"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Thursday, August 30, 2018

ALIPO NA ATAKAPOKUWEPO BIBI-ARUSI WA YESU KRISTO.

Wengi tunafahamu habari za Yusufu, tunajua alikuwa ni mmoja wa watoto wa Yakobo aliyependwa sana na baba yake, Lakini baada ya kuota zile ndoto tu, ndugu zake walianza kumwonea wivu, na mwisho wa siku wakaamua kumuuza kama mtumwa kwa watu wa mataifa (Wamisri). Na kama tunavyoisoma habari alipokuwa kule Misri Mungu alikuwa pamoja naye akamfanikisha katika mambo yote, akawa wa pili baada ya Farao mfalme wa Misri, kiasi cha kwamba hakuna mtu yoyote aliyeweza kufika kwa Farao bila kupitia kwanza kwake, Mali na vitu vyote vya Misri Farao alivikabidhisha kwa Yusufu,[Kumbuka Misri ndiyo iliyokuwa ngome yenye nguvu kuliko zote duniani kwa wakati ule], tunaweza kusema mfano leo hii taifa la Marekani lilivyo.

Lakini habari hii ya maisha ya Yusufu na yote aliyoyapitia imebeba siri na ujumbe mzito katika roho kwa kanisa,. Yusufu anafananishwa na Bwana wetu Yesu Kristo, na Farao anafananishwa na Baba yetu wa mbinguni. Wale wana 11 wa Yakobo wanafananishwa na wayahudi [yaani waisraeli], na Taifa la Misri Yusufu alipokimbilia linafananishwa na Kanisa la mataifa [wakristo], na Yule mke wa Yusufu (Asenathi) ambaye alimpata katikati ya wa-Misri kutoka katika jumba la kifalme la Farao, anafananishwa na BIBI-ARUSI safi wa Kristo.

Kama vile Yusufu alivyoonewa wivu na ndugu zake na kukataliwa, kisha kwenda kuuzwa utumwani, vivyo hivyo Bwana Yesu alipokuja duniani kwa ndugu zake wayahudi kama masihi wao waliyekuwa wanamtazamia kwa siku nyingi, walimwonea wivu, alipojishuhudia kuwa yeye ndiye mwana wa Mungu, wakamdharau hivyo wakamfanyia hila, wakamkataa kabisa na kumtia mikononi mwa warumi na kumuua [Huko ndiko kumuuza kwa watu wa Mataifa].

Na ndio maana ukisoma biblia utaona mtume Paulo anawaambia hivi wayahudi;

Matendo 13:46 “ Paulo na Barnaba wakanena kwa ushujaa wakasema, Ilikuwa lazima neno la Mungu linenwe kwenu kwanza [wayahudi]; lakini kwa kuwa mnalisukumia mbali, na kujiona nafsi zenu kuwa hamkustahili uzima wa milele, angalieni, twawageukia Mataifa.
47 Kwa sababu ndivyo tulivyoamriwa na Bwana, Nimekuweka uwe nuru ya Mataifa, Upate kuwa wokovu hata mwisho wa dunia.
48 Mataifa waliposikia hayo wakafurahi, wakalitukuza neno la Bwana, nao waliokuwa wamekusudiwa uzima wa milele wakaamini.
49 Neno la Bwana likaenea katika nchi ile yote".
Unaona hapo walimkataa Kristo, ambaye alikuja kwa ajili yao..Bwana hakuwahi kujidhihirisha kwa mataifa hapo kabla, ile neema ilikuwa ni kwa wayahudi tu ndugu zake waliokuwa wakimtazamia kwa muda mrefu, Na ndio maana alisema katika Mathayo 15:24 ".... Sikutumwa ila kwa kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli.” lakini kwa kuwa wao walimwonea wivu kama vile wale watoto wengine wa Yakobo walivyomwonea wivu ndugu yao Yusufu, basi ile neema ikaondoka kwao na kuja kwetu sisi watu wa mataifa [ambao katika habari hii tunaweza kusema wamisri],

Lakini jambo lingine pia la kuliangalia ambalo limejificha katika maisha ya Yusufu alipokuwa Misri, ni kwamba utaona watu wengi wa Misri hawakuwa na imani sana na Yusufu, kama alivyokuwa nayo Farao kwa Yusufu. Na ndio maana utaona, wakati wa kile kipindi cha miaka 7 ya neema, ni Yusufu peke yake aliyekuwa akifanya bidii kutimiza yale maono aliyoyaona juu ya njaa itakayokuja kuikumba karibia dunia nzima. Kama wale watu wa Misri wangekwenda sambamba na Yusufu baadaye utaona baada ya njaa kuanza kuipiga dunia wasingekuwa nao pia wanatangatanga kwenda kuomba na kununua chakula kwa Yusufu, kwa kuwa ni raia wa nchi yao, Yusufu asingewauzia chakula, wala kubadilishana nao chakula kwa mali na mashamba yao..angewapa bure, au kuwauzia kwa gharama ambayo isingelazimu mpaka kutoa mali zao na vitu vyao.

Inaonyesha wazi kabisa wale watu, hawakuyasadiki maono ya Yusufu kwa kiwango kikubwa pindi alipowaambia wakusanye hazina kwa wakati wa ukame unaokuja huko mbeleni. Ni mfano dhahiri wa wingi wa wakristo waliopo leo ambao ni kweli walimpokea Masihi (yaani Kristo) kama Mwokozi wao, lakini wameyapuuzia yale aliyowaambia yatakayokuja kuipata dunia huko mbeleni pindi itakapopitia miaka ya njaa na ukame wa rohoni na wa mwilini ( yaani wakati wa ile dhiki kuu).

Mtu pekee ambaye hakuathirika na ile dhiki ya njaa ilipokuja duniani kote ni MKE WA YUSUFU tu peke yake kwasababu yeye alikuwa katika JUMBA LA KIFALME..Akizipeleleza zile siri za ndani kabisa zilizokuwa katika moyo wa Yusufu..na kama ukichunguza vizuri utaona yule mke Yusufu hakumtwaa ovyo ovyo tu mahali popote hapana, bali alipewa na Farao mwenyewe.. Ni mfano halisi wa BIBI-ARUSI wa KRISTO, wateule wa Mungu, ambao ni Mungu pekee yake ndio anayempa KRISTO.

Kumbuka ndugu, katikati ya wanaojiita wakristo yapo makundi mawili, yupo BIBI-ARUSI wa Kristo yaani MKE wa Bwana Yesu, na wapo Masuria, hawa wanafananishwa na wanawali werevu na wanawali wapumbavu.(Mathayo 25). Katika siku za mwisho makundi yote mawili yatakuwepo, na litakalokwenda kwenye unyakuo ni lile tu la wanawali werevu yaani BIBI-ARUSI wa Kristo.

Sasa kama vile Yusufu alivyokuwa ni mkuu wa Wamisri wote (yaani watu wa mataifa), waliomwendea na kumwomba chakula wakati wa dhiki, ambapo kwa wakati huo mke wa Yusufu alikuwa anakula raha katika jumba la kifalme.

kadhalika na katika siku za taabu za ile dhiki kuu ya mwisho, wapo wakristo vuguvugu ambao wao wasingepaswa kupitia dhiki, lakini wataipitia kwa upumbavu wao, wakati wenzao (wale BIBI-ARUSI wa Kristo) wapo mbinguni kwa Baba kwenye enzi ya kifalme katika karamu ya mwana-kondoo.

Na kama vile dalili ya kipindi cha dhiki kuanza ni kuona ndugu zake Yusufu wanaanza kwenda kutafuta chakula Misri pamoja na wamisri wenyewe kuanza kutangatanga huku na kule kutafuta chakula, Vivyo hivyo Na katika kipindi hichi tunachoishi sasa, Njaa ya kulisikia Neno la kweli inaongezeka.

Wayahudi kwa miaka mingi wamekuwa wakimtazamia masihi wao aje kuwakomboa, lakini hawaoni chochote kwa kipindi chote hicho, lakini nyakati hizi kidogo kidogo, tunaona wanaanza kujua makosa yao, kwamba hakuna Masia mwingine atakayekuja, wanaanza kutambua kuwa kuna chakula Misri yaani kwa Wakristo, wanaanza kuona mbona Yule waliyemkataa ndiye amekuwa TEGEMEO LA DUNIA NZIMA?.

