"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Thursday, August 29, 2019

NJIA SAHIHI YA KUFUNGA.


Jina la Bwana YESU litukuzwe daima. Karibu tujifunze Neno la Mungu, leo kwa neema za Bwana tutajifunza juu ya njia sahihi ya kufunga.

Zipo aina nyingi za kufunga lakini kwa vyovyote vile, hatufungi ili Mungu atusikie au atujibu maombi yetu, Mungu hasubiri kwanza tuteseke ndio atusikie hapana kwani alishaweka wazi katika Neno lake, kuwa yeye anajua tunachohitaji kabla hata hatujamwomba (Mathayo 6:8)…Lakini pamoja na hayo Kufunga kunasaidia kuongeza uwezekano wa wewe kupata majibu ya maombi yako au kupata unachokitafuta kwa haraka tofuati na yule asiyefunga. Ni sawa tu na mwanafunzi anayesomea maktaba na Yule anayesomea nyumbani, anayesomea maktaba anaongeza uwezekano mkubwa wa kufaulu mitihani kuliko Yule anayesomea nyumbani, kwasababu kule maktaba kunakuwa na utulivu mkubwa na mazingira mazuri ya kujisomea kuliko nyumbani..Lakini hiyo haimfanyi afaulu mtihani moja kwa moja Yule wa nyumbani anaweza kufanya vizuri kushinda hata yeye..Lakini itampasa awe mtu wa kujitambua sana.
Vivyo hivyo na katika kufunga, Mtu mwenye desturi ya kuomba kwa kufunga anajijengea daraja zuri la yeye kuwasiliana na Mungu kuliko Yule apelekaye dua zake kwa Mungu bila kufunga, Kwasababu Kufunga kunampa utulivu Fulani wa Roho tofauti na mtu asiyefunga.

Na hiyo yote ni Kutokana na kutokuwa na Mungu katika mwili, au kutokumwona Mungu katika mwili ndio maana inatupelekea tumtafute Mungu kwa umakini zaidi kuliko kama tungekuwa tunamwona kwa macho…Mitume walipokuwa na Bwana duniani hakukuwa na sababu ya kufunga, ufunge ya nini wakati unayemtafuta upo naye hapo? Mpaka watu wengine wakashangaa inakuwaje hawa ni mitume wa Bwana lakini hawafungi, Ndipo Bwana alikawaambia wanachokifanya hawajakosea kwasababu mimi nipo, Siku zitakuja nitakapoondoka ndipo watakapofunga kama wengine...
Marko 2:18 “Nao wanafunzi wake Yohana na Mafarisayo walikuwa wakifunga; basi walikuja, wakamwambia, Kwani wanafunzi wa Yohana na wanafunzi wa Mafarisayo hufunga, bali wanafunzi wako hawafungi?
19 Yesu akawaambia, Walioalikwa arusini wawezaje kufunga maadamu bwana-arusi yupo pamoja nao? Muda wote walipo na bwana-arusi pamoja nao hawawezi kufunga.
20 Lakini siku zitakuja watakapoondolewa bwana-arusi, ndipo watakapofunga siku ile.”
Hivyo kitendo cha kufunga hakikwepeki sasa kwa mkristo yeyote. Na zipo aina nyingi za kufunga, lakini aina iliyozoeleka ni ile ya kuacha kula chakula. Lakini mfungo huu unafanywa kimakosa na wengi kwasababu ya kutokufahamu ni kwanini mtu anaacha kula..Na ndio hapo mtu mmoja atafunga vizuri kweli hata wiki tatu au mwezi au siku arobaini, lakini anafanya kama desturi za dini nyingine wanavyofanya, ukiangalia huku nyuma utamwona anaendelea na maisha yake ya kidunia anadhani kusikia kule njaa ndo Mungu anampa thawabu,. Hajui kuwa Mungu hamjibu mtu kwa mateso,(Maombolezo 3:31-35) sasa hapo mtu wa namna hiyo kaamua tu kujitesa bure..Hakuna chochote atakachokipata kutoka kwa Mungu.

