"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Monday, December 18, 2017

MAELEZO JUU YA UFUNUO 13


Tukisoma kitabu cha Ufunuo mlango wa 13 tunaona kuna wanyama wawili wanaozungumziwa pale; wa kwanza akiwa ni yule mwenye vichwa saba na pembe 10 aliyetoka baharini na wa pili ni yule aliyekuwa mfano wa mwanakondoo mwenye pembe 2 akitoka katika nchi.

Kwa ufupi tuwatazame hawa wanyama wanawakilisha nini na wanachukua nafasi gani katika siku hizi za mwisho:

MNYAMA WA KWANZA:

Ufunuo 13:1-5" Kisha nikaona mnyama akitoka katika bahari, mwenye pembe kumi, na vichwa saba, na juu ya pembe zake ana vilemba kumi, na juu ya vichwa vyake majina ya makufuru.
2 Na yule mnyama niliyemwona alikuwa mfano wa chui, na miguu yake ilikuwa kama miguu ya dubu, na kinywa chake kama kinywa cha simba, yule joka akampa nguvu zake na kiti chake cha enzi na uwezo mwingi.
3 Nikaona kimoja cha vichwa vyake kana kwamba kimetiwa jeraha la mauti, na pigo lake la mauti likapona. Dunia yote ikamstaajabia mnyama yule.
4 Wakamsujudu yule joka kwa sababu alimpa huyo mnyama uwezo wake; nao wakamsujudu yule mnyama, wakisema, Ni nani afananaye na mnyama huyu? Tena ni nani awezaye kufanya vita naye?
5 Naye akapewa kinywa cha kunena maneno makuu, ya makufuru. Akapewa uwezo wa kufanya kazi yake miezi arobaini na miwili.
6 Akafunua kinywa chake amtukane Mungu, na kulitukana jina lake, na maskani yake, nao wakaao mbinguni.
7 Tena akapewa kufanya vita na watakatifu na kuwashinda, akapewa uwezo juu ya kila kabila na jamaa na lugha na taifa.
8 Na watu wote wakaao juu ya nchi watamsujudu, kila ambaye jina lake halikuandikwa katika kitabu cha uzima cha Mwana-Kondoo, aliyechinjwa tangu kuwekwa misingi ya dunia.
9 Mtu akiwa na sikio na asikie.
10 Mtu akichukua mateka, atachukuliwa mateka. Mtu akiua kwa upanga, atauawa kwa upanga. Hapa ndipo penye subira na imani ya watakatifu. "



Hapa tunamwona huyu mnyama akiwa na vichwa saba na pembe 10, na juu ya zile pembe zake ana vilemba 10, sasa hivi vichwa 7 inafahamika vinawakilisha ngome/mamlaka ambazo shetani alizikalia na kuzitumia kupambana na kuuharibu uzao wa Mungu hapa duniani tangu taifa la Israeli lilipoundwa. Na tawala hizi tunaweza tukaziona katika biblia nazo ni 1) MISRI   2) ASHURU, 3) BABELI 4) UMEDI & UAJEMI   5) UYUNANI   6) RUMI   7) RUMI -KIDINI.


Lakini Yohana alimwona yule mnyama akiwa na PEMBE 10 katika kichwa chake, kumbuka zile pembe 10 hazikuwa zimesambaa juu ya vichwa vyote saba kama inavyofikiriwa na watu wengi, bali zote 10 Yohana alizoziona zilikuwa juu ya kichwa KIMOJA TU! na sio kingine zaidi ya kile kichwa cha saba. Kwahiyo kile kichwa cha saba ndicho Yohana alichokikazia macho kwasababu kilikuwa ni tofauti na vingine vyote.