Ndugu yangu siku ile watakapotubu tu!, basi ujue kile kipindi cha DHIKI KUU kimeshaanza, na neema haitakuwepo tena kwa watu wa mataifa, kama ndugu zake Yusufu walivyomlilia ndivyo itakavyokuwa kwa wayahudi kwa wakati huo, waisraeli watafumbuliwa macho kikabisa kabisa na kumtambua Yesu Kristo, biblia inasema watamwombolezea yeye waliyemchoma…

Zekaria 12: 10 “Nami nitawamwagia watu wa nyumba ya Daudi, na wenyeji wa Yerusalemu, roho ya neema na kuomba; nao WATAMTAZAMA YEYE AMBAYE WALIMCHOMA; nao watamwombolezea, kama vile mtu amwombolezeavyo mwanawe wa pekee; nao wataona uchungu kwa ajili yake, kama vile mtu aonavyo uchungu kwa ajili ya mzaliwa wake wa kwanza.
11 Siku hiyo kutakuwa na maombolezo makuu huko Yerusalemu, kama maombolezo ya Hadadrimoni katika bonde la Megido"

Sasa baada ya hapo itakuwa imebaki miaka michache tu mpaka ile miaka 7 ya mwisho iishe, na baada ya hiyo dunia itakuwa imeisha, wakati huo duniani kutakuwa na dhiki isiyokuwa ya kawaida, huo ndio wakati watu wote watakapojua kuwa YESU KRISTO NDIYE JIWE KUU LA PEMBENI LILE LILILOKATALIWA NA WAASHI, Watu wa ulimwengu wote watajua kuwa ufalme na mamlaka yote ya mbinguni na duniani amekabidhiwa YESU KRISTO, na Hakuna WOKOVU NA UZIMA nje ya yeye. Kama vile watu wa kipindi cha Yusufu walivyofahamu kuwa malmlaka yote na ufalme amekabidhiwa Yusufu.

Unaweza ukaona ni wakati gani tunaishi, Taifa la Israeli linazidi kunyanyuka, hivi karibuni waisraeli watafumbuliwa macho yao na kumtambua Yesu Kristo, je! Wewe ni miongoni mwa Bibi-arusi atakayeenda kwenye unyakuo siku ile kabla ya DHIKI KUU KUANZA? Unamchukulia Bwana Yesu Kristo kwako kama nani?, je! Unamchukulia kama ni mtu wa kawaida tu, au mfalme?, kumbuka Yusufu alivyokuwa gerezani sio sawa na alivyofanywa mfalme, na vivyo hivyo Bwana Yesu Kristo, alivyokuwa pale msalabani kalvari sio sawa na alivyo sasa, Biblia inasema ameketi katika NURU ISIYOWEZA KUKARIBIWA, na maneno yake ni kweli na uzima..

Hivyo kama hujaingizwa katika ile familia ya kifalme, hautaweza kuikwepa dhiki, kama hujazaliwa mara ya pili kwa maji na kwa Roho, hautaweza kuuingia katika karamu ya mwana kondoo kule mbinguni, kwanini ukose hayo yote?? Jitahidi kufanya hivyo sasa kabla mlango haujafungwa. Tubu leo mgeukie Bwana azioshe dhambi zako, naye atakupa neema ya kuwa miongoni mwa Bibi-arusi wake. UNYAKUO NI SIKU YOYOTE.

Ubarikiwe!

Tafadhali “share” ujumbe huu kwa wengine.

Kwa mpangilio mzuri wa masomo haya tembelea website yetu hii >>> www.wingulamashahidi.org

Wednesday, August 29, 2018

JE! NYWELE ZAKO ZINAOTA AU ZIMESIMAMA?

Mambo yote yaliyoandikwa katika agano la kale ni kivuli cha mambo yanayoendelea katika roho katika agano jipya tulilopo sasa. Kwamfano kama vile tunavyoweza kusoma Mungu alivyowaita wana wa Israeli kutoka Misri, kuelekea Kaanani kupitia jangwani, ndio hivyo hivyo Mungu anavyowaita watoto wake leo kutoka katika utumwa wa dhambi [Misri], kisha anawavusha katika bahari ya shamu [ambao ndio ubatizo 1Wakorintho 10], na baada ya hapo safari ya jangwani inaanza ambayo hiyo ni lazima kila mkristo aipitie, mahali ambapo atafundishwa kumcha Mungu, na kumtegemea yeye kwa kila kitu, mahali ambapo Mungu ataruhusu ajaribiwe kwa kila kitu lakini hataachwa. Na hatua ya mwisho ni Kuingia Kaanani, Ambayo nayo inaanzia hapa hapa duniani kisha kumalizikia kwenye nchi mpya na mbingu mpya..

Kadhalika tunajifunza pia jambo lingine katika habari ya Samsoni, ambayo nayo ni kivuli cha mambo yanayoendelea sasa hivi katika roho. Tunasoma Samsoni Mungu alimtia mafuta tangu alipokuwa tumboni mwa mama yake, akifananishwa na kanisa la Kristo jinsi lilivyoanza pale Pentekoste lilikuwa takatifu na safi lisilokuwa na waa lolote, Tunasoma pia Samsoni aliamuriwa na Mungu asikate nywele zake bali azifunge katika vishungi saba, Picha halisi ya kanisa la Kristo ambalo tunaona katika kitabu cha Ufunuo sura ya 2 &3 Bwana Yesu akitoa ujumbe kwa yale makanisa 7, Kumbuka kanisa la Kristo limekuwa likipita katika vipindi 7 tofauti tofauti vinavyojulikana kama NYAKATI 7 ZA KANISA kwa muda wa miaka 2000 sasa, na katika majira tunayoishi ni majira ya kanisa la mwisho la 7 linaloitwa LAODIKIA.

Kama vile Samsoni nguvu zake zilivyokuwa katika zile nywele, hivyo kanisa nalo katika nyakati zote saba limekuwa likitegemea nguvu zake katika NENO LA MUNGU ili likae. Lakini kwa habari mbaya tunasoma Samsoni alionyesha tabia za uasherati za kwenda kuzini na wanawake makahaba na wanawake wasio wa uzao wa Ibrahimu, na ndio hao baadaye waliokuja kujua siri ya nguvu zake, biblia inasema katika Mithali 31: 3 “Usiwape wanawake nguvu zako;”

Lakini Samsoni yeye hakufanya hivyo, badala yake alikubali kulaghaiwa na wale wanawake wasiomjua hata Mungu wa Israeli, wanawake wa kidunia, matokeo yake akaangukia katika mikono ya maadui zake wafilisti kwa muda mrefu, tunasoma;

Waamuzi 16: 15 “Mwanamke akamwambia, Wawezaje kusema, Nakupenda; na moyo wako haupo pamoja nami? Umenidhihaki mara hizi tatu, wala hukuniambia asili ya nguvu zako nyingi.
16 Ikawa, kwa vile alivyomsumbua kwa maneno yake kila siku, na kumwudhi, roho yake ikadhikika hata kufa.
17 Ndipo alipomwambia yote yaliyokuwa moyoni mwake, akamwambia, Wembe haukupita juu ya kichwa changu kamwe; maana mimi nimekuwa Mnadhiri wa Mungu, tangu tumboni mwa mama yangu; nikinyolewa, ndipo nguvu zangu zitanitoka, nami nitakuwa dhaifu, nitakuwa kama wanadamu wenzangu.
18 Delila alipoona ya kuwa amemwambia yote yaliyokuwa moyoni mwake, akatuma mtu akawaita wakuu wa Wafilisti, akisema, Njoni huku mara hii tu, maana ameniambia yote aliyo nayo moyoni mwake. Ndipo wakuu wa Wafilisti wakamwendea wakachukua ile fedha mikononi mwao.
19 Naye akamlaza usingizi magotini pake. Kisha akamwita mtu akavinyoa vile vishungi saba vya nywele za kichwa chake; akaanza kumsumbua, nguvu zake zikamtoka.
20 Kisha akasema, Samsoni, Wafilisti wanakujia. Akaamka katika usingizi wake, akasema, Nitakwenda nje kama siku nyingine, na kujinyosha. Lakini hakujua ya kuwa Bwana amemwacha.
21 Wafilisti wakamkamata, wakamng'oa macho; wakatelemka naye mpaka Gaza, wakamfunga kwa vifungo vya shaba; naye alikuwa akisaga ngano katika gereza.

