"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Thursday, June 20, 2019

SHUKURU KWA KILA JAMBO.


Shalom, mtu wa Mungu karibu tujifunze Neno la Mungu, Taa iongozayo miguu yetu..na mwangaza wa njia zetu…
Leo tutajifunza juu ya Kumshukuru Mungu kwa kila jambo…
Kwanini tunapaswa tumshukuru Mungu kwa kila jambo? Jibu ni rahisi kwasababu hatukukaa naye kikao cha yeye kutuumba sisi…tumejikuta tumetokea tu ulimwenguni, kwahiyo lolote lijalo mbele yetu sio sisi tulilolitengeneza bali ni yeye, na hatukumpa yeye kitu hata atakapokitwaa tumwulize kwanini anafanya hivyo (Ayubu 41:11)…kwahiyo tuna sababu zote za kumshukuru kwa mambo yoyote yatakayotokea mbele yetu yawe ni mazuri au mabaya…
 
Wakati mwingine Mungu anaruhusu maovu yaje juu yetu kama gharika… kama ilivyokuwa kwa Ayubu, wakati mwingine Mungu anaruhusu mambo hayo kwasababu zake yeye ambazo sio lazima wakati mwingine akuambie ni kwanini…Lakini unapaswa ushukuru.

Kama Biblia inavyotuambia katika 1 Wathesalonike 5:16 “ Furahini siku zote; ombeni bila kukoma; SHUKURUNI KWA KILA JAMBO; maana hayo ni mapenzi ya Mungu kwenu katika Kristo Yesu”.

Hata tukipitia misiba tushukuru? ndio..hata tukifilisika tushukuru? jibu ni NDIO?..Hata tukiwa katika magonjwa tushukuru? jibu ni NDIO…Kwasababu hayo ndio mapenzi ya Mungu.

Kitu ambacho wengi wetu hatujui ni kuwa…Mungu anaweza kuleta pia UOVU au UBAYA juu ya watu wake…haijalishi huo ubaya utatekelezwa na shetani, au malaika au mwanadamu…lakini Ana uwezo wa kuleta Ubaya juu ya mtu ambaye hata anayeupendeza moyo wake kabisa kwa kusudi Fulani…

Biblia inasema katika…Maombolezo 3:37 “Ni nani asemaye neno nalo likafanyika, Ikiwa Bwana hakuliagiza? 38 Je! Katika kinywa chake Aliye juu Hayatoki MAOVU NA MEMA?”
 
Unaona? Sio mema tu yanatoka kwake hata maovu…lakini Maovu anayoyaleta juu ya watu wake sio ya kuwaangusha bali kuwapa tumaini katika siku zao za mwisho(Yeremia 29:11)..Haleluya!..Bwana atajeruhi lakini ataponya! Ataangusha chini lakini atanyanyua! Ataua lakini atahuisha, Atafukarisha lakini atatajirisha N.k

1 Samweli 2:6 Bwana huua, naye hufanya kuwa hai; Hushusha hata kuzimu, tena huleta juu. Bwana hufukarisha mtu, naye hutajirisha; Hushusha chini, tena huinua juu.”

Hosea 6:1Njoni, tumrudie Bwana; maana yeye amerarua, na yeye atatuponya; yeye amepiga, na yeye atatufunga jeraha zetu.
2 Baada ya siku mbili atatufufua; siku ya tatu atatuinua, nasi tutaishi mbele zake.”

Kwahiyo kuna umuhimu mkubwa sana wa kutomnung’unikia Mungu pale jambo Fulani baya linapokuja juu yako…kinyume chake mshukuru kwasababu anakuwazia yaliyo mema katika siku zako za mwisho..Na pia kumbuka kuwa hakuna mwanadamu awezaye kumwuliza Mungu kwanini unafanya hivi au kwanini unafanya vile, au kwanini unaruhusu hili, au kwanini unaruhusu lile,…Kila kitu anafanya kama apendavyo. Na pia hatukuja na chochote hivyo hata vikichukuliwa vyote hatuna sababu ya kulaumu kwasababu hatukuja na kitu duniani..

Ayubu alizungumza sentensi moja ambayo ni muhimu sana kwetu sisi kuielewa…alisema …Ayubu 1:21 “ akasema, Mimi nilitoka tumboni mwa mama yangu nili uchi, nami nitarudi tena huko uchi vilevile; Bwana alitoa, na Bwana ametwaa; jina la Bwana na libarikiwe”.

Maana ya kutoka kwa mama yake uchi, alimaanisha hakuja na kitu duniani, hata nguo, wala watoto, wala mashamba, wala wale ng’ombe aliowapoteza, wala wale mbuzi na ngamia…bali alikuja bila chochote…kwahiyo hata siku atakapokufa atarudi huko alikotokea bila kitu…kwa ufunuo huo basi akahitimisha kwa kusema Bwana alitoa na Bwana ametwaa jina lake libarikiwe!!.

Ni ufunuo mkubwa sana aliupata…na sisi tunapaswa tuwe hivyo..tulikuja duniani bila ya kitu chochote na hivyo tutaondoka bila chochote…kwahiyo tukipata misiba,misiba, tukifilisika, tukipungukiwa tujue kuwa hatukuja na kitu..tukiyajua hayo tutaishi kwa Amani na kama wapitaji tu hapa duniani. Na hiyo itatufanya kuweka tumaini letu lote kwake, wakati Fulani mtume Paulo na wenzake walisongwa na taabu nzito mpaka wakakata tamaa ya kuishi..Lakini hiyo iliwafanya wazidi kumtumainie Mungu awaokoaye watu wote.
2Wakorintho1:8 “Maana ndugu, hatupendi, msijue habari ya dhiki ile iliyotupata katika Asia, ya kwamba tulilemewa mno kuliko nguvu zetu, hata tukakata tamaa ya kuishi.
9 Naam, sisi wenyewe tulikuwa na hukumu ya mauti katika nafsi zetu ili tusijitumainie nafsi zetu, bali tumtumaini Mungu, awafufuaye wafu,
10 aliyetuokoa sisi katika mauti kuu namna ile; tena atatuokoa; ambaye tumemtumaini kwamba atazidi kutuokoa;”
Kwahiyo tunapaswa tushukuru kwa kila jambo, na kuridhika kwa vile Mungu alivyotukiria, kwasababu hatukuja na kitu vile vile tutaona bila kitu chochote.

1 Timotheo 6:6 “Walakini utauwa pamoja na kuridhika ni faida kubwa. Kwa maana hatukuja na kitu duniani, tena hatuwezi kutoka na kitu.”

Bwana akubariki sana.
www.wingulamashahidi.org

No comments:

Post a Comment