaa ngao ya imani, ambayo kwa hiyo mtaweza kuizima mishale yote yenye moto ya yule mwovu.
17 Tena ipokeeni chapeo ya wokovu, na upanga wa Roho ambao ni neno la Mungu;
18 KWA SALA ZOTE NA MAOMBI MKISALI KILA WAKATI KATIKA ROHO, MKIKESHA KWA JAMBO HILO NA KUDUMU KATIKA KUWAOMBEA WATAKATIFU WOTE;
19 pia na kwa ajili yangu mimi, nipewe usemi kwa kufumbua kinywa changu, ili niihubiri kwa ujasiri ile siri ya Injili;
20 ambayo kwa ajili yake mimi ni mjumbe katika minyororo;
hata nipate ujasiri katika huyo kunena jinsi inipasavyo kunena.”
Kwa kumalizia kumbuka kuwa muda wa chini Bwana Yesu aliotuamuru tusali kwa siku ni LISAA LIMOJA.
Mathayo 26: 40 “Akawajia wale wanafunzi, akawakuta wamelala, akamwambia Petro, Je! Hamkuweza kukesha pamoja nami hata saa moja? 41 Kesheni, mwombe, msije mkaingia majaribuni; roho i radhi, lakini mwili ni dhaifu.”

Umeona hapo, roho zetu zipo tayari kuomba lakini miili ndio inayokataa, hivyo mambo mengine ni unalazimisha, kama Bwana asiyekuwa na dhambi aliomba Zaidi ya lisaa limoja, unafikiri inatupasaje sisi wenye dhambi?..unakataa usingizi na uvivu wa kuomba, unalazimisha mambo, utashangaa dakika za kwanza unapata shinda lakini baaada ya dakika 10-15 mbeleni unashangaa kuna nguvu Fulani inakuvaa unajikuta unazama kwenye maombi…Na kwa vipengele hivyo vitatu ukianza na kushukuru, kisha kupeleka maombi na kutangaza baraka..huwezi kuacha kumaliza lisaa na Zaidi..

Na pia kumbuka kuwaombea na wengine, katika vipengele vyote hivyo vitatu, hata hichi unachokisoma hakijapewa guarantee ya ulinzi asilimia 100, kinahitaji maombi kiweze kuendelea kuwepo, kwahiyo uombapo ukumbuke kugusia kila eneo, pamoja na sisi tunaoandika hizi habari, Ili injili ya Mungu izidi kwenda mbele, kwa Neema za Mungu.

Bwana akubariki sana.
www.wingulamashahidi.org

HATARI YA KUTOKUITAFAKARI BIBLIA VIZURI?


Shalom! Mtu wa Mungu, maandiko yanatuagiza tusiache kuonyana kila siku, maadamu iitwapo leo(Waebrani 3:13). Hivyo nakukaribisha tujifunze leo jambo moja lihusulo BIBLIA.

Nilipokuwa ninatafakari hili Neno linalosema ““Iko njia ionekanayo kuwa sawa machoni pa mtu, Lakini mwisho wake ni njia za mauti.”” Nikajiuliza hii njia ionekanayo kuwa sawa ni ipi?..Mtu akiwa mtukanaji, mtu akiwa muuaji, mtu akiwa ni fisadi n.k, njia yake haiwezi kuonekana ni sawa machoni pake, ni wazi kuwa anafahamu anapoeleka ni pabaya..Lakini njia inayoweza kuonekana ni sawa machoni pa mtu ni ipi?, ni ile inayotoka katika maandiko (BIBLIA), pale maandiko yanapomthibitishia mtu kuwa kitu hichi au kile anachokifanya kimeandikwa, basi hilo linampa amani ya kufahamu kuwa yupo katika njia sahihi.
Nataka nikuambie, biblia ni kitabu kitakatifu sana, kimekamilika na kujitosheleza kwa namna zote, hakiwezi kuongezwa wala hakiwezi kupungumzwa, lakini nataka nikuambie pia Biblia hii si ya watakatifu peke yao: Biblia si mti wenye tunda la aina moja, bali ni mti wenye matunda ya aina nyingi tofauti tofauti,. na kila mtu anachuma kinachomfaa na kuondoka kulingana na matakwa yake mwenyewe.

