"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Saturday, October 13, 2018

MASWALI NA MAJIBU: SEHEMU YA 39


 SWALI 1: Mfano wa serikali ya kifalme ya Uingereza(United Kingdom):Mahakimu ndio wenye sifa ndio waliopewa mamlaka yakutoa hukumu.Wakiwa katika viti vyao vya enzi vya HUKUMU hawaingiliwi na MFALME(Wakati huo Mfalme atakuwa ameketi katika KITI CHAKE CHA ENZI)..Sasa katika ule Ufalme wetu wa"Kikristo"..Tumeahidiwa sisi WATAKATIFU wenye sifa hiyo ndio waliopewa Mamlaka(MAHAKIMU)ya kuuhukumu ulimwengu,,,Sasa Wakati sisi Watakatifu tukiwa tumeketi katika Viti vya hukumu tukitoa hukumu kama MAHAKIMU,.MFALME wetu Bwana Yesu Kristo hatatuingilia katika hiyo kazi.."YEYE ATAKUWA AMEKETI KWENYE KITI CHAKE CHA ENZI"..Sasa kwakuwa tumefanana na Mungu saa hiyo tutakuwa tunayafahamu maisha ya hao tunaowahukumu Tangu walipoumbwa hadi saa hiyo wanayosimama mbele yetu..Sasa hapo ndipo sisi tutamwambia mtu fulani wewe ulijuwa uasherati ni dhambi kisha ukadhihaki ukaenda kufanya sasa adhabu yako ni ndio hii..kisha tunamuita malaika wa moto anamchukua anampeleka ZIWA LA MOTO kutumikia adhabu yake..JE! hivyo ndivyo ilivyo ndugu.

JIBU: Ubarikiwe kwa swali zuri, lakini kuna jambo la kujifunza zaidi hapo, siku ile tutakapoketi na Bwana kuhukumu, sisi ndio tutafanana na yeye lakini hukumu ya mwisho atatoa yeye peke yake YESU KRISTO. Sisi tutakuwa kama mawakili. Kwa mfano siku ile atasimamishwa mtu aliyekuwa anafanya uasherati, na huku anasema ameokoka, na Bwana atamwuluza kwanini ulikuwa unafanya vile, labda atasema kwasababu kizazi chetu kilikuwa na simu zenye internet hivyo ilikuwa ni ngumu kujizuia, sasa utaitwa wewe Michael ambaye saa hiyo utakuwa pembeni mwa Bwana, na Bwana atakuuliza ilikuwaje wewe uliushinda uasherati katika kizazi cha internet, utatoa sababu pale, sasa zile sababu zako utakazozitoa wewe mtakatifu ndizo zitakazo muhukumu yule mkosaji Unakumbuka yale maneno Bwana Yesu aliyoyasema katika..

Mathayo 12: 41 “Watu wa Ninawi watasimama siku ya hukumu pamoja na watu wa kizazi hiki, nao watawahukumu kuwa wamekosa; kwa sababu wao walitubu kwa mahubiri ya Yona; na hapa yupo aliye mkuu kuliko Yona. 42 Malkia wa kusini atasimama siku ya hukumu pamoja na watu wa kizazi hiki, naye atawahukumu kuwa wamekosa; kwa sababu yeye alikuja kutoka pande za mwisho za dunia ili asikie hekima ya Sulemani, na hapa yupo aliye mkuu kuliko Sulemani”.
 
 Kwa namna hiyo ya malkia wa sheba atakavyokihukumu kizazi kile, ndivyo na sisi tutakavyokihukumu kizazi hichi.
 SWALI 2: Bwana Yesu akubariki ndugu. Naomba unifafanulie huu mstari unamaana gani?...Luka14:26 '' kama mtu akija kwangu naye HAMCHUKII baba yake,na mama yake, na mke wake, na wanawe, na ndugu zake waume na wake; na naam, na hata nafsi yake mwenyewe , hawezi kuwa mwanafunzi wangu ''.

