"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Friday, December 7, 2018

JIWE LA KUSAGIA

Marko 9.41 “Kwa kuwa ye yote atakayewanywesha ninyi kikombe cha maji, kwa kuwa ninyi ni watu wa Kristo, amin, nawaambia, hatakosa thawabu yake.
42 Na ye yote atakayemkosesha mmojawapo wa wadogo hawa waniaminio, afadhali afungiwe jiwe la kusagia shingoni mwake, na kutupwa baharini. “Na ye yote atakayemkosesha mmojawapo wa wadogo hawa waniaminio, afadhali afungiwe jiwe la kusagia shingoni mwake, na kutupwa baharini”.
Bwana Yesu alisema Ishara hizi zitafuatana na hao waaminio? kwa jina langu watatoa pepo; watasema kwa lugha mpya; watashika nyoka; hata wakinywa kitu cha kufisha, hakitawadhuru kabisa; wataweka mikono yao juu ya wagonjwa, nao watapata afya (Luka 1:17-18).

Lakini pamoja na ishara hizo, zipo ishara nyingine zinazofuatana na hao waaminio..Na ishara hizo ni thawabu zinazoambatana nao, kadhalika na laana zitakazoambana nao kama wasipotii.

Mtu aliyemwamini Kristo, akatubu na kuacha dhambi zake kabisa, na kupokea Roho Mtakatifu, Bwana huwa anampa thawabu mkononi mwake katika ulimwengu wa roho na huwa hiyo thawabu inatembea naye…Inapotokea kafika mahali kakaribishwa na watu na kuhudumiwa vizuri hata nafsi yake ikafurahi na kuburudika, wale watu waliomhudumia mtu huyo kwakuwa ni mtu wa Kristo, huwa biblia inasema haimpiti kamwe thawabu yake. Kumbuka kumtendea wema Mkristo ni tofauti na kumtendea mema maskini ambaye sio Mkristo.

Ukimtendea mema Mkristo ni sawa umemtendea mema Kristo mwenyewe kwasababu ndani ya yule mtu, yupo Kristo mwenyewe. Ukimkaribisha umemkaribisha Kristo mwenyewe, ukimbariki ni sawa umembariki Kristo mwenyewe..Hivyo thawabu yake ni kubwa zaidi kuliko thawabu ya kumsaidia mtu mwingine yoyote ambaye sio mkristo.

Lakini pamoja na kwamba kuna Baraka zinazoambatana na watoto wa Kristo, wote waliozaliwa mara ya pili, zipo pia Laana zinazofuatana na hawa watoto wa Mungu. Biblia inasema “amlaaniye Israeli atalaaniwa na ambarikiye Israeli atabarikiwa…Sasa licha ya wale wa Israeli tunaowaona kule mashariki ya kati, wapo pia waisraeli ambao ni waisraeli hasa,.. na hawa sio wengine zaidi ya watoto wote wa Mungu,waliompokea Bwana Yesu Kristo na kumwamini na kuoshwa dhambi zao kwa damu yake. Hawa ndio waisraeli hasa biblia inayowataja.

Hivyo kumlaani mtu yoyote ambaye ni milki ya Bwana Yesu, mtu aliyeamua kuyasalimisha maisha yake kwake ni sawa na kumlaani Kristo mwenyewe na ni sawa na kujilaani wewe mwenyewe… Kwahiyo ni muhimu sana kuchunga midomo yetu, mbele za watoto wa Mungu. Usimwone ni Mpole ukamdharau wala usimwone ni wa huruma ukamtamkia maneno yasiyofaa utajitafutia matatizo ambayo chanzo chake hutakijua.

Sasa laana nyingine iliyo mbaya, ambayo inatembea na hili kundi la watoto wa Mungu, ni ile itokanayo na KUWAKOSESHA.

Ni heri umlaani mtu aliyempa Kristo maisha yake, kwasababu mtu huyo anaweza kukusamehe na pengine Mungu akaepusha ghadhabu yake juu yako, lakini kosa lolote mtu atakalofanya litakalomfanya yule mtoto wa Mungu aliyekuwa amesimama kiimani KUANGUKA…Hilo ni kosa ambalo halina msamaha ni baya kuliko kosa la kumlaani.

