"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Tuesday, May 1, 2018

YONA: Mlango wa 2


Jina la mwokozi wetu YESU KRISTO libarikiwe.

Karibu katika mwendelezo wetu wa kitabu cha nabii Yona. Tukiwa katika sura ya pili, tulishaona katika sura iliyopita jinsi Yona alivyojitenga na mapenzi ya Mungu kwa kukataa kwenda katika njia zake, na kujikuta akingukia mambo mabaya badala ya mema kwa kumezwa na yule nyangumi mkubwa, na tukaona kuwa habari hiyo inafunua siri ya kanisa la Kristo katika wakati wa siku hizi za mwisho, kwa wale wakristo vuguvugu wa kanisa la mwisho la Laodikia ambalo ndilo tunaloliishi kuwa wataangukia katika tumbo la yule mnyama anayezungumziwa katika (Ufunuo 13&17) hapo itakuwa ni baada ya unyakuo kupita ambacho ndicho kile kipindi cha Dhiki kuu kitakachodumu kwa muda wa miaka mitatu na nusu ya mwisho.

Lakini tunaona katika sura hii ya pili baada ya Nabii Yona kumezwa, kilichofuata akiwa ndani ya lile tumbo la samaki ilikuwa ni mapambano akiishindania NAFSI yake, isiteketee kabisa ndani ya lile tumbo la yule samaki, tunasoma Yona alipitia kipindi kilichokuwa kifupi lakini kigumu sana, kiasi kwamba kilimfanya awe katika MAJUTO makubwa sana, na MAOMBOLEZO yasiyoelezeka... Tusome.

Mlango wa 2

1 Ndipo Yona akamwomba Bwana, Mungu wake, katika tumbo la yule samaki,
2 Akasema, Nalimlilia Bwana KWASABABU YA SHIDA YANGU, Naye akaniitikia; Katika tumbo la kuzimu NALIOMBA, Nawe ukasikia sauti yangu.
3 Maana ULINITUPA VILINDINI, Ndani ya moyo wa bahari; Gharika ya maji ikanizunguka pande zote; Mawimbi yako yote na gharika zako zote zimepita juu yangu.
4 Nami nikasema, Nimetupwa mbali na macho yako; Lakini nitatazama tena kukabili hekalu lako takatifu.
5 Maji yalinizunguka, hata nafsini mwangu; Vilindi vilinizunguka; MWANI ulikizinga kichwa changu;
6 NALISHUKA HATA PANDE ZA CHINI ZA MILIMA; HIYO NCHI NA MAPINGO YAKE YALINIFUNGA HATA MILELE; Lakini umeipandisha nafsi yangu kutoka shimoni, Ee Bwana, Mungu wangu,
7 Roho yangu ilipozimia ndani yangu, Nalimkumbuka Bwana; Maombi yangu yakakuwasilia, Katika hekalu lako takatifu.
8 WATU WAANGALIAO MAMBO YA UBATILI NA UONGO HUJENGA NA REHEMA ZAO WENYEWE;
9 Lakini mimi nitakutolea sadaka kwa sauti ya shukrani; Nitaziondoa nadhiri zangu. Wokovu hutoka kwa Bwana.
10 Bwana akasema na yule samaki, naye akamtapika Yona pwani.
Amen. Hapo tunaweza kuona ni jinsi gani Yona alipitia taabu sana, ni rahisi kuisoma kama habari tu, lakini jaribu kutafakari kwa kina uelewe ni mateso ya namna gani, mtu kukaa kwenye tumbo la kiumbe ambacho hakijui, na kibaya zaidi kipo baharini ingekuwa heri kama kingekuwa ni cha nchi kavu, Yona anasema alipelekwa mpaka katika moyo wa bahari katikati ya vilindi, kwenye baridi kali huko chini, jaribu kifikiria mazingira ya tumboni, biblia inasema yule samaki alikuwa anakula pia na magugu ya baharini(mwani), ambayo yalikuwa yanamsumbua sana kule tumboni, jenga picha ni shida kiasi gani, kumbuka tumboni hamna mwanga, hata hewa yenyewe tunajiuliza alikuwa anapataje pataje katika tumbo lile, alikuwa hali wala hanywi muda wa siku tatu usiku na mchana, na tunafahamu kuna kemikali maalumu za kumeng'enya chakula ambazo ni lazima ziwepo ndani ya matumbo ya wanyama, hivyo mambo hayo yote yalimpata Yona. Na zaidi ya yote alifahamu kabisa hayo yote yalimpata kwasababu ya upumbavu wake, na ndio maana alipokuwa analia na kuomboleza alisema.. "8 WATU WAANGALIAO MAMBO YA UBATILI NA UONGO HUJITENGA NA REHEMA ZAO WENYEWE;". Yona alijitenga na Rehema zake mwenyewe na ndio maana yakampata mambo hayo,