Au unakuta mwingine anafunga kwa lengo la kumuomba Mungu mambo ambayo sio sawa na mapenzi yake, mwingine atamwomba Mungu ampe mali, lakini ndani ya moyo wake anawaza aitumie kwa anasa, mwingine atamwomba Mungu ampe hiki au kile, lakini nia yake moyoni ni kutumia kwa mambo maovu.. mtu wa namna hiyo pia asitazamie kupata kitu.
Isaya 58:3 “Husema, Mbona tumefunga, lakini huoni? Mbona tumejitaabisha nafsi zetu, lakini huangalii? Fahamuni, siku ya kufunga kwenu mnatafuta anasa zenu wenyewe, na kuwalemea wote watendao kazi kwenu.
4 Tazama, ninyi mwafunga mpate kushindana na kugombana, na kupiga kwa ngumi ya uovu. Hamfungi siku hii ya leo hata kuisikizisha sauti yenu juu.
5 Je! Kufunga namna hii ni saumu niliyoichagua mimi? Je! Ni siku ya mtu kujitaabisha nafsi yake? Ni kuinama kichwa kama unyasi, na kutanda nguo za magunia na majivu chini yake? Je! Utasema ni siku ya kufunga, na ya kukubaliwa na Bwana?
6 Je! Saumu niliyoichagua, siyo ya namna hii? Kufungua vifungo vya uovu, kuzilegeza kamba za nira, kuwaacha huru walioonewa, na kwamba mvunje kila nira?
7 Je! Siyo kuwagawia wenye njaa chakula chako, na kuwaleta maskini waliotupwa nje nyumbani kwako? Umwonapo mtu aliye uchi, umvike nguo; wala usijifiche na mtu mwenye damu moja nawe?
8 Ndipo nuru yako itakapopambazuka kama asubuhi, na afya yako itatokea mara; na haki yako itakutangulia; utukufu wa Bwana utakufuata nyuma ukulinde.
9 Ndipo utaita, na Bwana ataitika; utalia, naye atasema, Mimi hapa. Kama ukiiondoa nira; isiwepo kati yako, wala kunyosha kidole, wala kunena maovu;
10 na kama ukimkunjulia mtu mwenye njaa nafsi yako, na kuishibisha nafsi iliyoteswa; ndipo nuru yako itakapopambazuka gizani; na kiwi chako kitakuwa kama adhuhuri.
Unaona? Dhumuni la msingi kabisa la kujizuia kutokula mtu anapaswa afahamu ni kuyaleta mapenzi ya mwili chini na kuruhusu mapenzi ya Mungu yaje juu, ile njaa inakukumbusha kwenda mbele za Mungu kwa unyenyekevu mwingi , sikuzote mtu mwenye njaa anakuwa katika uhitaji sana kuliko mtu aliye shiba, hivyo mtu wa namna hiyo anapokwenda mbele za Mungu kumaanisha kwake kunakuwa kwa kiwango cha juu zaidi kuliko mtu aliyeridhika, hata maombi yake yanakuwa marefu sana, jaribu hata kwako utaligundua hilo..Na hiyo ndio faida kubwa ya kutokula wakati wa maombi. Hivyo inapelekea maombi yako kuwa na nguvu zaidi mbele za kuliko wengine.

Vile vile kuna kufunga ambako sio kwa kula, bali kwa kujizuia na mambo mengine yanayoweza kukusonga usiisikie sauti ya Mungu. Kufunga kwa namna hii kumekuwa kwa kawaida kwa watumishi wengi wa Mungu, Nabii Elisha ilimpasa atumie muda mwingi kujitenga na mazingira ya watu ili kudumisha joto la uhusiano wake na Mungu. Sio kwamba kuna shida kujihusisha na mambo ya kawaida ya kila siku, hapana lakini ni utaratibu wa Mungu kuzungumza katika sauti ya utulivu, na kama ni sauti ya utulivu hivyo naye huwa anahitaji mazingira tulivu ya kumwelewa.