Hivyo zile pembe 10 kulingana na maono aliofunuliwa Danieli juu ya ile sanamu ya Nebukadneza alioiona yenye miguu ya chuma na nyayo zenye vidole 10 zilizochanganyikana nusu chuma, nusu udongo, kama inavyojulikana ile miguu ya chuma ni utawala wa RUMI na vile vidole ni utawala wa RUMI uliokuja kugawanyika na kuwa yale mataifa kumi ya ULAYA wakati ule ambayo yalikuwa bado hayana nguvu kwasababu yalikuwa bado hayajavikwa vilemba(CROWNS). Hivyo vile vidole 10 ndio zile pembe 10 zinazoonekana juu ya yule mnyama na ni mataifa 10 yaliyopo katika umoja wa ULAYA (EU), na kama tunavyoona sasa kwa huyu mnyama zile pembe 10 zimetiwa VILEMBA inaashiria kuwa utakuja wakati haya mataifa yanayounda umoja wa ulaya yatapewa nguvu ya utawala na yule mnyama kutenda kusudi la kuwaua watakatifu katika kipindi cha ile miaka mitatu na nusu ya mwisho ya dhiki kuu.


Leo hii tunaona umoja wa ulaya unaundwa na mataifa zaidi ya 10, lakini yatakuja kuishia kuwa 10 tu ili kutimiza unabii wa kwenye biblia na yapo mbioni kuvikwa vilemba( yaani kupewa utawala wa dunia) yakiwa chini ya yule mnyama ( RUMI) chini ya utawala wa PAPA ambaye ndiye mpinga-kristo biblia inayomwitwa "mtu wa kuasi", mwana wa uharibifu ajiinuaye nafsi yake juu ya kila kiitwacho Mungu ama kuabudiwa.(2Thesalonike 2). Leo hii bado hayana nguvu kwasababu Danieli alionyeshwa kuwa vile vidole kumi nusu yake vitakuwa na nguvu na nusu yake vitakuwa vimevunjika ndivyo ilivyo sasa hivi Umoja wa ulaya hauna nguvu sana, lakini utakuja kupata nguvu duniani kote ili kutimiza kusudi la yule mnyama(mpinga-kristo)

Tukiendelea kusoma mstari wa tatu tunaona moja ya kichwa chake (ambacho ndio kile kichwa cha saba) kimetiwa jeraha la mauti nalo likapona. Kumbuka Rumi-ya kidini(UKATOLIKI) iliyokuwa chini ya UPAPA katika historia ilikuwa inatawala dunia nzima, na ilifanikiwa kupata nguvu dunani kote kiasi cha kwamba mtu yeyote aliyeonekana anakwenda kinyume na hiyo dini adhabu ilikuwa ni kifo tu, mamilioni ya wakristo waliouwa wote waliokataa kuisujudia miungu yao ya kipagani, jambo hili liliendelea na hii dini ilizidi kupata nguvu hadi kufikia karne ya 16 wakati wa matengenezo ya kanisa ambapo Mungu alianza kuwanyanyua watu wake kama Martin Luther ambaye alianza kufundisha watu "kuhesabiwa haki kwa imani" na kukosoa mafundisho potofu ya kanisa Katoliki lakini PAPA alipotaka kumuua mfalme wa Ujerumani alisimama kumuhifadhi Luther, ndipo watu wengi wakaanza kuacha hii dini ya uongo na kuligeukia NENO la Mungu hivyo Ukatoliki ukaanza kupungua nguvu, na wakati huo huo Mungu aliwanyanyua wengine kama Calvin, Zwingli, Knox n.k. ili kulitengeneza tena kanisa lililokuwa limeharibiwa na mafundisho ya uongo ya Kanisa katoliki.



Hapo ndipo ulipokuwa mwanzo wa lile jeraha la yule mnyama lakini pigo hasa lilikuja karne ya 18 mwaka 1798 katika mapinduzi huko Ufaransa Jenerali Berthier alipeleka vikosi vyake Roma na kumng'oa PAPA katika utawala wake, akamchukua mateka pamoja na mali zake zote za dini yake, Hivyo ikapelekea dini ya kikatoliki iliyokuwa inatiisha dunia kuwa karibuni na kutoweka kabisa, hilo lilikuwa pigo kubwa sana lilofananishwa na jeraha la mauti lakini tunaona Biblia inasema lile JERAHA LA MAUTI lilipona,


 Je! Jeraha hili liliponaje na lilipona lini?.