Unaona hapo?. Ndio jambo hilo hilo lililikuta kanisa la Kristo mara baada ya mitume kuondoka, Paulo aliandika hivi…Matendo 20: 29 “Najua mimi ya kuwa baada ya kuondoka kwangu mbwa-mwitu wakali wataingia kwenu, wasilihurumie kundi;
30 tena katika ninyi wenyewe watainuka watu wakisema mapotovu, wawavute hao wanafunzi wawaandamie wao.”


Hivyo katika agano jipya Delila anafananishwa na kanisa kahaba na hili kanisa si lingine zaidi ya kanisa Katoliki, ambalo lilianza kwa kuanza kupenyesha mafundisho potofu ya uongo ndani ya kanisa la Mungu, na hatimaye kufanikiwa kutengeneza dini kabisa, mnamo mwaka 325 WK katika Baraza la Nikea, lilifanikiwa kuyachanganya mafundisho ya kikristo na ibada za kipagani za kirumi, huko ndiko kulikozuka ibada za miungu mingi, ibada za sanamu, kusali rozari, kuomba kwa watakatifu waliokufa kale, mafundisho ya kwenda toharani, kanisa kuongozwa na vyeo vya kibinadamu badala ya karama za Mungu, mambo ambayo hayapo katika maandiko wala hayakuonekana katika kanisa la kwanza.

Na kanisa hili lilipozidi kupata nguvu kwa kuwashawishi watu na kuwadanganya kidogo kidogo nguvu za Roho Mtakatifu zikaanza kupungua katika Kanisa, na hatimaye kupoa kabisa isipokuwa kwa kikundi kidogo sana cha wateule, na kupelekea kanisa kupitia katika kipindi kirefu cha giza kwa zaidi ya miaka 1000, ni kipindi kinachojulikana katika historia kama KIPINDI CHA GIZA.

Katika siku ile kwenye hilo baraza la Nikea ndio siku hiyo huyu mwanamke kahaba [Kanisa Katoliki] anayefananishwa na Delila alifanikiwa kuzinyoa nywele za kanisa la Mungu kabisa, hivyo nguvu za kanisa zilipoa kwa muda mrefu sana, kukawa hakuna tena karama za rohoni, biblia ikazuiliwa kusomwa kwa washirika, zile nguvu za watu kumwamini Kristo zilizoanza pale Pentekoste zikafa, watu waliojaribu kushikilia mafundisho ya mitume waliuliwa, mafundisho ya watu kuhesabiwa haki kwa Imani katika Yesu Kristo yakafa badala yake watu wakawa wanafundishwa kuhesabiwa haki kwa kuwa mshirika wa kanisa Katoliki, utozwaji wa pesa wa vitu vinavyoitwa vya ki-Mungu ukaanza, kwamfano mtu akitaka kuombewa ni lazima atoe kiwango Fulani cha fedha kwa kasisi ili ahudumiwe, mtu akitaka kuwekewa wakfu mtoto wake au mali zake mbele za Mungu, sharti kwanza atoe kitu Fulani, na asipofanya hivyo basi hatapata huduma yoyote, mambo ambayo hayakuwepo katika kanisa la kwanza..n.k.

Lakini kama tunavyosoma baada ya Samsoni kutumika muda mrefu kusaga ngano katika magereza ya Wafilisti tunaona nywele zake zilianza kuota tena pasipo wao kujua. Na zilipomalizika kuota, madhara aliyoyaleta mwisho yalikuwa ni makubwa kuliko yale aliyoyafanya kule mwanzoni kama tunavyosoma..
Waamuzi 16: 22 “Lakini zile nywele za kichwa chake zikaanza kukua tena baada ya kunyolewa kwake.
23 Kisha wakuu wa Wafilisti wakakusanyika ili kumtolea sadaka Dagoni mungu wao, na kufurahi; maana walisema, Mungu wetu amemtia Samsoni adui wetu mikononi mwetu.
24 Na hao watu walipomwona wakamhimidi mungu wao, maana walisema, Mungu wetu amemtia mikononi mwetu huyu adui wetu, aliyeiharibu nchi yetu na kuwaua watu wengi miongoni mwetu.
25 Ikawa mioyo yao iliposhangilia, wakasema, Mwiteni Samsoni, ili atufanyie michezo. Basi wakamwita Samsoni atoke gerezani, akacheze mbele yao wakamweka katikati ya nguzo mbili.
26 Samsoni akamwambia yule kijana aliyemshika mkono, Niache nizipapase nguzo ambazo nyumba hii inazikalia, nipate kuzitegemea.
27 Basi nyumba ile ilikuwa imejaa watu waume kwa wake; na wakuu wote wa Wafilisti walikuwamo humo, na juu ya dari palikuwa na watu elfu tatu waume kwa wake waliokuwa wakitazama, wakati Samsoni alipocheza.
28 Samsoni akamwita Bwana, akasema, Ee Bwana MUNGU, unikumbuke, nakuomba, ukanitie nguvu, nakuomba, mara hii tu, Ee Mungu, ili nipate kujilipiza kisasi juu ya Wafilisti kwa ajili ya macho yangu mawili.
29 Kisha Samsoni akazishika nguzo mbili za katikati ambazo nyumba ile ilikaa juu yake, akazitegemea, moja kwa mkono wake wa kuume na moja kwa mkono wake wa kushoto.
30 Samsoni akasema; Na nife pamoja na hawa Wafilisti. Akainama kwa nguvu zake zote; ile nyumba ikawaangukia hao wakuu, na watu wote waliokuwa ndani yake. BASI WALE WATU ALIOWAUA WAKATI WA KUFA KWAKE WALIKUWA WENGI KULIKO WALE ALIOWAUA WAKATI WA UHAI WAKE”.

Kadhalika na katika kanisa jambo ni lile lile ulipofika wakati nywele za Kanisa kuanza kuota tena, [na kuota kwenyewe ni kurudi kwenye NENO kwenye mafundisho ya mitume]..Ndipo hapo Bwana akaanza kuwanyanyua watu wa kulitengeneza kanisa akawanyanyua wakina Martin Luther, mjumbe wa kanisa la tano, katika karne ya 16 akifundisha mafundisho ya kuhesabiwa haki kwa Imani katika Kristo Yesu, na sio katika dini ya kikatoliki, Bwana akawanyanyua wakina John Wesley na wenzake, katika karne ya 18 wakifundisha utakaso wa damu ya Yesu, kwamba Kristo amekuja ili umfanye mtu kuwa mtakatifu kwamba pasipo huo hakuna mtu atakayemwona Mungu, (Waebrania 12:14) na sio kwamba pasipo ushirika wa kanisa watu hawatamwona Mungu…

Vile vile katika kipindi cha kanisa la mwisho la Laodikia ambalo lilianza mwanzoni mwa karne ya 20 mpaka sasa, Bwana aliwanyanyua wakina William Seymor na wengine katika uamsho wa mtaa wa Azusa kule Marekani pamoja na William Branham ambaye ni mjumbe wa kanisa la mwisho la LAODIKIA, na mafundisho ya Ubatizo wa Roho Mtakatifu, ya kwamba Roho Mtakatifu ndio MUHURI WA MUNGU (Waefeso 4:30). Na wote wasiokuwa na Roho wa Mungu hao sio wake (Warumi 8:9), Na ndio maana inajulikana kuwa tunaishi katika nyakati ya KI-Pentekoste kama ilivyokuwa kule mwanzo, na ndio maana katika nyakati hii zile karama zilizokuwa zimeuliwa na Kanisa Katoliki Bwana alianza kuzirejesha tena kuanzia mwanzoni mwa karne ya 20..(Yaani kuanzia mwaka 1900 na kuendelea)
Lakini haya yote ni kwa ajili ya kumwandaa BIBI-ARUSI wa kweli wa KRISTO kwa ajili ya unyakuo uliokuwa karibu kutokea. Zile nywele zimeshafikia ukomo, ni jambo moja tu linasubiriwa, Uamsho wa mwisho wa BIBI-ARUSI kupitia ufunuo wa zile ngurumo 7 kama tunavyosoma katika ufunuo 10:14, Ambazo hizo zitampa Bibi-arusi imani timilifu (Luka 18:8) ya kwenda katika unyakuo, ni uamsho wa kipekee, nao utakuwa ni wa muda mfupi sana utakaokuwa wa nguvu na wa ajabu kuliko hata ule uamsho wa kwanza uliotokea kule Pentekoste kama vile Samsoni baada ya nywele zake kukua tena, maangamizi aliyoyaletea mwishoni yalikuwa ni makubwa kuliko hata yale ya kwanza. Ndivyo itakavyokuwa kwa Bibi-arusi wa Kristo katika hichi kipindi cha kukaribia na unyakuo.

