"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Saturday, January 5, 2019

FAHAMU ZA WATU HUWA ZINAONDOLEWA NA NINI?


Kama ukichunguza watu wote walioathiriwa na ulevi wa kupindukia huwa wanaonyesha tabia zinazofanana, moja ya tabia hizo ni kutokujali jambo lolote linaloweza kuja mbele yake, mtu akishalewa hata hajali tena thamani ya utu wake, anaweza akavua nguo mbele za watu, utakuta kabla hajanywa alikuwa ni mtu mwenye heshima lakini akishalewa tu, matusi yaanza kumtiririka mdomoni mwake, anakuwa sio mtu wa kujali, sio mtu wa kujizuia, sio mtu wa kuchukua tahadhari kwa kitu chochote kile kitakachokuja mbele yake, anaweza akasimama katikati ya barabara kuu sehemu ambayo magari yanapita na kuanza kujiongelea mwenyewe bila kujali kuwa anaweza kugongwa na gari akafa. Na ndio maana hata ajali nyingi zitokeazo zinasababishwa na madereva kuwa walevi..Ni kwasababu gani? Ni kwasababu FAHAMU ZAO zinakuwa zimeshawatoka kwa wakati huo na kama ufahamu umeshawatoka basi hata ule uwezo wa kufikiri, wa kujitawala na wa kuchukua tahadhari unakuwa umeondoka ndani yao. Lakini mtu huyo huyo uje umwangalie baadaye zile pombe zimeshaisha kichwani mwake, na hapo ufahamu wake umeshamrudia atajishangaa ni kwanini amelala mtaroni, ni kwanini alikuwa anawavunjia watu wengine heshima, na ni kwanini alikuwa hathamini uhai wake kusimama katikati ya barabara n.k..

Na ndio maana Biblia inasema Hosea 4: 11 “UZINZI NA DIVAI na divai mpya huondoa fahamu za wanadamu”.
Unaona? kwa namna hiyo hiyo pombe inavyoweza kuondoa ufahamu wa watu ndivyo hivyo hivyo hata UZINZI unavyoondoa FAHAMU za watu biblia inatuambia hivyo. Maneno hayo alithibitishiwa Nabii Hosea pale alipopewa maagizo na Mungu akaoe mke kahaba, na azae naye watoto, mwanzoni alidhani pengine atakuwa kahaba tu halafu basi wala hakutakuwa na madhara mengine yoyote ya ndani, lakini kwa jinsi alivyokuwa anakaa nae na kuona mwenendo wake jinsi ulivyokuwa wa hatari sana, jinsi huyo mwanamke asivyokuwa mtu wa kujali mambo ya Mungu, jinsi huyo mwanamke alivyokuwa anapoteza mapenzi na Mungu wake siku baada ya siku, jinsi huyo mwanamke anavyozidi kuwa mbali sana na wanawake wengine kwa kila kitu, jinsi roho yake ilivyozidi kupotea pasipo hata yeye mwenyewe kujitambua kutokana na ukahaba wake, ndipo alipopata ufahamu huo kutoka kwa Mungu na kusema maneno haya.

“Uzinzi na divai na divai mpya huondoa fahamu za wanadamu.”. Ni kwanini leo hii mtu hajali juu ya hatma ya maisha yake ya milele baada ya kufa hata kama aambiwe moto wa Jehanum ni mkali mara elfu ya huu, bado hajali, Sababu sio kwamba yeye ni sugu hasikii, hapana sababu ni roho iliyo ndani yake ya UZINZI imeshamwondolea ufahamu wa kujali maisha yake bila hata yeye mwenyewe kujijua, na ndio hapo hata akielezwe habari za hukumu inayokuja utaona anaanza kufanyia mzaha, au anapuuzia, au anakufuru Ni kwasababu ule UFAHAMU aliopewa na Mungu wa kupambanua na kufikiri, na kuchukua tahadhari ulishamtoka siku nyingi.

Utakuta mtu kuongea matusi ni kitu cha kawaida kwake hasikii hata kuhukumiwa ndani ya moyo wake, unadhani alianza hivyo? Hapana zamani alikuwa anaogopa kutukana lakini kwasababu muda wote amekuwa akiishibisha nafsi yake kwa uasherati, na uzinzi na zinaa, na maneno ya uchafu, na huku biblia ilishakataza hata uasherati usitamkwe vinywani mwetu, basi bila kujua yeye anaendelea kufanya hivyo hajui kuwa kidogo kidogo anaupoteza ufahamu wake, ndipo hapo anajikuta kutukana ni sehemu ya maisha yake.