Wakati wa vita vya kwanza na vya pili vya dunia, matatizo yalikuwa mengi duniani, uchumi ulishuka sana, mataifa ya ulaya yaliaanza kuanguka na kupoteza nguvu zao kutokana na athari ya vita, Hivyo kiu ya kutafuta amani duniani ikaongezeka kumbuka wakati huo huo Marekani ilianza kupata nguvu, na likiwa kama taifa la kikristo (protestant) lenye nguvu kubwa ya kiuchumi na kijeshi hivyo kwa kushirikiana na mataifa ya ulaya kwenye harakati za kutafuta amani, (isiyokuwa ya kivita) walianza kuutambua umuhimu wa PAPA Kwasababu alionekana kuwa ni mtu mwenye mvuto na anayekubalika na watu wengi duniani, hivyo mataifa mengi yakaanza kutuma mabalozi wake kwa papa ajihusishe na masuala ya AMANI YA DUNIA. Sasa kuanzia hapo jeraha lake la mauti likaanza kupona, wale ambao walikuwa wanafanya mageuzi kinyume chake(protestants) wakaanza kushirikiana nae tena, uprotestant ukabakia kuwa jina tu na ndio huko inapoundiwa ile sanamu ya mnyama nitakayoielezea zaidi mbeleni...



Tukiendelea mstari 4 & 5, Tunaona lile joka ambaye ni Shetani mwenyewe alimpa nguvu yule mnyama naye akaanza kunena maneno makuu ya makufuru. Tukisoma pia kitabu cha Danieli alizungumziwa kama ile PEMBE ndogo iliyozuka na kungo'a wale wafalme watatu na kunena maneno ya makufuru Danieli 7:25 "Naye atanena maneno kinyume chake Aliye juu, naye atawadhoofisha watakatifu wake Aliye juu; naye ataazimu kubadili majira na sheria; nao watatiwa mikononi mwake kwa wakati, na nyakati mbili, na nusu wakati. " Na huyu si mwingine zaidi ya mpinga-kristo ambaye ni PAPA,..Si ajabu PAPA leo anasimama "badala ya mwana wa Mungu duniani"..Vicarivs filii Dei, ..Papa leo amejivika uwezo wa kusaheme dhambi jambo ambalo BWANA YESU KRISTO mwenyewe ndiye anayeweza kulifanya ..haya yote ni maneno ya makufuru, na yapo mambo mengi zaidi ya hayo ambayo ni makufuru. Kumbuka ninaposema PAPA namaanisha kile "CHEO"..kwahiyo yeyote anayekikalia hicho cheo amejitwika cheo cha mpinga-kristo mwenyewe.


Na tunaona wakati wa mwisho atapewa uwezo wa kutenda kazi miezi 42, hii ni miaka mitatu na nusu, kati ya ile miaka saba ya mwisho ya lile juma la 70 la Danieli. Hichi kitakuwa kipindi cha DHIKI KUU, sasa hivi PAPA anaonekana kama mtu asiyekuwa na madhara yoyote, anakuja kwa njia ya kujipendekeza ili apate nguvu kiurahisi, kama kitabu cha Danieli kinavyomtabiri, leo hii duniani kote anajulikana kama "MTU WA AMANI", Ni mtu mwenye wafuasi wengi duniani, na aneyekubalika kuliko mwanasiasi yoyote duniani, dini nyingi zimeanza kuvutiwa naye, hata waislamu sasa wanamwona kama ni mtetezo wao mtu anayejali watu wote, PAPA anasema wote tunamwabudu Mungu mmoja ila kwa njia tofauti tofauti (yaani wakristo, waislamu wahindu, wabudha tunamwabudu Mungu mmoja), angali biblia inasema YESU ndiye njia pekee ya kumfikia Mungu, na cha ajabu umaarufu wake unaongozeka na watu wanamfurahia ili kutimiza ule unabii kwamba "watu wote ambao majina yao hayajaandikwa katika kitabu cha uzima cha mwanakondoo kabla ya kuwekwa misingi ya ulimwengu ndio watakaomsujudia." Na kumsujudia sio kumpigia magoti bali ni kukubaliana na mifumo yake na imani yake.


