"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Tuesday, October 8, 2019

KUOTA NYOKA.

Nakusalimu katika jina la mwokozi wetu YESU KRISTO, Suala la upambanuzi wa ndoto ni moja ya mambo ambayo yanawasumbua wengi, lakini kwa bahati mbaya watu wengi wamekosa kujua tafsiri ya ndoto zao, kulingana na maandiko…

Hivyo kabla ya mtu hukimbilia kupewa au kutafuta tafsiri ya ndoto yake ni vizuri kwanza akafahamu kuwa ndoto zimegawanyika katika makundi makuu matatu, kundi la kwanza ni zile ndoto zinazotokana na Mungu, kundi la pili ni zile zinazotokana na shetani na kundi la tatu ni ndoto zinazotokana na mtu mwenyewe, na hizi ndizo zinazochukua sehemu kubwa ya ndoto tunazoziota karibu kila siku, na aina hii ya tatu huwa inakuja kutokana na shughuli zetu tunazozifanya kila siku au mazingira yanayotuzunguka kila siku..Ndoto za namna hii huwa hazibebi ujumbe wowote, hivyo hazihitaji kutafsiriwa, mara nyingi zinapaswa zipuuziwe..ikiwa hujafahamu vizuri namna ya kuitambua ndoto yako kulingana na makundi haya basi bofya somo hii ulipitie kisha ukishamaliza tuendelee...>> NITAJUAJE KAMA NDOTO NI YA MUNGU AU YA SHETANI?
 
Watu wengi wamekuwa wakiniuliza tafsiri ya ndoto hii ya kuota nyoka, sasa ikiwa ni ndoto ambayo inajirudia rudia, basi izingatie sana..kumbuka Nyoka katika maandiko tangu mwanzo anasimama kama ishara mbaya,
 
Na nyoka amebeba tabia kuu tatu, ya kwanza ni kudanganya kama tunavyomsoma pale Edeni alivyomdanganya Hawa(Mwanzo 3:1-5), tabia ya Pili ni kuuma kama biblia inavyotuambia atakugonga kisigino(Mwanzo 3:15), na ya tatu ni kumeza, kama tunavyosoma katika kitabu cha Ufunuo 12:4), pale alipotaka kummeza mtoto yule alipotaka kuzaliwa,..Na tabia hizi zote Shetani anazo na ndio maana kila mahali alifananishwa na joka, na sio kiumbe kingine chochote kama vile kondoo au njiwa.
Hivyo ndoto za namna hii nyingi zinatoka kwa shetani, na chache sana zinakuja kutoka kwa Mungu, lakini tukianza kuchambua upande mmoja mmoja hatutamaliza, wengine wanaota wanakimbizwa na nyoka, wengine wanaota wanaumwa na nyoka, wengine wanaota wameviringishwa na nyoka, wengine wanaota wapo karibu na ziwa au bahari na lijoka likubwa linatoka huko, wengine wanaota wanamezwa na joka, wengine wanaongea nayo n.k. n.k. vyovyote vile chamsingi ambacho mtu anapaswa kufahamu hapo ni kuwa ziwe zinatoka upande wa Mungu au upande wa shetani,..Ni kwamba ADUI YUPO MBELE YAKO.
Hapo Shetani yupo karibu na wewe kutimiza kazi hizo tatu au aidha mojawapo,

Jambo la kwanza ni  kukudanganya au tayari ameshakudanganya: Sasa Ikiwa upo nje ya Kristo yaani hujaokoka basi fahamu kuwa upo chini ya udanganyifu wa shetani tayari, hivyo hapo unaonyeshwa hali yako ilivyo rohoni, Jambo unalopaswa kufanya ni kurudi kwa Kristo haraka sana kabla udanganyifu haujawa mkubwa zaidi ukakuzalia matunda ya mauti, hapo ulipo tayari umepofushwa macho pasipo hata wewe kujijua.Hivyo tubu umgeukie Mungu haraka sana.

Au kwa namna nyingine shetani anakaribia kukushawishi kuingia katika kosa au dhambi ambayo itakugharimu sana, hata maisha yako, hivyo angalia njia zako, uchukue tahadhari, funga milango yote ambayo unaona itakupeleka mbali na Kristo, acha kufanya vitu ambavyo sasa hivi unavifanya unaona kabisa havimpendezi Mungu, acha haraka sana, upo mtego wa shetani nyuma yake.

Pili shetani anakutegea mtego au anataka kukuletea madhara aidha katika huduma yako, au afya yako,au familia yako au shughuli yako, anataka kukugonga kisigino chako usisonge mbele, hapo unapaswa uongeze kiwango chako cha maombi kama Bwana Yesu alivyosema ombeni msije mkaingia majaribuni..Hivyo ili kumshinda silaha uliyonayo ni kuomba sana.

Tatu shetani anataka kukimeza kile ambacho Mungu amekipanda ndani yako: Na jambo la kwanza huwa anakimbilia ni NENO LA MUNGU hilo ndilo huwa anafanya bidii sana kupambana nalo kwasababu anajua likishakuwa ndani ya mtu litakwenda kuleta madhara makubwa sana katika ufalme wake hivyo anasimama hapo karibu na wewe ili akimeze kile ulichokisikia.. inafananishwa na zile mbegu ambazo zilingukia njiani ndege wakaja kuzila,
Mathayo 13:18 “Basi ninyi sikilizeni mfano wa mpanzi.
19 Kila mtu alisikiapo neno la ufalme asielewe nalo, huja yule mwovu, akalinyakua lililopandwa moyoni mwake. Huyo ndiye aliyepandwa karibu na njia.”
Hivyo kwa ufupi ikiwa upo nje ya Kristo fanya hima uingie ndani, na ikiwa upo ndani ya Kristo chukua tahadhari uimarishe uhusiano wako na Kristo kwasababu shetani yupo karibu na wewe kushindana nawe kwa kila hali..

Ubarikiwe.


kwa mtiririko mzuri wa masomo na mafundisho mengi ya Neno la Mungu fungua website yetu hii https://wingulamashahidi.org

No comments:

Post a Comment