Na wewe je! Ni miongoni mwa watu ambao nywele zao zimekuwa?? Au bado tu unatumikia katika dini na madhehebu? Kumbuka kuota nywele maana yake ni kurudi katika Neno, nguvu za mkristo yoyote Yule hazipo nje ya Neno la Mungu..Biblia inasema usiabudu sanamu, wala usijifanyie sanamu ya kuchonga, lakini kanisa lako linasema ni sawa kufanya hivyo..hapo unapaswa ufuate kile Neno linasema na uweke chini kile kanisa linasema.


Biblia inasema aaminiye na kubatizwa ataokoka, [na maana ya kubatizwa ni kuzamishwa kwenye maji mengi], lakini kanisa linasema haijalishi, linasema ubatizo wa kunyunyiziwa ni sawa..Hapo unapaswa uweke chini mapokeo ya kanisa na kuchukue kile mitume walichokifanya kwenye biblia…

Matendo 2: 37 “Walipoyasikia haya wakachomwa mioyo yao, wakamwambia Petro na mitume wengine, Tutendeje, ndugu zetu?
38 Petro akawaambia, Tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo, mpate ondoleo la dhambi zenu, nanyi mtapokea kipawa cha Roho Mtakatifu.”


Hivyo ndugu hizi ni siku za mwisho, huu ni wakati wa kuhakikisha nywele zako zinakuwa, tafuta uhusiano wako binafsi na Mungu, Rudi kwenye Neno la Mungu, dini na madhehebu hayatakufikisha popote, kumbuka watakaokwenda kwenye unyakuo ni wachache biblia inasema hivyo..Je! umezaliwa mara ya pili? Kwa kubatizwa na kupokea Roho Mtakatifu.?

Mungu akubariki.

Tafadhali “share” kwa wengine ujumbe huu.

Kwa mpangilio mzuri wa masomo haya tembelea website yetu >>> www.wingulamashahidi.org

UNAFANYA NINI HAPO?


1Wafalme 19: 9 Akafika kunako pango, akalala ndani yake. Na tazama Neno la BWANA likamjia, naye akamwambia, UNAFANYA NINI HAPA ELIYA?.
10 Akasema nimeona wivu mwingi kwa ajili ya BWANA Mungu wa majeshi ; Kwa kuwa wana wa Israeli wameyaacha maagano yako, na kuzivunja madhabahu zako, na kuwaua manabii wako kwa upanga; nami nimesalia mimi peke yangu; nao wanitafuta roho yangu, waiondoe.
11 Akasema, toka, usimame mlimani mbele za BWANA. Na tazama BWANA akapita; upepo mwingi wa nguvu ukaipasua milima, ukaivunjavunja miamba mbele za BWANA; Lakini BWANA hakuwamo katika upepo ule; Na baada ya upepo tetemeko la nchi; lakini BWANA hakuwamo katika lile tetemeko la nchi;
12 Na baada ya tetemeko la nchi kukawa na moto; Lakini BWANA hakuwamo katika moto ule; Na baada ya moto sauti ndogo ya utulivu.
13 Ikawa Eliya alipoisikia, alijifunika uso wake katika mavazi yake, akatoka, akasimama mlangoni mwa pango. Na tazama sauti ikamjia, Kusema, UNAFANYA NINI HAPA, ELIYA ?.

Tukirudi nyuma kidogo katika habari hii, tunasoma kabla ya Eliya kukimbilia mlima Horebu alienda kuwaua wale manabii wa Baali , baada ya kuona Israeli yote imekengeuka kwa kuigeukia miungu migeni, lakini pamoja na kuwaua hao, akapata taarifa nyingine kuwa malkia, [mke wa mfalme Ahabu aliyeitwa Yezebeli] anataka kumwangamiza yeye naye kama alivyowaua manabii wa baali, Kumbuka Yezebeli alikuwa ni mkatili sana alifanikiwa kuwaangamiza manabii wengi wa Mungu waliokuwa Israeli kwa wakati ule, na baadhi yao waliosalia walikuwa wanaishi kwa kujifichaficha mapangoni siku zote za maisha yao.

Hivyo njia pekee Eliya aliyoiona ya kupata suluhisho la mambo yote ni kukimbilia katika mlima wa Mungu uliokuwa mbali sana na Israeli, [Ni ule ule mlima ambao Mungu alisema na wana wa Israeli hapo kwanza] akae huko ajitete mbele za Mungu. Na ndio ule ule Mlima Mungu aliomwitia Nabii Musa ampe yale maagizo na sheria kwa wana wa Israeli kwamba wayashike siku zote za maisha yao, Sasa mlima huo ulikuwa ukijulikana kama mlima mtakatifu wa Mungu kwa wakati ule, ndio unaoitwa mlima Sinai au mlima Horebu.

Hivyo Eliya kwa kufikiria kwake aliona ni vema amwendee Mungu, kama Musa alivyomwendea, kwa kufuata kanuni zile zile,..Na ndio maana tunaona Eliya alifunga siku 40 usiku na mchana bila kula wala kunywa chochote, jambo ambalo Musa alilifanya. Akijua kuwa kule Mungu atazungumza naye kama alivyozungumza na Musa, pengine ataitikisa dunia tena na kuikomboa Israeli kwa Ishara na mapigo makubwa kutoka kwa ile miungu ya kipagani [ma-baali] aliyoacha Israeli kama kipindi kile Bwana alivyofanya kule Misri..Alifika mpaka kilele cha mlima Sinai na kukaa kule, katika pango mojawapo, akingoja Bwana azungumze naye. Na ni kweli tunasoma Bwana alishuka na kuzungumza naye kama alivyozungumza na Musa.

Ndipo sauti ya Mungu isiyoambatana na chochote ikasema naye na kumuuliza, ELIYA UNAFANYA NINI HAPA?. Lakini Eliya hakuielewa kwasababu matarajio yake hayakuwa hayo!!, yeye alitazamia Mungu atazungumza naye kwa moto, na tufani na upepo wa kisulisuli kama alivyofanya kwa Musa mtumishi wake na kwa wana wa Israeli zamani zile kwenye mlima huo huo.. Lakini baada ya kitambo kidogo Bwana akamwambia Eliya toka usimame nje! Utazame uone,…

Ndipo Mungu akapita kwa UPEPO mwingi sana uliopasua miamba, na MATETEMEKO, na MOTO kama Eliya alivyotazamia, kwa mfano ule ule aliojidhihirisha kwa wana wa Israeli na kwa Musa..Lakini pamoja na ishara zote hizo na maajabu yote yale Eliya alipata ufahamu na kugundua kuwa kuna kitu hakipo sawa kwenye hizo ishara zote kadhalika na kwenye ule mlima …

Na ndipo Mungu akazungumza naye tena kwa mara ya pili kwa sauti ya utulivu na kumuuliza.. ELIYA UNAFANYA NINI HAPA?, Hapo ndipo alipogundua ile ilikuwa ni sauti ya Mungu inayosema naye, hivyo kwa aibu na kwa hofu akijifunika uso wake jambo ambalo hapo mwanzo hakufanya iliposema naye kwa maneno hayo hayo!!.. Alipogundua kuwa Mungu hayupo katika mlima Sinai uwakao moto, Mungu hayupo katika matetemeko, Mungu hayupo katika upepo wa kisulisuli na tufani, Mungu hayupo katika nguzo ya moto, Mungu hayupo katika Wingu, Mungu hayupo katikati ya kijiti kinachowaka moto, Mungu hayupo katika mvua ya mawe..Alitambua kuwa Mungu yupo katika SAUTI NDOGO YA UTULIVU, Kwamba hata ishara zile wana wa Israeli Mungu alizokuwa anawaonyesha kule jangwani hazikuwa uthibitisho wa kuwa Mungu alikuwa katikati yao, Mungu alizutumia zile kama ishara tu, ili wamwamini atakapotaka kuzungumza nao wamsikie.. Eliya aliligundua hilo. Zile SHERIA Mungu alizompa Musa ndio iliyokuwa SAUTI NDOGO YA UTULIVU iliyokuwa inasema mioyoni mwao, > usiabudu miungu mingine, waheshimu baba yako na mama yako, usiue, usiibe, n.k..

