"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Monday, July 30, 2018

JINSI ITAKAVYOKUWA KATIKA SIKU ILE

Je! Unafahamu yatakayotokea muda mfupi sana kabla ya kuondoka kwetu kwenda kumlaki Bwana mawinguni?..Ni kweli unyakuo utakuja tu ghafla kwa watakatifu wa Mungu?, Kama haufahamu Biblia ilishatupa mwangaza juu ya suala hilo tunasoma katika;

1Wathesalonike 5: 1 “Lakini, ndugu, kwa habari ya nyakati na majira, hamna haja niwaandikie.
2 Maana ninyi wenyewe mnajua yakini ya kuwa siku ya Bwana yaja kama vile mwivi ajavyo usiku.
3 Wakati wasemapo, Kuna amani na salama, ndipo uharibifu uwajiapo kwa ghafula, kama vile utungu umjiavyo mwenye mimba, wala hakika hawataokolewa.
4 BALI NINYI, NDUGU, HAMMO GIZANI, HATA SIKU ILE IWAPATE KAMA MWIVI.
5 Kwa kuwa ninyi nyote mmekuwa wana wa nuru, na wana wa mchana; sisi si wa usiku, wala wa giza.
6 Basi tusilale usingizi kama wengine, bali tukeshe, na kuwa na kiasi.
7 Maana walalao usingizi hulala usiku, pia na walewao hulewa usiku.
8 Lakini sisi tulio wa mchana, tuwe na kiasi, hali tukijivika kifuani imani na upendo, na chapeo yetu iwe tumaini la wokovu”.

Unaona hapo maandiko yanaeleza wazi kabisa, siku ile itakuwa kama mwivi kwa wale mataifa(wasio watakatifu) wasiomjua Mungu, kwasababu wao wapo gizani siku zote na usingizi wa mambo ya ulimwengu huu umewalemea, lakini kwa watakatifu wa Mungu, muda mfupi kabla ya siku ya unyakuo kufika watafahamu, na hii ni kutokana na matukio ambayo yatakuwa yanaambatana nao katika siku ile.. Ni kweli biblia haijaeleza siku wala saa lakini imetoa majira(dalili) za kuja kwake, na hizi dalili zipo za ndani na za nje, Sasa za nje ndio kama hizi tunazozifahamu mfano, matetemeko, vita, manabii wa uongo, mji wa Israeli, chukizo la uharibifu n.k…Lakini za ndani zinahusu Ishara inayomuhusu Bibi-arusi wa Kristo peke yake, na hizo zipo tatu,

Leo tutazungumzia moja ya hatua (Ishara) ambayo ni ya mwisho kabisa, itakayowafanya watakatifu sasa wafahamu kuwa siku yao ya kuondoka imefika. Biblia imeeleza wazi unyakuo utaambatana na hatua tatu kuu. 1) MWALIKO WA BWANA, 2) ya pili ni SAUTI YA MALAIKA MKUU, 3) na ya tatu ni PARAPANDA YA MUNGU..

Hatua mbili kati ya hizo tulishazielezea kwa undani katika masomo yaliyotangulia, kama hujazijua unaweza ukazifuatilia kwenye somo linaloitwa UNYAKUO

Lakini leo tutamalizia na hatua ya mwisho ambayo ni PARAPANDA YA MUNGU, hii ni Ishara ya mwisho, kama tunavyoweza kuisoma katika…

1Wathesalonike 4: 13 “Lakini, ndugu, hatutaki msijue habari zao waliolala mauti, msije mkahuzunika kama na wengine wasio na matumaini.
14 Maana, ikiwa twaamini ya kwamba Yesu alikufa akafufuka, vivyo hivyo na hao waliolala katika Yesu, Mungu atawaleta pamoja naye.
15 Kwa kuwa twawaambieni haya kwa neno la Bwana, kwamba sisi tulio hai, tutakaosalia hata wakati wa kuja kwake Bwana, hakika hatutawatangulia wao waliokwisha kulala mauti.
16 Kwa sababu Bwana mwenyewe atashuka kutoka mbinguni pamoja na MWALIKO, na SAUTI YA MALAIKA MKUU, na PARAPANDA YA MUNGU; nao waliokufa katika Kristo watafufuliwa kwanza.
17 Kisha sisi tulio hai, tuliosalia, tutanyakuliwa pamoja nao katika mawingu, ili tumlaki Bwana hewani; na hivyo tutakuwa pamoja na Bwana milele.
18 Basi, farijianeni kwa maneno hayo”.

Sasa wakwanza watakaoisikia sauti ya Bwana hawatakuwa watakatifu walio hai, bali ni wale watakatifu waliotangulia kulala mautini, wakati huo wakiwa huko PEPONI walipo wataisikia sauti ya Bwana ikiwaita kutoka makaburini ikiwaambia wakati umefika wa kutoka huko, kama kipindi kile Lazaro aliposikia sauti ya Bwana ikimwita kutoka makaburini ikimwambia,, “Lazaro njoo huku nje”(Yohana 11) Kadhalika sauti hii hii itasikika tena kwa wale watakatifu waliokuwa wamekufa katika Bwana, kama Bwana Yesu alivyosema katika Yohana 5: 25 “Amin, amin, nawaambia, Saa inakuja, na sasa ipo, wafu watakapoisikia sauti ya Mwana wa Mungu, na wale waisikiao watakuwa hai.”..Hivyo hiyo itawafanya watoke makaburini na ile miili yao waliokuwa nayo zamani na kutembea duniani.

SASA SWALI KUU UNAPASWA UJIULIZE, BAADA YA HAO WATAKATIFU KUFUFUKA NI KITU GANI KITAFUATA?

Ili kuelewa vizuri mambo mafupi yatakayofuata hapo katikati, inatupasa tujifunze kwanza kwa yaliyotokea katika ufufuo wa kwanza, Kumbuka Bwana aliwafufua watakatifu wa kwanza, lakini hakuwapeleka mbinguni bali mahali panapoitwa (PEPONI/PARADISO). Lakini kabla ya kwenda huko kuna vitu vilionekana.

Tusome kwa ufupi ni vitu gani vilitokea baada ya wale watakatifu kufufuliwa katika ule ufufuo wa kwanza.
Mathayo 27: 50 “Naye Yesu akiisha kupaza sauti tena kwa nguvu, akaitoa roho yake.
51 Na tazama, pazia la hekalu likapasuka vipande viwili toka juu hata chini; nchi ikatetemeka; miamba ikapasuka;
52 MAKABURI YAKAFUNUKA; IKAINUKA MIILI MINGI YA WATAKATIFU WALIOLALA;
53 nao wakiisha kutoka makaburini mwao, baada ya kufufuka kwake, WAKAUINGIA MJI MTAKATIFU, WAKAWATOKEA WENGI”.
Kumbuka huu ufufuo wa kwanza tunaouna hapo ni kivuli cha ufufuo wa pili, kama vile katika ufufuo wa kwanza kabla ya watakatifu kuingia Peponi waliingia mji mtakatifu na kuwatokea watakatifu wengine waliokuwa hai duniani kwa wakati ule, Vivyo hivyo na katika ule ufufuo wa mwisho wa watakatifu, kabla ya kutoweka duniani kwa watakatifu na kwenda mbinguni kutakuwa na kipindi Fulani kifupi sana ambacho wale watakatifu waliokufa katika Bwana kabla yao, watawatokea wale wanaoishi..

