"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Sunday, July 14, 2019

FIMBO YA HARUNI!


Shalom! Karibu tujifunze Biblia..

Haruni alikuwa ni kaka yake Musa, waliozaliwa tumbo moja…isipokuwa Haruni alikuwa ni Mkubwa kwa Musa kwa miaka 3,Lakini Bwana alimchagua Musa kubeba kusudi lake la kuwatoa wana wa Israeli kutoka nchi ya Misri kuelekea Kaanani…Na biblia inasema Mungu alimchagua Haruni kaka yake Musa kuwa kama Nabii wa Musa…Na pia walikuwa na dada yao aliyeitwa Miriamu ambaye naye pia alikuwa ni Nabii (Kutoka 7:1).

Lakini haikuishia hapo, Mungu alillifanya kabila la Musa kuwa kabila kikuhani,(Kabila la LAWI) na alimchagua Haruni kaka yake Musa, baadaye kama Kuhani Mkuu wa kwanza katika Israeli’’.

Na wote wawili hawa, Musa na Haruni Mungu alikuwa anatembea nao kwa namna ya kipekee sana, na wote walipewa mamlaka Fulani na Mungu. Lakini kama ukijifunza Biblia kwa makini utaona, Mungu alitembea na Musa sana kwa kutumia ile fimbo aliyokuwa nayo kule nyikani aliyokuwa anaitumia kuchungia kondoo za Mkwe wake (aliyeitwa Yethro) baada ya kumkimbia Farao zamani..Fimbo ambayo alikuwa anatumia kuchingia mifugo ilikugeuka baadaye kuwa kuwa fimbo ya kuwachungwa wana wa Israeli, na fimbo ya adhabu kwa Farao.

Sasa hii fimbo mara ya kwanza ilikuwa ni ya Musa, na ilikuwa ni ya kwake tangu akiwa kwa Yethro, lakini baada ya Musa, kutomwamini Mungu na kuanza kujitetea kwamba yeye si msemaji, ndipo Mungu akamfanya Haruni awe anazungumzaji kwa niaba yake, …na ile fimbo akapewa Haruni kwasababu yeye ndiye atakayekwenda kufanya zile ishara zote mbele ya Farao kwa niaba ya Musa, kwahiyo ile fimbo ikaitwa FIMBO YA HARUNI. Ndio ile ile fimbo iliyogeuka nyoka mbele ya Farao, na kuwameza wale nyoka wa Farao, na ndio ile ile fimbo iliyogeuza maji yote ya Misri kuwa Damu.(Kutoka 7:19),na ndiyo ile ile iliyogeuza mavumbi kuwa chawa, na ndio iliyoigawanya bahari ya Shamu ili wana wa Israeli wapite na ndiyo iliyoifunga bahari ya Shamu ili Jeshi la Farao liangamie n.k

Sasa ilikuwa ni fimbo ya hukumu na mamlaka…Kama mchungaji, kazi ya fimbo ya mchungaji ni kuwaweka kondoo kwenye mstari na pia kuwapiga maadui wanaotaka kuwadhuru kondoo.

Sasa wakiwa jangwani katika safari ya kwenda Kaanani kuna baadhi ya watu walinyanyuka kinyume cha Musa na Haruni, na kusema inatosha sasa nyie kujifanya wakubwa juu yetu…Hivyo wakataka wao ndio wawe viongozi wa lile kundi lote…Mungu hakupendezwa na kile kitendo hivyo akawaua wote walijaribu kutekeleza hilo zoezi..Unaweza kusoma hayo katika kitabu cha Hesabu mlango wa 16.

Watu hao pamoja na kuona miujiza yote bado walikuwa wanadhani ni Musa na Haruni kwa akili zao ndio walioamua kuwatoa Misri, hawakujua kuwa ni Mkono wa Mungu, kwa ile fimbo ya kichungaji ndiyo iliyowatoa Misri…hivyo badala ya kumwangalia Mungu na uweza wake wakaanza kuwashambulia Musa na Haruni kana kwamba wao ndio waliowatoa Misri, waliwachoka hivyo wakataka kujichagulia watu wengine wa kuongoza.