Ufunuo wowote Mungu anaompa mwanadamu, hampi akiwa katika mazingira ya usumbufu wa akili, Usijidanganye kuwa Mungu atakupa ufunuo wowote katika hali ya masumbufu, kama utaisoma biblia na huku unasikiliza miziki ya kidunia, au huku una chat, au huku unafanya mambo mengine, Ni heri uifunge uje usome baadaye usiku peke yako…. inahitaji utulivu wa fikra na mawazo..Na hapo ndipo inakupasa ufunge baadhi ya vitu unavyovifanya, au ulivyozoea kuvifanya..Na kwa jinsi unavyovifunga kwa muda mrefu zaidi ndivyo unavyoongezeka uwezekano wa Mungu kusema na wewe kwa haraka na kwa mara nyingi zaidi.

Kufunga ni kuna faida kwasababu yeye mwenyewe anasema wote wafanyao hivyo huwapa thawabu kama hawatafanya kinafki na kwa nia mbaya..(Mathayo 6:16)

Ni ahadi yake kukulipa, Funga tu kwa kumaanisha kumsogelea Mungu zaidi, utapata zaidi ya kile ulichomwomba. Kuna mtu aliuliza swali je! Maandiko yanasema tunapaswa tufunge kuanzia saa ngapi hadi saa ngapi na ni kwa siku ngapi?..Jibu ni kuwa Biblia haijatoa masharti yoyote juu ya muda wa kufunga au siku za kufunga..Imezoeleka siku 3, siku 21 na siku 40 kwasababu ndio siku ambazo zimeonekana zikifungwa na wengi..Lakini hiyo haimaanishi kuwa nawe ufunge muda huo, ni vile Roho atakavyokuongoza na kulingana na aina ya dua uipelekayo kwa Mungu, unaweza ukafunga, siku moja, au wiki, au mwezi, au mwaka, na Mungu akaridhia, vile vile unaweza ukafunga saa 6 kwa siku, saa 12, au siku tatu bila kula, au siku 40 bila kula , ni vile tu Mungu atakavyokupa neema..Lakini vyovyote vile kufunga ni muhimu kwa kila mkristo. Na kuna manufaa na thawabu nyingi.

Ubarikiwe sana. 

Wednesday, August 28, 2019

KIFAA BORA CHA MATUMIZI.


Shalom, Jina la Bwana wetu Yesu Kristo libarikiwe, maandiko yanasema,
Mhubiri 10:10 “Iwapo chuma hakipati, wala mtu hakinoi; Ndipo hana budi kutumia nguvu zaidi. Walakini yafaa kutumia hekima, na kufanikiwa”.
Katika tafsiri nyingine hilo Neno Chuma limetafsiriwa kama shoka, ikiwa na maana kuwa kama shoka ni butu au halinolewi mara kwa mara basi itampasa mtu kutumia nguvu zaidi katika kukata vitu au kuchonga, au kuchanja kama anakata nyama itampasa atumie nguvu zaidi kuikata nyama ile, kama anakata mti basi itampasa atumie jitihada ya ziada yenye kuchosha kuudondosha mti kwasababu Shoka ni butu haliwezi kupenya kwa haraka ndani ya shina..Tofauti na kama kifaa hicho kingekuwa ni kikali, angetumia nguvu chache tu na matokeo kuwa makubwa ndani ya muda mfupi…
Ni kama tu kisu au kiwembe kikiwa ni kakali basi ukipitisha hata kwenye karatasi ni mara moja tu limegawanyika, lakini kama ni butu basi utakipeleka mbele na nyuma, na utachukua muda, na bado halitachanika vizuri kama lile lililochanwa na kiwembe kikali..

Lakini Mhubiri anaendelea kwa kusema, “walakini yafaa kutumia hekima, na kufanikiwa”,.. Ikiwa na maana usipoweza kutumia hekima, kuamua maisha yako kwa kukifanya kisu chako kuwa kikali basi mambo yako, licha tu ya kuwa magumu lakini pia utatumia nguvu nyingi kuyafikia...

Duniani Vipo visu vingi tofauti tofauti na mashoka tofuati tofauti na kila mtu analo lake, ambalo kwa namna moja au nyingine linamsaidia kufanya mambo yake kuwa mepesi, wengine ni elimu, wengine ni ujuzi, wengine ni fedha n.k..Lakini hasara moja ya vifaa hivyo vyote sio vya kudumu, huwa vinakuwa butu kwa jinsi muda unavyokwenda na kwa jinsi vinavyotumika…. Mtu akiviacha vinachakaa na pia isitoshe havitumiki kila mahali…huwezi kutumia elimu kutibu kifo, vile vile huwezi tumia pesa kununua furaha, au upendo au amani..

Ni kifaa kimoja tu ambacho Mtu mwenye akili na Hekima anaweza kukitumia kwa matumizi yote na kukata kila kitu pasipo kutumia nguvu, na bado kutokupungua ubora wake na makali yake…Nacho ni Neno la Mungu..
Waebrania 4:12 “Maana Neno la Mungu li hai, tena lina nguvu, tena lina ukali kuliko upanga uwao wote ukatao kuwili, tena lachoma hata kuzigawanya nafsi na roho, na viungo na mafuta yaliyomo ndani yake; tena li jepesi kuyatambua mawazo na makusudi ya moyo.
13 Wala hakuna kiumbe kisichokuwa wazi mbele zake, lakini vitu vyote vi utupu na kufunuliwa machoni pake yeye aliye na mambo yetu.”
 
Mtu akiwa na Neno la Mungu peke yake, hiyo ni salaha tosha, ya kurahisisha mambo yako..hili haliwi butu kama vile mengine, linao uwezo sio tu wa kukata kwa ukali zaidi ya upanga wowote, bali pia linaweza kuchoma hata kuzigawanya nafsi na roho, yaani linaingia ndani ya moyo wa mwanadamu na kugawanyisha kila kitu na kutambua mawazo yake, kitu ambacho pesa haiwezi kufanyi, elimu ya dunia hii haiwezi kufanya, ujuzi wowote ule wa mwanadamu hauwezi kufanya..

Ndio maana mtu yeyote aliyejaa Neno la Mungu ndani yake, hakuna jambo lolote linaloweza kumlemea hata liwe gumu kiasi gani kwasababu anafahamu vizuri silaha aliyonayo inaubora kiasi gani..

Mhubiri anatushauri NI HERI KUTUMIA HEKIMA NA KUFANIKIWA, tunapaswa tujue ni kifaa gani kitakachotufaa katika maisha yetu, katika mapori yanayotuzunguza mbele yetu ambayo yanapaswa yafyekwe kweli kweli, kifaa ambacho tunaweza kukabiliana na adui yetu ibilisi na kummaliza haraka sana bila kutumia nguvu nyingi… silaha hiyo si nyingine zaidi ya Neno la Mungu. 
Waefeso 6: 17 “Tena ipokeeni chapeo ya wokovu, na upanga wa Roho ambao ni neno la Mungu;”

Tunapoliishi Neno la Mungu, maisha yetu hatutayaona ni magumu, hatutasumbuka kama ulimwengu unavyosumbuka, Kwani ni Mungu mwenyewe ndiye atakayekuwa anatupigania,,Lakini tunapoliweka Neno la Mungu kando, tunapolidharau na kuchagua mambo mengine, au kuyaona mambo mengine ni ya muhimu zaidi ya Neno lake, tuwe na uhakika kuwa safari yetu itaishia ukingoni…Ni kutumia kifaa butu, kuufyeka msitu…Mambo yatakuwa magumu tu, huo ndio ukweli, Nira iliyo nyepesi ipo kwa Bwana Yesu tu, pengine kote ni Nzito na mateso yasiyoelezeka..(Mathayo 11:28)