Mfano kamili wa mambo yatakayokuja kulipata hili kanisa la mwisho tunaloishi, siku ile Unyakuo utakapokuwa umepita, Kumbukua watu watakaonyakuliwa watakuwa wachache sana na sio watu wote wa dunia watafahamu kama wengi wanavyodhania, kwasababu zitaonekana kuwa kama habari za kutunga machoni pa watu wengi, na pia hakutaonekana mabadiliko yoyote mbinguni wala duniani, wala hakutakuwa na maajali, au viashiria vyovyote kwamba unyakuo umepita kwasababu litakuwa ni kundi ndogo sana litakalonyakuliwa.

Watakaokuja kufahamu kuwa unyakuo umepita na wao wameachwa, ni wale wakristo wapumbavu ambao nao pia watakuwa wachache, Hawa ndio wale waliokuwa wanajua kabisa unabii wa siku za mwisho, wanafahamu kabisa kuwa Bwana wao yupo karibuni kurudi lakini hawakutaka kujiweka tayari (wapo vuguvugu) leo wanamwabudu Mungu, kesho wanatenda maovu, mfano wa wale wanawali 5 wapumbavu (Mathayo 25) ambao hawakubeba mafuta ya ziada pindi Bwana wao alipokuja awachukue waende karamuni Hivyo kundi hili ndilo litakalolia na kuomboleza mfano wa Yona. Kumbuka hawatukuwa waislamu, au watu wasiomjua Mungu, au wasiojua unabii wa biblia kuhusu habari za siku za mwisho (hawa watapokea chapa ya mnyama kwasababu hawafahamu chochote). Lakini Itakaye muhusu ni yule mkristo anayejua sana maandiko kama wewe unayesoma ujumbe huu na hautaki kugeuka, siku ile mpinga-kristo atatafuta watu wa namna hii ili awameze pale watakapojaribu kukataa mfumo wake(Chapa ya Mnyama).

Kama vile Yona alivyopitia dhiki kuu ndani ya lile tumbo kadhalika hawa nao watapitia dhiki isiyo ya kawaida kama Bwana alivyosema kutakuwa na dhiki kuu ambayo haijawahi kutokea tangu ulimwengu kuwako na wala hatakaa iwako. Usidhani itakuwa ni rahisi kuikataa ile chapa, usidanganyike ni heri usiwepo hicho kipindi kwasababu hutasalimika, kumbuka hutaweza kuajiriwa, kujiajiri kuuza wala kununua bila hiyo chapa, sasa utakula nini usipoweza kununua wala kuuza!..na utajifichia wapi katika jamii ya leo ni dhahiri kuwa mwisho wa siku utashikwa tu,(maana ule mfumo wa mpinga-kristo utashirikiana na vyombo vya dola,) na kupelekwa katika magereza maalumu ya mateso, huko hutakufa leo wala kesho, leo hii hayo magereza yapo tayari, kwasababu ni kikundi kidogo tu kitakacho kamatwa wengine wote watakuwa wanamfurahia mpinga-kristo kama mtu wa amani aliyekuja kuwaondolea watu waovu na wavuruga amani miongoni mwao, wakati huo wanawali wapumbavu walioachwa watakuwa wanalia na kuomboleza kwenye matumbo ya yule mnyama.