Hivyo mtu yeyote ambaye angezitii zile sheria hata asingeona ishara yoyote ile, Mungu angekuwa katikati yake, angekuwa ameisikia sauti ndogo ya Mungu ya utulivu..Lakini wengi wao waliona upepo, na matetemeko, na moto, na bahari kugawanyika, na miamba kutoa maji, lakini hawakuitambua sauti ya Mungu iliyokuwa inazungumza nao katikati yao, walidhani kuwa ile zile ishara ndio utimilifu wa wote wa Mungu, mwisho wa siku wengi wakaangamia jangwani.

Kadhalika na katika wakati wetu huu wa agano jipya Kanisa lilipoanza tunasoma katika ile siku ya Pentekoste [Ambao ndio mlima Sinai wetu], Mungu alishusha vipawa na ishara nyingi katikati ya wateule wake, Bwana alishuka na UPEPO wa KISULISULI kama ulivyowashukia wana wa Israeli kule jangwani na Eliya, Soma;

Matendo 2: 1 Hata ilipotimia siku ya Pentekoste walikuwako wote mahali pamoja. 2 Kukaja ghafula toka mbinguni uvumi kama uvumi wa UPEPO wa nguvu ukienda kasi, ukaijaza nyumba yote waliyokuwa wameketi. 3 Kukawatokea ndimi zilizogawanyikana, kama NDIMI ZA MOTO uliowakalia kila mmoja wao. 4. Wote wakajazwa Roho Mtakatifu, wakaanza kusema kwa lugha nyingine, kama Roho alivyowajalia kutamka.

Unaona hapo? siku ile ya Pentekoste, Moto ulishuka kama ndimi za moto ukakaa juu ya watu, karama tofauti tofauti zikaanza kujionyesha katikati ya watu, wakaanza kunena kwa Lugha mpya, watu wakaanza kutabiri, miujiza na ishara zisizokuwa za kawaida zikafanyika katikati ya watakatifu, nchi ikatikiswa kwa matetemeko ya nguvu za Roho wa Mungu (Soma Matendo 4:23-31)…Lakini Mungu hakuwepo katikati ya hivyo vitu vyote, Mungu aliviruhusu viwepo kama ishara tu ya watu kuwa tayari kumsikia ni kati gani anataka kusema katikati yao. 
Hivyo lile kundi dogo lililokuwa limekusudiwa kumwona Mungu baada ya zile ishara, na maajabu liliisikia ile sauti ndogo ya utulivu na ndio maana tunaona katika ile siku tu ya kwanza ya Pentekoste watu walipokuwa wanazistaajabia zile ishara kuona watu wanashukiwa na ndimi za moto, na kuzungumza katika lugha nyingine mbali mbali ndipo wale watu wakamwambia Petro na mitume wengine, sasa tutendeje ndugu zetu?...Ndipo Petro akawajibu,

Matendo 2: 37 Walipoyasikia haya wakachomwa mioyo yao, wakamwambia Petro na mitume wengine, tutendeje, ndugu zetu? 38 Petro akawaambia TUBUNI, MKABATIZWE KILA MMOJA KWA JINA LAKE YESU KRISTO, MPATE ONDOLEO LA DHAMBI ZENU, NANYI MTAPOKEA KIPAWA CHA ROHO MTAKATIFU.

Unaona hapo, wale watu hawakumwambia Petro moto huu ni wa ajabu, upepo huu ni wa kipekee,Hakika Mungu kaonekana, Mungu kajifunua, Mungu ni mwema, leo katutembelea haleluya hapana.! Bali wao moja kwa moja walimuuliza Petro na mitume wenzake, TUTENDEJE NDUGU ZETU?.. Na ndipo ile sauti ndogo ya Mungu ya utulivu ikawaambia “TUBUNI” maana yake ni Geukeni mwache njia zenu mbaya .. Kama tu vile ile sauti ndogo ya utulivu ilivyomwambia Eliya kule mlima, UNAFANYA NINI HAPA ELIYA? “RUDI” KATIKA NJIA YA JANGWA, [maana ya kurudi ni kugeuka urudi ulikotoka].

Lakini katika hichi kipindi cha siku za mwisho, kile ambacho Bwana Yesu alisema katika Mathayo 7:22 Wengi wataniambia siku ile, Bwana, Bwana, hatukufanya unabii kwa jina lako, na kwa jina lako kutoa pepo, na kwa jina lako kufanya miujiza mingi?. 23 Ndipo nitawaambia dhahiri, sikuwajua ninyi kamwe; ondokeni kwangu, ninyi mtendao maovu.” …Kimeshindwa kuisikia sauti ya Mungu inayonena katika utulivu badala yake kimeng’ang’ana na yale madhihirisho ya Roho kwamba ndio uthibitisho kuwa Mungu yupo katikati yao.

Ndugu yangu, ikiwa leo hii utadhani Mungu yupo katika karama yoyote uliyonayo, ukidhani kuwa kunena kwa lugha ndio uthibitisho kwamba umepokea kweli ubatizo wa Roho Mtakatifu, au kufanya miujiza, au kutoa pepo, ndio uthibitisho kwamba Mungu yupo na wewe, huku umeiweka kando ile sauti ya Mungu inayozungumza na wewe kwa utulivu na upole inayokuambia UACHE DHAMBI, NA UTUBU, UKABATIZWE KATIKA UBATIZO SAHIHI, wa jina la YESU KRISTO, Hutaki kuisikia, basi fahamu kuwa utakuwa umepotea bila hata wewe mwenyewe kujijua. 
Kama Leo hii hutaki kusikia Neno la Mungu, habari za TOBA na UTAKATIFU kwako hazina maana sana, wewe unachokifuata kanisani ni Upepo wa kisulisuli, na matetemeko na hisia za kiroho pamoja na moto wa Roho Mtakatifu na miujiza na uponyaji, ni kweli hivyo vinapaswa viwepo kanisani, na ni lazima kanisa liambatane navyo, lakini ile sauti ya Mungu iliyosema na Eliya hapo mwanzo bado itaendelea kusema na wewe ndani yako siku zote, UNAFANYA NINI HAPA? UNAFANYA NINI KATIKA DHAMBI??

Ni kitu gani unachokwenda kukitafuta katika nyumba ya Mungu, ni miujiza tu,? ni ishara? Ni uponyaji? Ni kufunguliwa biashara yako?, ni kuombewa upate mtoto?, ni Kufunguliwa upate mume/mke?, ni kuombewa tu ufaulu shuleni?. Ndugu kama ni mojawapo ya hayo ndio yanayokupeleka huko ukidhani kuwa Mungu kukufanikisha katika hivyo ndio uthibitisho kwamba yupo na wewe, basi hujaisikia bado sauti ya Mungu, yeye alisema wazi kabisa,“mtu asipozaliwa mara ya pili hawezi kuuona ufalme wa mbinguni Yohana 3:3” na kuzaliwa mara ya pili ni KUTUBU (KUGEUKA) kwa kumaanisha kuacha maisha uliyokuwa unaishi ya kale, ya ulevi, uasherati, usengenyaji, ushirikina, kutokusamehe, ya chuki, ya wivu, ya ugomvi, ya utukanaji,maisha ya anasa, maisha ya uvaaji vimini, na suruali, maisha ya upakaji wanja na lipstiki na uvaaji mawigi na hereni, maisha ya ibada za sanamu na uvuguvugu.

Na baada ya kugeuka, hatua inayofuata ni kubatizwa katika ubatizo sahihi wa maji mengi na kwa Jina la Yesu Kristo, ili hatia ya dhambi zako iondolewe mbele za Mungu na kisha Bwana mwenyewe atakupa uwezo wa kushinda dhambi kwa kupitia Roho wake Mtakatifu katika wakati uliobakia wa maisha yako.

Ndugu sauti ndogo leo ya utulivu inazungumza nawe kupitia maandiko kwamba hakuna mtu atakayemwona Mungu asipokuwa na huo UTAKATIFU, (waebrania 12:14.). Isikie sauti ya Mungu sasa inayosema katika kanisa lake na sio ishara, miujiza, maono, ndoto, uponyaji, n.k…Ukivifuata hivyo kanisani, bado ile sauti itakuuliza FULANI UNAFANYA NINI HAPA?..mimi sipo huko, nipo katika sauti ndogo ya utulivu..

Na kama ni ya utulivu basi ni rahisi kuidharau. Ni maombi yangu ndugu yangu sisi sote tusiiache itupite, Bwana atupe masikio ya kuisikia inaposema nasi katika Neno lake na sio katika miujiza. Hizi ni siku za mwisho tuwe macho.