Lakini Mungu kuthibitisha kuwa si mwanadamu anayeokoa bali ni Mungu, na kuwathibitishia kuwa hapangiwi mtu wa kulibeba kusudi lake..aliwaambia wakuu wote wa makabila kila mmoja alete fimbo yake mbele ya agano la ushuhuda, kwahiyo zikaletwa fimbo 12, Na hizi fimbo hazikutwaliwa tu kutoka kwa watu wa kawaida, hapana bali zilitwaliwa kutoka kwa Wakuu wa kila kabila la Israeli..Wakuu wa makabila walikuwa ni watu wa Mungu, na walioheshimika na kila kabila lilikuwa na mkuu mmoja, na kila mkuu alikuwa na fimbo yake kama vile Musa alivyokuwa na fimbo…Na hao Mungu aliwajalia hekima katika kuongoza, na pia fimbo zao zilikuwa na miujiza Fulani, hazikuwa fimbo za kawaida..

Kwahiyo fimbo zao zikakusanywa zote,na kila fimbo ikaandikwa jina la mhusika…. na katika kabila la Lawi wakaichagua ile fimbo ya Haruni, kwahiyo zikapelekwa mbele ya hema ya kukutania.
Hesabu 17:1 “Kisha Bwana akanena na Musa, akamwambia,
2 Nena na wana wa Israeli, kisha upokee kwao fimbo, fimbo moja kwa ajili ya nyumba ya kila baba, katika wakuu wao wote, kama nyumba za baba zao zilivyo, fimbo kumi na mbili; kisha andika jina la kila mtu katika fimbo yake.
3 Na katika fimbo ya Lawi utaliandika jina la Haruni; maana, itakuwa fimbo moja kwa kila kichwa cha nyumba za baba zao.
4 Nawe utaziweka katika hema ya kukutania mbele ya huo ushahidi, hapo nikutanapo pamoja nanyi.
5 Kisha itakuwa, mtu huyo nitakayemchagua, fimbo yake itachipuka; nami nitayakomesha kwangu manung'uniko ya wana wa Israeli, wanung'unikiayo juu yenu.
6 Basi Musa akawaambia wana wa Israeli, ndipo wakuu wao wote wakampa fimbo, fimbo moja kwa kila mkuu, kama nyumba za baba zao zilivyokuwa, fimbo kumi na mbili; na fimbo ya Haruni ilikuwa kati ya fimbo zao.
7 Kisha Musa akaziweka hizo fimbo mbele za Bwana katika hema ya kukutania”.
Kesho yake walipoingia ndani ya Hema… wakaikuta ile fimbo ya Haruni imechipuka na kuzaa matunda, na zile nyingine hazijachipuka…Ndipo wana wa Israeli wakajua kuwa ni Mungu ndiye aliyekuwa pamoja na Musa na Haruni, Na Mungu amewachagua hao kubeba kusudi lake.
“8 Ilikuwa siku ya pili yake, Musa akaingia ndani ya hema ya ushahidi; na tazama, ile fimbo ya Haruni iliyokuwa kwa nyumba ya Lawi ilikuwa imechipuka, imetoa michipukizi, na kuchanua maua; na kuzaa malozi mabivu.
9 Kisha Musa akazileta nje hizo fimbo zote kutoka hapo mbele za Bwana na kuziweka mbele ya wana wa Israeli wote; nao wakaangalia, na kila mtu akaitwaa fimbo yake.
10 Kisha Bwana akamwambia Musa, Irudishe fimbo ya Haruni mbele ya ushahidi, ili itunzwe iwe ishara juu ya hawa wana wa maasi; ili uyakomeshe manung'uniko yao waliyoninung'unikia, ili wasife.
11 Basi Musa akafanya vivyo; kama Bwana alivyomwagiza, ndivyo alivyofanya ”.
Malozi ni matunda Fulani yanayojulikana kama matipisi, au sehemu nyingine yanajulikana kama mapindigesi au mapichi. Ni matunda ambayo yakiiva yanakuwa matamu sana na yana mbegu ngumu sana ndani, na pia maua yake ni mazuri sana kupita kiasi..Sasa tabia ya mti wa Mlozi au mtipisi ni kwamba hautoi matunda msimu mmoja na maua, msimu wa maua huwezi kukuta tunda hata moja unakuta mti wote ni maua tu, na maua yake ni mazuri sana, ni mchanganyiko wa rangi ya pink na nyeupe..kadhalika msimu wa matunda huwezi ukakuta ua hata moja, mti wote unakuwa ni kijani tu, na umejaa matunda..lakini hapa kwenye hii fimbo ya Haruni unaona mwujiza matunda na maua yamechipuka kwa wakati mmoja…

Tabia yake nyingine ya kipekee ya mti wa Mlozi (mtipisi)..ni kwamba unachukua muda mrefu sana mpaka ukomae na kufikia kiwango cha kuzaa matunda, sio mti mkubwa sana ni kama mchungwa tu! Lakini unaweza kuchukua hata miaka 12 mpaka ufikie hatua ya kuzaa matunda…Lakini hapa katika hii fimbo ya haruni unaona imechukua usiku mmoja tu kuzaa, ina maana kubwa sana ambayo tutakuja kuona hapo mbeleni.

