"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Monday, September 10, 2018

MASWALI NA MAJIBU: SEHEMU YA 37



 SWALI 1:Matendo ya mitume2:1"Hata ilipotimia "SIKU YA PENTEKOSTE" walikuwako wote mahali pamoja.Ndugu zangu hiyo Siku ya Pentekoste ilikuwa ni siku gani? Pentekoste ilimaanisha nini ndugu.?

JIBU: Pentekoste ni neno la kigiriki lenye maana “YA HAMSINI” . Hivyo kwa wayahudi walikuwa wanasherekea siku ya hamsini baada ya sikukuu ya pasaka (waliagizwa na Bwana wafanye hivyo) lakini wenyewe walikuwa hawaiiti kwa jina hilo la pentekoste, walikuwa wanaiita hiyo sikukuu kama “SIKU KUU YA MAJUMA”.
Bwana Mungu aliwaambia wahesabu majuma 7 yaani sabato 7 baada ya pasaka, yaani siku 49, na siku ya hamsini ( ndiyo pentekoste) wafanye sikukuu…Soma(Kumbu. 16:9 na Walawi 23:15).

Kwahiyo sasa kwasababu mambo yaliyokuwa yanafanyika agano la kale yalikuwa ni kivuli cha agano jipya, ilikuwa ni lazima sikukuu hizo ziwe na uhusiano mkubwa na mambo ya agano jipya,. Kwahiyo wayahudi pasipo kujua lolote walishangaa Roho Mtakatifu anashuka juu yao siku ile ile ya Pentekoste ambayo walikuwa wanasheherekea hiyo siku kuu yao ya Majuma, kama tu kusulibiwa kwa Bwana kulivyoangukia katika siku kuu yao ya pasaka kadhalika kumwagwa kwa Roho kuliangukia katika siku kuu yao ya majuma (yaani pentekoste). Na ilikuwa ni siku ya HAMSINI baada ya sikukuu ya Pasaka.
SWALI 2: Naomba kujua utofauti wa ZAKA/FUNGU LA KUMI na SADAKA Utofauti wao niupi?

JIBU: ZAKA/FUNGU LA KUMI Ni moja ya kumi au sehemu ya kumi ya mapato yako yote, hicho huwa kinakwenda kwa Bwana na ni wajibu kwa kila mkristo mwenye shughuli ya kujipatia kipato kumtolea MUNGU sehemu hiyo ya mapato yake..

Walawi 27: 30 Tena zaka yote ya nchi, kama ni mbegu ya nchi, au kama ni matunda ya nchi, ni ya Bwana; ni takatifu kwa Bwana. Malaki 3: 8 Je! Mwanadamu atamwibia Mungu? Lakini ninyi mnaniibia mimi. Lakini ninyi mwasema, Tumekuibia kwa namna gani? Mmeniibia zaka na dhabihu. 9 Ninyi mmelaaniwa kwa laana; maana mnaniibia mimi, naam, taifa hili lote. 10 Leteni zaka kamili ghalani, ili kiwemo chakula katika nyumba yangu, mkanijaribu kwa njia hiyo, asema Bwana wa majeshi; mjue kama sitawafungulia madirisha ya mbinguni, na kuwamwagieni baraka, hata isiwepo nafasi ya kutosha, au la. 11 Nami kwa ajili yenu nitamkemea yeye alaye, wala hataharibu mazao ya ardhi yenu; wala mzabibu wenu hautapukutisha matunda yake kabla ya wakati wake katika mashamba, asema Bwana wa majeshi.

Sasa fungu la kumi au zaka ni tofauti na ‘sadaka/matoleo’. SADAKA yenyewe ni kile ulichonacho juu ya fungu la kumi, kile ulichokirimiwa pasipo sharti lolote la utoaji unampelekea Mungu, sasa zipo sadaka za aina tofauti tofauti kulingana na mahali au mtu mwenyewe, kwa mfano zipo.

1) sadaka za shukrani, hizi huwa mtu anatoa baada ya Mungu kumtendea au kumfanikisha katika jambo Fulani, aidha, afya, ulinzi, masomo, biashara, kazi, familia, n.k. Huwa anaambatanisha sadaka yake ya shukrani mahali Bwana anapolia kiroho ni tofauti na fungu la kumi. 
2) Zipo sadaka nyingine za michango: Hizo zipo nyingi kulingana na uhitaji wa kanisa, mfano jengo, uenezaji injili, vyombo vya nyumba ya MUNGU, mahitaji n.k. Hivyo sadaka/matoleo yapo ya aina nyingi, na pia Mungu hajaweka sharti lolote la utoaji ni jinsi mtu atakavyoguswa moyo na Mungu wake, ndicho atakachotoa.

Kutoka 35: 5 Katwaeni kati yenu matoleo kwa Bwana; mtu awaye yote aliye na moyo wa kupenda, ayalete matoleo; dhahabu na fedha na shaba;

Kwahiyo jambo la kukumbuka pia katika agano jipya, ni kwamba Mungu hajamwekea mtu sheria au tanzi yoyote katika kutoa ZAKA hata kama hajisikii tu atoe , hapana hiyo haipo katika Ukristo kwasababu Mungu hapendezwi na mtu atoaye kwa moyo wa huzuni au wa kulazimishwa. Lakini ni vizuri pia ikumbukwe kuwa ni wajibu wa kila mkristo yoyote kumtolea MUNGU wake aliyemuokoa. Ni ngumu kwa mtu yeyote kusema amejazwa Roho halafu suala la utoaji kwake ni mzigo.

