"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Friday, November 2, 2018

DALILI ZIPI ZITAMTAMBULISHA MTU KUWA AMEFANYIKA KIUMBE KIPYA?

Mtu anapozaliwa mara ya pili, siku hiyo hiyo anafanyika kuwa kiumbe kipya, na mtu aliyezaliwa mara ya pili ni lazima awe ametubu dhambi zake kwanza kwa kumaanisha kuziacha kabisa, kisha akabatizwe kwa maji na kwa Roho. (Yohana 3:1-5), Ndipo awe na uhakika kuwa amezaliwa mara ya pili na kafanyika kiumbe kipya.

Lakini hiyo peke yake haitoshi kukupa uhakika huo kwasababu biblia pia inasema katika Yakobo 2:17 “Vivyo hivyo na imani, isipokuwa ina matendo, imekufa nafsini mwake...haizai” 

Hii ikiwa na maana kuwa siku ile unapofanyika kuwa kiumbe kipya ni lazima matendo yaambatanayo na huko kuwa kiumbe kipya yajidhihirishe ndani yako.

Wapo watu wanaodhani mioyoni mwao kuwa siku ile walipotubu na kubatizwa katika ubatizo sahihi ilitosha wao kukubaliwa na Mungu na huku wakiendelea kuishi katika maisha yao ya kale. Kumbuka ndugu nyakati hizi za mwisho biblia ilishatabiri kutakuwa na makundi mawili ya waaminio, Ukisoma katika Mathayo 25 utaona habari ya wale wanawali 10, ambao wote walikuwa kweli ni mabikra, na wote walikuwa wanamngojea Bwana arusi aje kuwachukua waende pamoja Arusini, lakini tofuati yao ilikuwa ni kwamba watano walikuwa ni werevu na watano wao walikuwa wapumbavu.

Wale warevu walibeba mafuta ya ziada katika katika vyombo vya pembeni pamoja na taa zao, lakini wale wapumbavu hawakubeba mafuta ya ziada isipokuwa yale tu yaliyokuwa katika taa zao. Na Bwana arusi alipokuja usiku wa manane wale wapumbavu taa zao zilikuwa zinakaribia kuzima, hivyo ikiwalazimu waende kutafuta mafuta ili waweze kwenda kumlaki Bwana arusi, lakini waliporudi wakakuta wenzao wameshaingia karamuni na mlango umefungwa.

Mfano huo unaonyesha aina mbili za wakristo watakaokuwepo katika siku hizi za mwisho, angali sisi sote tukifahamu kuwa unyakuo upo karibuni kutokea siku yoyote, lakini ni wazi kuwa wapo watakaoenda na Bwana na wapo watakaoachwa. Kumbuka hapo wote ni wakristo [wanawali] wote walizaliwa mara ya pili, lakini wapo waliodumisha mafuta ya Roho mtakatifu ndani yao na wapo ambao waliyazimisha.. Na hawa walioyazimisha ndio watakaoachwa na watakaopitia dhiki kuu ya mpinga-Kristo siku ile ikifika.

Mtu unapokuwa kiumbe KIPYA. Ni lazima uwe MPYA kweli kweli kama neno lenyewe linavyosema KIUMBE KIPYA. Kuanzia huo wakati ulipotubu na kubatizwa katika ubatizo sahihi wa kuzamishwa katika maji mengi kwa jina la YESU KRISTO na kupokea Roho Mtakatifu wa Mungu ndani yako, safari ndio inaanza na sio imeisha.  


kuanzia huo wakati ni kuanza maisha yako UPYA tena, yaani kuyasahau (kuyaaga) mambo yote ya nyuma uliyokuwa unayafanya na kuyatenda na kumwishia Kristo siku za maisha yako yaliyobaka hapa duniani, ulikuwa ni mwasherati ulikuwa ni mtukanaji, ulikuwa ni mwizi, ulikuwa unakwenda disco, ulikuwa unatazama Pornography, ulikuwa unafanya mustarbation, ulikuwa unasengenya, ulikuwa ni mla rushwa, ulikuwa ni mshirikina, ulikuwa ni mvaaji vimini na suruali, ulikuwa ni mtembeaji uchi, ulikuwa ni mwabudu sanamu, ulikuwa unasikiliza miziki ya kidunia, n.k.. Kuanzia huo wakati na kuendelea ni kuyasahau na kukaa nayo mbali, sasa hiyo ndiyo dalili itakayokuthibitisha kuwa kweli wewe umefanyika kiumbe kipya.

Lazima ufikie hatua inayokuonyesha kuwa jana yako ni tofuati na leo yako.
Neno la Mungu linasema

2Wakorintho 5:17 Hata imekuwa, mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya; YA KALE YAMEPITA TAZAMA! YAMEKUWA MAPYA.