Ndugu/Kaka Ikiwa hujayakabidhi maisha yako kwa BWANA Mlango wa Neema upo wazi, usisubiri baadaye au kesho, muda umekwenda sana kama unyakuo hautakukuta moja ya hizi siku, hujui baadaye yako itakuwa vipi, waliokufa leo asubuhi sio kwamba walikuwa waovu zaidi yako wewe, au walikuwa wameshajiandaa kwa safari ya kwenda huko ng’ambo, hapana lakini kifo kiliwakuta kwa ghafla tu, na ndivyo kitakavyotukuta wote walio haki na wasio haki…Hivyo fanya uamuzi wa busara wakati huu kwa kutubu dhambi zako kama hujatubu na kumgeukia Bwana sasa hivi.. kumgeukia Bwana Yesu sio kuwa vuguvugu, ni kitendo cha kumaanisha kabisa….Kisha utafute mahali wanapobatiza ubatizo sahihi wa kuzamishwa katika maji mengi kwa Jina la YESU KRISTO, kama pia bado hujafanya hivyo..Upate ondoleo la dhambi zako, kulingana na (Matendo 2:38) ili Bwana akupe kipawa cha Roho wake Mtakatifu ambaye ndio muhuri wetu, Mungu anaotutia mpaka ile siku wa ukombozi wetu (Waefeso 4:30).

Bwana azidi kukubariki.

Maran atha!

SEHEMU ISIYO NA MAJI.


Maji yanawakilisha uhai, mahali ambapo hapana maji hapana uhai hiyo inajulikana na watu wote….Sayari zilizopo huko juu hazina maji, na ndio moja wapo ya sababu inazozifanya zisiwe na uhai…Hivyo hata hii dunia tunayoishi iliumbwa kutoka katika maji.
2Petro 3: 5 “Maana hufumba macho yao wasione neno hili ya kuwa zilikuwako mbingu tangu zamani, na nchi pia, imefanyizwa kutoka katika maji, na ndani ya maji, kwa neno la Mungu;
6 kwa hayo dunia ile ya wakati ule iligharikishwa na maji, ikaangamia”.
Mwanzo 1: 1 “Hapo mwanzo Mungu aliziumba mbingu na nchi. 2 Nayo nchi ilikuwa ukiwa, tena utupu, na giza lilikuwa juu ya uso wa vilindi vya maji; Roho ya Mungu ikatulia juu ya uso wa maji”.

Kwahiyo sehemu yoyote isiyo na maji ni makazi ya kifo…Kadhalika katika roho, yapo maji ya rohoni, ambayo hayo mtu yeyote asiyekuwa nayo, moyo wake unakuwa ni nchi kavu, au nchi kame, makao ya kifo… Na hivyo Roho Mtakatifu hawezi kushuka mahali palipo pakame, yeye anashuka mahali penye maji, kama alivyotua wakati wa kuitengeneza upya dunia ya kwanza, alitua juu ya uso wa vilindi vya maji, ndipo akaanza uumbaji….Maji na Roho vinakwenda pamoja, (1 Yohana 5:9

“Kisha wako watatu washuhudiao duniani], Roho, na maji, na damu; na watatu hawa hupatana kwa habari moja.) ndio maana kuna umuhimu sana wa kubatizwa ubatizo wa maji mengi na si wa kunyunyiziwa ndipo Roho aingie ndani ya mtu, kwasababu dunia ya kwanza biblia inasema Roho Mtakatifu hakutua juu ya chemchemi, au juu ya unyevunyevu bali juu ya uso wa vilindi, ikiwa namaana kuwa ni dunia yote ilikuwa imejaa maji sio sehemu baadhi tu! hapana Bali yote..ndipo uumbaji ukaanza.