Kwa nje! Anaweza akajiona ni mwenye akili na mjanja, anaonyesha kuwa yeye naye ni kijana, lakini nyuma ya pazia hajui kuwa FAHAMU zinamtoka kidogo kidogo, na roho ya kutokujali inamvaa mpaka inafikia wakati hata aelezejwe habari za Mungu hawezi tena kugeuka, ndio inakuwa basi tena, anaishia kupinga Neno la Mungu na kuutukana msalaba. Zinaa ni mbaya kama ulivyo ulevi. Tuikimbie zinaa ndugu!!
Na ndio maana sehemu nyingine biblia inasema
Mithali 6: 32 “Mtu aziniye na mwanamke HANA AKILI KABISA; Afanya jambo litakalomwangamiza nafsi yake”.
Unaona, uasherati, uzinzi, ni mambo ambayo yanapoteza nafsi za watu kwa spidi kubwa kushinda hata mambo mengine yote. Na ndio maana shetani anapenda sana kuitumia hiyo kuwanasa watu, Anajua kabisa miili ya wanadamu ni mahekalu ya Roho Mtakatifu hivyo anafanya juu chini ayaharibu makao hayo ya Mungu ili Mungu akose mahali pa kutua, Na kama tunavyofahamu hata hii Dunia mfano kama Roho wa Mungu asingetua na kuanza kuipendezesha tena, basi ingeendelea kubakia katika hali ile ile ya utupu na ukiwa na giza milele, Sasa kama na sisi hatutaihifadhi miili yetu, na kumjengea Roho wa Mtakatifu mazingira ya kutua na kututengeneza unadhani tutapataje kupona au kuokoka?. Ni wazi kuwa tutaendelea kuwa katika giza mpaka siku ya hukumu na kuishia kutupwa katika ziwa la moto.

Ndugu/kaka kaa mbali na zinaa. Kaa mbali na vichochezi vyote vya zinaa, kaa mbali na mustarbation hivyo vyote vinaondoa ufahamu wako ndugu, unaweza ukajiona upo sawa lakini hujui ni jinsi gani nafsi yako inavyoharibika kwa spidi kubwa sana, kaa mbali na pornography na utazamaji wa picha za uchi mitandaoni, hivyo vinaondoa ufahamu wako kama vile pombe inavyoondoa ufahamu wa mtu. Weka mbali muvi na vitabu vinavyoonekana kuchochea zinaa ndani yako, hiyo ni kwa usalama wa roho yako ndugu kwa kizazi hichi Bwana anachokiona ni kizazi cha zinaa. Kaa mbali na watu au marafiki ambao muda wote mazungumzo yao ni habari za uasherati tu, disco na anasa..Hao watakupeleka kuzimu.

Usiruhusu roho ya kutokujali ikuingie, usikubali kupoteza ufahamu wako Mungu aliokupa, kwa Uzinzi. Mungu alikusudia wewe uwe mtakatifu kama yeye alivyo, hayo ndio mapenzi yake kwako 
1Petro 1: 15 “bali kama yeye aliyewaita alivyo mtakatifu, ninyi nanyi iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote;
16 kwa maana imeandikwa, Mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu”.

Lakini ni kwanini ulikuwa ukisikia maneno hayo ya Mungu unapuuzia, na huku mwingine akiusikia anaogopa na kutetemeka, unadhani tatizo ni wewe? Hapana tatizo lipo kwenye ufahamu wako ambao umeshaliwa kwa roho za uasherati na uzinzi uliokuwa ndani yako. Lakini unayo sasa nafasi ya kugeuka, na kuacha mambo hayo ili Bwana ayatengeneze upya maisha yako. Embu tufuatilie pamoja maonyo haya mafupi Sulemani aliyotupa yahusianayo na mambo haya haya ya zinaa naamini yataongeza kitu katika mienendo yetu sote. Tusome:

