"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Monday, June 18, 2018

MASWALI NA MAJIBU: SEHEMU YA 30

SWALI: Kwanini kuna watu wanafanyiwa delivarance (Maombi ya kufunguliwa), lakini baada ya muda wanarudiwa tena na hali ile ile sababu ni nini?.

JIBU: Tunakosa maarifa tukidhani kuwa tunapowaombea watu maombi ya kufunguliwa kwa mfano kutoa Pepo.Ni kwamba tunawatoa kweli wale Pepo na hapo hapo mtu yule anakuwa ameshafunguliwa, Hapana ukweli ni kwamba hatutoi pepo moja kwa moja bali tunakuwa TUNAWAFUKUZA PEPO KWA MUDA TU wanakwenda  mahali watakapokaa  pale kwa kipindi fulani cha muda. Na baadaye wakisha tulia kwa muda,wana tabia ya kurudi kuangalia maskani zao za kwanza zikoje, Kwasababu kama ingekuwa ndio hivyo kirahisi rahisi tu Bwana asingesema tena maneno haya;

Mathayo 12: 43 Pepo mchafu, amtokapo mtu, hupitia mahali pasipo maji, akitafuta mahali pa kupumzika, asipate.
44 Halafu husema, Nitarudi nyumbani kwangu nilikotoka; hata akija, aiona tupu, imefagiwa, na kupambwa.
45 Mara huenda, akachukua pamoja naye pepo wengine saba walio waovu kuliko yeye mwenyewe, nao huingia na kukaa humo; na mtu yule hali yake ya mwisho huwa mbaya kuliko ya kwanza. Ndivyo itakavyokuwa kwa kizazi hiki kilicho kibaya.
Unaona? Watu wengi wanaosumbuliwa na vifungo vya shetani au mapepo, kwa kudhani kuwa mtumishi yule anapomwombea na pepo kulipuka ndio kafunguka moja kwa moja, hapana hiyo ni hatua ya kwanza ya yule pepo kukuacha, ila bado yupo na wewe, bado ana hati zote za kukumiliki wewe.



Hivyo kwa wakati ule mfupi baada ya kuombewa kwa Imani huyo Pepo ataondoka,  na baada ya hapo  utaanza kuona unafuu mkubwa katika maisha yako kwa kipindi kifupi tu cha wakati. Lakini yule pepo aliyefukuzwa hawezi kuiachia milki yake kirahisi hivyo anachofanya, ni kurudi kuona je! yule mtu analo badiliko lolote katika maisha yake?. Na kama asipoona ndio anakwenda kuchukua mapepo mengine saba maovu kuliko yeye (anafanya hivyo ili kwamba siku nyingine asisumbuliwe kutolewa kirahisi), na ndio unakuta yule mtu yale matatizo aliokuwa nayo kwanza yanarudi na kuzidi kuwa  mengi, hali yake ya mwisho inakuwa mbaya kuliko ile ya kwanza.
Zipo shuhuda nyingi ndio utasikia mtu anasema nilikwenda kuombewa na mtumishi fulani, nikapona ugonjwa uliokuwa unanisumbua pale pale lakini baada ya mwezi ile hali imenirudia tena, na safari hii ndio imekuwa mbaya zaidi kuliko hata ya mwanzo..Sasa wengi wa watu kama hawa hawajajua au hawajafundishwa utendaji kazi wa hizi roho ovu.Kumbuka KUFUNGULIWA kwa mtu, kunaanzana na yeye mwenyewe, ikiwa mtu hataki kufunguliwa basi hata aombeweje hawezi kufunguka. Kadhalika watu hawajui kuwa vipo vifungo/mapepo mengine ambayo hayajidhihirishi kwa nje(yaani hayalipuki) kama mengine mapepo mengine yanavyofanya. yamekaa ndani tu,na mengine yanakuja ndani ya mtu na kuondoka, hivyo haya yote huwezi kuyatambua kwa kutegemea kusubiria uombewe. Ni lazima ufahamu mtu yoyote ambaye hajazaliwa mara ya pili (yaani kwa kumwamini YESU KRISTO na kubatizwa katika ubatizo sahihi) kwa namna moja au nyingine kuna roho au vifungo vya uovu vinaambatana naye hatakama yeye anajiona yupo sawa. 

Hivyo basi pepo linapofukuzwa ndani ya mtu, ni wakati wa mtu yule haraka sana kuchukua hatua ya kumkabidhi Bwana maisha yake yote kwa kumaanisha kuacha maisha ya dhambi na kubatizwa katika ubatizo sahihi na kupokea Roho Mtakatifu. Kwa kufanya hivyo atakuwa ameondoa hati miliki zote za pepo lile kurudi, na sio tu mapepo yale yanayojidhihirisha bali hata na yale  yasiyojidhihirisha yanakuwa hayana nafasi ya kurudi na hivyo mtu yule anakuwa UMESHAFUNGUKA KIKABISA KABISA. Na ndio maana Bwana alipokwisha kuwafungua watu aliwaambia wasitende dhambi tena, maana ya kutokutenda dhambi ni kumwamini yeye (Bwana Yesu, kwa kutubu na kuzaliwa mara ya pili).
Hivyo deliverance ambayo itaweza kumfungua mtu MOJA KWA MOJA ni kuzaliwa mara ya pili, na sio kuombewa tu na pepo kulipuka halafu basi.

Ubarikiwe.

SWALI:Inaruhusiwa kwa mkristo aliyeokolewa na BWANA WETU YESU kuangalia michezo ya mpira?(Kombe la dunia)?