Mtu aliyempa Kristo Maisha yake kwa kudhamiria kabisa kuacha dhambi, na kubatizwa katika ubatizo sahihi wa maji mengi, na kwa jina la Yesu Kristo, hapo mtu huyo ni sawa na anaujaza moyo wake na maji ya uzima..Moyo wake unakuwa umejaa maji mpaka juu kabisa, vilindi vya maji ya uhai vinakuwa juu yake, na hivyo tayari Roho Mtakatifu kushuka juu yake na kuanza uumbaji, anakuwa amezaliwa mara ya pili na kuwa kiumbe kipya. Roho Mtakatifu anaanza kusema na iwe Nuru juu yake, na inakuwa hivyo, Roho Mtakatifu anaanza kutenga maji na maji,na kutengeneza ndani yake mito, chemichemi, na vipindi vya mvua, na kuchipusha kile ki-kijani ndani yake n.k

Bwana Yesu alisema katika 
Yohana 7: 38 “Aniaminiye mimi, kama vile maandiko yalivyonena, mito ya maji yaliyo hai itatoka ndani yake. 39 Na neno hilo alilisema katika habari ya Roho, ambaye wale wamwaminio watampokea baadaye; kwa maana Roho alikuwa hajaja, kwa sababu Yesu alikuwa hajatukuzwa”.
Sasa tumeshaona ni namna gani Roho ya mtu aliyezaliwa mara ya pili mbele za Mungu inaonekana kama ni mahali penye maji, penye uhai na mahali ambapo ni makazi ya Roho Mtakatifu, na tumeshaona kuwa Ili Roho Mtakatifu akae ndani ya mtu ni lazima ubatizo sahihi wa kimaandiko wa maji mengi uhusike..Kama Ilivyokuwa katika uumbaji.

Vivyo hivyo mtu yeyote ambaye hajamwamini Yesu Kristo, wala hajabatizwa inavyopaswa wala hajapokea Roho Mtakatifu, moyoni mwake ni nchi kavu..Na hakuna namna yoyote ile ambayo Roho Mtakatifu atatua juu yake…Na kama Roho Mtakatifu hatatua juu yake basi ni Dhahiri kuna roho nyingine zitatua juu yake…Na hizo si zaidi ya roho chafu za Mapepo…Roho za Mapepo ndizo zinazotafuta sehemu kavu isiyo na maji na kushuka juu yake..Tusome..
Mathayo 12:43 “Pepo mchafu, amtokapo mtu, hupitia mahali pasipo maji, akitafuta mahali pa kupumzika, asipate.
44 Halafu husema, Nitarudi nyumbani kwangu nilikotoka; hata akija, aiona tupu, imefagiwa, na kupambwa.
45 Mara huenda, akachukua pamoja naye pepo wengine saba walio waovu kuliko yeye mwenyewe, nao huingia na kukaa humo; na mtu yule hali yake ya mwisho huwa mbaya kuliko ya kwanza. Ndivyo itakavyokuwa kwa kizazi hiki kilicho kibaya”.
Unaona hapo?..Biblia inasema anapitia sehemu isiyo na maji, na hiyo si nyingine Zaidi ya mtu ambaye hajamwamini Kristo, na hajabatizwa na kupokea Roho Mtakatifu.Kitu kimoja watu wengi wasichokijua ni kwamba shetani sasa hayupo kuzimu...wala haungui moto sasahivi…shetani yupo hapa hapa duniani na baadhi ya mapepo yake, yapo mapepo baadhi biblia imesema kuwa ndio yapo kuzimu sasa kwenye vifungo, lakini sio yote! (2 Petro 2:4) Idadi kubwa ya mapepo yapo huru ulimwenguni, yakisubiri siku ya mwisho ifike yakusanywe yote pamoja na shetani yakatupwe katika lile ziwa la moto.
Haya yaliyopo huru sasa hayatamani kwa namna yoyote kwenda huko kuzimu(au kwa lugha nyingine shimoni), kwasababu yanajua mateso yaliyopo kule, ndio maana yalimsihi sana Bwana wakati ule yasipelekwe shimoni (soma Luka 8:30-32).