Sasa nini maana ya KUKOSESHA.


Kukosesha ni jambo lolote ambalo mtu anaweza kumfanyia mtoto wa Mungu kwa makusudi aliyesimama kiimani kuanguka na kurudi nyuma au kutenda dhambi, au kosa lolote litakalomfanya mtoto wa Mungu amkosee Mungu wake.

Kwamfano imetokea Binti kampa Kristo maisha yake kweli na kakusudia kuacha dhambi kabisa, na kabatizwa, Na akaanza kuishi maisha ya ukristo kulingana na maandiko, lakini kijana mmoja pale pale kanisani anayejua kabisa maandiko anatokea na kuanza kumsumbua na kumtaka, na hatimaye kumdanganya, na kwasababu ya ule uchanga wa kiroho wa yule binti akanaswa na mtego wa Shetani na kuanguka katika dhambi ya uasherati na kumkosea Bwana Mungu wake, sasa yule binti Bwana atamwadhibu … Lakini yule kijana aliyemkosesha ana adhabu kubwa zaidi kuliko ya yule binti.. Au binti anayejua kabisa kijana Fulani kaokoka na anamtumikia Bwana kwa moyo,lakini kwa tama yake ya macho anaanza kumtafuta kijana yule na kumshawishi, kwa kujipendekeza hata akamwangusha yule kijana kwenye dhambi ya uasherati wake hapo Ndio biblia inasema… “Ingemfaa zaidi mtu huyo JIWE LA KUSAGIA LIFUNGWE SHINGONI MWAKE, akatupwe baharini, KULIKO KUMKOSESHA MMOJAWAPO WA WADOGO HAWA.”

JIWE LA KUSAGIA NI NINI BASI?.

Zamani watu walikuwa hawasagi nafaka kwa mashine kama tulizonazo sasa, walikuwa wanasaga kwa kutumia mawe mawili, lile kubwa linakaa chini na lile dogo linakuwa juu ndio linalotumika kusagia…mawe haya yanakuwa ni mazito sana ili kusudi kusaidia nafaka ile iweze kusagika na kuwa unga…Sehemu chache sana katika nyakati hizi ndio bado zinatumia huo ustaarabu wa usagaji wa nafaka. Lakini zamani ilikuwa ni lazima kila nyumba iwe na hilo jiwe, hata kama hiyo nyumba ni maskini vipi, ilikuwa ni kitu cha muhimu sana, ni kama tu kinu kwa sasa..usipokuwa na jiwe hilo ilikuwa huwezi kula kwasababu ndio kifaa cha msingi kabisa cha riziki kilichokuwa kinahitajika katika nyumba kwa wakati huo.

Sasa Bwana Yesu alitumia mfano wa jiwe la kusagia, kufunua kwamba mtu yoyote atakayemkosesha “mmojawapo wa wadogo wamwaminio yeye” ingelimfaa zaidi mtu huyo jiwe hilo la kusagia lifungwe shingoni mwake na kwenda kutupwa baharini…Yaani kwa lugha nyepesi ni kwamba INGEMFAA ZAIDI MTU HUYO RIZIKI YAKE YOTE ANAYOIPATA IONDOLEWE, NA IWE KITANZI KWAKE CHA KUMWUA KATIKA MAANGAMIZI AMBAYO YANATOKANA NA HIYO RIZIKI. na pale anaposema akatupwe katika bahari alimaanisha mtu huyo, ATUPWE KATIKA ZIWA LA MOTO”

Unaona hiyo laana jinsi ilivyo mbaya?? Ina maana kuwa katika mahali popote unapopatia riziki, hiyo sehemu inakuwa kitanzi kwako cha kukufanya wewe uangamie kwa kuzama kama mtu anavyozama katika maji akiwa na jiwe shingoni, na hatimaye hiyo sehemu yako ya kujipatia riziki (kazi yako) inakuua na kuwa sababu ya kukupeleka katika ziwa la Moto.