Ndugu yangu mpinga-kristo hatakuja na mapembe kichwani, akilazimisha watu wamwabudu, kumbuka biblia inasema shetani ana HEKIMA kuliko Danieli, na sehemu nyingine biblia inasema ile roho itataka kuwadanganya yamkini hata wateule. Siku zote anakuja kama malaika wa nuru, usitazamie kuwa mpinga-kristo atakuwa muislamu au muhindi au freemason, hapana ndugu yupo kanisani amebeba biblia na anafanya kampeni za amani duniani na watu wanamshangilia na kumbusu, biblia inasema hapo ndipo "PENYE HEKIMA " .

Kwahiyo inahitajika Hekima kumjua vinginevyo utachukuliwa na mafuriko yake kama wengi walivyochukuliwa huu ni wakati wa kuwa macho sana, jali maisha yako ya umilele yanayokuja. Chunguza maandiko kama watu wa Beroya, sio kila roho inayoshabikiwa na wengi unaipokea moyoni mwako kwasababu biblia inasema IPO NJIA IONEKANAYO KUWA NJEMA MACHONI PA WATU..LAKINI MWISHO WAKE NI UPOTEVU, na BWANA YESU alisema njia iendayo upotevuni ni PANA na wengi wanaiendea hiyo.


MNYAMA WA PILI:

Ufunuo 13:11-18"
11 Kisha nikaona mnyama mwingine, akipanda juu kutoka katika nchi; naye alikuwa na pembe mbili mfano wa Mwana-Kondoo, akanena kama joka.
12 Naye atumia uwezo wote wa mnyama yule wa kwanza mbele yake. Naye aifanya dunia na wote wakaao ndani yake wamsujudie mnyama wa kwanza, ambaye jeraha lake la mauti lilipona.
13 Naye afanya ishara kubwa, hata kufanya moto kushuka kutoka mbinguni uje juu ya nchi mbele ya wanadamu.
14 Naye awakosesha wale wakaao juu ya nchi, kwa ishara zile alizopewa kuzifanya mbele ya huyo mnyama, akiwaambia wakaao juu ya nchi kumfanyia sanamu yule mnyama, aliyekuwa na jeraha la upanga naye akaishi.
15 Akapewa kutia pumzi katika ile sanamu ya mnyama, hata ile sanamu ya mnyama inene, na kuwafanya hao wote wasioisujudu sanamu ya mnyama wauawe.
16 Naye awafanya wote, wadogo kwa wakubwa, na matajiri kwa maskini, na walio huru kwa watumwa, watiwe chapa katika mkono wao wa kuume, au katika vipaji vya nyuso zao;
17 tena kwamba mtu awaye yote asiweze kununua wala kuuza, isipokuwa ana chapa ile, yaani, jina la mnyama yule, au hesabu ya jina lake.
18 Hapa ndipo penye hekima. Yeye aliye na akili, na aihesabu hesabu ya mnyama huyo; maana ni hesabu ya kibinadamu. Na hesabu yake ni mia sita, sitini na sita. "


Tunaona huyu mnyama wa pili ana pembe kama mwanakondoo, lakini sio mwanakondoo, na huyu anaonakana ametoka katika nchi na sio katika bahari na yeye hana vichwa saba Kama yule mnyama wa kwanza, ikiwa na maana kuwa utawala wake haukuanzia mbali kama yule mnyama wa kwanza bali ulizuka mwishoni. Hivyo huyu mnyama si mwingine zaidi ya MAREKANI. Ukiangalia katika ile nembo ya Marekani katika ile dola yao utaona yule tai akiwa ameshika mishale 13, ile piramidi kuna ngazi 13, kuna nyota 13 juu ya yule tai, matawi 13 ya ule mzeituni ulioshikwa ..nk. kila mahali 13..13... na taifa la Marekani linaonekana katika UFUNUO 13.


Pia huyu mnyama alipewa uwezo wa kufanya watu wote wakaao duniani wamsujudie yule mnyama wa kwanza na kuunda ile SANAMU YA YULE MNYAMA.