JIBU: Bwana Yesu aliposema yeye “asiyemchukia” baba yake na mama yake, hakumaanisha, kumdharau, au kuweka uadui naye, hapana kwasababu Bwana Yesu hawezi kufundisha upande mmoja upendo na mwingine chuki, bali pale alimanisha kupenda mapenzi ya wazazi au ya mtu binafsi Zaidi ya mapenzi ya Mungu, mtu wa namna hiyo hawezi kuwa mwanafunzi wake.

Leo hii mtu atafahamu kabisa kuwa mlevi au kufanya matambiko ya kimila ni dhambi sawa sawa na Neno lake katika..
 
 Kumbukumbu 18: 10 “Asionekane kwako mtu ampitishaye mwanawe au binti yake kati ya moto, wala asionekane mtu atazamaye bao, wala mtu atazamaye nyakati mbaya, wala mwenye kubashiri, wala msihiri,
11 wala mtu alogaye kwa kupiga mafundo, wala mtu apandishaye pepo, wala mchawi, wala mtu awaombaye wafu.
12 Kwa maana mtu atendaye hayo ni chukizo kwa Bwana; kisha ni kwa sababu ya hayo Bwana, Mungu wako, anawafukuza mbele yako.
13 Uwe mkamilifu kwa Bwana, Mungu wako".

lakini kwasababu mzazi wake anamshurutisha afanye vile kwasababu wazee wa ukoo wameagiza ,na asipofanywa hivyo atatengwa na ukoo, yeye anaamua awe mlevi, au apige ramli ili tu kuwaridhisha wazazi wake. Mtu wa namna hiyo biblia inasema hawezi kuwa mwanafunzi wa YESU.

Kadhalika Bwana anasema mtu asipozaliwa kwa maji na kwa Roho hawezi kuuona ufalme wa mbinguni, lakini mtu kwasababu dini ya wazazi wake haiamini hivyo, anaona vema abaki hivyo hivyo tu, angali akijua kabisa ubatizo sahihi ule wa kuzamishwa katika maji tele tena katika Jina la YESU KRISTO ndio Bwana anaouhitaji kwa mtu kwa ajili ya ondoleo la dhambi zake, lakini yeye hataki kutii akiwaogopa wazazi au ndugu zake..Sasa mtu kama huyu hawezi kuwa mwanafunzi wa YESU.

Na maagizo mengine yote Bwana aliyotupa, hatupaswi tutazame kwanza wanadamu wanatoa maoni gani kuhusu hayo.Kama ni Bwana kasema moja kwa moja tunatii pasipo kuwatazama wanadamu wanasema nini.

Ili kufanyika wanafunzi kweli kweli wa Kristo hatuna budi kuingia gharama, Hivyo Bwana atupe rehema tuweze kuzishinda hatua zote.
 SWALI 3: Tujua kuwa pombe inatengenezwa na mtama Je! ni sawa kwa mkristo wa kweli kulima mtama na kuuza na hata hiyo hela kutolea sadaka?.

JIBU: Hakuna zao lolote lililoumbwa na Mungu lenye ubaya wowote ndani yake, zao linafanyika kuwa baya pale tu linapotumiwa kwa matumizi yasiyo sahihi, kwamfano mtama ni zao la chakula, wengine wanatumia kama ugali, lakini baadhi ya watu wanatumia fursa ya zao hilo ili kuunda pombe.

Hivyo mtu anayeligeuza zao kuwa hivyo , au kupanda kwa ajili hiyo, atakuwa na hatia mbele za Mungu. Lakini zao lenyewe kama zao halina shida kama mtu akilipanda kwa ajili ya matumizi ya asili, kwasababu yapo mazao mengine mengi tu kwamfano zao kama miwa, ambayo ingetumiwa kutengenezea sukari wengine wanaundia pombe, minazi ambayo ingetumika kuzalisha nazi na mafuta wengine wanaigema kutolea pombe, ulezi na ndizi ambazo zingetumika kama chakula wengine wanatumia kutengeneza pombe n.k.

