"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Thursday, July 25, 2019

SI SHETANI BALI NI WEWE. (CHAGUA MEMA)


Moja ya kazi kubwa PIA shetani anayoifanya ni kuhakikisha watu hawaelewi dhambi ni nini?...Na hivyo anatumia nguvu kubwa kuwafanya watu waamini kuwa chanzo cha matatizo yote ni yeye!...hata mtu akifanya uasherati ni shetani! Mtu akiua ni shetani! Mtu akiiba ni shetani!...Lakini wengi hawajui kuwa shetani naye pia hakudanganywa na mtu, hakukuwa na mtu juu yake wa kumdanganya…alijidanganya mwenyewe (moyo wake ulimpoteza mwenyewe Yeremia 17:9).

Sababu ya kutenda dhambi watu wengi ambao hawaelewi huwa wanamtupia shetani…lakini kumbe ni wao..Shetani, anachokifanya yeye ni kupalilia UOVU tu duniani…lakini yeye sio aliyeuumba uovu, Uovu upo katikati yetu uliumbwa na Mungu, kwa makusudi maalumu ya kutambua wema, kwamfano uovu usingekuwepo basi hata wema usingekuwepo, ili kutambua kitu hiki ni kitamu lazima kiwepo kichungu, lakini kama hakuna kichungu, umejuaje kuwa kile ni kitamu?. (Vivyo hivyo na sisi tumeumbiwa tayari mema na mabaya ni sisi kuchagua)…..Na malaika nao waliumbiwa hicho kitu ilikuwa ni kitendo tu cha wao kuchagua…Na shetani na malaika zake wakachagua mabaya (na huko ndiko kuasi), na matokeo yake wakatupwa duniani…

Na huku duniani tayari kulikuwa kuna mti wa mema na mabaya pale Edeni…Kiasi kwamba hata kama shetani asingekuwepo bado Hawa alikuwa anao uwezo wa kuchagua mabaya, kama angetaka……kwahiyo asili ya uovu sio shetani! Uovu ulikuwepo tangu asili, ni kitendo cha watu kuchagua..(pale Edeni shetani alikuwa ni kama dalali tu! Wa kumvutia na kumshawishi mwanadamu achague uovu). Kwahiyo shetani anachofanya sasahivi yeye na malaika zake ni kuipalilia tu ile njia ya ouvu izidi kuwa pana kwa watu….Ukilijua hilo litakufanya kuwa makini kutokufikiria kila kitu chanzo ni shetani.

Kwahiyo mtu anayekwenda kufanya uasherati leo, ni yeye mwenyewe amechagua uovu kwa ushawishi wa nguvu za shetani…zingati hili (Ni huyo mtu kafanya na sio shetani kafanya kwa niaba yake)…Kwahiyo hapo anayestahili kulaumiwa wa kwanza ni huyo mtu, kwasababu kachagua kufanya mabaya…
Ni sawa leo uende sokoni kununua nguo, ukute maduka mawili mbele yako, moja linauza nguo nyeupe lingine jeusi…na ndani kila mmoja anakushawishi ununue kwenye duka lake…maamuzi ya mwisho yanatoka kwako wewe, na sio kwa mwenye duka…hapo kama utachagua nyeusi au nyeupe na kwenda nyumbani kukuta kasoro, hapo anayestahili kulaumiwa wa kwanza sio muuzaji bali ni wewe ambaye ulikwenda kuchagua…ulipaswa ukague nguo yote kwa makini kabla ya kuinunua, sio kusikiliza tu maneno ya wauzaji na kuamini!

Na ndivyo ilivyo sasa hivi duniani kuna maduka mawili, moja linauza mavazi meupe(ya uzima wa milele), na lingine meusi ni jukumu lako wewe kuchagua lipi linakufaa…kila moja lina watu ndani yake wanaokushawishi na kukuvutia, maamuzi ya mwisho unatoa wewe..sio muuzaji!...Muuzaji anakazi tu ya kukudalalia basi! Mambo mengine unafanya wewe, uchaguzi unafanya wewe na gharama unaingia wewe.