Mungu akubariki.

Tafadhali “share” kwa wengine ujumbe huu.

Kwa mpangilio mzuri wa masomo haya tembelea website yetu hii >>> www.wingulamashahidi.org

Monday, August 27, 2018

UMETEKWA NA UPENDO WA KRISTO?

Ni rahisi kudhania kuwa mtu akizaliwa mara ya pili, basi anakuwa anampenda sana Mungu kiasi kwamba kukitokea kitu mfano shida, au tabu,au magonjwa, au dhiki na kadhalika anakuwa yupo tayari kupambana nacho ili asimwache Mungu wake au asimkane Kristo,..yaani kwa jinsi anavyompenda Bwana hataweza kuruhusu tabu zimtenge na yeye kama tunavyosoma ilivyoandikwa katika maandiko haya;

Warumi 8: 31 “Basi, tuseme nini juu ya hayo? Mungu akiwapo upande wetu, ni nani aliye juu yetu?
32 Yeye asiyemwachilia Mwana wake mwenyewe, bali alimtoa kwa ajili yetu sisi sote, atakosaje kutukirimia na mambo yote pamoja naye?
33 Ni nani atakayewashitaki wateule wa Mungu? Mungu ndiye mwenye kuwahesabia haki.
34 Ni nani atakayewahukumia adhabu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea.
35 NI NANI ATAKAYETUTENGA NA UPENDO WA KRISTO? Je! Ni dhiki au shida, au adha, au njaa, au uchi, au hatari, au upanga?
36 Kama ilivyoandikwa, ya kwamba, Kwa ajili yako tunauawa mchana kutwa, Tumehesabiwa kuwa kama kondoo wa kuchinjwa.
37 Lakini katika mambo hayo yote tunashinda, na zaidi ya kushinda, kwa yeye aliyetupenda.
38 Kwa maana nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo,
39 wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote HAKITAWEZA KUTUTENGA NA UPENDO WA MUNGU ULIO KATIKA KRISTO YESU BWANA WETU.”

Je! Ni kweli hiyo ndiyo maana halisi ya hiyo mistari hapo juu kwamba sisi tunao uwezo wa kupambana na dhiki, tabu, na mateso kwasababu ya upendo wetu mwingi kwa Kristo?. Jibu ni hapana, hakuna mwanadamu yeyote mwenye upendo wa kiwango hicho, ni muhimu kufahamu maana ya huo mstari hapo juu, Biblia inasema JE! NI NANI ATAKAYETUTENGA NA UPENDO WA KRISTO?..Unaona hapo, inasema ni UPENDO WA KRISTO na sio UPENDO WETU SISI KWA KRISTO.

Kuna tofuati kati ya upendo wetu sisi kwa Kristo, na upendo wa Kristo kwetu sisi.

Mtu anapozaliwa mara ya pili kweli kweli [Tutakuja kuona huko mbeleni mtu anazaliwaje mara ya pili], Kuanzia huo wakati na kuendelea ule Upendo wa Kristo unaingia ndani yake, huo sio upendo wake[huyo mtu] kwa Kristo, hapana! bali Upendo wa Kristo kwake. Hivyo Bwana Yesu ndiye anayekuwa anachukua jukumu lote la kuhakikisha ule upendo wake kwako unadumu milele haupotei kwa namna yoyote ile.

Hivyo kuanzia huo wakati linapotokea jambo lolote juu yako mfano iwe ni dhiki, shida, njaa, hatari, adha, upanga n.k. Ni Yesu Kristo ndiye anayehakikisha wewe haujitengi na yeye, na sio wewe utakayehakikisha kwamba hujitengi na yeye. Watu wanaojaribu kufanya hivyo, kwa kujizuia kwa akili zao kutokujitenga na Kristo hawafiki mbali, wanajikuta wanaanguka na watu wa namna hiyo huwa bado hajazaliwa mara ya pili.

Mtume Paulo anasema, … 38 Kwa maana nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo,
39 wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote HAKITAWEZA KUTUTENGA NA UPENDO WA MUNGU ULIO KATIKA KRISTO YESU BWANA WETU.”

Hii ni faida kubwa sana kwa mtu aliyezaliwa kweli kweli mara ya pili, Unakuwa UMETEKWA na UPENDO WA YESU KRISTO mwenyewe, ndio hapo unakuta dhiki inapomjia mtu wa namna hiyo kwamfano, shetani anapomjaribu kwa misiba, badala ya yeye kufarijiwa yeye ndio anawafariji wengine, anapokuwa katika magonjwa ya kufisha, badala amkufuru Mungu yeye ndiye anaonekana mwenye tumaini kushinda hata mtu aliye na mzima, kama vile Ayubu, utashangaa mtu wa namna hiyo anapita katika hali ya kupungukiwa kupita kiasi na njaa lakini bado anafuraha na kumshukuru Mungu, mpaka watu wa nje wanamshangaa ni mtu wa namna gani, yupo katika hali kama hizi lakini bado anashikamana na Mungu wake,

Kadhalika utakuta mtu mwingine [tunawazungumzia waliozaliwa kweli kweli mara ya pili] ni tajiri, lakini hauangalii na kuutumainia utajiri wake kama ni kitu cha thamani sana katika maisha yake, mpaka watu wengine wa nje wanamshangaa wanasema tungekuwa na mali kama za kwako dunia nzima ingetujua, tungetembelea magari ya thamani, tungetia heshima, lakini mtu kama Ayubu pamoja na utajiri wake alisema maneno haya,

Ayubu 31: 25 “Kama nilifurahi kwa kuwa mali yangu yalikuwa mengi, Na kwa sababu mkono wangu umepata vitu vingi; ….28 Hilo nalo lingekuwa uovu wa kuadhibiwa na waamuzi; Kwani ningemwambia uongo Mungu aliye juu. “

Unaona sasa uwezo wa namna hiyo, wa kuweza kuendana nayo na kushinda mambo yote hayo pasipo kumwacha Mungu, sio kwa jitihada za mtu binafsi kupambana na hizo hali, hilo haliwezekani kwa mtu yeyote Yule, hiyo ni YESU KRISTO mwenyewe ndio anafanya ndani ya mtu ili kuhakikisha kwamba hakupotezi wewe kipenzi chake, haungamii, hivyo tatizo linapokuja, kabla ya kukufikia wewe, linawasili kwanza kwake, kisha analipatia utatuzi, ndipo litakaposhuka kwako, na litakaposhuka linakuja na dawa madhubuti ya kulishinda, Uwezo wa kipekee unatoka kwa Mungu, na nguvu ya kushinda majaribu na mitikisiko yote..

Ndio hapo watu wa nje watakushangaa unawezaje kushinda hayo yote?, unawezaje kukaa katikati ya jamii ya wazinzi na wewe sio mmojawao?, unawezaje kuwa katika hali ya kutokuwa na pesa lakini bado unamtumikia Mungu, na unayo amani?, Unawezaje kuwa mgonjwa lakini unawaombea wengine, na hauna hofu ya kufa? Unawezaje kuwa na mali na usitamani anasa za ulimwengu huu, wala kiburi, unawezaje kuwa mzuri na bado huvai mavazi yasiyo na heshima n.k…Hawajui kwamba hayo yote hayatokani na upendo wako wewe kwa Mungu..hapana bali yanatokana na UPENDO wa KRISTO kwako .. Yeye ndiye anayefanya juu chini, wewe usipotee katika hizo njia mbovu na majaribu..kama biblia inavyosema:

Zaburi 125: 1 “Wamtumainio Bwana ni kama mlima Sayuni, Ambao hautatikisika, wakaa milele.
2 Kama milima inavyouzunguka Yerusalemu, NDIVYO BWANA ANAVYOWAZUNGUKA WATU WAKE , TANGU SASA NA HATA MILELE. “

Sasa karama hii ya UPENDO WA MUNGU KWA MTU, haiji kwa watu wote wa ulimwenguni hapana! Bali inakujua kwa wale tu waliomtumainia yeye {yaani wale tu WALIOZALIWA MARA YA PILI}, wengine ambao hawajazaliwa mara ya pili hawataweza kushinda majaribu na misukosuko, yatakapotokea mawimbi wataanguka tu, zitakapotokea dhiki watakufuru, ikitokea misiba watalaani, hawana raha usiku na mchana, watajitahidi kwa nguvu zao kushinda dhambi na ulimwengu lakini hawataweza, hata wakipata utajiri utawaangamiza, hata wakiwa wagonjwa na maskini watataka kujaribu kuishikilia imani lakini watamkana Kristo, kwasababu hawajazaliwa mara ya pili.

