"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Friday, April 14, 2017

MASWALI NA MAJIBU: SEHEMU YA 13

 
SWALI 1: Je! ni sahihi mtu kuning'iniza  picha nyumbani mwako kama ya Yesu? maana imeandikwa kutoka 20:4 "Usijifanyie sanamu ya kuchonga, wala mfano wa kitu cho chote kilicho juu mbinguni, wala kilicho chini duniani, wala kilicho majini chini ya dunia. " Sasa naomba kufahamu kufanya hivyo ni makosa?

JIBU: kwa kulijibu hili swali tumalizie kusoma mstari huo..

 kutoka 20:4-5" Usijifanyie sanamu ya kuchonga, wala mfano wa kitu cho chote kilicho juu mbinguni, wala kilicho chini duniani, wala kilicho majini chini ya dunia.
5 Usivisujudie wala kuvitumikia; kwa kuwa mimi, Bwana, Mungu wako, ni Mungu mwenye wivu; nawapatiliza wana maovu ya baba zao, hata kizazi cha tatu na cha nne cha wanichukiao,"

Sasa tunaona katika huo mstari wa tano msisitizo umewekwa pale katika neon “USIVISUJUDIE WALA KUVITUMIKIA”, lakini sio kuwa na picha yoyote kama ya  Yesu nyumbani mwako ni vibaya hapana! unaweza kuweka picha yoyote upendayo ilimradi iwe ni njema, maana tukisema tusiweke picha yoyote basi hata tunaponing'iniza picha zetu wenyewe ukutani majumbani mwetu tunafanya vibaya kwasababu maandiko yanasema usijifanyie mfano wa kitu chochote sio tu kilicho juu mbinguni bali hata kilichopo chini duniani. unaona hapo msisitizo ni kwamba unapoweka picha yoyote au sanamu yoyote hupaswi kuiabudu  wala kuisujudia kwa kufanya hivyo ni machukizo makubwa mbele za Mungu. Lakini leo hii kuna baadhi ya watu,na dini na madhehebu yanaabudu sanamu za Yesu na bikira Mariamu au watakatifu waliokufa kale hao ni dhahiri kuwa wanamwabudu shetani aidha kwa kujua au kwa kutokujua. Kwahiyo hakuna shida yoyote kuweka picha ilimradi isihusishwe na mambo yoyote ya ibada mfano wa kuabudiwa au kusujudiwa.




SWALI 2: Naomba ufafanuzi wa huu mstari Yohana 11:25-26"  Yesu akamwambia, Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi;naye kila aishiye na kuniamini hatakufa kabisa hata milele. Je! Unayasadiki hayo? " hususani hapo anaposema (naye kila aishiye na kuniamini mimi hatakufa kabisa hata milele.) ana maana gani?

JIBU :
Tunajua Yesu Kristo ndio ule mti wa uzima uliozungumziwa katika bustani ya Edeni kule mwanzo kwamba ukila matunda yake utaishi milele, na matunda yake leo hii tunayajua ni NENO lake, na neno lake ndio UZIMA wenyewe na siku zote palipo na uzima hapana kifo. 

Tukichunguza katika mstari huo tunaona Bwana Yesu alizungumza kwa watu wa aina mbili tofauti,


Aina ya kwanza: ni "yeye aniaminiye mimi ajapokufa atakuwa anaishi". Hili ni kundi ambalo linajumuisha watu wote waliomwamini Bwana watakaokufa watakuwa wanaendelea kuishi katika paradiso wakingojea ufufuo wa mwisho lakini kundi hili halikufanikiwa kufikia utimilifu wa imani ya kumwamini Mwana wa Mungu, hivyo basi itawapasa wafe lakini kwa kuwa walimwamini Mungu kwa sehemu ya imani watakuwa wanaendelea kuishi huko paradiso. Na ni watu wengi leo hii wanakufa katika hali hii.


Aina ya pili : "naye kila aishiye na kuniamini mimi hatakufa kabisa hata milele". Hili ni kundi lililofikia imani timilifu ya kumwamini na kumjua sana mwana wa Mungu inayozungumziwa katika kitabu cha...

 (waefeso 4:13”hata na sisi sote tutakapoufikia umoja wa imani na kumfahamu sana Mwana wa Mungu, hata kuwa mtu mkamilifu, hata kufika kwenye cheo cha kimo cha utimilifu wa Kristo; )

hata kufikia hatua ya kushinda kifo na mauti. Mfano wa watu kama hawa tunawaona kama Henoko, Eliya, na kanisa ambalo litakuja kunyakuliwa siku ya mwisho. Hata leo hii inawezekana mtu kutokuonja mauti kabisa tukimwamini mwana wa Mungu (YESU KRISTO) katika utimilifu wote, tutachukuliwa juu hatutakufa kama  ilivyokuwa kwa Eliya na Henoko, maana biblia inasema Eliya alikuwa ni mtu mwenye tabia sawa na sisi lakini kwa bidiii na kwa imani akachukuliwa juu. Mahali pengine Bwana Yesu alisema katika...
 Yohana 8:51-54 "Amin, amin, nawaambia, Mtu akilishika neno langu, hataona mauti milele.
52 Basi Wayahudi wakamwambia, Sasa tumeng'amua ya kuwa una pepo. Ibrahimu amekufa, na manabii wamekufa; nawe wasema, Mtu akilishika neno langu, hataonja mauti milele.
53 Wewe u mkuu kuliko baba yetu Ibrahimu, ambaye amekufa? Nao manabii wamekufa. Wajifanya u nani?
54 Yesu akajibu, Nikijitukuza mwenyewe, utukufu wangu si kitu; anitukuzaye ni Baba yangu, ambaye ninyi mwanena kuwa ni Mungu wenu. " mstari huu unaelezea jinsi Bwana alivyokuwa akijaribu kuwaeleza juu ya jambo hili lakini wayahudi hawakutaka kulipokea.
Sehemu nyingine Bwana Yesu aliwaambia wanafunzi wake, mathayo 16:28"Amin, nawaambieni, Pana watu katika hawa wasimamao hapa, ambao hawataonja mauti kabisa, hata watakapomwona Mwana wa Adamu akija katika ufalme wake. " leo hii zipo shuhuda nyingi duniani za watu waliochukuliwa na Bwana pasipo kuonja mauti lakini shetani anataka kuwafanya watu waamini kuwa hilo jambo haliwezekani kwamba ni manabii tu wa zamani ndio walikuwa na uwezo wa kufanya hivyo siku hizi hayo mambo hamna. usidanganyike katika kila kizazi Bwana ana watu wake wanaoshinda. Hivyo maneno haya yanatupa changamoto ya sisi kuongeza uhusiano wetu na Mungu kwasababu hata kanisa litakalokuja kunyakuliwa halitaonja mauti na ni lazima liwe na hiyo imani swali je! wewe unayo? kama hauna ndio wakati wa kuitafuta sasa maana Bwana Yesu mwenyewe alisema luka 18:8”......walakini atakapokuja Mwana wa Adamu, je! Ataiona imani duniani?” kwahiyo ni lazima aione imani kwanza ndipo aje hivyo tuitafute hii imani vinginevyo hatutakwenda kwenye unyakuo kumbuka ni Kristo anayetungojea sisi tuwe wakamilifu ndipo aje kutuchukua na sio sisi tunayemngojea yeye.

Mungu akubariki.

No comments:

Post a Comment