Ulikuwa unafanya kazi nzuri, na kupata kipato kizuri, hiyo kazi inageuka kuwa kitanzi kwako inaanza kukushusha chini, inakuzamisha kwenye matatizo ambayo hayajawahi kutokea, inakutafuna na mwisho wa siku inakuua, na baada ya kifo inakupeleka katika ziwa la moto. Hata kama bado hujafikia hatua ya kujitafutia mwenyewe lakini ikiwa unafanya dhambi hizo za makusudi, itafika tu wakati utatatufa kitu kwa ajili ya maisha yako. Na ndiko huko huko utakapokwenda kujimalizia mpaka kuzimu.

Ndugu yangu unayesoma haya, jiepushe na watoto wa Mungu, wewe binti kaa mbali na walioamua kumfuata Bwana Yesu, usijaribu kuwashawishi wawe kama wewe ulivyo, usijaribu kuwashawishi watoke katika mstari ili kumkosea Bwana wao wawe kama wewe. Kama wewe umeamua kuwa vuguvugu basi kuwa kwa nafsi yako mwenyewe, usiwafanye watoto wengine wa Mungu wajikwae kwasababu yako, ni kujitafutia matatizo yasiyokuwa na utatuzi.

Usiwashawishi wengine, kuvaa vimini, kuvaa suruali, kupaka wanja, kwenda disco, na ndani ya dhamira yako unajua kabisa, mambo hayo ni makosa kuyafanya kwa watumishi wa Mungu…Usijaribu kuyafanya hayo, kwasababu ni sawa na unamfanyia Kristo mwenyewe.

1Wakoritho 8: 12 “Hivyo, mkiwatenda dhambi ndugu zenu na kuitia jeraha dhamiri iliyo dhaifu, mnamtenda dhambi Kristo”.

Kwa nje utamwona katika hali ya udhaifu, lakini ndani yake yupo Kristo, Siku ile ya Mwisho Bwana Yesu alisema atawatenga kondoo na mbuzi, mbuzi ni wale wote waliolikwaza na kulihuzunisha na kulikosesha kundi hili la watoto wa Mungu, wale wote ambao waliwalaani, na kuwatesa na kuwakosesha watoto wa Mungu hao wote watakaa mkono wa kushoto wa YESU Kristo siku ile, watahukumiwa na kisha watatupa katika lile ziwa liwakalo moto na kiberiti.

Mathayo 25: 41Kisha atawaambia na wale walioko mkono wake wa kushoto, Ondokeni kwangu, mliolaaniwa, mwende katika moto wa milele, aliowekewa tayari Ibilisi na malaika zake;
42 kwa maana nalikuwa na njaa, msinipe chakula; nalikuwa na kiu, msininyweshe;
43 nalikuwa mgeni, msinikaribishe; nalikuwa uchi, msinivike; nalikuwa mgonjwa, na kifungoni, msije kunitazama.
44 Ndipo hao pia watajibu, wakisema, Bwana, ni lini tulipokuona wewe una njaa, au una kiu, au u mgeni, au u uchi, au u mgonjwa, au u kifungoni, tusikuhudumie?
45 Naye atawajibu, akisema, Amin, nawaambia, Kadiri msivyomtendea mmojawapo wa hao walio wadogo, hamkunitendea mimi.
46 Na hao watakwenda zao kuingia katika adhabu ya milele; bali wenye haki watakwenda katika uzima wa milele”.
Kama ulikuwa unafanya hayo pasipo kujua, Bwana ni mwenye Rehema, anachotaka kwako ni ukiri tu ulifanya hayo pasipo kujua na kwamba unahitaji kugeuka na kuwa kiumbe kipya, kwa kudhamiria kabisa kumuishia Mungu, na kuishi maisha matakatifu ya kumpendeza yeye.. Na kuwa katika kundi lake lililobarikiwa la kondoo na sio mbuzi. Baada ya kutubu Bwana alitupa maagizo ya kwenda kubatizwa, hivyo katafute haraka mahali panapobatiza ubatizo sahihi wa kuzamishwa kwenye maji mengi na kwa JINA LA YESU KRISTO na baada ya kufanya hivyo Bwana atakupa kipawa cha Roho wake Mtakatifu atakayekusaidia kushinda dhambi na kukuongoza katika kweli yote. Baada ya hapo utakuwa na uhakika wa uzima wa milele, na umekamilisha hatua za muhimu za wokovu.

Bwana akubariki.

2 comments: