"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Wednesday, February 27, 2019

SIRI YA MUNGU.


Shalom Mwana wa Mungu, karibu tujifunze biblia, chakula cha uzima, kitupacho afya rohoni, leo kwa Neema za Bwana tutajifunza kwa ufupi, juu ya SIRI YA MUNGU.
Biblia imetaja sehemu kadha wa kadha juu ya Siri ya Mungu, na leo tutajifunza hii siri ya Mungu ni ipi.
Warumi 16: 25 “Sasa na atukuzwe yeye awezaye kuwafanya imara, sawasawa na injili yangu na kwa kuhubiriwa kwake Yesu Kristo, sawasawa na ufunuo wa ile SIRI iliyositirika tangu zamani za milele”.
Unaona hapo, biblia imetaja kuwa ipo SIRI iliyokuwa imesitirika tangu zamani za milele.
Sasa kabla ya kwenda kujifunza hiyo siri ni ipi, ni vizuri kwanza tukaelewa neno SIRI lina maana gani kama lilivyotafsiriwa katika biblia yetu hii ya Kiswahili, Kumbuka lugha yetu ya Kiswahili haijajitosheleza kwa maneno mengi, kwamfano yapo maneno katika lugha ya kiingereza au kigiriki ambayo ukiyaleta katika lugha yetu ya Kiswahili yanakosa tafsiri. Na pia yapo maneno yetu ya lugha ya Kiswahili ambayo ukiyapeleka katika lugha ya kiingereza yanakosa tafsiri, kwa mfano neno “shikamoo” halina tafsiri kwa kiingereza. Lakini pia yapo maneno ya kiingereza yenye tafsiri zinazokaribiana sana hivyo yakiletwa katika lugha yetu ya Kiswahili yanatumia tafsiri moja, kwamfano neno la kingereza “mouse” na “rat” tafsiri yake kwa kiswahili ni moja tu ambayo ni panya, hali kadhalika maneno mengine kama “rabbit” na “hare” yote kwa Kiswahili tafsiri yake ni “sungura”

Lakini pia kuna maneno mawili ya kiingereza yenye maana zinazokaribiana sana lakini hayafanani..na maneno hayo ni “Secret” na “mystery”…yote tukiyaleta katika lugha yetu ya Kiswahili yana tafsiri moja yaani “SIRI” lakini yana maana mbili tofauti.
“Secret” ni neno la kiingereza lenye maana ya “kipande cha taarifa ambacho kinajulikana na mtu mmoja au zaidi ya mmoja, na kimehifadhiwa kisijulikane na watu wengine zaidi ya hao wanaokijua”…kwamfano wahalifu wawili wanapopanga njama ya kuvamia mafali fulani hiyo njama ni “siri”, au vikundi fulani vya upelelezi huwa vinafanya kazi zao katika siri, ikiwa na maana vina baadhi ya taarifa ambazo ni wao tu wanaozijua na hawampi mtu mwingine yeyote taarifa hizo, (wanafanya kazi zao katika siri).

Lakini tukirudi kwenye neno la pili la kiingereza linaloitwa “mystery” ambalo kwa Kiswahili limetafsiriwa hivyo hivyo “siri” lenyewe lina maana tofauti kidogo, neno hili mystery tafsiri yake halisi ni hii “ni taarifa ambazo hazijulikani na mtu hata mmoja, hazijulikani chanzo chake, wala sababu ya jambo hilo”..kwamfano mtu anapowasha taa na giza kuondoka, ulishawahi kujiuliza lile giza linakwenda wapi? Hakuna mtu anayejua, wala huwezi kupata jibu la hilo swali kwa mtu yeyote Yule, kwahiyo hiyo inajulikana kama mistery “Mystery”, ambapo kwa Kiswahili tunaweza kusema ni siri ya ndani sana isiyoweza kueleweka wala kuchunguzika.
Biblia inasema katika: 

Ayubu 38: 19“Iko wapi njia ya kuyafikia makao ya nuru? Na giza pia, mahali pake ni wapi? 20 Upate kuipeleka hata mpaka wake, Upate kuelewa na mapito ya kuiendea nyumba yake?”
 
Ayubu 38: 24 “Je! Nuru hutengwa kwa njia gani, Au upepo wa mashariki hutawanywaje juu ya nchi?”
 
Hizo zote ni mystery au siri za ndani zisizoelezeka. Hali kadhalika jinsi mtoto anavyoumbika katika tumbo la mwanamke, hakuna ajuaye ni nani alipeleka mifupa migumu kule, ni nani aliingiza nywele, n.k. vyote hivyo vinabakia katika siri kuu sana (Mysteries), zisizojulikana na kushangaza watu.

Sasa baada ya kuelewa hayo, tukirudi kwenye biblia kuna kitu kinachoitwa SIRI YA MUNGU, kama tulivyotangulia kusema…sasa hiyo siri inayozungumziwa hapo sio siri yenye tafsiri ile ya kwanza “secret” bali ni siri yenye tafsiri ile ya pili “mystery”, Kwahiyo siri ya Mungu haikuwa ni kipande cha taarifa fulani kilichojificha kilichojulikana na baadhi ya watu wachache tu, na kwamba kisingepaswa kijulikane na watu wengine, hapana badala yake bali siri ya Mungu ilikuwa ni taarifa au jambo ambalo lililokuwa halijulikani na mtu awaye yeyote Yule hata MALAIKA wa mbinguni, walikuwa hawalijui wala hawalielewi, hakuna taarifa zozote kuhusiana na hilo jambo, mtu anaweza akakisia tu lakini asiwe na taarifa zozote sahihi kuhusiana na hilo jambo, kama tu vile tusivyoelewa giza huwa linakwenda wapi pindi mwanga unapokuja, na linatokea wapi pindi mwanga unapoondoka..wala hakuna mtu yeyote anaweza kutupa majibu ya hayo maswali, kadhalika na siri ya Mungu ndio ilikuwa hivyo hivyo(ilikuwa ni mystery na sio secret).
 
Sasa hii SIRI ya ajabu ya Mungu ilikuwa ni ipi?

Mtume Paulo alitoa majibu ya swali hilo kwa uwezo wa Roho.

Wakolosai 1:26 “SIRI ile iliyofichwa tangu zamani zote na tangu vizazi vyote, bali sasa imefunuliwa kwa watakatifu wake; 27 ambao Mungu alipenda kuwajulisha jinsi ulivyo utajiri wa utukufu wa SIRI HII KATIKA MATAIFA, nao ni KRISTO NDANI YENU, TUMAINI LA UTUKUFU 28 ambaye sisi tunamhubiri habari zake tukimwonya kila mtu, na kumfundisha kila mtu katika hekima yote, tupate kumleta kila mtu mtimilifu katika Kristo”.

Unaona hapo, biblia inasema siri ambayo ilikuwa imefichwa tangu vizazi vyote, ikiwa na maana hakuna mtu aliyekuwa anaijua, lakini ilifunuliwa zamani za mitume, na siri hiyo haikuwa nyingine zaidi ya KRISTO YESU KUINGIA ndani yetu sisi watu wa MATAIFA. Haleluyaa!!

Tangu zamani yote, hakuna mtu angeweza kudhania kuwa sisi watu wa mataifa tungekuja siku moja kuwa wana wa Mungu, sisi tuliokuwa tunaitwa najisi, watu tuliokuwa mbali na Mungu, hakuna mtu angetegemea siku moja Wana wa Farao waliowatesa wana wa Israeli kwamba wangekuja kuitwa wana wa Mungu aliye juu, hakuna mtu angedhania kuwa wafilisti watu waliokuwa wanaitwa wasiotahiriwa kwamba siku moja watakuja kuitwa wana wa Mungu aliye juu, hakuna mtu angekuja kujua kuwa wamoabi waliowalaani wana wa Israeli wakati wanaelekea nchi ya ahadi, siku moja watakuja kuitwa wabarikiwa wateule wa Mungu aliye juu kwa kupitia Yesu Kristo, Ingekuwaje kuwaje kwanza ni sawasawa na sasahivi mtu akwambie kuna wakati utafika wachina wote wataitwa wamasai tena wamasai wa damu kabisa, ni jambo lisilosadikika. hakika hiyo ilikuwa ni siri ya ajabu ambayo isingeweza kudhaniwa na mtu yeyote, ni siri ambayo hata malaika walikuwa hawaijui. Lakini ilikuja kufunuliwa siku za mwisho.

Hakuna mtu angeweza kudhania kuwa MASIHI ambaye ametabiriwa kuja kuwaokoa wana wa Israeli peke yao, angekuja kwanza kuanza wokovu kwa watu wa mataifa, wanaoabudu sanamu, hakuna mtu au malaika angeweza kudhania kuwa siku moja Roho mwenyewe wa Mungu atakaa ndani ya watu wa mataifa. Hata malaika wa mbinguni hawakujua hiyo neema imetoka wapi, kama vile tusivyojua giza chanzo chake ni wapi, hiyo ni mystery.

