"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Monday, August 26, 2019

ACHENI MJUE YA KUWA MIMI NI MUNGU.


Shalom, mtu wa Mungu natumai u buheri wa afya kwa pumzi unayopewa na mwenyezi Mungu. Leo kwa furaha ya Bwana nakukaribisha tuutafakari ukuu wa Mungu na matendo yake jinsi yalivyo makuu.

Tabia mojawapo ya Mungu ni kuwa, huwa hajisifii au kujionyesha moja kwa moja mbele za watu kuwa yeye ni mkuu, badala yake huwa anawaacha wanadamu wavumbue wao wenyewe kazi zake, na pale wanapoona mambo ya kutisha na kusema he! Kumbe na hili kalifanya yeye, kumbe na lile kalifanya yeye!, na yule mtu kumpa Mungu utukufu Sasa hapo ndipo Mungu anapoipokea sifa yenyewe. Tofauti na sisi wanadamu, Kwanza tunataka tusifiwe kwa kitu ambacho si chetu, pili tunapenda kuwaonyesha watu kuwa sisi tunacho, kwa lengo la kujitafutia utukufu bandia..

Sasa yapo mambo ambayo, laiti watu wa vizazi vya Nuhu wangeona, leo hii wasingeangamizwa, vile vile yapo mambo ambayo laiti watu wa Sodoma wangeyaona leo hii wangemuheshimu Munguna kumwogopa sana, Halikadhalika yapo mambo ambayo mitume wangeyaona kama tunavyoyaona sisi , leo hii wangemtukuza Mungu kwa nguvu zao zote..Vile vile yapo mambo ambayo Mfalme Daudi angeyaona leo hii angemwabudu Mungu Zaidi hata ya pale alipomwabudu alipodondokewa na nguo.

Sisi watu wa leo hii Teknolojia imeturahisishia mambo sana, na hivyo kwa kutumia simu zetu tu au computa au television tunaweza kuona uweza mwingi wa Mungu duniani kote.

Mfano zamani, watu walikuwa wakitazama juu, walikuwa wanaona nyota na mwezi tu peke yake, napengine walidhani kuwa kuvifikia hivyo sio mwendo sana lakini sisi tunaoishi kizazi hiki ndio tunajua, kumbe baadhi ya zile nyota tunazoziona ni Ma-Jua mengine mengi, kama tu jua letu hili, na kila nyota inayo sayari zake nyingi kama Jua letu hili lilivyo na sayari 9, Dunia yetu ikiwa ni mojawapo ya sayari hizo.

Sasa karibu kila kitu unachokiona angani, vyote hivyo ni kama punje moja kati ya nyingi. Kama vile punje moja ya mahindi katikati ya gunia, sasa punje yetu tuliyopo sisi ndio inaitwa Milky way galaxy(Giligili), ambayo inatengenezwa na mamilioni ya mifumo ya jua..Hivyo ukiendelea juu zaidi unakutana na punje nyingine ambayo pia inayo ma-jua yake mengi, mabilioni kwa mabilioni, na sayari zake kama hii yetu ya Milk-way..nayo inaitwa Andromeda Galaxy, sasa jumlisha punje zote hizi za Magalaxy, katengeneza Mungu mmoja, inasemekana yapo magunia mengine kama hayo mabilioni kwa mabilioni, hapo bado haijasisha ukiyajumlisha magunia hayo yote unatengeneza tenarumbesa moja lijulikanalo kama Clusters, sasa hayo marumbesa nayo yapo mabilioni kwa mabilioni, nayo ukiyajumlisha utapata kitu kimoja kinachoitwa Super clusters, Hizi nazo zipo mabilioni kwa mabilioni, ukijumlisha unapata kitu kinachotwa Universe,…Na hizi Universe nazo zinaonekana zipo mabilioni kwa mabilioni ambayo hayo upeo wa wanasayansi wa sasa hawajaweza kugundua chochote kinachoendelea juu Zaidi ya hapo.

Sasa tukizungumzia kutoka kwenye mfumo wetu tu wa Jua, kutoka sayari moja hadi nyingine, yaani sayari iliyokaribu na sisi ujulikanayo kama Mars inaweza kukuchuka Zaidi ya miaka 57.4 kufika kama ukisafiri kwa gari lenye spidi ya juu sana..sasa jiulize kukatisha kutoka galaxy moja hadi nyingine inaweza kukuchukua miaka mingapi?
Inasemekana zipo sayari zenye mfano wa dunia hii, na nyingine Zaidi hata ya dunia hiii nazo hizo zipo Zaidi ya BILIONI 40, Yaana kama kila mwanadamu apewe dunia yake, atepewa amiliki dunia 6.

Hapo bado hatujazungumza kwa viumbe vya ajabu vilivyogunduliwa hivi karibuni duniani, nabado vinaendelea kugunduliwa, laiti mfano watu wa zamani wangeweza kuyaona haya au kuyasikia wasingemchukulia Mungu katika taswira iliyo bora zaidi. Ukirudi baharini vipo viumbe vingi vya ajabu ambavyo kila siku vinazidi kugunduliwa...

Lakini sasa ni kwanini tunajikumbusha haya?

Hiyo yote ni kuonesha kuwa Mungu ni mkuu na mwenye uweza kushinda sisi tunavyoweza kufikiri, hata kama uliwahi kumwomba kitu na hujakipata, hilo lisikufanye kumuona kuwa Mungu hawezi kukupa chochote, kumbuka ikiwa anamiliki matrilioni ya Sayari angani, atashindwaje kukupa wewe kipande cha mita 20 za ardhi,? Jaribu kufikira tu hayo mambo.

Ikiwa anamlisha tembo kila siku kilo Zaidi ya 200 na maji Zaidi ya lita 100 atashindwaje kukupa wewe chakula kilo 2 tu kwa siku?, ikiwa umemwomba chakula na hujaona kimekuja kwa muda huo, basi usinung’unike ujue kuwa anakuandalia kilicho bora Zaidi..

Hali yoyote unayopitia leo, uwe ni shida, au magonjwa visikuvunje moyo ukadhani kuwa Mungu hakuoni, au hawezi kukutoa katika hali uliyopo..Anao uwezo huo, wewe endelea kuyatafakari tu matendo yake.Poteza muda mrefu, kuuchunguza ukuu,wake na kumsifu kwa kila unachokiona, Nakuambia wakati utafika utasema asante Mungu kwa kuwa umenipa au umenitendea katika wakati huu, ambao ndio bora ziadi kuliko kama ungenipa wakati ule.

Hivyo ikiwa wewe ni mkristo, usiache kuishindani Imani yako, uliyokabidhiwa mara moja tu… Pia kama bado upo nje ya Kristo, acha kuyahatarisha Maisha yako, mgeukie yeye sasa atakuponya Roho na Mwili wako.
Zaburi 46:8 “Njoni myatazame matendo ya Bwana, Jinsi alivyofanya ukiwa katika nchi.
9 Avikomesha vita hata mwisho wa dunia; Avunja uta, akata mkuki, achoma moto magari.
10 Acheni, mjue ya kuwa Mimi ni Mungu, Nitakuzwa katika mataifa, nitakuzwa katika nchi.”
Bwana akulinde,Bwana akufunike, Bwana akubariki.

Shalom.

No comments:

Post a Comment