Sasa Sanamu ya mnyama ni ipi?

Marekani kama taifa lilokuwa la kiprotestant ambalo hapo kwanza lilikuwa halishakamani wala halishirikiani na kanisa Katoliki kwa namna yoyote, lakini katika karne ya 20 baada ya vita ya pili Vya dunia liliacha njia ya kweli ya NENO LA MUNGU, na kurudi kuiga tabia za yule mnyama,kazi nzuri na juhudu zote zilizofanywa na wale wana-matengenezo zikawa ni bure, ni sawa na mbwa aliyerudia matapishi yake.


Baada ya kuibuka jopo kubwa la madhehebu ya kiprotestant duniani, viongozi wa madhehebu ya kimarekani walikutanika kwa agenda ya kutaka kuondoa tofauti katikati ya wakristo ili kufikia muafaka mmoja wa IMANI, ndipo walipounda BARAZA LA MAKANISA ULIMWENGUNI (World Council Of Churches), na NATIONAL COUNCIL OF CHURCHES , na ndio chimbuko la EKUMENE. (Ecumenical council)
Na Kanisa Katoliki likiwa kama washirika wao wa karibu wakiwasaadia.


Baraza hili la UMOJA WA MAKANISA liliazimu kuyarudia mambo yale yale ya ukahaba yaliyofanywa na kanisa Katoliki, Iimekuwa ni SHIRIKA LA KI-DINI, na Linasheria zake na itakadi zake ambazo zinaenda kinyume na mpango na NENO LA MUNGU. Kwahiyo UMOJA HUU ndio unaoitwa SANAMU YA MNYAMA..Kwasababu tabia zote zilizokuwa katika kanisa kahaba katoliki zipo nazo kule na hivi karibuni yule mnyama (America) ataenda kuipa PUMZI ILE SANAMU INENE, ili watu wote waiabudu, hii ikiwa na maana siku sio nyingi watu wote duniani watenda kulazimishwa kuwa washirika wa muunganiko wa hayo makanisa mtu yeyote atakayeonekana kwenda kinyume atauawa.

Na kama tunavyoona huyu mnyama wa pili (MAREKANI) anaweza kufanya ishara kubwa hata kufanya moto kushuka kutoka mbinguni, jambo hili linatupa picha nguvu za kijeshi walizonazo Marekani kama uwezo wa kushusha makombora makubwa ya vita kutoka angani mabomu ya atomic n.k.


Hili baraza la makanisa duniani sasa linafanikiwa kuzivuta dini zote ulimwenguni pamoja, ikiasisiwa na PAPA kiongozi wa kanisa katoliki duniani, itafika wakati kama hautakuwa mshirika wa dini au kanisa ambalo halijaunganishwa katika huu UMOJA WA MAKANISA NA DINI hutaweza kuuza wala kununua wala kuabudu, wala kuishi katika jamii,


Leo hii tunaona vitendo vya kigaidi na vya mauaji vikiongezeka, wanasiasa wameshindwa kuirejesha amani ya dunia, na matatizo yote yahusuyo amani yanatokana na mizozo ya kidini tunaweza kuona mambo yanayoendelea mashariki ya kati mfano Israeli, syria-kuna ISIS,Iraq, Lebanoni-kuna hezbolah, myanmar huko Asia kuna warohighya, sehemu za Afrika nchi kama Nigeria kuna Boko kuna haramu, Somalia-alshabaab, central Africa- antibalaka ..na makundi mengine mengi sana,. tunaona mizizi yote ya migogoro inaanzia katika DINI. Hivyo atahitajika mtu wa KIDINI mashuhuri kutatua migogoro ya kidini na sio wanasiasa au watu wa kijamii - Na huyu atakuwa si mwingine zaidi ya PAPA kwasababu yeye ndiye anayekubaliwa na dini zote pamoja na wafalme wote wa dunia.