Kumbuka pia walikuwa hawawatokei tu ilimradi,labda kuwafurahisha hapana, bali walikuwa na huduma maalumu ya kuifanya kwa muda mfupi, na hii si nyingine zaidi ya kuwashuhudia wale watakatifu waliokuwa hai kwamba ni kweli wao waliisikia sauti ya waliyemsulibisha YESU KRISTO ikiwaita kutoka katika vifungo vya mauti, na kwamba yeye kweli ndiye MASIHI aliyetabiriwa kuwaokoa watu na uthibitisho ni wao,..

Embu jaribu kutengeneza picha wale wayahudi ghafla wanamwona Baba yao Ibrahimu, na Yakobo na Yusufu wamesimama mbele yao wakiwashuhudia habari za Yesu, unadhani wale watu kuanzia ule wakati walikuwa thabiti kiasi gani?, utawaeleza kitu chochote kuhusu Bwana Yesu?. Ni wazi kuwa yale matukio yaliwapa nguvu wale watakatifu ambao walikuwa wanamtumaini Bwana kama mwokozi wao.

Kadhalika pia na katika ufufuo wa mwisho wa wafu, biblia ilisema hatutawatangulia wale waliolala mautini, kwamba wao ndio watakaofufuliwa KWANZA, ikiwa na maana kuwa wao ndio watakaoisikia sauti ya Mungu kwanza,ikiwaita na kutoka makaburini,. Hivyo kuanzia huo wakati nao pia watawatokea watakatifu wengi watakaokuwa hai duniani. Na hawatawatokea ilimradi kuwafurahisha tu, hapana, bali nao pia watakuwa na hudumu ya muda mfupi sana, watawashuhudia kwamba, ni wameisikia sauti yake ikiwaita watoke makaburini, na ndio maana wapo pale, hivyo ule wakati kwa kwenda KUMLAKI BWANA MAWINGUNI UMEFIKA,

Jambo hilo litawapa nguvu wale watakaokuwa hai,na kwa matukio kama hayo itawaongezea imani kubwa sana ya kuondoka, hii kitakuwa ni kipindi kifupi sana, kumbuka pia watu wengine wasiokuwa watakatifu jambo hili litakuwa haliwahusu, hawatamwona mtu yeyote, hata wale watakatifu waliofufuka kwanza hawakumtokea tu kila mtu Israeli hapana bali watakatifu waliokuwa mji mtakatifu Yerusalemu…Na kwasasa hivi Mji Mtakatifu wa Mungu (Yerusalemu ya mbinguni) ni Kanisa lake takatifu, Hivyo watakao yaona hayo wafu wakipanda makaburini ni watakatifu tu, siku hiyo itakuwa ni furaha kubwa isiyokuwa ya kawaida, na ndio maana biblia inasema siku hiyo haitawajilia kama mwivi kwa kuwa hampo gizani,

Ndipo hapo utashangaa wakati huo, ndugu yako katika Bwana, aliyekufa pengine miaka 20 iliyopita anakutokea na kuzungumza na wewe na kukwambia ule wakati wa kwenda kwa Baba umewadia, wakati huo hata ukijaribu kuwashirikisha watu wengine wasiowatakatifu watakuona kama umerukwa na akili, au umeona mizimu, kwa kipindi hicho kifupi ufahamu wako utakuwa umebadilika na mawazo yako yatakuwa mbinguni,..Pengine utamwona dada aliyekuwa amelala muda mrefu nyuma ambaye alijisitiri kwa usafi wote wa roho na mwili mliokuwa mnafanya wote ushirika kanisani anakujia wakati upo katika shughuli zako za kujipatia rizki, akiwa pamoja na kundi la watakatifu wengine,

Sio hatu tu pia na watakatifu wengine wengi hata wa agano la kale watawatokea wengi…Na kwa muda mfupi sana kuanzia hapo, kufumba na kufumbua miili ya wote itageuka na kuwa ya utukufu, ataungana na wenzako kisha kwa pamoja mtaisikia Parapanda ya Mungu ikiwaita hapo juu, ..HALELUYA hapo tutamwona Bwana.…

Wakati huo dunia yote haitaelewa chochote mambo yanayoendelea, ndio ghafla wale watu ambao ulikuwa unaishi nao watakuona haupo, kumbuka watakaonyakuliwa watakuwa ni wachache sana duniani, hivyo halitakuwa ni jambo la kuishutusha sana dunia, wao wataendelea na shughuli zao kama kawaida wakingojea kufunuliwa kwa mpinga-kristo.

Lakini kama leo hii wewe ni mlevi, ni mwasherati, ni mzinzi, ni mtukanaji, mvaaji wa vimini, mtazamaji wa pornography na bado unajiita mkristo, unategemea mtakatifu gani akutokee siku ile?. Ni dhahiri kuwa haitakuhusu hivyo itakujia kama mwivi tu, kama leo hii tu unajitenga na watakatifu kutokana na uvaaji wako, na ulevi wako, na tabia zako,na anasa zako, kama umeshindwa kuungana nao hapa, utawezaje kuungana nao kule,?, utawezaje siku ile kutokewa na mtume Paulo, mtume Petro, Musa, Stephano, utawezaje siku ile kumwona mchungaji wako aliyekuwa akikufundisha na kukuonya uache dhambi na ukawa unakataa?. hatua ndogo tu kama hiyo ya kuwaona watakatifu ni shida, unategemea vipi kumwona BWANA mwenyewe MFALME WA WAFALME atakapokuja pale mawinguni..????.

Biblia inasema tusilale usingizini kama wengine walalavyo,bali sisi tulio wa mchana, tuwe na kiasi, hali tukijivika kifuani imani na upendo, na chapeo yetu iwe tumaini la wokovu”(1Wathesalonike 5:7-8). Muda umeenda kuliko tunavyodhani Bwana yupo mlangoni kurudi je! Umempa Bwana maisha yako sasa, je! Umebatizwa katika ubatizo utakaokupelekea upate ondolea la dhambi zako na kupokea Roho Mtakatifu?, Kama hujafanya hivyo ni vema ufanye hivyo sasa kabla mlango wa neema haujafungwa, hatimaye siku ile nawe uwe mmojawapo wa watakaokwenda na watakatifu wa Mungu kumlaki Bwana mawinguni.

Biblia inasema Waebrania 12: 14 “Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, NA HUO UTAKATIFU, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao”;

Ubarikiwe sana.

Tafadhali “share” kwa wengine ujumbe huu.

Friday, July 27, 2018

LENGO LA SHETANI KWA WATOTO WA KIZAZI HIKI.


Hekima ya dunia hii inasema “Samaki mkunje, angali mbichi”, Hii ikiwa na maana kuwa Samaki akisha kauka hawezi kukunjika tena, ukijaribu kufanya hivyo atavunjika, Na ndivyo ilivyo kwa watoto wetu, Hekima ya Neno la Mungu pia inatumbia, Mithali 22: 6 “Mlee mtoto katika njia impasayo, Naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee”.

Neno hili kinyume chake ni kweli mtoto asipolelewa katika njia impasayo, hataiacha hiyo njia mbovu hata atakapokuwa mzee. Hivyo Mungu yupo hapo sana katika kuhakikisha hatma yake inakuwa salama kadhalika na shetani naye yupo hapo kutaka kuharibu hatma ya maisha ya mtoto yule angali ni mchanga. Hivyo nguvu ya ziada inahitajika katika kutengeneza maisha ya mtu katika utoto wake kuliko katika utu uzima.

Tunafahamu kabisa dunia ya sasa sio kama ile ya zamani, mambo maovu yaliyopo leo ni mengi kuliko yale ya zamani, ngoja nikupe kisa changu mwenyewe ambacho ni mfano hai kabisa ya mambo yanayoendelea katika ulimwengu wa watoto: 
 
Nakumbuka tulipokuwa watoto (mimi na ndugu yangu), ilikuwa ni kati ya umri wa miaka 4-7 hivi, kuna vitu vilikuwa tunaviona vinaendelea katika mazingira yaliyokuwa yanatuzunguka, nyumbani kulikuwa na tv, na kwa kipindi hicho cha zamani kidogo, nyimbo za Michael Jackson, na nyimbo za kikongo ndizo zilikuwa zinavuma sana, hivyo ilikuwa ni ngumu kwenda katika nyumba yoyote yenye TV na kukosa mkanda wa (VHS) wa hizo nyimbo, Cha ajabu tulikuwa tunaona watu wazima wanaangalia na kufurahia lakini sisi tulikuwa tunaogopa kwamfano kama ulishawahi kutazama video za Michael Jackson nyingi zilikuwa na maudhui ya kutisha tisha tu, mara utaona anajigeuza kuwa mchanga, mara yupo makaburini,n.k. Sasa yale mambo watu wazima walikuwa wanaona ni kawaida tu, lakini sisi ilikuwa inatuathiri ndani kwa ndani na hauwezi ukasema kwasababu wewe ni mtoto na hujui maana ya hayo mambo, mpaka ilifikia kipindi vile vitu tulivyokuwa tunaviona kwenye TV vikaanza kujidhihirisha nje, tukaanza kuviona wazi wazi.

Tulikuwa tunaviona sana sana wakati wa usiku tunashutuka, na kuona vijiwatu vidogo vidogo vinafungua milango ya jiko, wanaingia na kuanza kucheza mbele yetu kama wale wale tuliokuwa tunawaona wanaocheza kwenye TV, ni wale wale tu isipokuwa hapa tunawaona dhahiri. Na mfano mtu mzima akijaribu kuingia ndani kwa ghafla vilikuwa vinakimbia na kujificha. Vilikuwa vinajidhihirisha kwetu tu, (kumbuka hizo sio ndoto au imagination, ni vitu dhahiri kabisa tulikuwa tunaviona, kwasababu wote wawili tulikuwa tunaviona, na mpaka sasahivi na utu uzima wetu tunavikumbuka) ..sasa ilifikia kipindi ilikuwa vikitokea tunaona kawaida tu, hatuoni tena ni ajabu, wala hatuviogopi, badala yake tunacheka, kumbuka wakati mambo haya yanaendelea hakuna mtu mwingine alikuwa anajua, kadhalika na vitu vingine vingi vya ajabu ajabu tulikuwa tunaviona ambavyo vilitokana na mambo tuliokuwa tunayatazama kwenye TV. Lakini mambo haya yalianza kupotea pale mzazi wetu mmoja alimpompa Bwana maisha yake.

Kadhalika mdogo wetu mmoja alituambia jambo kama hilo hilo liliwahi kumtokea alipokuwa mdogo, alikuwa anaona mtu anamtokea mwenye ngozi kama ya nyoka na kuzungumza naye usiku. Wakati huo wazazi hawaelewi chochote ni yeye tu na hilo pepo basi.

Sasa mambo hayo yalikuwa ni zamani wakati utandawazi haujawa mkubwa je! leo hii itakuwaje? Kwa watoto wa leo, siku hizi sio TV tu peke yake, kuna simu tena zenye internet, Kuna magemu, ya kila aina kwenye simu za wazazi, na kibaya zaidi magemu yenyewe ukiangalia karibu yote yanadhima za kipepo ndani yake, kwamfano, magemu kama , House of the dead, mortal combat, spiderman, Zuma, Diablo.Titan n.k.Pia Kuna magemu mengine yanakuwepo sana kwenye simu unakuta mtu analiendesha au anakimbizwa na limnyama fulani la ajabu kutoka pangoni , na yeye anajaribu kulikimbia,(Nadhani utakuwa unalifahamu) sasa vitu kama hivi watu waliovitengeneza hawajavibuni tu ilimradi hapana bali wamevitoa kama vilivyo katika ulimwengu wa roho wa kishetani (ni vikundi maalumu kabisa vya kishetani vinavyofanya hizi kazi), wanachofanya ni kuchukua taswira yenye uwezo wa kama hayo mapepo na kuyatengenezea magemu yanayofanana nao pamoja na kazi zao.

Kama vile tu wanavyotengeneza magemu ya mipira, utakuta aina ya mchezaji na uwezo wake ndani ya gemu ndio yuko hivyo hivyo katika ulimwengu wa kawaida duniani, kadhalika magemu yote yanayohusiana na viumbe na vitu vya ajabu ajabu vipo kweli katika ulimwengu wa roho,na kazi zao ndio hizo hizo, kukimbiza watu, kuua, kupaa, kutesa watu, kushusha watu kuzimu, kunywa damu za watu, n.k.

Sasa unakuta mtoto akitazama au akicheza magemu ya namna hiyo kidogo kidogo anaanza kuwa na ushirika na ile roho, mwisho wa siku kile kitu alichokuwa anakiona kwenye tv au gemu kinakuja kumtokea wazi, aidha kwa njia ya ndoto au dhahiri kabisa..Na kibaya zaidi mtoto hawezi kukwambia na wakati mwingine kinamwonya asikwambie, Kumbuka lile ni pepo kidogo kidogo linaanza kumpa maagizo, na uwezo wa kutenda kama lile pepo lilivyokuwa linafanya ndani ya gemu, ndio hapo unakuta mtoto anaanza kubadilika tabia anaanza kuwa mtundu, saa nyingine mtoto anafanya mambo yasiyoeleweka, anazungumza maneno yasiyoeleweka mara nyingine anakuwa na hisia ambazo unaona kabisa sio kawaida kwa mtoto kuwa nazo, unakutaa mtoto mdogo lakini anaonyesha tabia za kiutu uzima, tabia za kizinzi, mwingine anajithiri sehemu zake za siri,n.k. hii yote ni kutokana na hizo roho alizozipata kutoka katika ma- TV na Magemu,

Zipo shuhuda nyingi za namna hiyo, wazazi wanashuhudia baada ya watoto wao kwenda kufanyiwa mahojiano wanakiri kuwa vile vitu walivyokuwa wanaviona kwenye tv (cartoons,) na magemu vilikuwa vikiwatokea dhahiri, na kuwaendesha.
 
Hivyo wewe kama mzazi au dada, au kaka, una watoto wako au wadogo zako, unadhani unawapenda unapowawekea magemu kwenye simu, au unapowawekea programu za ajabu, unapowaruhusu watazame TV na miziki ya kidunia, unapowaruhusu watazame tamthilia na filamu zisizokuwa na misingi yoyote ya kikristo au kuelimisha, unadhani hapo umempenda mtoto? La! kinyume chake unamuharibu, biblia inasema mlee mtoto katika njia impasayo naye hataiacha hata atakapokuwa mtu mzima, mtoto anapolilia mambo hayo unatakiwa utumie nguvu pasipo hurumu tena akemewe kabisa aogope kuulizia vitu kama hivyo siku nyingine.

Kuna wazazi au walezi wengine wanaogopa na wengine hawataki kabisa kuwaadhibu watoto wao, kwa kisingizio eti tunaishi kazazi kipya kile ni cha zamani kimeshapita, watoto wa siku hizi hawapigwi wanaelekezwa tu…Huo ni uongo wa shetani, ndio inafikia hatua mpaka mtoto anamtukana mtu mzima na mzazi anamwangalia tu, anaiba na mzazi anamwangalia tu, akidhani kuwa akimwadhibu mwanaye atajisikia vibaya au atapata matatizo fulani ya kiafya,..Au ataona kama haonyeshi upendo kwa familia yake..Hivyo anaepuka kabisa kumudhi mwanae.. Lakini biblia inasema..

Mithali 22: 15 “Ujinga umefungwa ndani ya moyo wa mtoto; Lakini fimbo ya adhabu itaufukuzia mbali”.

Na pia inasema …

Mithali 23: 13 “Usimnyime mtoto wako mapigo; MAANA UKIMPIGA KWA FIMBO HATAKUFA.
14 Utampiga kwa fimbo, NA KUMWOKOA NAFSI YAKE NA KUZIMU”. ..Unaona hapo siku ile wazazi wengi watawajibika kujibu ni kwanini watoto wao wapo kuzimu, angali wasingepaswa kuwepo huko. Tunasema watoto wa siku hizi wamebadilika, lakini ki-ukweli wazazi wa siku hizi ndio waliobadiliaka, watoto ni wale wale.


Unaweza ukadhani ukimwadhibu mwanao, atakuja kukuchukia baadaye, lakini akizoeshwa hivyo atakapokuja kuwa mtu mzima, na yeye kupata akili kama wewe atakushukuru sana kwa kumlea vizuri, kwasababu ndivyo hivyo Neno la Mungu linavyosema:

Waebrania 12: 11 “Kila adhabu wakati wake haionekani kuwa kitu cha furaha, bali cha huzuni; lakini baadaye huwaletea wao waliozoezwa nayo matunda ya haki yenye amani”
Na matunda ya kumlea vizuri mwanao utakuja kuyaona mwishoni…Biblia inasema hivyo pia..Mithali 29: 17 “Mrudi mwanao naye atakustarehesha; Naam, atakufurahisha nafsi yako”

Wewe kama mzazi/mlezi anza kumjenga mwanao/mdogo wako leo katika misingi ya Kikristo, badala ya kumwacha asikilize miziki ya kidunia katika TV, anza kumfundisha kuimba tenzi za rohoni, mapambio na nyimbo za kumsifu Mungu, badala ya kumwacha aangalie Tamthilia zisizokuwa na maana anza kumfundisha hadithi za biblia (kama safari ya wana wa Israeli, hadithi za Eliya, wafalme, Yona, Danieli n.k.) kuliko kubaki kujazwa hadithi mbovu za watu wasioamini katika TV, Anza kumfundisha jinsi ya kutumia jina la YESU, mzoeshe kutumia jina la YESU kila mahali alipo, anza kumfundisha kusali, mfundishe umuhimu na madhara ya kuwa na tabia zisizofaa, mpeleke katika madarasa ya biblia ya watoto jumapili kanisani, kama watu wa dini nyingine wanafanya hivyo wewe kwanini usifanye.??..Kadhalika jenga desturi ya kuwaombea na kuwawekea mikono watoto wako mara kwa mara wewe mwenyewe na kuwatamkia maneno ya baraka.. Kwa kufanya hivyo utakuwa umeiokoa roho ya mwanao katika kizazi hiki kibaya kilichopotoka na dhidi ya roho chafu zinazozunguka kuwanasa watoto.

Ubarikiwe sana.

Tafadhali “share” kwa wazazi wengine ujumbe huu ili na wanao pia wapone.

Wednesday, July 25, 2018

UKOMA NA UJANE ULIO NDANI YAKO, UMEUPATIA TIBA?

Luka 4: 22 “Wakamshuhudia wote[YESU KRISTO], wakiyastaajabia maneno ya neema yaliyotoka kinywani mwake, wakasema, Huyu siye mwana wa Yusufu?
23 Akawaambia, Hapana shaka mtaniambia mithali hii, Tabibu, jiponye nafsi yako; mambo yote tuliyosikia kwamba yametendeka Kapernaumu, yatende na hapa pia katika nchi yako mwenyewe.
24 Akasema, Amin, nawaambia ya kwamba, Hakuna nabii mwenye kukubaliwa katika nchi yake mwenyewe.
25 Lakini, kwa hakika nawaambia, Palikuwa na wajane wengi katika nchi ya Israeli zamani za Eliya, wakati mbingu zilipofungwa miaka mitatu na miezi sita, njaa kuu ikaingia nchi nzima;
26 wala Eliya hakutumwa kwa mmojawapo, ila kwa mjane mmoja wa Sarepta katika nchi ya Sidoni.
27 Tena, palikuwa na wenye ukoma wengi katika Israeli zamani za nabii Elisha, wala hapana aliyetakaswa ila Naamani, mtu wa Shamu”.

Neno la Mungu ni mwongozo wa kutufundisha sisi kutokurudia makosa yaliyofanyika nyuma na waliotutangulia, Katika habari hii Bwana Yesu anatuonyesha madhara ya kulinganisha Neno la Mungu, na mazingira ya nyuma ya mtu, Kama tunavyosoma tunaona wale wayahudi baada ya kusikia na kuona maneno mazuri ya wokovu yaliyokuwa yanatoka kinywani mwa Bwana, badala ya kuyasadiki wao moja kwa moja wakaanza kutazama mambo mengine yasiyokuwa na msingi na kurejea kuchunguza ameitolea wapi neema hiyo kwa kuilinganisha na chimbuko lake..

Na ndio maana utaona wanasema..huyu sio yule seremala mwana wa Yusufu, dada zake na kaka zake sio hawa tunao hapa mjini kwetu?, na mama yake sio yule Mariam tunayemfahamu?, n.k. Sasa kama ndivyo katolea wapi ujuzi huu wote na maarifa haya yote,?. Wakahitimisha; hawezi akawa na jipya lolote la kutueleza sisi, tumeshamfahamu tangu zamani huyu ni wa hapa hapa…Kwahiyo kwa kufanya vile ikawapelekea ile neema iliyokusudiwa juu yao kuwapita. Na ule wokovu ambao wangepaswa wapate wao kwanza kutoka kwa Bwana kuupoteza.

Kadhalika na ndivyo ilivyokuwa kwa Nabii Eliya wayahudi hawakuupokea ujumbe aliokuwa anawapelekea siku zote, na badala yake wakayatazama maisha yake ya nyuma, pengine walisema huyu mzee kutoka Gileadi kwanza haijui vizuri Israeli, Ndugu zake si ndo hawa wakulima na wafugaji tunaowaona huku, hawana elimu,?..Hivyo wakahitimisha nao pia kuwa Eliya hawezi akawa na jambo la kuwaongezea kitu, kwasababu historia yake ipo wazi. Lakini wakati Bwana anakaribia kuleta njaa kuu juu ya nchi, Eliya hakutumwa kwa mojawapo ya wajane waliokuwepo Israeli kwa wakati ule badala yake alitumwa kwa mjane mmoja katika nchi ya mbali, asiyemjua hata vizuri Mungu wa Israeli lakini kwa kusikia tu kwamba mtu Yule katumwa na Mungu, alimuheshimu sana. Na kupelekea kupata neema ya chakula tele kipindi chote cha njaa.
 
 
Kadhalika hata katika kipindi cha Nabii Elisha jambo ni lile lile, walikuwepo wakoma wengi katika Israeli lakini wenyewe walimwona Elisha ni kama mtu wa kwao tu, hawezi kuwa mtumishi wa kulibeba Neno la Mungu, hawezi kuundoa ukoma wetu huu, tunamjua ni mfugaji, na baba yake na mama yake ndio wale wale wafugaji wasioijua sheria ya Mungu sana, kaka zake na dada zake kila siku tunawaona huku mtaani kwetu ni watu wa kawaida tu, hivyo tuende kufanya nini kwa mtu kama Yule?? Wakakwazika na maisha ya Elisha. Hivyo kwa dharau zao ziliwafanya wabakie na ukoma wao daima..Lakini mtu mmoja kutoka nchi ya mbali (Iitwayo Shamu) aliposikia habari za Elisha tu kutoka wa kijakazi wake, alimwamini na kuamua kufunga safari kwenda kuomba kuponywa, na ndivyo ilivyokuwa alipokea uponyaji wake wote, na wale wengine wenye kiburi walibakia na ukoma wao siku zote za maisha yao.Swali ni je! Kwanini hakukuwa na mkoma yoyote wa Israeli aliyeponywa?. Au mjane yoyote Israeli aliyepewa chakula na Eliya Na badala yake watu wasiomjua Mungu wa Israeli kutoka mbali kuja kuponywa na kupewa chakula?

Jambo hilo hilo linajirudia leo hii, kwanini wanaojiita wakristo wengi hawataenda mbinguni? Sababu ni ile ile, wanajua historia yote ya Bwana Yesu na biblia yote, wanajua mwanzo wote wa ukristo na utakavyokuwa mwisho wake, lakini bado ni wakoma wa rohoni, bado ni wajane wa rohoni, wasiotaka msaada,.. Wanapoletewa habari ya wokovu, na kuhubiriwa watubu dhambi, na waponywe nafsi zao, wanajiona hawawezi kuongezewa kitu kingine cha ziada, sababu tu wao wamezaliwa katika ukristo, na wamepitia mafundisho yote ya biblia na vyuo vyote vya biblia, lakini ndani yao wanapinga maneno ya neema ya Kristo yahusuyo wokovu, utakuta ni mkristo lakini ni mlevi, ni mkristo lakini ni mzinzi, ni mkristo lakini ni msengenyaji, ni mkristo lakini ni mtazamaji wa pornography na mfanyaji wa mustarbation, ni msagaji, ni mvaaji wa vimini, ni mtukanaji, mtu asiyesamehe n.k. Na akiambiwa habari za kutubu dhambi na kujazwa Roho atasema naifahamu biblia, nilishaenda katika mafundisho hayo zamani, huo ni ulokole tu, atakwambia hayo yote chimbuko lake ni hili au hili n.k. hivyo anakuona huna chochote cha kumwongezea yeye…

Biblia inasema siku zinakuja ambazo Bwana ataleta njaa juu ya nchi Soma

Amosi 8: 11” Angalia, siku zinakuja, asema Bwana MUNGU, ambazo nitaleta njaa katika nchi; si njaa ya kukosa chakula, wala kiu ya kukosa maji, bali ya kukosa kuyasikia maneno ya Bwana.
12 Nao watatanga-tanga toka bahari hata bahari; na toka upande wa kaskazi hata upande wa mashariki; watapiga mbio, wakienda huko na huko, kulitafuta neno la Bwana, wasilione.
13 Siku hiyo wanawali wazuri na wavulana watazimia kwa kiu”.

Hizo siku ndio hizi ndugu, kama zilivyokuwa katika siku za Nabii Eliya..Leo hii duniani kote kuna njaa ya Neno la Mungu, ndani ya Ukristo na nje ya ukristo. Wajane na wakoma walikuwepo ndani ya Israeli na nje ya Israeli, Kadhalika na katika ukristo wenye njaa wapo ndani ya ukristo na nje…Lakini kama vile wale wa ndani waliipinga neema iliyoletwa kwao na Nabii Eliya na Nabii Elisha, na kupelekea watu wengine wa mbali kupewa neema, Vivyo hivyo na katika ukristo wanaoipinga neema hii sasa ihusuyo toba na ondoleo la dhambi, wakati utafika itaondolewa kwao na kuhamishiwa kwa watu wengine wasiomjua Mungu wa kweli na Bwana wetu Yesu Kristo na wao wataponywa roho zao, wakati wanaojiita wakristo watakuwa wanakufa kwa njaa.

Leo hii unajiita mkristo na bado ni mkoma wa rohoni, unajiita mkristo na bado ni mjane wa rohoni mwenye njaa, ni kwasababu gani? Ni kwasababu matendo yako hayaendani na ukristo halisi huku unadai unamfahamu Kristo?..Unakuwa huna tofauti na wale watu waliokuwa wanajua chimbuko la Bwana Yesu, mpaka kazi ya baba yake, na ndugu zake walivyo lakini wasione uzima uliokuwa ndani yake...ndivyo ilivyo kwa wewe unayejiita mkristo, unazini, unakunywa pombe, unatazama pornography, unasengenya, unaenda disco,n.k. Hujui kuwa chakula kile ambacho kingepaswa kije kwako kwanza kinapelekwa kwa mtu mwingine ambaye hata hajawahi kusikia habari za ukristo.

Kila siku unahubiriwa utubu dhambi ugeuke, unakataa, lakini wapo wasiomjua Mungu leo hii wanasikia tu mara moja na kugeuka wakati huo huo, waislamu, wahindu, wabudha, wasio na dini, ndio Bwana anaowaangalia kuwapa chakula chake huu wakati wa njaa..Wewe utaendelea kutangatanga huku na kule, hujui kama Mungu alishakuacha siku nyingi na mwisho wa siku utakufa kwa njaa na kuishia jehanum ya milele kwenye mateso yasiyoelezeka. ..

huu sio wakati wa kujisifia dini au kujisifia kuzaliwa katika ukristo, au ujuzi wa maandiko, au chuo cha biblia ulichopitia ,au vinginevyo, Huu ni wakati wa kunyenyekea na kutafuta wokovu na utakatifu kwa bidii kwasababu biblia inasema .

Waebrania 12: 14 “Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, NA HUO UTAKATIFU, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao;”

Ubarikiwe.

Tafadhali “share” kwa wengine ujumbe huu na wao wapone.

Monday, July 23, 2018

MKUMBUKE MKE WA LUTU.

Luka 17:28 “Na kadhalika, kama ilivyokuwa katika siku za Lutu, walikuwa wakila na kunywa, walikuwa wakinunua na kuuza, wakipanda na kujenga;
29 lakini siku ile Lutu aliyotoka Sodoma kulinyesha moto na kibiriti kutoka mbinguni vikawaangamiza wote.
30 Hivyo ndivyo itakavyokuwa siku ile atakayofunuliwa Mwana wa Adamu.
31 Katika siku ile, aliye juu ya dari, na vyombo vyake vimo ndani ya nyumba, asishuke ili kuvitwaa; na kadhalika, aliye shambani asirejee nyuma.
32 MKUMBUKENI MKEWE LUTU.
33 Mtu ye yote atakaye kuiponya nafsi yake, ataiangamiza; na ye yote atakayeiangamiza ataiponya”.
Ni wazi kuwa kizazi tunachoishi kinafananishwa na kile cha Sodoma na Gomora, kadhalika kinafananishwa pia na kizazi cha Nuhu, Na ni kwanini ni hichi na sio kizazi kingine?. Ni kwasababu yale mambo yaliyokuwa yanafanyika kule wakati ule ndio yanayofanyika sasa na zaidi hata ya pale, Kumbuka Jambo kuu lililopelekea Miji ya Sodoma na Ghomora kuteketezwa ni tabia ya ulawiti na ushoga, tafsiri ya neno lenyewe Sodoma ni Ulawiti, Hivyo wakati ule hiyo roho ya kuingiliana kwa watu kinyume na maumbile ilikuwa imekithiri jambo ambalo lilianza tena kuonekana likijirudia kwa kasi sana mwanzoni mwa karne ya 20 na kuendelea mpaka sasa.

Roho hii imekithiri katika karne hizi 2 kuliko vizazi vingine vyote vya nyuma vilivyotangulia. Mpaka sasa hivi vitendo hivyo vimehalalishwa kisheria, kwamba vimepewa haki ya kuitwa ndoa kama ndoa nyingine halali, Kama Bwana Yesu alivyotabiri siku hizo watu watakuwa wakioa na kuolewa. Sasa Kuoa na kuolewa kwenyewe kunakozungumziwa hapo sio ndoa za mke na mume hapana, bali ni ndoa za mume na mume, na mke na mke. Mambo ambayo tunayaona sasahivi yakihalalishwa hata katika nyumba zinazojiita ni za ibada.

Sasa madhara ya haya mambo ni nini?

Madhara yake ni kupelekea jamii nzima kuathiriwa na adhabu hata watu wanaoonekana kutokuwa na hatia wanashiriki adhabu yao. Kwamfano tukitazama katika kipindi cha Nuhu, makosa ya wanadamu yaliwasababisha hata wanyama wasiokuwa na hatia kuangamizwa, ilisabababisha nchi na mimea isiyokuwa na hatia kuharibiwa, ilisababisha watoto wachanga wasiotenda hayo makosa kuteketezwa pia. Kadhalika na katika kipindi cha Lutu vivyo hivyo Na ndivyo itakavyotokea hata katika kizazi hiki cha siku za mwisho, wataathirika hata na watu wengine na viumbe vingine visivyokuwa na makosa (visivyostahili hayo madhara).

Lakini kabla Bwana hajaleta maangamizi huwa anatuma kwanza wajumbe wa kuwaonya watu wajitenge na kizazi hicho, Na ndio tunakuja kuona katika wakati wa Nuhu waliotii sauti ya Mungu ni watu wachache (yaani watu 8 tu! kati ya mamilioni), Kadhalika katika wakati wa Lutu waliotii ni watu 4 tu lakini Yule wanne (ambaye leo tutajifunza habari zake) alilikuja kuangamia, na kupelekea watu 3 tu kupona kati ya maelfu na mamilioni waliokuwa mijini.

Siku zote tunajua ni jambo la kawaida kwa mwanadamu kufuata au kuamini kitu kinachopendwa na watu wengi, hata kama ni cha kipuuzi kiasi gani, kikiwa kimekubaliwa na wengi basi ni rahisi kupata wafuasi wengi pasipo hata kupata ukinzani.kwamfano jamii nyingi za zamani watu walikuwa na hofu ya kumiliki televisheni katika manyumba yao wakiogopa kuwa zinaweza kuharibu maadili ya familia au jamii zao, lakini kwa jinsi zinavyozidi kuongezeka na kuaminiwa na wengi, zinakuja kuwa ni kitu cha kawaida kadri muda ulivyozidi kuendelea hata wale wachache waliokuwa wanazitilia mashaka wanaanza kuona kama ulikuwa ni ushamba kuogopa kumiliki televisheni, 
Kadhalika pia zamani mtoto mdogo kumiliki simu ya mkononi wengi iliwashangaza sana, kuona kama mtoto ataharibikiwa, lakini kutokana na simu kuwa nyingi na wazazi wanaowawaruhusu wanao kuzitumi kuongezeka, inapelekea hata wale wazazi waliokuwa wanazipinga zisimilikiwe na watoto wao, wajione kama walikuwa washamba na wanahofu ya bure tu!, hii inakuja kutokana na presha ya watu wengine, hivyo husababisha yale madhara yalikuwa yanadhaniwa mwanzo kumezwa na mabadiliko ya kijamii.

Mfano mwingine ni kuwasili kwa fasheni, zamani ilikuwa mwanamke akionekana amevaa suruali alijulikana kama ni kahaba Fulani hivi, lakini kwa siku zilivyozidi kwenda na wavaaji kuongezeka, suruali zikaanza kuonekana kuwa ni kitu cha kawada sana kwa wanawake, hata wale wachache waliokuwa wanazipiga vita wanaanza kujiona kuwa walikuwa ni washamba..Na ndivyo ilivyo hata kwa ushoga, zamani ilikuwa hata kutamkwa hilo neon tu, ilikuwa ni aibu lakini leo hi kutokana na kwamba mambo haya yanazidi kuongezeka hata Eneo linalojiita la Kanisa mada hizo zinazungumziwa na kupewa kipaumbele na kuhalalishwa, limekuwa ni jambo la kawaida hata wale waliokuwa wanapinga mwanzoni, wanaanza kujiona kama walikuwa watu wa itikadi kali…Kwahiyo roho hii ya kubadilika kutokana na mikumbo ya watu wengi imeendelea mpaka sasa katika kanisa la Mungu..

Sasa mambo haya ndivyo yalivyokuwa katika zama za Lutu, Na Mungu kwa kumuhurumia Lutu na familia yake akamwambia atoke, lakini kabla ya wao kutoka walipewa nafasi ya kwenda kuwahubiria ndugu zao pia , lakini biblia inasema walionekana kama wanacheza mbele zao (mwanzo 19:24), Hivyo ikawalazimu watoke wao tu.

Tukizidi kusoma habari ile tunaona, Mkewe Lutu alikuja kugeuka nyuma na kuwa nguzo ya chumvi.

Kwanini Mke wa Lutu ageuke nyuma na anamwakilisha nani Sasa?

Mke wa Lutu anamwakilisha MKRISTO ambaye alishaokolewa huko nyuma, kumbuku Mke wa Lutu mwanzoni aliitika kabisa wito wa kutoka Sodoma, kwa kuyatambua maovu yote yaliyokuwa yanatendeka kule, kwamba wale watu walikuwa wanastahili hukumu , kwa kujua hilo aliamua kabisa kuyaacha mambo ya Sodoma na kuondoka, Lakini baadaye katikati ya safari alianza kujiona anavutiwa na mambo ya nyuma kuliko ya mbele, akianglia mbele haoni majumba, mali, wala raha, akiangalia nyuma anaona fahari, mali, starehe, karamu, mashamba, n.k. Hivyo akaanza kushawishika kidogokidogo kuyafikiria na kuyatamani aliyoyoaacha nyuma Hivyo matokeo yake akageuka, akaangamia na kuwa jiwe la chumvi.

Mke wa Lutu alidanganyika kama vile kanisa linavyodanganyika leo, pengine aliambiwa maneno haya na wale watu aliowahubiria huko nyuma;…, aah! Ni nyie tu wanne Mungu aliowaona ndio watakatifu kuliko watu wote hapa Sodoma!, Vipi kuhusu watoto,? Unataka kusema watoto wasio na hatia Mungu atawaangamiza pia?, Na vipi kuhusu viongozi wetu wa kidini tulio nao huku, wao nao wataangamizwa, nyie ni bora kuliko wao? Na majengo yetu, na masinagogi yetu Mungu ataanzia wapi kuyaangamiza?..Kwa kosa gani kubwa hivyo mji wote uteketezwe?..Nyie ni lazima mtakuwa mmesikia roho zidanganyazo..ambazo haziwatakii mema, zinawataka muache mali zetu mkimbilie milimani na kufa huko!...Vipi kuhusu mifugo kwani nayo imemkosea nini Mungu, hata iangamizwe? Mungu ni wa haki bwana, hawezi kufanya hivyo vitu….wapo wengi waliojaribu kama nyie wakapotea, embu tulieni hapa, muwe kama sisi acheni hizo itikadi zenu kali rudini kwenu, msije mkawa vichaa.

Ndivyo mke wa Lutu alivyodanganyika wakati akiwa katikati ya safari yake kwa kuyatafakari hayo maneno, akagundua kweli inawezekana ni upuuzi anaoufanya, kwamba hakuna kitu kama hicho, Mungu hawezi kuleta madhara kama yale kwa idadi kubwa ya watu kama ile,ni kweli vipi kuhusu mali zetu, vipi kuhusu mifugo yetu, vipi kuhusu ndugu zetu na watoto, vipi kuhusu viongozi wa kidini n.k…Kwa ushawishi mwingi kama huo Mke wa Lutu akageuka nyuma moja kwa moja na kuangamia milele.Na ndio maana Bwana alisema “Mkumbukeni mkewe Lutu”


Ulikuwa mkristo mzuri zamani ulipoamini, macho yako yalikuwa yapo mbinguni, hukujali ulimwengu unakuchukuliaje, ulijua kabisa unaishi katika siku za mwisho na siku yoyote ghadhabu ya Mungu itamwagwa juu ya nchi, ulikuwa tayari kuacha sigara, pombe, uasherati, anasa, disco, ulawiti, usagaji, pornography, mustarbation, mizaha, matusi, vimini, suruali, mapambo yote ya kikahaba n.k. na zaidi ya yote ulikuwa umeshajumuika na wenzako katika safari ya kuukimbia ulimwengu.. Lakini ulifika wakati ukaanza kuona kama safari yako ni ngumu na ni wachache tu mpo, ukaanza kukumbuka mafundisho ya ya mashetani uliyohubiriwa huko nyuma..yaliyokuwa wanakuambia: Yesu haji leo wala kesho, ukakumbuka pia mtu mmoja alishawahi kukwambia dunia haiwezi kuangamizwa Mungu hawezi kuangamiza watu wasiokuwa na hatia, hawezi kuangamiza watoto wadogo, hawezi kuteketeza viongozi wetu wa kidini, kwani ni nyie tu kikundi kichache kinachojiona kitakatifu ndio mtakao okoka,? Mungu haoni wengine? Mungu ni Mungu wa upendo, Na zaidi ya yote unaacha uzuri wako, unaacha kujipa raha kama kijana unaenda kuwa mshamba,..utakumbuka kuna mwingine alikwambia kuna watu waliopita njia kama yako na mwisho wake ukawa ni matatizo, utakumbuka kuna kiongozi wa kidini alikuambia uzichunguze hizo roho…watakambia hizo ni roho za shetani zinazowafanya mtoke katika hali ya kawaida na kuwa katika hali ya kutazamia mambo yasiyokuwepo ya uongo n.k..

Sasa hapo na wewe unashawishika na kuyatazama mambo ya nyuma, ndugu/dada usigeuka nyuma maana kabla ya kurudi nyuma utakuwa umeshakuwa JIWE LA CHUMVI. Biblia inasema.
2Petro 2: 20 “Kwa maana wale waliokwisha kuyakimbia machafu ya dunia kwa kumjua Bwana na Mwokozi Yesu Kristo, kama wakinaswa tena na kushindwa, hali yao ya mwisho imekuwa mbaya kuliko ile ya kwanza.
21 Maana ingekuwa heri kwao kama wasingaliijua njia ya haki, kuliko kuijua, kisha kuiacha ile amri takatifu waliyopewa.
22 Lakini imetukia kwao sawasawa na ile mithali ya kweli, Mbwa ameyarudia matapiko yake mwenyewe, na nguruwe aliyeoshwa amerudi kugaa-gaa matopeni”.

Ndugu yangu mkumbuke MKE WA LUTU. Kumbuka dunia ya leo hii imejaa maovu ya kila namna, hivyo usitazame wimbi la watu wengi wanafanya nini, usitazame kwasababu vijana wote wanafanya anasa na wewe ufanye, kwasababu wanawake wote wanavaa vimini na wewe uvae kwasababu watu wote wanazini na wewe uzini, Biblia ilishatabiri katika siku za mwisho watakatifu watakuwa wachache, na upendo wa wengi utapoa, kama zilivyokuwa katika siku za Nuhu na siku za Lutu, Hivyo ukiwa wewe ni mkristo na umeacha mambo ya ulimwengu huu, zidi kujitakasa, maana siku si nyingi Mungu atauteketeza huu ulimwengu kabisa na watakaopona ni watakatifu ambao watakuwa ni wachache sana, mimi na wewe tuwe miongoni mwao....

2Petro 3: 3 “Mkijua kwanza neno hili ya kwamba katika siku za mwisho watakuja na dhihaka zao watu wenye kudhihaki, wafuatao tamaa zao wenyewe,
4 na kusema, Iko wapi ahadi ile ya kuja kwake? Kwa maana, tangu hapo babu zetu walipolala, vitu vyote vinakaa hali iyo hiyo, tangu mwanzo wa kuumbwa.
5 Maana hufumba macho yao wasione neno hili ya kuwa zilikuwako mbingu tangu zamani, na nchi pia, imefanyizwa kutoka katika maji, na ndani ya maji, kwa neno la Mungu;
6 kwa hayo dunia ile ya wakati ule iligharikishwa na maji, ikaangamia.
7 Lakini mbingu za sasa na nchi zimewekwa akiba kwa moto, kwa neno lilo hilo, zikilindwa hata siku ya hukumu, na ya kuangamia kwao wanadamu wasiomcha Mungu.
8 Lakini, wapenzi, msilisahau neno hili, kwamba kwa Bwana siku moja ni kama miaka elfu, na miaka elfu ni kama siku moja.
9 Bwana hakawii kuitimiza ahadi yake, kama wengine wanavyokudhani kukawia, bali huvumilia kwenu, maana hapendi mtu ye yote apotee, bali wote wafikilie toba.
10 Lakini siku ya Bwana itakuja kama mwivi; katika siku hiyo mbingu zitatoweka kwa mshindo mkuu, na viumbe vya asili vitaunguzwa, na kufumuliwa, na nchi na kazi zilizomo ndani yake zitateketea.
11 Basi, kwa kuwa vitu hivi vyote vitafumuliwa hivyo, imewapasa ninyi kuwa watu wa tabia gani katika mwenendo mtakatifu na utauwa,
12 mkitazamia hata ije siku ile ya Mungu, na kuihimiza; ambayo katika hiyo mbingu zitafumuliwa zikiungua, na viumbe vya asili vitateketea na kuyeyuka?”

Ubarikiwe.

Tafadhali “share” ujumbe huu kwa wengine na Mungu atakubariki.

