"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Wednesday, May 2, 2018

YONA: Mlango wa 3

Bwana wetu YESU KRISTO ahimidiwe milele na milele. AMEN.

Karibu tujifunze Neno la Mungu, leo tukiwa katika ile sura ya 3 ya kitabu cha Nabii Yona. Katika sura zilizotangulia tuliona jinsi taabu na dhiki alizopitia Yona zinafananishwa na dhiki watakazokuja kupitia wakristo waliovuguvugu (wanawali wapumbavu mathayo 25) watakaokosa unyakuo. Pia tuliona kama vile Yona alivyomezwa na Yule samaki mkubwa atokaye baharini na kukaa muda wa siku tatu katika lile tumbo, hawa nao watamezwa na Yule mnyama atokaye baharini mwenye vichwa 7 na pembe 10 (ambaye ni Mpinga-kristo na mfumo wake) kwa muda wa miaka mitatu na nusu katika ile dhiki kuu.(soma Ufunuo 13&17). Hivyo habari ya Yona ni unabii halisi wa mambo yatakayokuja kutokea mwishoni.

Lakini tukiendelea katika hii sura ya 3 tunasoma:

Mlango 3

1 Neno la Bwana likamjia Yona mara ya pili, kusema,
2 Ondoka, uende Ninawi, mji ule mkubwa; ukaihubiri habari nitakayokuamuru.
3 Basi Yona akaondoka, akaenda Ninawi, kama Bwana alivyonena. Basi Ninawi ulikuwa mji mkubwa mno, ukubwa wake mwendo wa siku tatu.
4 Yona akaanza kuuingia mji mwendo wa siku moja, akapaza sauti yake, akasema, BAADA YA SIKU AROBAINI NINAWI UTAANGAMIZWA.
5 Basi watu wa Ninawi WAKAMSADIKI MUNGU; WAKATANGAZA KUFUNGA, wakajivika nguo za magunia, tangu yeye aliye mkubwa hata aliye mdogo.
6 Habari ikamfikia mfalme wa Ninawi, naye akaondoka katika kiti chake cha enzi, akavua vazi lake, akajivika nguo za magunia, na kuketi katika majivu.
7 Naye akapiga mbiu, akatangaza habari katika mji wa Ninawi, kwa amri ya mfalme na wakuu wake; kusema, Mwanadamu asionje kitu, wala mnyama wala makundi ya ng'ombe, wala makundi ya kondoo; wasile, wala wasinywe maji;
8 bali na wafunikwe nguo za magunia, mwanadamu na mnyama pia, nao wakamlilie Mungu kwa nguvu, naam, NAWAGEUKE, kila mtu AKAACHA NJIA YAKE MBAYA, na udhalimu ulio mikononi mwake.
9 Ni nani ajuaye kwamba Mungu hatageuka na kughairi, na kuiacha hasira yake kali, ili msiangamizwe?
10 MUNGU AKAONA MATENDO YAO, YA KUWA WAMEIACHA NJIA YAO MBAYA. Basi Mungu akalighairi neno lile baya, ambalo alisema atawatenda; asilitende”.
Kama tunavyosoma habari hii baada ya Yona kutapikwa na yule samaki, Bwana alimtuma tena kwa mara ya pili Ninawi akawahubirie watu habari za Toba na kwamba wasipotubu baada ya siku 40, Ninawi itaangamizwa. Lakini tunaona watu wale walitii sauti ya Mungu na kutubu.

Lakini ni kitu gani kilichowafanya watubu kirahisi rahisi hivyo?.

Kumbuka kwa wakati ule Ninawi haikuwa na tofauti sana na mji wa Sodoma au Gomora, kwasababu ilikuwa yote ni miji ya kimataifa, watu wasiozijua sheria za Mungu wa mbinguni, ni mataifa yaliyoabudu maelfu ya miungu, yaliyojaa maovu ya kila namna, hivyo ingekuwa ni ngumu sana mtu kujizukia asiye na kitu na asiyejulikana na kuanza kuhubiri habari za kuteketezwa mji wao na mahubiri ya kubadilisha mtindo wa maisha yao. Hivyo ilihitajika kitu kingine cha ziada kuwashawishi wale watu waamini kuwa ni Mungu kweli wa mbinguni anazungumza na wao.