KAMA ILIVYOKUWA KATIKA SIKU ZA NUHU:

Siku hizo Bwana alizifananisha na kama zile za Nuhu, kumbuka kabla ya gharika haijaja duniani, HENOKO aliyekuwa mtu wa SABA (7) baada ya Adamu, alinyakuliwa juu asione uharibifu biblia inasema hivyo. Na aliyepata ufunuo wa kuondoka kwa HENOKO alikuwa ni Nuhu pekee yake, hivyo akalazimika kuingia katika ile SAFINA ili aiponye nafsi yake katika mawimbi na misukosuko ya MAJI MENGI kabla ya pepo hazijaanza kuvuma na madirisha ya mbinguni kufunguka.

Vivyo hivyo Henoko anawakilisha watu wa kanisa la 7, ambalo ndilo la mwisho, wakristo waliojiweka tayari bikira safi watakaoenda na Bwana kwenye unyakuo. Hawa Bwana atawaepusha na ile dhiki inayokuja. Lakini Nuhu na familia yake akiwakilisha Wale wanawali waliosalia wasiokuwa werevu iliwabidi waingie kwenye ile NYAMBIZI(SAFINA),hivyo wakagharimika kupitia misukosuko ya mafuriko makubwa katikati ya vilindi vya maji kama tu Yona alivyopitia misukosuko katika tumbo la yule mnyama. Wengi tunadhani Nuhu na familia yake walikuwa wamestarehe kwenye safina wakipata raha, kuna raha gani! kukaa katika kijumba kile chenye giza kwa siku 150, huku mkirushwarushwa na tufani na mafuriko,radi na mingurumo huko nje?..Ni dhahiri kuwa hofu ya Mungu iliwaangukia, kila siku ilikuwa ni kulia na kuomboleza, yamkini Mungu asiwajumuishe pamoja na wale wengine katika adhabu ile.Kumbuka pia ile safina ilikuwa haielei tu muda wote, kutoka na tufani kubwa ilikuwa inazamishwa chini ya maji na kupandishwa juu, na ndio maana biblia inasema ilipigwa LAMI NDANI na NJE, ili maji yasipenye ndani. Kadhalika kama ilivyokuwa katika siku za Nuhu ndivyo itakavyokuwa katika siku zetu, ni mmoja tu aliyeenda kwenye unyakuo ikifunua ni kundi dogo sana litakalonyakuliwa, na pia ni wachache tu waliostahimili misukosuko ambao ni watu 8 tu, ikifunua kuwa wataostahimili dhiki ya siku ile watakuwa ni watu wachache sana.

Hivyo ndugu usitamani uwepo kule, anza kuweka mambo yako sawa, hizo siku zimekaribia sana, ulimwenguni wote umeshadanganywa na shetani, ni kundi dogo la wakristo ndilo analolitafuta, na shabaha yake sio kukufanya uwe baridi la! bali ni kukufanya uwe vuguvugu na ndio tabia iliyotabiriwa kwa kanisa la LAODIKIA kwasababu anajua Bwana anamchukia zaidi mtu aliyevuguvugu kuliko aliye baridi kabisa. Tubu umgeukie Mungu, epuka ibada za sanamu, injili za mafanikio tu huku roho yako unaicha nyuma inaangamia zitakupoteza, acha mavazi ya kutokujisitiri hayo hayamfai kabisa bibi-arusi wa Kristo, tafuta utakatifu, ambao pasipo huo hakuna atakayemwona Mungu asipokuwa nao.Shika NENO la Mungu kwa kudumu katika mafundisho ya biblia tu. 
 
Ubarikiwe.

Pia washirikishe na wengine mambo haya.

No comments:

Post a Comment