MITHALI: MLANGO 7
1 Mwanangu, yashike maneno yangu, Na kuziweka amri zangu akiba kwako.
2 Uzishike amri zangu ukaishi, Na sheria yangu kama mboni ya jicho lako.
3 Zifunge katika vidole vyako; Ziandike juu ya kibao cha moyo wako.
4 Mwambie hekima, Wewe ndiwe umbu langu; MWITE UFAHAMU JAMAA YAKO MWANAMKE.
5 WAPATE KUKULINDA NA MALAYA, Na mgeni akubembelezaye kwa maneno yake.
6 Maana katika dirisha la nyumba yangu Nalichungulia katika shubaka yake;
7 Nikaona katikati ya WAJINGA, Nikamtambua miongoni mwa vijana, Kijana mmoja asiyekuwa na akili,
8 Akipita njiani karibu na pembe yake, Akiishika njia iendayo nyumbani kwake,
9 Wakati wa magharibi, wakati wa jioni, Usiku wa manane, gizani.
10 Na tazama, mwanamke akamkuta, Ana mavazi ya kikahaba, mwerevu wa moyo;
11 Ana kelele, na ukaidi; Miguu yake haikai nyumbani mwake.
12 Mara yu katika njia kuu, mara viwanjani, Naye huotea kwenye pembe za kila njia.
13 Basi akamshika, akambusu, Akamwambia kwa uso usio na haya,
14 Kwangu ziko sadaka za amani; Leo hivi nimeziondoa nadhiri zangu;
15 Ndiyo maana nikatoka nikulaki, Nikutafute uso wako kwa bidii, nami nimekuona.
16 Nimetandika kitanda changu, magodoro mazuri, Kwa matandiko ya Kimisri yenye mistari.
17 Nimetia kitanda changu manukato, Manemane na udi na mdalasini.
18 Haya, na tushibe upendo hata asubuhi, Tujifurahishe nafsi zetu kwa mahaba.
19 Maana mume wangu hayumo nyumbani, Amekwenda safari ya mbali;
20 Amechukua mfuko wa fedha mkononi; Atarudi wakati wa mwezi mpevu.
21 Kwa maneno yake mengi na ulaini akamshawishi, Kwa ubembelezi wa midomo yake akamshinda.
22 Huyo akafuatana naye mara hiyo, Kama vile ng'ombe aendavyo machinjoni; Au mpumbavu kuadhibiwa katika pingu;
23 Hata mshale umchome maini; Kama ndege aendaye haraka mtegoni; Wala hajui ya kuwa ni hasara ya nafsi yake.
24 Basi, wanangu, nisikilizeni sasa, Mkayaangalie maneno ya kinywa changu.
25 MOYO WAKO USIZIELEKEE NJIA ZAKE, WALA USIPOTEE KATIKA MAPITO YAKE.
26 Maana amewaangusha wengi waliojeruhi, NAAM, JUMLA YA WALIOUAWA NAYE NI JESHI KUBWA.
27 Nyumba yake ni njia ya kwenda kuzimu, Hushuka mpaka vyumba vya mauti".
      
Unaona? Zinaa ni kama vile mtu apelekwaje machinjoni, wala hajui kuwa ni kwa hasara ya nafsi yake mwenyewe,Na biblia inatuambia walionaswa katika mtego huu si watu wawili au watatu, bali ni jeshi kubwa sana.. Hivyo mimi na wewe tusiwe miongoni mwa hilo jeshi kubwa, tuikimbie zinaa kama biblia inavyotuambia, tumpe Roho Mtakatifu nafasi ya kuyatengeneza upya maisha yetu. Ni dhambi mbaya ambayo mtume Paulo aliitaja inafanyika juu ya mwili wa mtu.

Ikiwa bado hujampa Bwana maisha yako bado hujachelewa muda ndio huu, unachopaswa kufanya ni kutubu mwenyewe kutoka ndani ya moyo wako, kukusudia kwa kumaanisha kabisa kuwa hutaki kurudia njia hizo mbovu za mauti, hutaki kuwa tena mlevi, hutaki kufanya zinaa tena, hutaki kufanya mustarbation(punyeto) tena, hutaki kutazama pornography tena, hutaki kuvaa “mavazi ya kikahaba” kama huyo mwanamke anayezungumziwa na Sulemani na mavazi ya kikahaba yanayozungumziwa kwa sasa ni vimini, suruali kwa wanawake, migongo wazi na vitop, na sketi zinazobana ambavyo ni vichocheo vikubwa vya uasherati n.k. hutaki tena kutazama picha za utupu na pornography na mengine yote. Ikiwa kweli umeonyesha nia hiyo mbele za Mungu ya kutaka kuacha basi Mungu naye kuanzia huo wakati atakupa NGUVU ya kuweza kuvishinda hivyo vyote.

Na mwisho wa siku utashangaa ni rahisi kuacha, hata mimi nilikuwa mzinzi, mlevi, mtazamaji wa pornography na kila kitu kiovu lakini siku ile Neema ya Bwana iliponifikia, nilipotubu kwa kumaanisha kuacha , Uwezo huo wa ajabu ulikuja ndani yangu, mpaka sasa dhambi ya zinaa si kitu kwangu. Na vivyo hivyo na wewe ukiamua kugeuka, Bwana atakupa Uwezo huo, Hivyo fanya maamuzi sasa angali nafasi unayo. Na mara baada ya kutubu kwako jambo linalofuata ni kubatizwa, kwa ajili ya ondoleo la dhambi zako,hivyo tafuta mahali popote wanapobatiza ubatizo sahihi wa kimaandiko, nao ni ule wa kuzamwishwa katika maji mengi na uwe kwa Jina la YESU KRISTO. Kama hujafahamu bado mahali pa kubatiziwa na unahitaji msaada wa kwa jambo hilo,unaweza kuwasiliana nami nitakuelekeza mahali karibu na wewe unaweza kupata hudumu hiyo ya kiroho.

Mwisho kabisa nikutakie mwanzo mema wa Mwaka huu, uwe wa mafanikio kwako ya kiroho na ya kimwili, na ya kukaa mbali na zinaa kwa jina la Bwana wetu YESU KRISTO.

Amen.

Tafadhali “share” ujumbe huu kwa wengine na Mungu atakubariki,

No comments:

Post a Comment