2Wakorintho 9: 7 Kila mtu na atende kama alivyokusudia moyoni mwake, si kwa huzuni, wala si kwa lazima; maana Mungu humpenda yeye atoaye kwa moyo wa ukunjufu. 8 Na Mungu aweza kuwajaza kila neema kwa wingi, ili ninyi, mkiwa na riziki za kila namna siku zote, mpate kuzidi sana katika kila tendo jema; 9 kama ilivyoandikwa, Ametapanya, amewapa maskini, Haki yake yakaa milele.




 SWALI 3:Maana yake ni nini Bwana anaposema""Maana wako 1.MATOWASHI-waliozaliwa hali hiyo toka MATUMBONI MWA MAMA ZAO;""Tena wako 2.MATOWASHI-waliofanywa na WATU kuwa matowashi; tena wako 3.MATOWASHI-WALIOJIFANYA KUWA MATOWASHI KWAAJILI YA UFALME WA MBINGUNI.Awezaye kulipokea neno hili,na alipokee.

JIBU: Matowashi ni watu waliojitoa wakfu kwa Mungu, wasiojihusisha na mambo ya wanawake,(yaani kuwa na mke au watoto), mfano wa matowashi katika biblia ni Bwana wetu Yesu, Mtume Paulo,Barnaba, Yohana mbatizaji na Eliya Mtishbi.

Sasa wapo wa aina tatu, wapo ambao tangu kuzaliwa tumboni mwa mama zao Mungu aliwaumba hivyo, hawana uwezo wa kuzalisha, wengi miongoni mwa hao Mungu amewachagua wawe wakfu kwake…kwa ajili ya utumishi wake.

Kadhalika wapo wengine wamehasiwa, hao ndio waliofanywa na watu kuwa hivyo kwa ajili ya ufalme wa mbinguni…

Na pia wapo ambao wameamua kujifanya wenyewe kuwa matowashi..hawa hawajahasiwa wala hawana shida yoyote isipokuwa wao wenyewe wameamua kubaki hivyo hivyo wasioe kwa ajili ya ufalme wa mbinguni yaani wajishughulishe na mambo ya ufalme wa mbinguni kwa uhuru zaidi..mfano wa hao ni Bwana wetu Yesu, Mtume Paulo, Barnaba, Yohana mbatizaji, Eliya mtishbi n.k..

Na kama Bwana Yesu alivyosema mtu yoyote awezaye kulipokea neno hilo na alipokee alikuwa anamaanisha kwamba “mtu akitaka kuwa hivyo na awe” ila sio lazima kama kama Mtume Paulo pia alivyosema kwa uweza wa Roho katika 1 Wakorintho 7:26-40.

Na pia kumbuka hiyo ni KARAMA watu wa namna hiyo huwa wanaona mke/mume kwao si kitu cha thamani kubwa sana kama kuwa tu karibu na Mungu. Hawajilazimishi wala kutumia nguvu nyingi kufanya hivyo, tofuati na wengi wanavyodhani.


SWALI 4:Bwana Yesu Kristo anapokataza Mwanamke kumuongoza mwanaume hii inalihusu KANISA tu ndugu?au ni pamoja na Wapagani/Makafiri (mfano Mwanamke kuwa mtawala, raisi au mwalimu wa chuo kikuu kuwafundisha wanaume,au kuwa askari na kumwamrisha mwanaume..Hayo ni sahihi mbele za Bwana?..) 


JIBU: Biblia haijaeleza moja kwa moja nafasi ya mwanamke nje ya “kanisa na familia”….Kama maandiko yanavyosema ndani ya kanisa mwanamke anapaswa kujifunza kwa utulivu, na kutii, na hana ruhusa ya kufundisha na kumtawala mwanamke(1Timothe 2:11)..Kadhalika na katika familia mwanamke anapaswa awe chini ya mwanaume, amtambue kama kichwa cha familia, na kumtii mume wake.


 Lakini nje! Ya kanisa, haijasema lolote kwamba anaweza akawa raisi au waziri, au mbunge n.k. kutokana na kwamba huko nje wapo wapagani, na shughuli zinazofanyika nyingi ni za dunia hii tu, pengine za kujipatia rizki kama ualimu, udaktari, nk zinaweza zinaweza zisiwe ni kosa kwasababu hazihusiani na masula yoyote ya uongozi wa kiroho, lakini pia biblia imetuonywa mienendo yetu kwa watu wa nje inapaswa iwe kielelezo..ikiwa unamweshimu mumeo nyumbani, huwezi ukawa unawavunjia heshima wanaume wengine nje ya nyumba yako.


 Ikiwa una cheo kikubwa mahali ulipo, timiza wajibu wako kama mwanamke wa kikristo, lakini sio kushiriki katika kampeni za dunia hii kwamfano za kutafuta haki sawa, na kujihusisha na kampeni kama za watu wa kiulimwengu ambazo ni kinyume na maagizo ya Mungu.. 


Mfano mzuri wa kuiga kwenye maandiko ni Esta, yeye alikuwa malkia lakini nafasi aliyokuwa nayo hakuigeuza kuwa kama VASHTI ambaye alitumia umalkia wake kuonyesha kiburi mbele ya mume wake mfalme AHASUERO (Esta 1) au ATALIA mtoto wa YEZEBELI, ambaye alijifanya mtawala kwa nguvu baada ya mumewe kufa, na kushughulika kuumaliza uzao wote wa Mungu, (ukisoma 2 Wafalme 11) na kusababisha machafuko makubwa katikati ya nyumba ya Israeli kama vile mama yake Yezebeli alivyokuwa..

Kwahiyo nafasi ya uongozi wa mwanamke nje ya kanisa ni tofauti na ndani ya kanisa.
 

No comments:

Post a Comment