Na mti wa Mtipisi, ni mti ambao unahitaji mizizi mirefu ili iweze kukua, mizizi ya mti huu inakadiriwa kuwa na urefu mara mbili ya mti wenyewe…kwahiyo unaweza kuona ni mtu unaohitaji sana mizizi ili ukue..lakini hapa kwenye fimbo ya Haruni kulikuwa hakuna mizizi.

Kwahiyo ile fimbo ya Haruni ilikuwa inawakilisha Mkono wa Mungu juu ya wana wa Israeli, kwamba anawachunga wana wa Israeli kwa miujiza, kwa fimbo ya kimiujiza, kwamba Bwana anatoa chakula mahali ambapo hakuna chanzo cha chakula, ndio maana umeona ile fimbo imechipua na haina mizizi, Wana wa Israeli walikula mana na nyama jangwani mahali ambapo hakuna mashamba wala mvua… pia Bwana anaweza kuumba jambo leo leo kwa jambo ambalo lingeweza kuchukua miaka mingi kufanyika ndio maana unaona ile fimbo imechipuka kwa usiku mmoja tu na kuzaa matunda mengi.
Pia Bwana ana uwezo wa kuikusanya misimu miwili au zaidi na kuileta pamoja, kwa Bwana inawezekana kuzaa na kuchanua kwa wakati mmoja ndio maana unaona ile fimbo ilizaa matunda na kuzaa maua kwa wakati mmoja.

Kadhalika Kristo ndiye Kiongozi wetu sasa, yeye ndiye aliyepokea mamlaka yote ya Mbinguni na Duniani kutoka kwa Baba kama vile Haruni alivyopokea uongozi kutoka kwa Musa na fimbo ya kichungaji, na sisi leo tukimpokea Kristo na kumwamini, basi tutakuwa chini ya FIMBO YA KICHUNGAJI YA BWANA YESU KRISTO, ambayo hiyo haina msimu maalumu wa kutupa mema, hiyo tukiumwa haihitaji mamia ya miaka ndipo tupone, ni papo kwa hapo…hiyo haihitaji kuhofia tutakula nini wala tutakunywa nini?...inatoa chakula mahali pasipo na chakula na kutoa maji mahali pasipo na maji, kama fimbo ya Haruni ilivyotoa maji mwambani kule jangwani… na inatengeneza njia mahali pasipokuwa na njia..

Lakini sharti kwanza lazima ukubali kuwa kondoo wake, ndipo uchungwe na unakuwa kondoo wake kwa kumwamini na kwa kutubu dhambi kwa kumaanisha kuziacha na kisha kwenda kubatizwa katika ubatizo sahihi wa maji mengi na kwa jina la Yesu, na kupokea kipawa cha Roho Mtakatifu, hapo utakuwa kondoo wake, na utashiriki Baraka zote za uchungaji wake..

Fimbo za wengine hazina nguvu ya kiungu, haziwezi kufanya lolote haziwezi kuchipuka zinahitaji mizizi, zinahitaji muda mrefu kukupatia msaada, vile vile haziwezi kukutetea, wakati wa maadui, fimbo ya Haruni iligeuka pia kuwa nyoka kwa Farao pale ilipopasa…Si zaidi fimbo ya BWANA wetu YESU KRISTO?.
Zaburi 23:1 “Bwana ndiye mchungaji wangu, Sitapungukiwa na kitu.
2 Katika malisho ya majani mabichi hunilaza, Kando ya maji ya utulivu huniongoza.
3 Hunihuisha nafsi yangu; na kuniongoza Katika njia za haki kwa ajili ya jina lake.
4 Naam, nijapopita kati ya bonde la uvuli wa mauti, Sitaogopa mabaya; Kwa maana Wewe upo pamoja nami, GONGO LAKO NA FIMBO YAKO VYANIFARIJI”.
Ubarikiwe.
www.wingulamashahidi.org

No comments:

Post a Comment