Na hiyo yote ni kwasababu biblia ni Neno la Mungu, na Neno la Mungu tunajua ndio lililoumba kila kitu (Yohana 1:1), halikuumba vyema tu bali hata na viovu pia, hivyo pumzi ya kila kitu inategemea hilo Neno. kwahiyo kila mtu na kila mmoja na inaweza kumnufaisha kulingana na matakwa yake mwenyewe. Shetani inamnufaisha katika lengo lake la kupoteza watu, na amefanikiwa kweli kupoteza mamilioni ya watu kwa kupitia biblia unayoisoma, hata alijaribu kuitumia hiyo hiyo kumwangusha Bwana akashindwa..

Madaktari wanaitumia hii kuwasaidia kubuni aina mbalimbali za matibabu, hata ukiangalia nembo yao kubwa maarufu inayotumiwa na Shirika la Afya ulimwenguni (WHO), utaona ni Yule nyoka wa shaba ambaye Musa aliwaagiza wana wa Israeli wamtazame ili wapone kutokana na sumu ya nyoka. Utamaduni huo ambao baadaye uligeuka kuwa wa kipagani, ulirithiwa na mataifa mengine ya kipagani kama Ugiriki wakahusisha na tiba za kienyeji na mambo hayo, na ndio huko huko mpaka ikawa maarufu katika masuala yote ya tiba duniani leo hii.

Biblia hii hii inayoisoma inatumiwa na majeshi, kubuni mbinu mpya za kupigani: Na wanafanikiwa vizuri sana. Wakati wewe unafurahia kusoma zile habari za vita vya Yoshua na waamuzi, wengine huko wanaiga mbinu za kivita. Biblia hii hii inatumiwa na wanasiasa kutengeza sera zao za kampeni na wanafanikiwa katika hilo, Msome mtu kama kwame Nkrumah raisi wa kwanza wa Ghana,si jinsi alivyoupindua utawala wa kikoloni kwa maandishi ya maandiko.

Biblia hii hii inatumiwa na wachawi na wanajimu, kuwasaidia kufanya uchawi wao: Wasingefahamu kitu kinachoitwa kafara na nguvu iliyokatika damu kama wasingesoma katika biblia..Katika Agano la kale kafara za Wanyama zilikuwa zinafanyika kwaajili ya upatanisho…Asili ya kuvaa hirizi si kutoka kwa wachawi…Wana wa Israeli waliagizwa na Mungu wazivae kwenye vipaji vya nyuso zao, ili kuwakumbusha sheria za Mungu, (vilikuwa ni viboksi vidogo vilivyokuwa vimebeba baadhi ya maneno ya kwenye Torati) lakini Baadaye shetani akaja kuiba huo utamaduni na kutengeneza za kwake kwa lengo la kulogea watu.

Wafanya-biashara na matajiri: Kanuni za kufanikiwa zote wanazitolea katika maandiko,kupanda na kuvuna. Kufanya kazi kwa bidii,n.k. zipo huko, wanazitumia na zinawaletea mafanikio makubwa sana.

Vile vile biblia hii hii inatumiwa na manabii wa Uongo, kutimiza matakwa yao: Wanasoma na kufahamu kuwa ndani ya jina la YESU, kuna uweza wa kipekee, kila kitu kinatii, hivyo hata mtu ambaye alishamkufuru Mungu siku nyingi, anaouwezo wa kulitumia hili jina ili kuamirisha chochote na kikamtii, hata kuamisha milima…hivyo anaweza kutumia fursa hiyo kujipatia mali, au kuwapoteza, kwa kisingizio cha miujiza, na anafanikiwa kabisa, na ndio maana Bwana Yesu alisema wengi watakuja siku ile wakisema Bwana Bwana…, hatukufanya unabii kwa jina lako, na kwa jina lako kutoa pepo, na kwa jina lako kufanya miujiza mingi? Ndipo nitawaambia dhahiri, Sikuwajua ninyi kamwe; ondokeni kwangu, ninyi mtendao maovu. (Mathayo 7:21).