Lakini biblia ilishasema katika

Isaya 5: 20 "Ole wao wasemao kwamba uovu ni wema, na kwamba wema ni uovu; watiao giza badala ya nuru, na nuru badala ya giza; WATIAO UCHUNGU BADALA YA UTAMU, NA UTAMU BADALA YA UCHUNGU!."
 
Unaona hapo? Biblia imetoa onyo kali kwa wale wote wanaopenda kupundia, vitu ambavyo Mungu aliviumba vitumike ipasavyo katika uhalisia wake, Kuzalisha mtama kwa ajili ya kutengenezea pombe ni sawa na kutia uchungu katikati ya jamii badala ya utamu. Kuzalisha ulezi na ndizi kwa dhumuni la kuviuzia viwanda vya utengenezaji pombe, ni sawa na kutia uchungu katikati ya jamii badala ya utamu.

Kadhalika na mambo mengine yote ambayo yangepaswa yatumike kwa matumizi ya asili lakini watu wanayageuza, kwamfano wanaume kwa wanaume, na wanawake kwa wanawake ni sawa na kutia nuru badala ya giza..Bwana alishasema OLE WAO wafanyao hivyo.

 SWALI 4: Je! ni vizuri mkristo kwenda hospitali au kutumia miti shamba anapougua?

JIBU: Kama tukisoma Marko 2: 17 tunaweza kuona Bwana Yesu aliwaambia watoza ushuru na Mafarisayo maneno haya, “…WENYE AFYA HAWAHITAJI TABIBU, BALI WALIO HAWAWEZI; sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi.”
 
Bwana alitumia mfano huo wa kidunia kueleza mambo ya rohoni, akimaanisha kuwa ni jambo la kawaida kwa mtu aliye mgonjwa kumtafuta daktari amuhudumie afya yake. Kwasasa tunaweza kusema kwenda hospitali. Hivyo mkristo kuumwa na kwenda hospitali hafanyi kosa lolote, maadamu anafanya tendo ambalo halimwathiri Imani yake.

kadhalika pia anaweza kutumia aina zozote za mimea ambazo anaweza kuona zitamsaidia kuimarisha afya ya mwili wake, mwingine anaona kutumia mwarobaini, au alovera ni nafuu zaidi kwake kuliko dawa za hospitalini kwasababu pia dawa nyingi za hospitalini zinatengenezwa kutoka kwenye hiyohiyo mimea ya asili. Lakini la kuzingatia mkristo anapotumia dawa hizo, hapaswi kuzihusisha na ibada zozote za Kiroho isipokuwa kwa Mungu wake.

Kwamfano mtu anapewa dawa za miti shamba labda mwarobaini, halafu anaambiwa achinje kuku, au aweke uvunguni, au aseme maneno Fulani au afanye kafara kisha ndio anywe, sasa hizo tayari ni ibada za sanamu ambazo ni machukizo makubwa mbele za Mungu. Lakini mtu akiwa na mwarobaini wake nyumbani, akatengeneza akanywa kwa jina la YESU hakuna tatizo lolote. Akizingatia tu lile Neno katika Wakolosai 3: 17 “Na kila mfanyalo, KWA NENO au KWA TENDO, fanyeni yote KATIKA JINA LA BWANA YESU, mkimshukuru Mungu Baba kwa yeye”.

Lakini pia kuna mwingine kwa Imani yake anaamini kuwa Mungu ndiye mponyaji wake kwa asilimia zote pasipo kupitia nyenzo yeyote, hivyo anaposikia kuumwa anaamini kuwa Mungu atamponya pasipo kwenda hospitali, akiliamini lile Neno (Mathayo 8:17 “…Mwenyewe aliutwaa udhaifu wetu, Na kuyachukua magonjwa yetu.” ) hivyo mtu wa namna hii pia hafanyi kosa, Kwasababu Mungu ni yule yule anayeweza kumponya mtu kwa kupitia daktari au pasipo daktari..Hapo ni kulingana na Imani ya mtu kwa Mungu wake.

Ubarikiwe.


No comments:

Post a Comment