Hivyo atapokwisha kupata nguvu, ataibua mfumo mmoja wa kutambua watu wote duniani kwa imani zao, kwa kivuli cha kuleta amani na kukomesha vitendo vya uvunjifu amani duniani kumbe nia yake itakuwa ni kuwateka watu wote duniani na kuwatia ile CHAPA YA MNYAMA. Wakati huo watu wengi duniani wataufurahia huo mfumo pasipo kujua ndio wanaipokea chapa hivyo. Wengi watasajiliwa katika madhehebu na dini zao zilizokuwa na ushirika huo wa UMOJA WA MAKANISA ULIMWENGU , Vitatumika vitu kama CHIPS, IDS, na utambulisho mwingine utakotengenezwa ili kuyafikia makundi yote, sasa wale watakaokaidi ndio watakaopitia dhiki kuu, hao ndio watakaoonekana magaidi na wavunjifu amani, kama sivyo kwanini wasikubali utambulisho huo mpya? na kumbuka watakuwa ni wachache sana watakaogundua kuwa ndio CHAPA YENYEWE ,Kwa maelezo marefu zaidi kuhusu chapa ya mnyama fuatilia link hii >>>
https://wingulamashahidiwakristo.blogspot.com/2016/10/chapa-ya-mnyama.html


Hivyo ndugu injili tuliyonayo sasa hivi inasema ..UFUNUO 18:4-5" Kisha nikasikia sauti nyingine kutoka mbinguni, ikisema, TOKENI KWAKE, ENYI WATU WANGU,MSISHIRIKI DHAMBI ZAKE, wala msipokee mapigo yake.Kwa maana dhambi zake zimefika hata mbinguni, na Mungu amekumbuka maovu yake. "


Ndugu toka katika mifumo ya madhehebu kwasababu yameshirikiana na yule mnyama(kanisa katoliki) kufanya ukahaba, na kuua watakatifu wa Mungu wengi, yeye anaitwa BABELI MKUU, MAMA WA MAKAHABA ikiwa na maana kama yeye ni mama wa makahaba ni dhahiri kuwa anao mabinti na wao pia ni makahaba kama mama yao alivyo na hao mabinti sio wengine zaidi ya madhehebu yote yaliacha uongozo wa Roho mtakatifu na kuandamana na desturi za kanisa kahaba Katoliki, hivi karibuni tumesikia WALETHERANI wameungana rasmi wakatoliki.!! Biblia inasema TOKENI KWAKE ENYI WATU WANGU, kama ukishirikiana naye inamaanisha kwamba na wewe pia utashiriki mapigo yake ndivyo Mungu anavyokuchukulia.


Ufunuo 14:9 " Na mwingine, malaika wa tatu, akawafuata, akisema kwa sauti kuu, Mtu awaye yote akimsujudu huyo mnyama na sanamu yake, na kuipokea chapa katika kipaji cha uso wake, au katika mkono wake, yeye naye atakunywa katika mvinyo ya ghadhabu ya Mungu iliyotengenezwa, pasipo kuchanganywa na maji, katika kikombe cha hasira yake; naye atateswa kwa moto na kiberiti mbele ya malaika watakatifu, na mbele za Mwana-Kondoo. "


Bwana ametuita kuwa BIKIRA SAFI, na bikira tu ndiye atakayeingia katika karamu ya mwanakondoo, toka kwenye mifumo ya madhehebu umwabudu Mungu katika ROHO NA KWELI.


Mungu akubariki, na Mungu atusaidie katika safari yetu tuumalize mwendo salama

Amen.

8 comments:

  1. May the Lord Almighty be our strong shield.Ameen

    ReplyDelete
  2. Hapo kwenye hayo maelezo kuna walakini

    ReplyDelete
  3. Mungu akubaliki sana mtumishi, nimejarb kuchukua Somo hili kushea na Wenzetu wa kiroho sehemu mbalimbali ili Ujumbe huu ufike mbali zaidi, wengi wapate ufahamu wa kuyatambua haya, Na kuyashika. Barikiwa sana

    ReplyDelete
  4. Ngoja nitafte popcorn za afu 50 aisee nimalize hapa

    ReplyDelete
  5. Oya bro dah nimefunguka vitu vingi saana๐Ÿ™๐Ÿ™

    ReplyDelete