Lakini pia biblia hii hii inatumiwa na watu wengine, na inawapa UZIMA WA MILELE.
Unaweza ukaona hapo, jinsi Biblia inavyofungua milango ya mambo mengi, hata yale maovu, lakini sio milango yote mtu akiingia kwa kupitia biblia inamletea mwisho mwema. Na ndio maana ukisoma maneno ya kwanza kabisa Bwana Yesu aliyoyahubiri ni haya, TUBUNI, KWA MAANA UFALME WA MBINGUNI UMEKARIBIA(Mathayo 4:17)..Na habari zake zote zilikuwa zinalenga ufalme wa mbinguni, kama ukitafuta mahali Bwana Yesu anakufundisha utajiri na mafanikio ya kidunia nataka nikuambie unaweza ukavunjika moyo, zaidi ya yote watu waliojaribu kumfauta kujaribu kumuuliza kuhusu mambo kama hayo aliishia kuwaambia “Uzima wa mtu haupo katika mwingi wa vitu alivyonavyo”(Luka 12:15).

Alikuwepo kwa lengo moja tu la msingi, nalo ni kumpa mtu uzima wa milele. Na wote waliomfuata waliupokea bali waliomkataa hawakaupata bali walipata sehemu ya vipengele vingine katika maandiko.,Leo hii usifurahie na kusema biblia inahimiza hichi ninachokifanya..ukadhani kuwa upo sahihi wakati wote katika hiyo njia…Unapaswa ujiulize je! matokea ya hichi ninachokifanya mwisho wake ni nini?,..Ni uzima wa milele au Mauti, au huna-uhakika?. Ikiwa ni mauti au huna-uhakika, hata kama kuna vifungu vinakusapoti, achana nacho, tafuta kilicho cha msingi kwanza, na biblia imeshaturahisishia kufahamu kilicho cha msingi, nacho ni YESU KRISTO..
Yohana 14:6 “Yesu akamwambia, Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi.”
Ni heri ukakifanya hicho, lakini huku nyuma jambo la msingi la wokovu wako na uzima wa milele lipo pamoja na wewe, hiyo haina shida kabisa,lakini unaacha mambo ya wokovu na habari za kwenda mbinguni, unasema biblia inaniambia hivi au vile …Kumbuka Yesu anasema “hapa yupo aliye mkuu zaidi ya Sulemani”.

Hivyo kwa kumalizia ni vizuri tukajua jinsi ya kuyavunja vunja maandiko na kuchagua vile vilivyo vya muhimu kwanza, ambavyo ni vya UFALME WA MBINGUNI NA HAKI YAKE NA HIVYO VINGINE VILIVYOSALIA TUTAZIDISHIWA tu Bwana ameahidi hilo, yeye si mwongo. Tunajua hizi ni nyakati za kumalizia, Kristo yupo karibuni kurudi kushinda hata sisi tunavyoweza kufikiria..Ikiwa utasikia unyakuo umepita leo na wewe umebaki utakuwa katika hali gani?. Kumbuka atakayeona uchungu zaidi sio mlevi, au jambazi, atakayeona uchungu ni Yule mkristo aliye vuguvugu ambaye aliitupilia injili za wokovu na kwenda mbinguni akageukia injili za namna nyingine za faraji, ambazo thawabu zake zinaishia hapa hapa duniani…siku hiyo huyo ndio atakayeomboleza..Kwasababu alidhani kuwa ndio njia aindeayo uzimani..Lakini mwisho wake umekupeleka kuingia katika dhiki kuu.

Utasema siku ile, Hatukupata mali kwa jina lako Bwana?, hatukufunguliwa matumbo yetu yaliyokuwa tasa kwa jina lako?, hatukufungua biashara nzuri kwa unabii wako?.nk Ni kweli mambo hayo yote uliyafanya kwa jina la Yesu lipitalo majina yote na lifungualo vifungo vyote, lakini siku ile Bwana atasema ondokeni kwangu! Kwanini? kwasababu jina hilo ulipaswa ulitumie pia kukuletea wokovu wako wa milele, si tu vitu vya ulim:wengu huu vinavyopita, jina hilo ulipaswa pia ubatiziwe kwalo, kulingana na Matendo 2:38, Matendo 8:16, Matendo 19:5 na Matendo 10:48. ili upate ondoleo la dhambi zako na upokee kipawa cha Roho Mtakatifu..Umepata fahari zote na ulimwengu mzima kwa jina hilo lakini umekosa uzima kwa jina hilo, itakufaidia nini?.

Jihadhari na njia zinazoonekana ni nzuri, zinazopendwa na kufuatwa na wengi kwa kivuli cha biblia, nyingi zinaelekea upotevuni. kumbuka njia ni nyembamba ielekeayo uzimani

Ubarikiwe sana.Tafadhali “share” ujumbe huu kwa wengine. Na Bwana atakubariki.