Kwahiyo YESU KRISTO, kuja kutuokoa sisi watu wa MATAIFA hiyo ndiyo ilikuwa SIRI YA MUNGU, iliyofichika tangu zamani za milele, hata Musa alikuwa hajui kwamba siku moja Uzao wa Farao utamwabudu Mungu wa Israeli kupitia Masihi, hata Eliya alikuwa hajui kwamba siku moja wale alioomba moto ushuke juu yao watoto wao watakuja kumjua Mungu wa kweli na kupata kibali mbele za Mungu, Hata Daudi hakujua kwamba wale aliokuwa anawaimbia maadui maadui siku moja watakuja kuwa marafiki wa karibu wa Mungu kupitia BWANA WA UTUKUFU YESU KRISTO.
Waefeso 3:1 “Kwa sababu hiyo mimi Paulo ni mfungwa wake Kristo Yesu kwa ajili yenu ninyi Mataifa;
2 ikiwa mmesikia habari ya uwakili wa neema ya Mungu niliyopewa kwa ajili yenu;
3 ya kwamba kwa kufunuliwa nalijulishwa SIRI HIYO, kama nilivyotangulia kuandika kwa maneno machache
4 Kwa hayo, myasomapo, mtaweza kuutambua ufahamu wangu katika SIRI YAKE KRISTO.
5 SIRI HIYO HAWAKUJULISHWA WANADAMU KATIKA VIZAZI VINGINE; kama walivyofunuliwa mitume wake watakatifu na manabii zamani hizi katika Roho;
6 YA KWAMBA MATAIFA NI WARITHI PAMOJA NASI WA URITHI MMOJA, na wa mwili mmoja, NA WASHIRIKI PAMOJA NASI WA AHADI YAKE ILIYO KATIKA KRISTO YESU KWA NJIA YA INJILI”
7 Injili hiyo ambayo nalifanywa mhudumu wake, kwa kadiri ya kipawa cha neema ya Mungu niliyopewa kwa kadiri ya utendaji wa uweza wake.
8 Mimi, niliye mdogo kuliko yeye aliye mdogo wa watakatifu wote, nalipewa neema hii ya kuwahubiri Mataifa utajiri wake Kristo usiopimika;
9 NA KUWAANGAZA WATU WOTE WAJUE HABARI ZA MADARAKA YA SIRI HIYO, ambayo tangu zamani zote ilisitirika katika Mungu aliyeviumba vitu vyote;
10 ili sasa, kwa njia ya kanisa, hekima ya Mungu iliyo ya namna nyingi ijulikane na falme na mamlaka katika ulimwengu wa roho;
11 kwa kadiri ya kusudi la milele alilolikusudia katika Kristo Yesu Bwana wetu”.
Mstari wa 9 unasema “NA KUWAANGAZA WATU WOTE WAJUE HABARI ZA MADARAKA YA SIRI HIYO”.
Ndugu unayesoma ujumbe huu, ukimjua Yesu Kristo, kwa mapana haya au zaidi ya haya, utaogopa!! Utajua ni jinsi gani hatukustahili lakini tumefanywa tustahili, utajua ni jinsi gani Neema ya Mungu inatisha,..kwasababu kama linafanyika jambo ambalo kwa namna ya kawaida haliwezekani, wala halielezeki, hiyo inatisha!! Hakuna mtu yeyote anayeweza kuelezea hii neema imetoka wapi? Kila mtu anashangaa hata malaika…iweje hawa watu wasiofaa wapokee kipawa cha neema kubwa namna hii? Manabii wa zamani na wenyewe walionjeshwa kidogo tu! Lakini bado hawakuielewa. Waliona tu lakini wasielewe chochote, pengine walidhani watu wa mataifa watakujua kumweshimu masihi tu, lakini sio kufanywa na wao warithi wa ahadi za Mungu.
 
Ndugu, usiudharau msalaba, Kristo amehubiriwa kwako mara ngapi?..utapataje kupona usipouthamini wokovu MKUU namna hii?? Waebrania 2:3…kumbuka maisha yako ni kitabu na matendo yako ni kalamu yenye wino, yanaandika matendo yako kila siku, kila mwezi na kila mwaka,. siku inapopita ni unaanza aya mpya, kila mwezi ni unafungua ukurasa mpya, na kila mwaka ni unaanza sura mpya ya kitabu chako,. Na kitabu chako unaanza kukiandika siku unapozaliwa…na kinaanza na JINA LAKO kwa nje, ndio maana baada ya kuzaliwa tu unapewa jina, na pengine umeshaandika nusu ya kitabu chako mpaka kufikia sasa, jitathmini katika hiyo nusu uliyoiandika umeandika ipasavyo?, siku ile ya mwisho kitabu chako kitafunguliwa tena maandiko yanasema hivyo na kitalinganishwa na kile kitabu cha uzima kama matendo yaliyoandikwa kwenye kitabu chako hayafanani na matendo ya kile kitabu cha Uzima, sehemu yako itakuwa ni katika lile ziwa la moto. Huko ndiko kukosekana jina lako katika kitabu cha uzima. Na kumbuka mbinguni hakuna makaratasi, hivyo kitabu cha uzima sio makaratasi yaliyoandikwa majina kama nakala za ankra, hapana bali na chenyewe ni maisha yaliyoandikwa, na cha kuogopesha ni kwamba hayo maisha sio mengine zaidi ya maisha ya watu yaliyoandikwa kwenye biblia, maisha ya mitume, maisha ya Yesu Kristo, maisha ya watakatifu wote, na Maneno yao waliyoyahubiri katika Roho, Ndio maana unaona biblia ni kitabu kilichojaa habari za maisha ya watakatifu, watu siku ya mwisho ndio watahukumiwa kulingana na hayo. Paulo anasema katika kitabu cha Warumi 2:16 “katika siku ile Mungu atakapozihukumu siri za wanadamu, sawasawa na injili yangu, kwa Kristo Yesu”

Ufunuo 20: 11Kisha nikaona kiti cha enzi, kikubwa, cheupe, na yeye aketiye juu yake; ambaye nchi na mbingu zikakimbia uso wake, na mahali pao hapakuonekana.
12 Nikawaona wafu, wakubwa kwa wadogo, wamesimama mbele ya hicho kiti cha enzi; NA VITABU VIKAFUNGULIWA; na kitabu kingine kikafunguliwa, AMBACHO NI CHA UZIMA; na hao wafu wakahukumiwa katika mambo hayo yaliyoandikwa katika vile vitabu, sawasawa na matendo yao……… 15 Na iwapo mtu ye yote hakuonekana ameandikwa katika kitabu cha uzima, alitupwa katika lile ziwa la moto”

Kwahiyo usiidharau sauti ya Mungu inapozungumza nawe moyoni, Bwana anataka kukupa uzima wa milele na kukuepusha na hukumu unayokuja, tumefunuliwa hii siri ya Mungu, ambao wakina Musa walitamani kuijua lakini hawakuijua, na manabii wengine wote vivyo hivyo, kwahiyo saa ya wokovu ni sasa, sio baadaye wala kesho, kama hujayakabidhi maisha yako kwa Bwana fanya hivyo leo, hata kama wewe ni muislamu au mbudha unasoma ujumbe huu, siku ile hutasema hukusikia, na kumpa Bwana maisha sio kumpa lisaa, au masaa au siku, hapana unampa maisha yako yote yaani kuanzia leo na kuendelea mpaka siku utakapoondoka duniani, unakusudia kuishi kwa kumfuata yeye, katika njia zake zote, unakusudia kuacha dhambi zote ulizokuwa unafanya kama uasherati, ulevi, anasa, usengenyaji, chuki, kutokusamehe, usagaji, utoaji mimba,ushoga, utazamaji pornography, masturbation, disco, uvaaji wa vimini na suruali, na upakaji wa makeup mpaka unatoka kwenye asili yako ya ubinadamu n.k .

Yeye anakubali wakosa na atakupa uwezo wa kushinda dhambi, , kwasababu kwa nguvu zako hutaweza kushinda dhambi hata kidogo....yeye ndiye atakuwezesha kwa namna ya ajabu utajikuta unashinda mambo hayo endapo utakubali kumfuata, wengine tulikuwa wabaya kuliko wewe lakini Bwana alitutengeneza, tulikuwa tunadhani ilikuwa haiwezekani kuishi bila kufanya hayo mambo, lakini tumeahakikisha maneno ya Mungu ni kweli kuwa ni rahisi na ni raha sana kuishi bila hayo mambo, na hatuna tena mizigo wa dhambi,na hakuna kiu tena hata kidogo ya hayo mambo, kama aliyafanya kwetu, atayafanya na kwako pia, isipokuwa Bwana anataka watu wanaomaanisha sio watu wanaositasita katika mawazo mawili, ukishakusudia kwa matendo kuacha hayo mambo haraka sana bila kupoteza muda nenda kabatizwe katika ubatizo sahihi kulingana na maandiko ambao ni wa kuzamishwa katika maji mengi na kwa Jina la Yesu Kristo kulingana na (Matendo 2:38), ili upate ondoleo la dhambi zako. Na baada ya hapo utakuwa milki halali ya Roho wa Mungu, utafanyika kuwa hekalu la Mungu kwa Roho atakayeingia ndani yako.
 
Na kama ulirudi nyuma, shetani anataka urudi zaidi ya hapo, nia yake ni akupeleke kwenye ziwa la Moto, hiyo ndiyo ndoto yake kubwa, sasa usikubali ndoto ya shetani itimie juu ya maisha yako, ziwa la moto aliandaliwa yeye na malaika zake..lakini anataka na wewe uende huko, hivyo mpinge na Bwana atakuwa upande wako.

Mungu akubariki sana.

No comments:

Post a Comment