"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Friday, May 4, 2018

UTHABITI WA AGANO LA MUNGU KWA MKRISTO.


Wakati ule baada ya watu kumuudhi sana Mungu hata kufikia hatua ya BWANA kuleta GHARIKA juu ya dunia nzima, Na kama tunavyoijua habari ni Nuhu tu na familia yake ndio waliopona, lakini baada ya hapo BWANA akaweka UPINDE kama ishara ya agano aliloingia na Nuhu pamoja na uzao wake kwamba hataiteketeza tena dunia kwa maji..Tunasoma;

Mwanzo 9: 8 “Mungu akamwambia Nuhu, na wanawe pamoja naye, akisema,
9 Mimi, tazama, NALITHIBITISHA AGANO LANGU NANYI; tena na uzao wenu baada yenu;
10 tena na kila kiumbe hai kilichoko pamoja nanyi, ndege, na mnyama wa kufugwa, na kila mnyama wa mwitu katika nchi pamoja nanyi; wote wanaotoka katika safina, hata kila kilicho hai katika nchi.
11 Na agano langu nitalithibitisha nanyi; wala kila chenye mwili hakitafutwa tena kwa maji ya gharika; wala hakutakuwa tena gharika, baada ya hayo, kuiharibu nchi.
12 Mungu akasema, Hii ndiyo ishara ya agano nifanyalo kati yangu na ninyi, na kila kiumbe hai kilichoko pamoja nanyi, kwa vizazi vyote hata milele;
13 MIMI NAUWEKA UPINDE WANGU WINGUNI, nao utakuwa ni ISHARA YA AGANO kati yangu na nchi.
14 Hata itakuwa NIKITANDA MAWINGU JUU YA NCHI, upinde utaonekana winguni,
15 nami nitalikumbuka agano langu, lililoko kati yangu na ninyi, na kila kiumbe hai katika wote wenye mwili, wala maji hayatakuwa gharika tena kuwaharibu wote wenye mwili.
16 Basi huo upinde utakuwa winguni; nami nitauangalia nipate kulikumbuka agano la milele lililoko kati ya Mungu na kila kiumbe hai katika wote wenye mwili kilichoko katika nchi.
17 Mungu akamwambia Nuhu, Hii ndiyo ishara ya agano nililoliweka kati yangu na wote wenye mwili walioko katika nchi.”

Ni rahisi kulichukulia agano hili kivyepesi vyepesi kwamba linafanya kazi pale tu tufani na gharika kubwa inapotaka kushuka juu ya nchi. Ni kweli kabisa Bwana alimwambia Nuhu ishara hii ya UPINDE wa RANGI SABA, Utaonakana mawinguni, lakini swali! je! ni kweli huu upinde unaonekana mawinguni tu peke yake??.

Kama ulishawahi kuona au kama hujawahi jaribu kufanya utafiti, utagundua kuwa huu upinde upo kila mahali palipo na asili au dalili ya maji. Mimi huwa nikinyeshea bustani kwa mpira nauona ukijiunda maji yanapochuruzika,,wakati mwingine nikiwa naoga na maji ya juu, unaonekana, ukiangali hata sehemu zenye maporomoko ya maji unaonekana, hata katika mito hususani pale jua linapopiga maji n.k. naamini nawe pia ulishawahi kuuona huo upinde mahali fulani tofauti na angani?. Lakini ulishawahi kujiuliza nikwanini unauona hata katika mambo madogo na sio tu mbinguni kwenye mawingu mengi ya mvua?, Hapo kuna jambo Mungu anatufundisha.


Biblia inasema Zaburi 12:6 “Maneno ya Bwana ni maneno safi, Ni fedha iliyojaribiwa kalibuni juu ya nchi; ILIYOSAFISHWA MARA SABA”. Hii ikiwa na maana kuwa AGANO Mungu analoingia na watu wake alilolinena kutoka katika kinywa chake ni thabiti kama madini ya fedha yaliyohakikiwa mara 7, si ajabu hata tunauona UPINDE ukiwa na rangi SABA(7). Ikionyesha kwamba ni agano lililothibitishwa sana..Na ndio maana unaweza ukaliona katika mambo makubwa na madogo, unaweza ukaliona mbinguni na bado ukaliona kwenye ndoo ya maji.

Kumbuka upinde huu unafunua agano Mungu aliloingia na watu wake kwa kupitia damu ya YESU KRISTO mwana wake. Ni Agano lililo thabiti na kuhakikiwa sana, ni Imara kiasi kwamba kwa yeyote atakayeingia katika hilo, iwe ni katika MAMBO MAKUBWA AU MADOGO litakuwa naye kumwepusha na tufani shedtani atakayoileta. Mtu aliye ndani ya hilo agano, Iwe ni katika kushiba au njaa, iwe yupo katika raha au shida, iwe katika kupungukiwa au kuwa ni vingi litakuwa nawe, maadamu tu ameingizwa humo, HAKUNA GHARIKA yoyote ITAKAYOMGHARIKISHA. Na ndio maana biblia inasema;

Warumi 8: 33 "Ni nani atakayewashitaki wateule wa Mungu? Mungu ndiye mwenye kuwahesabia haki.
34 Ni nani atakayewahukumia adhabu? KRISTO YESU NDIYE ALIYEKUFA; NAAM, NA ZAIDI YA HAYO, AMEFUFUKA KATIKA WAFU, yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea.
35 Ni nani atakayetutenga na upendo wa Kristo? Je! NI DHIKI au SHIDA, au ADHA, au NJAA, au UCHI, au HATARI, au UPANGA?
36 Kama ilivyoandikwa, ya kwamba, Kwa ajili yako tunauawa mchana kutwa, Tumehesabiwa kuwa kama kondoo wa kuchinjwa.
37 Lakini katika mambo hayo yote tunashinda, na zaidi ya kushinda, kwa yeye aliyetupenda.
38 Kwa maana nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo,
39 wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu".

