"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Monday, October 15, 2018

TUSIPOUTHAMINI WOKOVU TUTAPATAJE KUPONA?

Mathayo 5: 13NINYI NI CHUMVI YA DUNIA; lakini chumvi ikiwa imeharibika itatiwa nini hata ikolee? Haifai tena kabisa, ila kutupwa nje na kukanyagwa na watu.
14 Ninyi ni nuru ya ulimwengu. Mji hauwezi kusitirika ukiwa juu ya mlima.
15 Wala watu hawawashi taa na kuiweka chini ya pishi, bali juu ya kiango; nayo yawaangaza wote waliomo nyumbani.
16 Vivyo hivyo nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni.”

Bwana Yesu aliwafananisha watakatifu waliopo duniani na CHUMVI,. Tunafahamu sifa ya chumvi, ni kiungo kisicholika chenyewe kama chenyewe, bali ni lazima kwanza kichanganywe na kitu kingine kama chakula ili kilete ladha, kadhalika chumvi huwa haitengenezwi na mchanganyiko mwingine wowote isipokuwa ni chumvi kama chumvi tu, ikichanganya na vingine inakuwa tena si chumvi bali ni kitu kingine.

Vivyo hivyo mkristo yeyote aliyekolewa, kwa kuzaliwa mara ya pili, mbele za Mungu ni kama chumvi katika ulimwengu. Anapoamua kuacha dhambi na maisha mabovu aliyokuwa anaishi huko nyuma, mbinguni yeye anaonekana kama chumvi safi katikati ya ulimwengu. Lakini chumvi tunafahamu inaharibika pale tu inapojichanganya na kitu kingine au inapomwagika. Kwa mfano chumvi ikiingia mchanga ni wazi kuwa hakuna mtu atakayeweza kutenganisha punje moja moja kutoka katika huo mchanga, badala yake itakuwa ni ya kutupwa tu, hata kama ilinunuliwa kwa thamani kubwa kiasi gani, haifai tena.

Na ndivyo ilivyo kwetu, tunapokuwa wakristo tunapaswa tuwe makini sana, tunapaswa tujilinde sana, tunapokaa katikati ya ulimwengu, kwasababu biblia inasema tunakuwa kama Nuru katikati yao, Kwa mienendo yetu na matendo yetu. Lakini sasa matendo yetu yakiwa mabovu ni sawasawa na chumvi iliyoharibika. Tunapotazamwa na dunia tuwe na mienendo inayostahili na bora kuliko yao halafu tunaonekana ni walevi, watukanaji, waasherati, wasengenyaji, watoaji wa maneno ya mizaha, wagomvi, fitna, wivu, na chuki, tunakosa nidhamu katika jamii, je! Tutatiwa nini hata tukolee?. Kilichobaki ni kutupwa tu nje! Na kukanyagwa na watu. Hatua hiyo ni sawa na ile hatua ya kutapikwa, kwasababu unakuwa vuguvugu na si baridi wala si moto,..Ni chumvi iliyoingia mchanga.

Biblia imesema katika 1Wakorintho 10: 12 “Kwa hiyo anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke”. Unaona hapo? Ukristo ni wakutunzwa sana kuliko kitu kingine chochote, kwasababu ukristo wako ukishaharibika tu mara moja unakuwa haufai tena kwasababu maandiko ndivyo yanavyosema.

Wafilipi 2:11”… .UTIMIZENI WOKOVU WENU WENYEWE KWA KUOGOPA NA KUTETEMEKA 13 Kwa maana ndiye Mungu atendaye kazi ndani yenu,”

Tunapaswa tujilinde kila siku, kila mahali, kama tumekusudia kweli kwa kumaanisha kuacha mambo ya ulimwengu na kufanyika kuwa chumvi safi, tudumu katika hali hiyo hiyo, tusiitie chumvi uchafu, kwasababu chumvi si kama maharage ambayo yakianguka yanaweza yakaokoteka na kuosheka….Kwasababu biblia inasema sisi watakatifu IMANI tumekabidhiwa MARA MOJA TU (Yuda 1:3). Ikiwa na maana kuwa ukristo si wa kwenda na kurudi, kwenda na kurudi tu kama tunavyotaka..
2Petro 2: 20 “Kwa maana wale waliokwisha kuyakimbia machafu ya dunia kwa kumjua Bwana na Mwokozi Yesu Kristo, kama wakinaswa tena na kushindwa, HALI YAO YA MWISHO IMEKUWA MBAYA KULIKO ILE YA KWANZA.
21 Maana ingekuwa heri kwao kama wasingaliijua njia ya haki, KULIKO KUIJUA, KISHA KUIACHA ILE AMRI TAKATIFU WALIYOPEWA.
22 Lakini imetukia kwao sawasawa na ile mithali ya kweli, MBWA AMEYARUDIA MATAPIKO YAKE MWENYEWE, NA NGURUWE ALIYEOSHWA AMERUDI KUGAA-GAA MATOPENI.

Hivyo kama wewe ni mkristo ambaye ulishaokolewa na hujasimama imara huu ni wakati wa kufanya hivyo maadamu mlango wa neema bado haujafungwa, unayo nafasi ya kuwa moto,unayo sasa nafasi ya kufanyika CHUMVI, Unachopaswa kufanya ni kuanza maisha yako ya ukristo upya na kuamua kujikana nafsi yako kila siku kwa Bwana, na kukaa mbali na vishawishi vyote vya dunia ambavyo vitakufanya ukristo wako uwe vuguvugu, marafiki, disco, anasa, uvaaji mbaya, fashion,ulevi, usengenyaji, pornography, kujihusisha na ku-chat na kupost vitu visivyofaa katika mitandao, n.k. vifanye kuwa ni adui yako, na Bwana mwenyewe atakuongezea nguvu ya kuvishinda.

Kama wewe hujazaliwa mara ya pili ni afadhali ukafanya hivyo sasa. Na kuzaliwa mara ya pili maana yake ni kutubu kwa kumaanisha kuacha dhambi zako, kisha kubatizwa katika ubatizo sahihi wa maji mengi, katika JINA LA YESU KRISTO. Na Bwana atakupa kipawa cha Roho Mtakatifu. Kumbuka Bwana Yesu alisema mtu asipozaliwa mara ya pili [yaani kwa maji na kwa Roho] hawezi kuuona ufalme wa mbinguni. Ni maombi yangu ufanye hivyo sasa.

Waebrania 2: 3 “SISI JE! TUTAPATAJE KUPONA, TUSIPOJALI WOKOVU MKUU NAMNA HII? Ambao kwanza ulinenwa na Bwana, kisha ukathibitika kwetu na wale waliosikia;”

Bwana akubariki sana.

Tafadhali “share” ujumbe huu kwa wengine.

Kwa mpangilio mzuri wa masomo haya  tembelea website yetu >>> www.wingulamashahidi.org

No comments:

Post a Comment