Hivyo Bwana kwa kulijua hilo akaruhusu Yona kwa makusudi akae katika tumbo la samaki siku tatu usiku na mchana bila kufa, kabla ya kwenda Ninawi. Pengine wale watu wa Ninawi walimuuliza Yona ni Ishara gani aliyonayo ili wasadiki kwamba ametumwa na Mungu wa mbinguni?. Na Yona akawasimulia ushuhuda wa maisha yake kwa muda wa siku tatu katika ule mji. Na pia mashuhuda wa jambo hilo walikuwepo, ambao ni wale mabaharia waliosafiri na Yona, ambao ndio baadaye walikuja kumtupa baharini, pengine baadaye walimwona ng'ambo ya pili akihubiri na kuwathibitishia watu kwamba ni kweli alikaa tumboni mwa samaki siku tatu. ndipo watu wa Ninawi wakaogopa sana, na kuchukua hatua ya kulia na kuomboleza juu ya dhambi zao, hivyo wakageuka na kuacha njia zao mbaya.

Vivyo hivyo hukumu ya Mungu ilipokaribia ya kuuteketeza ulimwengu wote tena, kwamba baada ya kipindi kisichokuwa kirefu kutokana na maovu ya watu ghadhabu ya Mungu itamwagwa juu ya ulimwengu mzima kama watu wasipotubu, Hivyo Mungu kwa kuwa ni wa rehema alianza kutanguliza kwanza manabii wake kuhubiri habari za TOBA kwa watu wote ambapo hapo kabla zilikuwa hazihubiriwi kama kiini cha wokovu, ndipo tunamwona Yohana mbatizaji akiwaonya watu watubu kwasababu hukumu ya Mungu imekaribia. Kadhalika na mwisho ya yote akamtuma nabii mfano wa Yona, mwenye ishara kama ya Yona, yamkini watu wa ulimwengu wakiiona hiyo WATUBU kama walivyofanya watu wa Ninawi lakini wasipotubu hukumu ya Mungu inakuja juu yao.

Ndipo Mungu akamtuma mwanae mpendwa Bwana Yesu ambaye kiini cha ujumbe wake kilikuwa ni TOBA ilioambata na ISHARA KUU. Tunasoma katika Mathayo 12:38 mafarisayo walio mfano wa watu wa Ninawi walimuuliza kwa ishara gani unatuonyesha tuamini kuwa hiyo hukumu inayokuja unayoizungumzia ni kweli, ili tupate kutubu...Tunasoma:

"38 Hapo baadhi ya waandishi na Mafarisayo wakamjibu, wakasema, Mwalimu, twataka kuona ishara kwako.
39 Akajibu, akawaambia, Kizazi kibaya na cha zinaa chatafuta ishara, wala hakitapewa ishara, ila ishara ya nabii Yona.
40 Kwani kama vile Yona alivyokuwa siku tatu mchana na usiku katika tumbo la nyangumi, hivyo ndivyo Mwana wa Adamu atakavyokuwa siku tatu mchana na usiku katika moyo wa nchi.
41 Watu wa Ninawi watasimama siku ya hukumu pamoja na watu wa kizazi hiki, nao watawahukumu kuwa wamekosa; kwa sababu wao walitubu kwa mahubiri ya Yona; na hapa yupo aliye mkuu kuliko Yona. "

Umeona hapo? hukumu ya huu ulimwengu ilishatamkwa siku nyingi, na Yona wetu ni Bwana Yesu Kristo kitendo cha kufa na kufufuka kwake haikuwa bure, baada ya kumaliza kazi yake hapa duniani angepaswa apae juu moja kwa moja kama Eliya au Henoko, lakini kizazi hichi kingesadiki vipi kama kisingepewa ISHARA KAMA HIYO?. Hivyo kitendo cha kufa kwake na kukaa siku tatu kaburini na kufufuka ni ishara tosha ya kumfanya kila mwanadamu atubu kwa kuvaa magunia na kuomboleza kama watu wa Ninawi na kuacha njia zake mbaya. Lakini Bwana Yesu alisikitika sana na kusema katika siku ya hukumu watu watakaokihukumu kizazi hiki watakuwa ni wale watu wa Ninawi, Jaribu kutafakari Yona hakufanya miujiza wala kuponya watu, zaidi ya ile ishara ya kumezwa na samaki lakini watu wa Ninawi walitubu, lakini sisi watu wa kizazi hiki tumeona Ishara nyingi za Yesu Kristo licha ya hiyo ya kufa na kufufuka kwake, kuna miujiza na uponyaji wa kiungu vinaambatana naye kila siku lakini bado watu hawataki kutubu. Alisema pia..