Unaona hapo je! ya kale yako yamepita? Mtume Paulo kabla ya kuokolewa kwake alikuwa ni mwuaji, mtukanaji, mpinga-kristo,n.k. lakini baada ya kuzaliwa mara ya pili na kufanyika kiumbe kipya alisema maneno haya..
Wafilipi 3:11 “ili nipate kwa njia yo yote kuifikia kiyama ya wafu.
12 Si kwamba nimekwisha kufika, au nimekwisha kuwa mkamilifu; la! Bali nakaza mwendo ili nipate kulishika lile ambalo kwa ajili yake nimeshikwa na Kristo Yesu.
13 Ndugu, sijidhanii nafsi yangu kwamba nimekwisha kushika; ILA NATENDA NENO MOJA TU; NIKIYASAHAU YALIYO NYUMA, NIKIYACHUCHUMILIA YALIYO MBELE;
14 nakaza mwendo, niifikilie mede ya thawabu ya mwito mkuu wa Mungu katika Kristo Yesu”.
Unaona Imani ni lazima iambatane na matendo yake, unasema umekuwa kiumbe KIPYA je! Yale ya kale bado yapo ndani yako? Huo upya ulio nafsini mwako upo wapi Kama bado kuupenda ulimwengu kuko ndani yako?. Bwana YESU akirudi leo kulichukua kanisa lake, kuwachukua wale wanawali werevu na wewe utakuwa mmoja wapo?.

Utajisikiaje siku hiyo, utakapoona umeachwa na mkristo mwenzako uliyekuwa unamwona kila siku ambaye yeye alijikana nafsi yake ameenda na Bwana katika utukufu milele na wewe umebakia hapa chini?. Ni hali mbaya sana ambayo hakuna mtu yeyote atatamani aipitie.

Lile neno linalosema kutakuwa na kilio na kusaga meno, halitakuwa kwa mtu asiyemjua Kristo, hapana yao itakuja huko baadaye, lakini zaidi litakuwa kwa Yule mkristo aliyejidhania kuwa angekwenda kwenye unyakuo lakini badala yake ameachwa.

Na alibaki kwasababu gani?. Ni kwasababu hajakamilishwa katika wokovu wake, aliiishi mguu mmoja nje, mwingine ndani, leo wa Mungu kesho wa ulimwengu huu, Anasema amezaliwa mara ya pili lakini bado hataki kuacha baadhi ya mambo ya kidunia,Ni heri kuwa moto au baridi kuliko kuwa vuguvugu biblia inasema hivyo.

Kama yanavyosema maandiko: Mungu hadhihakiwi, apandacho mtu ndicho atakachovuna. Ni maombi yangu sisi sote (mimi na wewe) tusiwe katika hilo kundi kubwa la wanawali wapumbavu ambalo limeenea katika ukristo wa sasa. Badala yake tuwe miongoni wa wale wanawali werevu, tukiwa na mafuta ya ziada katika chupa chetu ili taa zetu zisizime wakati wowote hata Bwana ajapo.

Tufanyike viumbe vipya kweli kweli kila siku, yale tuliyoyaacha baada ya kutubu na kubatizwe tusitamani yaingie akilini mwetu hata kidogo. Tuishindanie Imani tuliyopewa mara moja tu na Bwana wetu, Tuishindanie hiyo hata ajapo. Naye atatupa TAJI YA UZIMA.

1Yohana 2:15 “Msiipende dunia, wala mambo yaliyomo katika dunia. Mtu akiipenda dunia, kumpenda Baba hakumo ndani yake.
16 Maana kila kilichomo duniani, yaani, tamaa ya mwili, na tamaa ya macho, na kiburi cha uzima, havitokani na Baba, bali vyatokana na dunia.
17 Na dunia inapita, pamoja na tamaa zake, bali yeye afanyaye mapenzi ya Mungu adumu hata milele.

18 Watoto, ni wakati wa mwisho; na kama vile mlivyosikia kwamba mpinga Kristo yuaja, hata sasa wapinga Kristo wengi wamekwisha kuwapo. Kwa sababu hiyo twajua ya kuwa ni wakati wa mwisho.”

DUNIA INAPITA NA MAMBO YAKE.

AMEN.

Tafadhali sambaza ujumbe huu wa Mungu kwa ndugu zako nao wapone, na Bwana atakubariki.

Ukihiaji msaada wa mafundisho ya ziada usisite kutembelea websites yetu /wingulamashahidi/.

Bwana akubariki sana.

No comments:

Post a Comment