Na kitu kingine kisichojulikana na wengi ni kuwa, mtu yeyote ambaye hajampa Kristo Maisha yake, anayo mapepo ndani yake, anaweza akawa anayo machache au mengi, na yanatofautiana ubaya, yapo yaliyo mabaya sana na yapo ya wastani, yapo ambayo madhara yake ni ngumu kuonekana kwa wazi na yapo ambayo madhara yake yanaonekana waziwazi, lakini yote katika yote mtu ambaye hajampa Kristo Maisha yake, mwili wake ni makao ya roho chafu…aidha anajua au hajui..Na wengi wenye mapepo hawajijui kama wanayo, Mpaka siku watakapobadilika ndio watakapojijua kuwa hawakuwa sawa hapo kwanza.

Sasa mtu anayempa Kristo Maisha yake leo na kukusudia kubatizwa na kupokea Roho Mtakatifu mapepo yanamtoka, na kumbuka mapepo yakimtoka mtu sio lazima yalipuke! Hapana! Kufikiri hivyo ni kufikiri kichanga! Mapepo mengi yanawatoka watu pasipo hata kulipuka wala kuonesha mabadiliko yoyote ya mwili, baada ya kipindi Fulani tu mtu ndio atajiona amekuwa tofuati kuliko alivyokuwa hapo kwanza. Kwahiyo baada ya mapepo haya kutoka ndani ya mtu hayaendi kuzimu wala hayaendi jangwani, yanakwenda kutafuta mahali ambapo hapana maji, na huko si kwingine Zaidi ya mtu ambaye hajampa Kristo Maisha yake au kwa Wanyama, kwasababu Wanyama hawana Roho Mtakatifu, kipawa hicho hawajaahidiwa wao…Lakini yanapendelea Zaidi watu kuliko ya Wanyama…Kwahiyo mtu huyo kila siku anakuwa anaongeza mapepo juu ya mapepo ndani yake pasipo kujijua, ndio maana mtu ambaye hajampa Kristo Maisha yake, hali yake ya kiroho kila siku inazidi kuwa mbaya…Kwanini? Kwasababu kila siku anaongoza idadi ya mapepo ndani yake?

Unaweza kutengeneza picha yule mtu Bwana Yesu aliyemwombea alikuwa ana mapepo wangapi? Biblia inasema ni jeshi! Sasa hebu fikiri nguruwe pale walikuwa 2,000 na kila nguruwe tuseme kaingiwa na mapepo mawili tu! Kwa hesabu hizo jumla ya mapepo yaliyokuwa ndani ni wazi kuwa ni Zaidi ya mapepo 4,000 ndani ya mtu mmoja!.. na kila pepo linatabia yake..

Hivyo ndugu ambaye hujampa Kristo Maisha yako au ambaye mguu mmoja leo huko mwingine kule…hayo ndio madhara yatakayokupata endapo hutaamua kufanya maamuzi thabiti sasa…Kama hali yako itazidi kuwa mbaya kila kukicha, shetani yupo na anafanya kazi sasa…Mkabidhi Yesu Kristo Maisha yako ukabatizwe kama hujafanya hivyo, ili akupe na Roho wake Mtakatifu ili vijito vya maji ya uzima vianze kububujika ndani yako. Na ufanikiwe katika roho yako, na mwili wako usiwe makazi ya roho chafu za shetani. Nguvu za shetani sasa zinafanya kazi sana, kuliko kipindi cha nyuma, na hiyo yote biblia inatumbia ni kwasababu anajua kuwa muda wake umebakia mchache, na ndio maana utaona leo hii matendo mengi maovu ya ajabu ajabu yanatokea ulimwenguni, vitu ambavyo huwezi ukadhani kama mwanadamu anaweza kuvifanya..Hivyo fanya bidii uingie katika ulinzi wa Damu ya Yesu Kristo kwa kutubu na kumwamini Yeye.

Bwana akubariki sana.

Tembelea www.wingulamashahidi.org kwa mtiririko mzuri wa masomo kwa masomo Zaidi.
Maran atha!.