Mathayo 11: 20 “Ndipo akaanza kuikemea miji ile ambamo ndani yake ilifanyika miujiza yake iliyo mingi, KWA SABABU HAIKUTUBU.
21 Ole wako, Korazini! Ole wako, Bethsaida! Kwa kuwa kama miujiza iliyofanyika kwenu ingalifanyika katika Tiro na Sidoni, WANGALITUBU ZAMANI kwa kuvaa magunia na majivu.
22 Walakini nawaambieni, itakuwa rahisi Tiro na Sidoni kustahimili adhabu zao siku ya hukumu kuliko ninyi.
23 Nawe Kapernaumu, je! Utakuzwa mpaka mbinguni? Utashushwa mpaka kuzimu; kwa kuwa kama miujiza iliyofanyika kwako ingalifanyika katika Sodoma, ungalikuwapo mji huo hata leo.
24 Walakini nawaambieni, itakuwa rahisi nchi ya Sodoma kustahimili adhabu yake siku ya hukumu kuliko wewe”.

Na kumbuka pia watu wa Ninawi walipewa muda wa kutubu, nao ni siku 40, na si zaidi, baada ya hapo hakuna tena wokovu ghadhabu ikishamiminwa hakuna tena Toba. Vivyo hivyo na sisi tumewekewa muda wa kutubu, sio kila siku tutaliliwa Tubu! tubu! hapana, kuna muda utafika mlango wa neema utakuwa umefungwa, pale Bwana Yesu atakaposimama na kuufunga mlango.

Luka 13: 23 "Mtu mmoja akamwuliza, Je! Bwana, watu wanaookolewa ni wachache? Akawaambia,
24 Jitahidini kuingia katika mlango ulio mwembamba, kwa maana nawaambia ya kwamba wengi watataka kuingia, wasiweze.
25 Wakati mwenye nyumba atakaposimama na kuufunga mlango, nanyi mkaanza kusimama nje na kuubisha mlango, mkisema, EE BWANA, TUFUNGULIE; yeye atajibu na kuwaambia, SIWAJUI MTOKAKO;
26 ndipo mtakapoanza kusema, Tulikula na kunywa mbele yako, nawe ulifundisha katika njia zetu.
27 Naye atasema, Nawaambia, Siwajui mtokako; ondokeni kwangu ninyi nyote mlio wafanyaji wa udhalimu.
28 Ndipo kutakapokuwa na kilio na kusaga meno, mtakapomwona Ibrahimu na Isaka na Yakobo na manabii wote katika ufalme wa Mungu, nanyi wenyewe mmetupwa nje".
Ndugu huu ulimwengu unakaribia kutimiza 40 zake, na dalili zote zinaonyeshwa huu ni wakati wa siku za mwisho, utafika wakati hutaisikia tena injili ya Toba, na hata ukisikia haitakufaidia chochote kilichobaki kwako ni siku ile ya hukumu kusimama mbele ya watu wa Ninawi wakikuhukumu kwanini hukutubu kwa Ishara kuu kama hizi, na zaidi ya yote utakutana na watu wa sodoma na Gomora nao pia watakuhukumu kwamba umestahili adhabu kubwa kuliko wao kwa kuwa uliona ishara nyingi na miujiza mingi kuliko wao na bado haukutubu. Siku hiyo yatakuwa ni maombolezo na majuto kiasi gani.Na siku hiyo inakaribia.

TUBU leo ndugu angali muda upo kumbuka Kutubu maana yake ni KUGEUKA na kuacha njia mbaya, sio kusali sala ya toba tu, halafu basi, ndio maana tunasoma pale Mungu aliyatazama MATENDO ya watu wa Ninawi kama kweli wamegeuka au la!! . na sio maombolezo yao peke yake na alipoona matendo yao wamegeuka alighahiri mabaya yale.,Na wewe fanya vivyo hivyo, Kristo bado hajaja, ila hivi karibuni anakuja kumnyakua yule aliyekuwa tayari kwenda nae.

Mungu akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine mambo haya. usikuose mwendelezo wa kitabu hichi.

No comments:

Post a Comment