Sasa Kuzaliwa mara ya pili kunakuja kwanza baada ya mtu kutubu dhambi zake, [kumbuka maana ya kutubu ni KUGEUKA], sio kuongozwa sala ya toba, unageuka kwa kudhamiria na kumaanisha kabisa kuacha dhambi zako, kuyaacha ya kale na kuanza maisha mapya kwa Kristo, na baada ya kutubu, bila kukawia hatua inayofuata ni kubatizwa katika ubatizo sahihi wa maji tele, na kwa JINA LA YESU KRISTO, (kulingana na Matendo 2:38), upate ondoleo la dhambi zako, na hatua ya tatu na ya mwisho ni Roho wa Kristo kuingia ndani yako, sasa hapo ndio lile PENDO LA KRISTO linamiminwa ndani yako. Mtu yeyote akiruka hatua yoyote kati ya hizo, bado hajazaliwa mara ya pili..Kumbuka ndugu hii sio dini wala dhehebu ni maagizo ya Bwana Yesu mwenyewe ambayo yapo kwenye biblia.

Biblia inasema wazi kabisa, katika Yohana 3: 5 “Yesu akajibu, Amin, amin, nakuambia, Mtu asipozaliwa kwa maji na kwa Roho, hawezi kuuingia ufalme wa Mungu.”

Sasa kumbuka kuzaliwa kwa maji kunakozungumziwa hapo ndio UBATIZO WA MAJI, na kuzaliwa kwa Roho ndio UBATIZO WA ROHO MTAKATIFU. Hapo ndipo unakuwa umeshazaliwa mara ya pili. Lakini Wapo wengine wanataka kubatizwa lakini hawajadhamiria kuacha maisha yao ya kale ya dhambi, hao hata wakienda kubatizwa wanafanya kazi bure, hakuna chochote kitakachotokea katika maisha yao.. Kadhalika wapo wengine, wametubu lakini hawataki kwenda kubatizwa katika ubatizo sahihi wanasema ubatizo wa maji hauna maana sana hawa nao pia hawataona mabadiliko yoyote katika maisha yao.. Maagizo yote aliyoyatoa Bwana Yesu hakuna hata moja lisilokuwa na maana, alisema aaminiye na kubatizwa atakoka, na sio aaminiye tu peke yake. Hapana bali vyote viwili vinakwenda pamoja.

Hivyo mtu akizingatia hizo hatua zote za yeye kuzaliwa mara ya pili utapokea UWEZO, wa kutokutenganishwa na chochote kile, iwe shida, dhiki, uzima, mauti, raha, malaika, mamlaka, utajiri, kupungukiwa, upanga, misiba, n.k. kwasababu lile PENDO LA YESU KRISTO tayari litakuwa limeshamiminwa ndani yake. Hivyo ANASHINDA siku zote na ZAIDI YA KUSHINDA.

Ubarikiwe.

Tafadhali “share” ujumbe huu kwa wengine na Mungu atakubariki.

Kwa mpangilio mzuri wa masomo haya tembelea website yetu >>> www.wingulamashahidi.org

Thursday, August 23, 2018

WAKATI WA JIONI KUTAKUWAKO NA NURU.

Zekaria 14: 6 “Tena itakuwa siku hiyo, ya kwamba nuru yake haitakuwa na mwangaza na kiwi;
7 lakini itakuwa siku moja, iliyojulikana na Bwana; si mchana, wala si usiku; lakini itakuwa, ya kwamba wakati wa jioni kutakuwako nuru”.

Jaribu kutengeneza picha mfano Inatokea siku moja, wakati wa jioni labda tuseme saa moja hivi muda ambao umezoea kila siku kuona jua likizama ghafla unashangaa kuona mwanga ni ule ule haufifii, tena inafikia saa mbili jioni jambo ni lile lile, kunamulika mwangaza kama wa saa 11 jioni hivi, ni wazi kuwa kwa namna ya kawaida utashangaa sana hiyo siku kimetokea nini?, mbona giza haliingii maana muda wa usiku umeshaanza na sasa ni saa 2 usiku lakini kunaonekana kama saa 11, kwa namna ya kawaida mtu yeyote atakayeliona jambo hilo atashtuka sana.

Kadhalika na katika roho pia Bwana alitabiri itakuja siku moja inayofanana na hiyo, kwamba wakati wa jioni kutakuwa na NURU. Lakini kwa hekima hatuna budi tufahamu huo wakati ni wakati gani, je! Umeshatimia au bado?. Hivyo ili kufahamu ni lazima pia tujue Nuru ni nini na giza ni nini? Na huo wakati wa jioni ni upi?.

Kama tunavyojua nuru ya dunia inaletwa na jua, na hili jua huwa linaangaza katika majira matatu yaani asubuhi, mchana na jioni,..Kadhalika na katika roho Bwana Yesu alisema:

Yohana 8: 12 “…, MIMI NDIMI NURU YA ULIMWENGU, yeye anifuataye hatakwenda gizani kamwe, bali atakuwa na nuru ya uzima”.

Unaona hapo yeye katika roho ndio jua letu lililoanza kuangaza asubuhi, na likaja kuangaza mchana, kadhalika na litaangaza jioni. Kazi yake ni kutia nuru ulimwengu, alianza kutia nuru asubuhi (yaani kanisa la kwanza lilioanza na mitume), akaendelea kutia nuru mchana(yaani katika wakati way ale makanisa 5 yaliyofuata), na akamaliza kuangaza Nuru yake wakati wa jioni (katika kanisa lile mwisho la 7 linaloitwa Laodikia ambalo ndilo hili tunaloishi sasa ). Ufunuo 2 & 3

Na kanisa hili la Laodikia ni wazi kabisa na inajulikana na watu wote kwamba lilianza katika karne ya ishirini, yaani kuanzia mwaka 1906 na kuendelea.. Hivyo sisi wote tuliopo leo tunaishi katika ile NURU ya BWANA ya jioni, kumbuka hakutakuwa na kanisa lingine zaidi ya hili, ni kanisa ambalo litashuhudia kuja kwa pili kwa Kristo. Ilijulikana Katikati ya wakristo wote kuanzia huo wakati wa mwanzoni mwa karne ya karne ya 20 kwamba wao ni WANA WA JIONI, kwasababu walikuwa wanafahamu kabisa ni kweli wanaishi wakati wa jioni kabisa wa nuru ya Kristo kumalizikia.

Sasa katikati mwa karne ya ishirini yaani kipindi cha miaka ya 1940-1980, wakristo wote kutokana na matukio yaliyokuwa yanayaona yakitokea duniani, wakilinganisha na unabii wa kibiblia, walifahamu kuwa karne ile haitaisha bila Kristo kurudi mara ya pili, na ni kweli walikuwa sahihi, ukizingatia kwamba asilimia kubwa wa yale Bwana Yesu aliyoyazungumza katika Mathayo 24 yalitimia katika huo wakati, kwamfano, Bwana alisema.

Kutakuwa na matetemeko ya nchi mahali na mahali, kwa wakati ule yalikuwa ni mengi mno duniani, alisema pia kutakuwa na vita na matetesi ya vita, taifa litaondoka kwenda kupigana na taifa lingine…Jambo ambalo lilionekana wazi katikati ya ile karne ya 20, vita viwili vikubwa vya dunia vilitokea kwa mpigo, jambo ambalo halikuwahi kuonekana hapo kabla katika historia ya dunia, mamilioni ya watu kufa, magonjwa ya ajabu ndio yalianzia kuzuka katika hicho kipindi, kansa, ukimwi, kisukari, Malaria n.k. mambo ambayo Bwana aliyatabiri yatatokea katika siku za mwisho, na kikubwa zaidi kilichowafanya watakatifu wa karne ya ishirini kunyanyua vichwa vyao juu, kama Bwana alivyowaambia katika

Luka 21:28 “Basi mambo hayo yaanzapo kutokea, changamkeni, mkaviinue vichwa vyenu, kwa kuwa ukombozi wenu umekaribia”

Ni kutokea kwa kitendo cha kihistoria katika nchi takatifu Israeli, pale waliposhuhudia taifa la Israeli likichipuka tena baada ya ma-karne ya miaka kupita bila kuwa taifa huru, walishuhudia kuona Israeli kupata uhuru wao tena mwaka 1948 na kuwaona wayahudi wakitoka katikati ya mataifa yote ulimwenguni na kurudi katika nchi yao tena.

