"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Monday, August 19, 2019

ROHO I RADHI, LAKINI MWILI NI DHAIFU.

Mathayo 26:40 "26.40  Akawajia wale wanafunzi, akawakuta wamelala, akamwambia Petro, Je! Hamkuweza kukesha pamoja nami hata saa moja? 26.41  Kesheni, mwombe, msije mkaingia majaribuni; roho i radhi, lakini mwili ni dhaifu"


Mathayo 26:39 “Akaendelea mbele kidogo, akaanguka kifulifuli, akaomba, akisema, Baba yangu, ikiwezekana, kikombe hiki kiniepuke; walakini si kama nitakavyo mimi, bali kama utakavyo wewe.
40 Akawajia wale wanafunzi, akawakuta wamelala, akamwambia Petro, Je! Hamkuweza kukesha pamoja nami hata saa moja?
41 Kesheni, mwombe, msije mkaingia majaribuni; ROHO I RADHI, LAKINI MWILI NI DHAIFU”.
Sentensi hiyo inamaanisha… ‘Roho ipo tayari lakini Mwili ni dhaifu’…Tunapotaka kufanya kitu chochote cha KiMungu…roho zetu zipo tayari kufanya jambo hilo, likini miili yetu haipo tayari…
Katika habari hiyo hapo juu tunasoma, Baada ya Bwana Yesu kuzunguka mchana kutwa pamoja na wanafunzi wake kuifanya kazi, jioni ilipofika hawakupata muda wa kupumzika walikwenda kwenye nyumba moja ambayo waliandaliwa wakae, wakiwa humo Bwana aliendelea kuzungumza na wanafunzi wake mambo mengi, pamoja na kuwaaga, maana huo ndio ulikuwa usiku wa mwisho kukaa nao, hivyo walikaa masaa mengi kwenye hiyo nyumba, wakiwa wanaimba, na kuonywa katika safari yao, na kutiwa moyo na Bwana..zaidi ya hayo katika usiku huo huo ndio Bwana aliwaosha miguu wanafunzi wake kuwapa kielelezo, pamoja na kushiriki meza ya Bwana…hivyo walichelewa sana muda wa kulala…Ukifuatilia kwa makini utakuja kugundua kuwa sio chini ya saa nane usiku ndio waliacha kuzungumza…Kwahiyo ni wazi kuwa walikuwa wamechoka mno.. Lakini cha kipekee ni kwamba, baada ya mazungumzo hayo ya muda mrefu hivyo, bado Bwana aliwaambia wakasali pamoja naye wasilale…
Hebu tafakari mchana kutwa mmetembea huku na huko, na bado mpaka muda wa usiku mmechelewa kulala, badala mpunzike ndio kwanza mnaambiwa mkasali, kwa hali ya kawaida ni ngumu kidogo lakini Bwana alijua hilo linawezekana…Na ndio maana akawaambia ya kuwa ‘siku zote roho ipo radhi, lakini mwili ndio dhaifu’…Hivyo hapo ni vita vya kupambana na mwili..Ikiwa na maana kuwa tukiweza kuushinda mwili basi tutafaidika sana katika roho.

Sasa ni namna gani ya kuushinda mwili?

Kwanza ni muhimu kufahamu kuwa, sisi kuwa na mwili sio dhambi! Kusudi la Mungu kututengenezea mwili pamoja na tamaa zake halikuwa baya tangu mwanzo, wala halikuwa mtego! Bwana alitutengenezea hii miili, pamoja na tamaa zake ili tuweze kuishi katika hii dunia kwa raha na furaha pasipo kuboreka, ndio kusudi la mwili, kwamba ili tusikwazike kipindi mwili unataka kupumzika, akauumbia kitu kinaitwa usingizi, hivyo wakati mwili ukitaka kupumzika, unazama kwenye usingizi mzito, ambao unampa mtu raha sana anapolala…hebu tafakari kusingekuwa na usingizi, na miili yetu inajizima ghafla tu inapochoka halafu tunaisubiria masaa labda 7 au 8 ndio ijiwashe tena, tuweze kuendelea na shughuli zetu, tungeichoka hii miili kiasi gani?? kadhalika ili mtu asiboreke katika kula, Mungu akauwekea mwili hamu ya kula kiasi kwamba mtu atatamani kula hata kama wakati mwingine hana njaa…lakini kusudi kuu la kula si kutupa sisi raha, bali kuupa mwili nguvu…tafakari endapo kungekuwa hakuna raha yoyote katika kula, lakini tunalazimika kula hivyo hivyo tungeichoka hii miili kiasi gani?..na tungeilisha hata vitu visivyofaa..n.k

Vivyo hivyo ili tuufurahie ulimwengu huu, tusije tukajihisi tumewekwa sehemu isiyo na maana Mungu katuumbia tamaa nyingi tofauti tofauti, ambazo hizo ni kama zinaongeza ladha za kuishi katika huu ulimwengu, tamaa ya kukusanyika pamoja, kucheza pamoja, kufurahi pamoja, na nyingine nyingi….Ndilo lilikuwa ni kusudi la Mungu tuishi katika ulimwengu huu pasipo kuboreka wala kuona ni mahali pabaya….

Lakini baada ya Adamu na Hawa kuasi, dunia yote ikaingiliwa na uovu, hivyo sio kila kitu kikawa kinafaa tena kutamani katika ulimwengu…Adamu akampa shetani milki ya ulimwengu huu, shetani akavumbua na kuwekeza mambo yapotezayo mengi, hivyo kwa yeyote atakayeangukia kwa tamaa moja wapo ya mambo yake aliyoyavumbua yeye, atakuwa amepotea, hivyo ndio maana biblia inatuambia tutoke katika ulimwengu, wala tusiutamani ulimwengu, kwasababu ulimwengu umeshaharibika.
Sasa tukirudi kutafakari ni namna gani tutaushinda mwili.
Mwili hatutaushinda kwa kuukemea, kwasababu tamaa hizi ziliumbwa na Mungu mwenyewe,wala hazikuwekwa na shetani…. huwezi kukemea njaa, wala usingizi, wala huwezi kukemea pua zako zisisikie harufu nzuri, wala huwezi kukemea mwili wako usisimke unapopitia hali Fulani ya kuusisimua.

Njia pekee ya kuushinda mwili, ni kujitenga mbali na vishawishi vinavyosababisha tamaa, kwamfano ukitaka mate yasikutoke, dawa ni moja tu! Kukaa mbali na sehemu wanazotengeneza vyakula unavyovipenda, huwezi kujizuia usitamani chakula mbele ya chakula, ni vita ngumu ambayo hutaiweza, kadhalika unapotaka kujizuia usiwake tamaa za mwili, dawa ni kukaa mbali na vichochezi vyote kama utazamaji wa picha chafu( pornography) pamoja na kampani za kidunia, ambazo kutwa kuchwa ni kuzungumzia hayo mambo, miziki ya kidunia, na pia kutakaa kuwa katika mahusiano na mtu yeyote kabla ya ndoa,Hilo tu! Utasikia mtu anakumbia niombee nishinde tamaa, tamaa zinanisumbua!!! Hakuna maombi yoyote ya kushinda hayo mambo ndugu yangu! Usidanganyike!! Dawa ni kukaa mbali na hivyo vitu.

Kadhalika ukitaka kushinda usingizi dawa ni kukaa mbali na kitanda na kuwa bize!..Unatoa mawazo yako katika kulala na kuyapeleka katika kitu kilichopo mbele yako.. Hakuna maombi yoyote ya kuuzuia usingizi…Bwana Yesu hakuwaambia wakina Petro waamke waanze kukemea pepo la usingizi!! Hapana…aliwaambia waamke wasali!...ikiwa na maana kuwa hakuna cha pepo hapo..Ni jambo la kuamua tu!.

Nimekutana na mtu akiniambia kila nikiingia kwenye ibada, au nikiwa katika kusali au kusoma Neno usingizi unanijia? Lakini nikitazama movie Fulani usingizi haunijii…kwahiyo hilo litakuwa ni Pepo Fulani linalonizuia kusoma Neno!...Ndugu hilo sio pepo! Ni wewe mwili wako umeupa nafasi ya kulala unapotaka kusoma Neno..Utauliza kivipi?...Hebu tafakari kama ni shetani ndiye anayekupa usingizi wakati wa kusoma biblia, jiulize ni movie ngapi za kidunia ambazo pia ulipozifungua kuziangalia tu haijapita dakika tano umelala?..utagundua kuwa hata hizo za kidunia kama umeboreka nazo unalala pia! Sasa kama ni shetani ndiye anayekuletea usingizi unaposoma Neno, vipi unaposinzia wakati unaangalia hizo za kidunia zinazokuboa?..je! na hapo ni shetani? Kwamba anakuletea usingizi usiangalie movie za kidunia?...Hivyo utaona usingizi unakuja wenyewe popote pale unapofanya jambo lisilokunufaisha au lisilokusisimua sana…

Kwahiyo dawa ya kushinda usingizi unaposali ni kwenda kujifunza kwa kina umuhimu wa maombi, ukishajua umuhimu wa maombi, na ukijifunza kutotoa udhuru kuwa ni shetani kakupitia kamwe hutalala!..usingizi utakapokuja utauzima tu!..Wengine wasiolala wala hakuna chochote cha kipekee ndani yao kinachowafanya wasilale wala wasikudanganye kuwa ni pepo lipo juu yako! Hakuna pepo hapo ni wewe mwenyewe hujaamua kuwa makini tu!…Mimi sijawahi kulala ibadani, na wala hakuna chochote cha kipekee kinachoendelea ndani yangu, wala hakuna pepo lolote ninaloshindana nalo ndani, wala hakuna maono ninayoona kujizuia kufanya jambo hilo…Nikujizuia tu! Na kuelewa umuhimu wa hicho kitu! Basi!..Na wote wasiolala wasikudanganye kuwa wao ni wa kiroho sana!...hapana! ni wameelewa tu umuhimu wa kinachoendelea pale na wamejifunza kuuzuia usingizi! Wengine wametambua kuwa kila wakiingia kwenye ibada wakiwa wamekula ni rahisi kulala, hivyo wanajifunza kula baada ya kutoka kwenye ibada n.k….ndicho kinachowafanya wao wasilale, hakuna cha ziada!, wala wasikudanganye kuwa unahitaji kufanyiwa maombi ya deliverance!..hakuna !Ni wewe kubadilika tabia tu!.

Biblia inasema Roho I radhi lakini Mwili ni dhaifu….Roho zetu zipo tayari kutenda mapenzi ya Mungu, vita kubwa ni sisi kuishinda kwa kuelewa ufunuo wa maombi, na kusoma Neno..Kadhalika, tutaishinda kwa kukaa mbali na vitu vinavyonyanyua tamaa ya mambo hayo. Pia nenda kasali mbali na kitanda chako, kama upo mwenyewe, lakini ni vizuri zaidi ukisali na mwenzako au wenzako, kwasababu mtatiana nguvu.
Kwa kumalizia Kumbuka kuwa! Ulimwengu huu, sio ule Bwana alioukusudia tuuishi kwa tamaa za miili yetu, ulimwengu huu shetani amekabidhiwa hivyo, matendo yote ya mwili na tamaa zake zote mwisho wake ni ziwa la moto..Biblia inasema…
Wagalatia 5:16 “Basi nasema, Enendeni kwa Roho, wala hamtazitimiza kamwe tamaa za mwili.
17 Kwa sababu mwili hutamani ukishindana na Roho, na Roho kushindana na mwili; kwa maana hizi zimepingana, hata hamwezi kufanya mnayotaka.
18 Lakini mkiongozwa na Roho, hampo chini ya sheria.
19 Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi,
20 ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi,
21 husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu”.
Bwana akubariki sana.

No comments:

Post a Comment