Unaona hapo? Unapokuwa katika hilo agano ule upinde ambalo ni agano uliloingia na Bwana kwa kupitia damu ya Yesu Bwana utakupigania usijitenge na Mungu katika hali yoyote ile utakayokuwepo...

Ndugu unapokuwa mkristo fahamu kuwa upo safarini, na kama tunavyofahamu uthibitisho ya kwamba upo safarini ni kukatisha katika mazingira tofuati tofauti, kuna wakati utakutana na milima, kuna mahali utafika utakutana na mabonde, mahali pengine tambarare, kuna mahali utakuta mvua, sehemu nyingine joto n.k. lakini ukiona mazingira hayabadiliki nje basi ujue haupo safarini..upo pale pale...Hivyo usishangae kukutana na hizo hali ni jambo la kawaida.

Mkristo kupitia dhiki, shida, wakati mwingine magonjwa, au kupungukiwa, au njaa haimaanishi kuwa Mungu kakuacha kama wengi wadhanivyo, maadamu upo katika lile AGANO THABITI la Damu ya YESU KRISTO, fahamu kuwa wewe ni MBARIKIWA, japo utapitia hayo tena kwa kitambo tu, Mungu hataruhusu chochote kikugharikishe kabisa..ukumbuke ule upinde unaonekana katika mambo makubwa na madogo. Wapo watu wanahubiri kipimo kwamba kipimo cha kwamba upo katika lile agano ni mafanikio ya kimwili tu wakati wote, kwahiyo mtu yeyote asiyefanikiwa kifedha amelaaniwa..ni safari gani hiyo isiyokuwa na mabonde na milima? biblia inasema; Mhubiri 3:3......... kuna wakati wa Wakati wa kubomoa, na wakati wa kujenga;
4 Wakati wa kulia, na wakati wa kucheka; Wakati wa kuomboleza, na wakati wa kucheza;
5 Wakati wa kutupa mawe, na wakati wa kukusanya mawe; Wakati wa kukumbatia, na wakati wa kutokumbatia;
6 Wakati wa kutafuta, na wakati wa kupoteza; Wakati wa kuweka, na wakati wa kutupa;

Vile vile mambo mengine unaweza ukayaona ni madogo au usiyaone kabisa shetani aliyoyapanga dhidi yako, lakini Mungu anakuepusha nayo pasipo hata wewe kujua, kwa mfano wachawi kwa siri wamepanga kuidhuru familia yako, lakini Mungu anawaepushia mbali na Mungu hakwambii, wakati mwingine unakatisha njiani na nyoka anapita pembeni yako pasipo kukuuma, na wewe hujamwona, pengine utasema mimi sijawahi kukutana na nyoka maisha yangu yote, lakini fahamu umeshapishana nao wengi na kwamba wangekung'ata ungepata madhara makubwa mpaka leo..wakati mwingine umekula chakula chenye sumu pasipo hata wewe mwenyewe kujua, lakini Mungu anakiponya, utasema mimi mwaka mzima nina afya, ninazidi kunawiri lakini kumbuka mfano angeutoa ule UPINDE WAKE katika mambo madogo kama hayo ungekuwa umeshakufa siku nyingi. kila siku kwenye shughuli zako unakutana na mamilioni ya mapepo na majini pengine kukusababishia ajali, wakati mwingine kukuletea uchonganishi, ugomvi, visa, malumbano yasiyokuwa na maana, tamaa, uasherati n.k. vyote hivi Mungu anakuepusha navyo pasipo hata kukwambia. Kwako wewe siku inakuja siku inaenda upo salama...Hujui kuwa ni ule UPINDE wa Agano unatenda kazi ndani yako katika mambo madogo usiyoyajua wewe.

Kwahiyo ndugu ikiwa wewe ni Mkristo nikimaanisha kuwa umeokolewa kwa kumwamini BWANA YESU, na kubatizwa katika ubatizo sahihi kwa kuzamishwa kwa jina la YESU KRISTO kwa ajili ya ondoleo la dhambi na kujazwa Roho mtakatifu na kuishia maisha matakatifu fahamu tu kuwa upo katika mahali salama kabisa kwasababu lile AGANO LA UPINDE linafanya kazi sehemu zote, halipo kwenye tufani kubwa tu, hata katika ndogo. Ni thabiti katika hali zote katika utajiri na umaskini. Lakini kwa yeyote aliye nje ya hilo Agano la Damu ya Yesu hana ulinzi wowote iwe katika utajiri atagharikishwa tu, iwe katika umaskini atagharikishwa tu, iwe katika raha, shida, mafanikio, afya, magonjwa vyovyote vile gharika ikija hata ikiwa ndogo kiasi gani itampeleka tu ...Kwa sababu hakuna UPINDE wa Agano katika maisha yake la kumfanya Mungu akumbuke agano aliloingia na yeye ili amrehemu.

Ndugu nje ya YESU KRISTO hakuna uzima. Yeye ndio njia kweli na uzima, na kumbuka kumwamini Bwana Yesu sio kuongozwa sala ya Toba tu, bali ni kuchukua uamuzi wa kutubu kwa kumaanisha kuziacha kabisa dhambi zako na maisha yako ya zamani, hapo utakuwa umezaliwa mara ya pili, na ndipo lile AGANO LA UPINDE litakapoanza kuonekana katika maisha yako, likitenda kazi katika nyakati za mambo makubwa na mambo madogo.

Ubarikiwe sana.

No comments:

Post a Comment