Leo utasikia mtu anakwenda kuzini, halafu anakwambia ni shetani kafanya vile, atakuambia shetani kanipitia tu!... hajakupitia ndugu ni wewe umechagua mwenyewe uovu, kwa kukubali ushawishi wake…Kama ingekuwa ni shetani, basi Mungu asingesema “siku ile kila mtu atasimama mbele ya kiti cha hukumu kutoa hesabu ya mambo yake”…asingesema hivyo, badala yake angesema “shetani atasimama kueleza ni kwanini kawaingia watu na kuwalazimisha wafanye dhambi”…Lakini siku ile kila mtu atahukumiwa kwa aliyoyatenda…kwanini? kwasababu si shetani aliwalazimisha watu kutenda, bali ni watu kwa uchaguzi wao wenyewe walichagua uasi…
Yohana 3: 19 “Na hii ndiyo hukumu; ya kuwa nuru imekuja ulimwenguni, na watu wakapenda giza kuliko nuru; kwa maana matendo yao yalikuwa maovu”.
Kwahiyo mtu yeyote anayetenda dhambi, ni katenda dhambi kwa idhini yake mwenyewe baada ya kuzidiwa na ushawishi wa shetani kufanya hilo jambo. Hivyo hapo shetani ni mtu wa pili kulaumiwa baada yake yeye…wa kwanza kabisa kulaumiwa ni yeye na ndio afuate shetani.

Hebu tafakari juu ya hili ili upate kuelewa kuwa kuna upofu Fulani unaendelea…..Mtu atakapotenda jambo fulani jema, labda amsaidie maskini hatasema ni Mungu kafanya lile jambo…atasema ni yeye kafanya…ukimwuliza imekuaje umefanya hivyo, atakwambia nimeguswa tu kufanya hilo jambo! Na tena ukimwuliza ni wewe au Mungu ndio kafanya hilo jambo atakwambia ni yeye ndiye aliyefanya 100%..... Mungu ni kama kamsaidia tu…na tena ataamini kuwa anastahili baraka kutoka kwa Mungu kwa alichokifanya lakini huyo huyo mtu hebu afanye uasherati utasikia anasema ni shetani huyo!..sio mimi ni shetani, utaona malaumu yote na sababu zote anamtupiwa shetani na kuanza kumlalamikia Mungu kwanini hakumwua shetani…lakini alipotenda mema hakusema ni Mungu kafanya bali alisema ni yeye, tena alipokea utukufu kutoka kwa watu kuwa yeye ndiye aliyefanya ule wema!.

Ndugu kama ni haki yako kupata baraka kutoka kwa Mungu kwa kutenda mema…jua pia ni haki yako kupata laana kutoka kwa Mungu kwa uovu unaoufanya!..Uovu unaoufanya, Mungu wala shetani hawahusiki, ni wewe ndio unaoamua kuufanya..wao ni kama washauri tu!..Ndio maana Mungu pia atawapa thawabu watakatifu wake watakaoshinda mbinguni, siku ile hatajipa yeye thawabu, atawapa watakatifu kwasababu ni wao ndio walioamua kufanya mema, sio Mungu.

Kumbuka pia unapotenda mema ni Mungu ndiye atakubariki, na unapotenda mabaya ni Mungu ndiye atakulaani na sio shetani, kwasababu sio shetani aliyeuumba uovu, ndio maana unaona pale Edeni baada ya Adamu na Hawa kuasi ni Mungu ndiye aliyewalaani na sio shetani!...aliyesema tutakula kwa jasho sio shetani ni Mungu!...aliyesema tutazaa kwa uchungu sio shetani ni Mungu! Aliyeilaani ardhi sio shetani ni Mungu!. Kwahiyo ukitenda uovu leo hii ni umeuchagua kwa hiyari yako mwenyewe na hivyo utakuwa unaishi katika laana kutoka kwa Mungu. Shetani hahusiki hapo!.
Wengi wanawalaumu pia Adamu na Hawa kuwa ndio sababu ya mambo yote..Ni kweli wao walichangia kuifanya njia ya upotevu iwe pana Zaidi lakini ni vyema ukafahamu kitu kimoja…hata kama Adamu na Hawa wasingekula lile tunda, kusingemzua shetani kuwajaribu Watoto wao, na hata kama watoto wao pia wasingekula tunda kwa kukataa ushawishi wa shetani pia isingemzua shetani kuwajaribu wajukuu wao na vitukuu vyao…na ingeendelea hivyo hivyo mpaka mwisho wa vizazi vyote, shetani angekuwa anandelea kuwajaribu tu wanadamu….hata siku wewe unazaliwa ungemkuta shetani naye pia asingeacha kukujaribu kula tunda hata kama vizazi vyako vya nyuma vyote vimeshinda…Kwahiyo hata kama Adamu na Hawa wasingenaswa pengine ungeweza kunaswa wewe!...uthibitisho ni hizo dhambi za makusudi unazozifanya sasa….

Ndio maana huoni mahali popote kwenye Biblia Mungu akiwalaumu Adamu na Hawa, baada ya kutoka pale Edeni..kwasababu wote tumefanya dhambi… Hivyo geuza mtazamo wako wa kuwasingizia baadhi ya watu na shetani kuwa ndio chanzo cha matatizo Fulani, ni kweli wanaweza kuwa wamehusika kwa sehemu Fulani…lakini sehemu kubwa ya maamuzi ipo kwako!!.

Kristo leo anagonga moyoni mwako umegeukie kumbuka shetani anapenda umsingizie yeye ili siku ile ya hukumu ujute! Useme laiti ningepata huu ufahamu angali nipo duniani nisingekuwa mtu wa visingizio…Chagua mema leo usichague mabaya yaletayo laana. Ni rahisi kuchagua mema, yupo mmoja ambaye aliweza kuchagua mema, yeye ndiye anayeweza kutufundisha na sisi namna ya kuchagua mema…na huyo si mwingine Zaidi ya YESU KRISTO, aliyemzungumziwa mahali Fulani hivi…
Isaya 7: 14 “Kwa hiyo Bwana mwenyewe atawapa ishara. Tazama, bikira atachukua mimba, atazaa mtoto mwanamume, naye atamwita jina lake Imanueli.
15 Siagi na asali atakula, WAKATI AJUAPO KUYAKATAA MABAYA NA KUYACHAGUA MEMA”.

Huyu ndio Mkuu wa Uzima, aliyebeba wokovu, hakuna aliyemfuata yeye akajuta, alituambia maneno haya..
Mathayo 11: 27 “Akasema, Nimekabidhiwa vyote na baba yangu; wala hakuna amjuaye Mwana, ila Baba; wala hakuna amjuaye Baba, ila Mwana, na ye yote ambaye Mwana apenda kumfunulia.
28 Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha.
29 Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu;
30 kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi”.
Hivyo tunamtii na kumfuata kama tulivyo, na mizigo yetu.. kama ni mwasherati unaenda kama ulivyo, kama ni mtazamaji wa pornography unaenda kama ulivyo, kama ni msengenyaji vivyo hivyo, kama ni mlawiti, shoga, mlevi,mtoaji mimba, mwizi,muuaji,mla rushwa, mcheza kamari, mwenye huzuni, mwenye msongo wa mawazo, uliyefungwa na nguvu za giza,..msogelee leo, utue mzigo wako pale… hapo ulipo Tubu kwa kumaanisha kuacha kabisa kufanya hayo mambo, na yeye ni mwaminifu atakusamehe…

Na baada ya kufanya hivyo ili ukamilishe toba yako nenda katafuta ubatizo sahihi wa kuzama mwili wote katika maji na kwa jina la YESU KRISTO, kwaajili ya ondoleo la dhambi zako kulingana na Matendo 2:38, dhambi zinakamilika kuondolewa kwa ubatizo sahihi…na baada ya Hapo Roho mwenyewe ataingia ndani yako na kukuongoza katika kuijua kweli yote ya Biblia na kukusaidia katika kuchagua yaliyo mema na kukataa mabaya..na utakuwa na uhakika wa uzima wa milele.

Kumbuka tunaishi siku za mwisho, siku yoyote Parapanda inalia, na watakatifu watanyakuliwa kwenda juu mbinguni, tujitahidi mimi na wewe tuwe miongoni mwao walioalikwa Karamuni.

Bwana akubariki sana, Tafadhali share kwa wengine ujumbe huu.

No comments:

Post a Comment