Friday, July 20, 2018

USIACHE KUJIFUNZA NENO LA MUNGU

Neno la Mungu limefananishwa na MBEGU (Luka 8:11), na siku zote mbegu ina uhai na inapopandwa ndani ya mtu, ule uhai wake unajidhihirisha ndani ya mtu huyo kulingana na umeaji wa mbegu hiyo. Hivyo kwa jinsi ile mbegu inavyoendelea kukua ndipo tabia ya Yule mtu inavyoendelea kubadilika kidogo kidogo. Kumbuka hapo sio mtu anajibadilisha kwa jitihada zake hapana bali ni ile mbegu iliyopandwa ndani yake ndiyo inayombadilisha kutoka hatua moja hadi nyingine kulingana na ukuaje wake.

Bwana Yesu alitoa mfano huu.

Marko 4: 26 “Akasema, Ufalme wa Mungu, mfano wake ni kama mtu aliyemwaga mbegu juu ya nchi;
27 akawa akilala na kuondoka, usiku na mchana, nayo mbegu ikamea na kukua, ASIVYOJUA YEYE.
28 Maana nchi huzaa yenyewe; KWANZA JANI, tena SUKE, kisha NGANO PEVU, katika suke.
29 Hata MATUNDA yakiiva, mara atapeleka mundu, kwa kuwa mavuno yamefika”.

Huu mfano unalinganishwa na jinsi Neno la Mungu linavyomea ndani ya mtu, kwanza linaanza kama mbegu, pale mtu anapoliruhusu lile Neno liingie ndani yake, hii inakuja kwa kutamani kujifunza kila siku Neno lile,kwa kutamani kumjua Mungu, na kujifunza maandiko, sasa kidogo kidogo, kwasababu ile mbegu imetengenezewa mazingira yanayostahili kumea yenyewe inaanza kukua taratibu taratibu pasipo hata yeye mwenye kuipanda kujijua ndio hapo unakuta mtu Yule anaanza kubadilika tabia zake na mwenendo wake, anaanza kujikuta anachukia mambo ya kidunia ambapo hapo mwanzo alikuwa hawezi, na hii haiji kwa jitihada za mtu hapana yeye mwenyewe tu anajikuta anapoteza hamu ya kufanya hivyo vitu, hapa mtu anajikuta vitu kama kiu ya sigara, pombe, uasherati, mavazi yasiyo na heshima n.k. vinakata vyenyewe, ataona tu ni kama vile kwa akili zake ameacha hayo mambo lakini hajui kuwa ni ile mbegu ambayo amekuwa akiiruhusu imee ndani yake ndiyo iliyotenda kazi ndani yake.

Na kwa jinsi atakavyoendelea kuiwekea mazingira mazuri zaidi ya kukua, kwa kujifunza na kutamani kudumu zaidi katika Neno la Mungu sasa ile mbegu inageuka na kuwa JANI, hapa ni pale mtu ufahamu wake wa kumjua Mungu unaongezeka na kuwa mpana pasipo hata yeye mwenyewe kujijua kumbuka hii mbegu inachohitaji ni kuwekewa mazingira tu ya kutuzwa, kuhusu ukuaji huwa inajikuza yenyewe. Hatua hii inamfanya mtu ufahamu wake wa rohoni kuongezeka, yale mambo ambayo alikuwa hayaelewi kuhusu maandiko anaanza kuyaelewa taratibu taratibu.
 
Hatua inayofuata ni SUKE. Hatua hii mtu anakuwa anatoka katika ile hali ya “unyasi unaotikiswa na upepo”. Waefeso 4: 14 “ili tusiwe tena watoto wachanga, tukitupwa huku na huku, na kuchukuliwa na kila upepo wa elimu, kwa hila ya watu, kwa ujanja, tukizifuata njia za udanganyifu.
15 Lakini tuishike kweli katika upendo na kukua hata tumfikie yeye katika yote, yeye aliye kichwa, Kristo”.

Hapa unakuwa umekomaa kutoka katika jani na kuwa suke gumu, hatua hii shetani hawezi kukuchukua tena na kila wimbi la mafundisho ya uongo kwa sababu Neno la Mungu limeshaweka mizizi migumu ndani yako. Unafika hatua ya kuwa na ujuzi wa kuitofautisha Kweli ya Neno na Uongo, kwasababu yale mafuta ya Roho yanakaa ndani yako. Mpaka hapo mtu anakuwa tayari kwa hatua inayofuata ya kuzaa matunda.



NGANO PEVU: Hii ni hatua ya kudhihirisha matunda, Hapa inatokea lile Neno lilipandwa ndani yako lenyewe linakupa uwezo wa kwenda kulipanda kwa watu wengine..na kuzaa matunda, Hapa ndipo Mungu kwa maarifa aliyoyaweka ndani ya mtu, anampa neema na uwezo wa kwenda kuwafundisha na wengine, na hii nguvu ya kufanya hivyo haiji kwa jitihada za mtu binafsi au kujilazimisha hapana bali mtu anajikuta anatamani mwenyewe kufanya hivyo kutoka ndani kwasababu ile nguvu za kuzaa matunda imeshajitengeneza ndani yake..,Ni kama tu vile mwanamke anapofikia wakati wa kuzaa, ule uchungu unapokuja hawezi kujizuia, vivyo hivyo na mtu akishafikia hatua hii, anajikuta mwenyewe anaanza kumzalia Mungu matunda.
 

Na hatua ya mwisho ni Mavuno: Hapa ndipo kazi ya kila mtu itavunwa na Bwana mwenyewe, na hii itakuja katika mwisho wa dunia.

Hivyo ndugu je! Ni mbegu gani imepandwa ndani yako?, Ni ya Neno la Mungu au ni ya Yule mwovu.?..Na kama ni ya Neno la Mungu, je! Mbegu hiyo imekuwa kwako katika hatua gani, ni jani?, ni suke au ni ngano?. Kama huna uwezo wa kushinda ulevi, uasherati, sigara, uzinzi, usengenyaji basi ujue ile mbegu imekufa ndani yako.. Kwasababu uliposikia Neno la Mungu hukutaka kuliwekea mazingira mazuri ya kukua lenyewe. Kumbuka mkristo yoyote anayezingatia kulitunza na kujifunza Neno la Mungu kila siku katika maisha yake, hatapata shida kuishida dhambi. Kwasababu Biblia inasema..

1Yohana 3: 9 Kila mtu aliyezaliwa na Mungu hatendi dhambi, kwa sababu uzao [MBEGU]wake wakaa ndani yake ; wala hawezi kutenda dhambi kwa sababu amezaliwa kutokana na Mungu.

Ni maombi yangu sisi sote tujue nguvu ya Neno la Mungu, tukijua kuwa tukilipinga Neno la Mungu ndani yetu ni kujitenga na uzima wetu wenyewe. Hivyo nakutia moyo ndugu usomaye haya usichoke kujifunza Neno la Mungu kila iitwapo leo, jifunze Biblia. Kwasababu hujui wewe lile Neno linatendaje kazi ndani yako. Wewe jifunze na kulitii tu, hata kama hutaona leo mabadiliko lakini fahamu tu, linakuwa kwa njia usioijua wewe, wakati Fulani ukipita ukiendelea hivyo utaona tofauti ya leo yako na jana yako ilivyokuwa.
 
Mungu akubariki.

Tafadhali share ujumbe huu kwa watu wengine na Mungu atakubariki.