Ezekieli 36: 24 “Maana nitawatwaa kati ya mataifa, nami nitawakusanya na kuwatoa katika nchi zote, na kuwarudisha katika nchi yenu wenyewe. “

Huko ndiko kuchipuka kwa mtini Bwana Yesu alikokuzungumzia,Maana Taifa la Israeli linafananishwa na MTINI kadhalika pia watakatifu walipokuwa wanaona na miti mingine ikichipuka (yaani mataifa mengine tofauti na Israeli kupata uhuru wao yaani mataifa ya Afrika, Asia na Marekani ya kusini),ambayo hayo yote yalianza kupata uhuru wao mara baada tu ya Israeli kutangazwa kuwa taifa huru, wakilinganisha na maandiko Bwana Yesu aliyoyasema katika..

Luka 21:29 “Akawaambia mfano; Utazameni MTINI na MITI MINGINE YOTE.
30 Wakati iishapo kuchipuka, mwaona na kutambua wenyewe ya kwamba majira ya mavuno yamekwisha kuwa karibu.
31 Nanyi kadhalika, mwonapo mambo hayo yanaanza kutokea, tambueni ya kwamba ufalme wa Mungu u karibu.
32 Amin, nawaambieni, Kizazi hiki hakitapita hata hayo yote yatimie. ”

Hivyo walivyokuwa wanayaona hayo yote yanatimia, walitambua kabisa kwamba karne ya 21 haitafika (yaani miaka ya 2000 haitakuwepo), na walikuwa wapo sahihi kabisa, Sasa kilichotokea na cha kustaajabisha, ni kuona mpaka karne ya 21 inaanza na mwisho bado haujafika…

Na ndio hapo tunarudi kwenye lile andiko letu la msingi..
 
Zekaria 14: 6 “Tena itakuwa siku hiyo, ya kwamba nuru yake haitakuwa na mwangaza na kiwi;
7 LAKINI ITAKUWA SIKU MOJA, ILIYOJULIKANA NA BWANA; si mchana, wala si usiku; lakini itakuwa, YA KWAMBA WAKATI WA JIONI KUTAKUWA NURU”.

Huo wakati ambao Bwana alisema JIONI KUTAKUWA NA NURU, ndio huu tunaoishi sasa (wakati huu wa karne ya 21), Mambo yote yalipaswa yaishe tokea karne ya 20, lakini kwa jinsi Mungu alivyokuwa wa rehema na neema, hataki mtu yeyote apotee bali wote waifikilie toba, akalazimika kuisimamisha NURU ya ulimwengu isizame ( yaani Neema ya Yesu Kristo isiishe) katika hichi kipindi cha wakati wa jioni wa kumalizia..
 
Ndugu yangu mwisho ungepaswa uwe umeshafika siku nyingi, moja ya hizi siku mambo yote yatabadilika ghafla, kama vile jua linavyokaribia kuzama kidogo kidogo giza linaingia..ndivyo walivyoweza kutambua watu wa karne ya 20, lakini sisi tunaoishi katika Hii NURU ya nyiongeza (watu wa karne ya 21), tupo katika hatari kubwa sana kwasababu Nuru hii haitadumu kwa kipindi kirefu, kadhalika na haitabiriki, siku ya kuondoka kwake haitakuwa taratibu taratibu tena kama mwanzo, hapana, bali itaondoka kwa ghafla, na saa hiyo hiyo giza nene sana litaikumbuka dunia (huo ndio uharibifu wake)…

Ndio lile neno litatimia 1Wathesalonike 5: 1 “Lakini, ndugu, kwa habari ya nyakati na majira, hamna haja niwaandikie.
2 Maana ninyi wenyewe mnajua yakini ya kuwa siku ya Bwana yaja kama vile mwivi ajavyo usiku.
3 WAKATI WASEMAPO, KUNA AMANI, NA SALAMA, NDIPO UHARIBIFU UWAJIAPO KWA GHAFULA, kama vile utungu umjiavyo mwenye mimba, wala hakika hawataokolewa. “

Watu wengi wametokea badala ya kumkaribia Mungu awape neema ndio kwanza wanaanza kudhihaki, wakisema hakuna kitu kama hicho kurudi kwa Yesu, Yesu harudi leo wala kesho, miaka na miaka mambo yapo vilevile hawajui kwamba wanaishi katika muda wa nyiongeza wa ILE NURU YA JIONI.. ili watubu..

1Petro 3: 1 “Wapenzi, waraka huu ndio wa pili niwaandikiao ninyi; katika zote mbili naziamsha nia zenu safi kwa kuwakumbusha,
2 mpate kuyakumbuka yale maneno yaliyonenwa zamani na manabii watakatifu, na ile amri ya Bwana na Mwokozi iliyoletwa na mitume wenu.
3 Mkijua kwanza neno hili ya kwamba KATIKA SIKU ZA MWISHO WATAKUJA NA DHIHAKA ZAO WATU WENYE KUDHIHAKI, WAFUATAO TAMAA ZAO WENYEWE,
4 na kusema, IKO WAPI AHADI ILE YA KUJA KWAKE? Kwa maana, tangu hapo babu zetu walipolala, vitu vyote vinakaa hali iyo hiyo, tangu mwanzo wa kuumbwa.
5 Maana hufumba macho yao wasione neno hili ya kuwa zilikuwako mbingu tangu zamani, na nchi pia, imefanyizwa kutoka katika maji, na ndani ya maji, kwa neno la Mungu;
6 kwa hayo dunia ile ya wakati ule iligharikishwa na maji, ikaangamia.
7 Lakini mbingu za sasa na nchi zimewekwa akiba kwa moto, kwa neno lilo hilo, zikilindwa hata siku ya hukumu, na ya kuangamia kwao wanadamu wasiomcha Mungu.
8 Lakini, wapenzi, msilisahau neno hili, kwamba kwa Bwana siku moja ni kama miaka elfu, na miaka elfu ni kama siku moja.
9 BWANA HAKAWII KUITIMIZA AHADI YAKE, kama wengine wanavyokudhani kukawia, bali huvumilia kwenu, MAANA HAPENDI MTU YE YOTE APOTEE, BALI WOTE WAFIKILIE TOBA.
10 Lakini siku ya Bwana itakuja kama mwivi; katika siku hiyo mbingu zitatoweka kwa mshindo mkuu, na viumbe vya asili vitaunguzwa, na kufumuliwa, na nchi na kazi zilizomo ndani yake zitateketea.
11 Basi, kwa kuwa vitu hivi vyote vitafumuliwa hivyo, imewapasa ninyi kuwa watu wa tabia gani katika mwenendo mtakatifu na utauwa,
12 mkitazamia hata ije siku ile ya Mungu, na kuihimiza; ambayo katika hiyo mbingu zitafumuliwa zikiungua, na viumbe vya asili vitateketea na kuyeyuka? "

Unaona ndugu,..tunaishi wakati wa muda wa nyongeza muda wa ile siku iliyojulikana na Bwana, wakati wa jioni, wakati wa NURU YA NEEMA. Je! Bado unaishi katika dhambi? Bado hujazaliwa mara ya pili? Utajitetea vipi siku ile pamoja na huu muda wa nyongeza uliopewa katika hili giza lililopo duniani, utatoa udhuru gani mbele ya hukumu. Kumbuka baada ya hii nuru kuondoka, (ambayo itaisha na UNYAKUO), kutakuwa kumebakia miaka saba tu mpaka dunia kuisha, huko ndiko ile dhiki kuu ya mpinga-kristo pamoja yale mapigo yote yaliyoandikwa katika kitabu cha ufunuo 8 & 16 yatatimia, kisha baada ya hapo itakuja hukumu na kisha ziwa la moto.

Kama hujatubu kwa kumaanisha kuziacha dhambi zako, fanya hivyo leo, ukabatizwe katika ubatizo sahihi wa kuzamishwa katika maji tele na kwa jina la YESU KRISTO upate ondoleo la dhambi zako (kulingana na Matendo 2:38), na Bwana atakupa kipawa cha Roho Mtakatifu..

Bwana akubariki sana.

Tafadhali “share ” ujumbe huu kwa wengine na Bwana atakubariki.

Kwa mpangilio mzuri wa masomo haya, tembelea >>> wingulamashahidi.org