 JIBU: Michezo kwa ujumla hatuwezi tukasema  moja kwa moja kama inaruhusiwa au hairuhusiwi, Jambo la Msingi biblia inatuonya ni hili. Mithali 4: 23 “Linda moyo wako kuliko yote uyalindayo; Maana ndiko zitokako chemchemi za uzima”. Hivyo tukilijua hilo kwa jinsi tulivyo hapa duniani hususani katika kizazi hichi tunachoishi sasa hivi mambo MAOVU, yasiyokuwa na maana yameongezeka na kuwa mengi, unakuta hata ile nafasi ya Mungu inachukuliwa na mambo ya kidunia, burudani, michezo na starehe, kiasi kwamba hata ule muda mtu angeweza kukaa chini kumtafakari Mungu au kwenda ibadani anaugeuza na kuwa muda wake wa kufanya starehe na kwenda kuburudika viwanjani sasa mambo kama hayo ni IBADA ZA SANAMU ZA HALI YA JUU na ni machukizo makubwa mbele za Mungu. Kwa maana siku za mwisho biblia ilishatabiri na kusema:
(2Timotheo 3:4) watu watakuwa wakipenda ANASA kuliko kumpenda Mungu. Unaona hapo? Biblia pia inatuambia tuwe na kiasi katika mambo yote.

 Kwahiyo kutazama mpira au kucheza au kushiriki katika mchezo wowote ule ni lazima uangalie au uzingatie mambo yafuatayo. 
1) Je! Yanachukua muda wako kwa Mungu.
2) Na je!Yana madhara yoyote katika Imani yako?. 
Wapo watu wameathiriwa na michezo mpaka wanakuwa hawawezi tena kufanya mambo mengine pasipo hiyo(kwamfano MIPIRA), kadhalika ipo michezo anayoenda kinyume kabisa na misingi ya kibiblia hivyo moja kwa moja huathiri Imani ya mtu huyo anapocheza au anapoitazama kwamfano “mieleka”, n.k. Zote hizo ni machukizo mbele za Mungu aidha kushiriki au kutazama. Lakini pia mtu kujishughulisha ni michezo kama sehemu ya mazoezi kwamfano riadha, kuogolea, n.k. Hii haina madhara kwa mkristo uyafanye tu katika BWANA na kwa utukufu wa Mungu, labda ihusishwe na mambo mengine, (hususani katika eneo la mavazi  na mitindo ya maisha) lakini kiujumla kama ikiwa ni kwa kiasi hakuna tatizo. Kushiriki au kutazama.
Kwahiyo kikubwa zingatia lile Neno kama tulivyosema “Mithali 4: 23 “Linda moyo wako kuliko yote uyalindayo; Maana ndiko zitokako chemchemi za uzima”. Kama vinakukosesha au vinakuathiri basi moja kwa moja usishiriki wala kutazama kwa usalama wa Roho yako. Wala usivizunguzie kabisa.

Marko 9:43 “Na mkono wako ukikukosesha, ukate; ni afadhali kuingia katika uzima u kigutu, kuliko kuwa na mikono miwili, na kwenda zako jehanum, kwenye moto usiozimika; 44 ambamo humo funza wao hafi, wala moto hauzimiki. 45 Na mguu wako ukikukosesha, ukate; ni afadhali kuingia katika uzima, u kiwete, kuliko kuwa na miguu miwili, na kutupwa katika jehanum; 46 ambamo humo funza wao hafi, wala moto hauzimiki. 47 Na jicho lako likikukosesha, ling'oe, ulitupe; ni afadhali kuingia katika ufalme wa Mungu, una chongo, kuliko kuwa na macho mawili, na kutupwa katika jehanum; 48 ambamo humo funza wao hafi, wala moto hauzimiki.”

SWALI: Mtumishi mti wa MLOZI alioonyeshwa nabii Yeremia 1:12 tafsiri yake ni nini?

Ubarikiwe ndugu...Mlozi ni mti fulani, unaositawi sana sana huko mashariki ya kati (Lebanoni, Israeli, Palestina n.k.).Jina lake kwa kiyahudi unaitwa "SHAKEI" na tafsiri yake ni  KUTAZAMA/KUANGALIA...Kwahiyo Yeremia kuonyeshwa pale Mti wa Mlozi ni lugha tu ya picha anayoonyesha kwamba Bwana ANATAZAMA, na je! anatazama nini?..Anatazama NENO lake ili alitimize alilinena juu ya Israeli..na ndio maana ukisoma hapo anasema..

Yeremia 1: 11 Tena neno la Bwana likanijia, kusema, Yeremia, waona nini? Nikasema, Naona ufito wa mlozi.
12 Ndipo Bwana akaniambia, Umeona vema, kwa maana ninaliangalia neno langu, ili nilitimize...
Kumbuka pia Mungu huwa anatazama Neno lake ili alitimize kwa namna zote, Hivyo kama ni jema, ni lazima alitimize, na kama ni baya juu ya watu wake ni lazima alitimize pia!.Kote kote.

Lakini tunaona Israeli walikuwa waasi kwa Mungu tangu zamani, ukisoma katika habari za wafalme utaona jambo hilo, jinsi walivyokuwa wanamuasi Mungu mpaka akawaapia kuwa wataenda utumwani tena Babeli, kwa vinywa vya manabii wake waliotangulia kabla ya Yeremia mfano Isaya n.k. Na ndio maana hapo Yeremia anaonyeshwa kama  UFITO(FIMBO) tu, ya mlozi, Ikimaanisha kuwa Mungu analitazama NENO lake, na kulitimiza juu yao kama ADHABU na sio BARAKA...kwasababu FIMBO ni kwaajili ya kuadhibu siku zote tunajua hilo. Hivyo Ukizidi kuendelea mistari inayofuata ndio utaona mabaya yote Mungu aliyoyanena juu ya yao.

Ubarikiwe sana ndugu.

No comments:

Post a Comment