"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Saturday, June 15, 2019

UFUNUO: Mlango wa 9.


Shalom.Karibu katika mwendelezo wa kitabu cha Ufunuo, ni vizuri ukakisoma kitabu hichi peke yako kwanza kwa utulivu, na katika uwepo wa Bwana, na kufuatilia mfululizo huu tangu mwanzo ili tunapoendelea katika sura hizi zinazofuata usibakie nyuma twende pamoja.

Katika sura iliyopita tuliona jinsi wale malaika 7 walivyopewa baragumu zao na  pindi walipozipuliza/kuzipiga ni nini kilitokea, Na tulishaona baragumu nne za mwanzo…kama hujapitia pia ni vizuri ukapitia au bofya hapa⏩ Ufunuo:Mlango wa 8. Na tuliona kuwa baragumu hizo ni kama mwanzo wa utungu tu! Wa vile vitasa saba vitakavyokuja kuachiwa huko mbeleni katika siku ile kuu ya Bwana.…Ni sawa na mtu anayenawa uso kwa muda tu! Lakini baadaye atakuja kuoga mwili mzima.

Vile vile tuliona  pia  hizi baragumu zitaanza kupigwa mara baada ya unyakuo kupita tu! Na zile tatu za kwanza Zitawaathiri sana wayahudi walioopo Israeli (na watu wanaoishi mashariki ya kati), isipokuwa lile la 4 ambalo litaathiri dunia nzima, kwasababu jua likipigwa ni dunia nzima itaathirika na sio sehemu tu!..na mapigo hayo yatatekelezwa kupitia wale mashahidi wawili waliozungumziwa katika ufunuo 11.

Ufunuo 11:3 “Nami nitawaruhusu mashahidi wangu wawili, nao watatoa unabii siku elfu na mia mbili na sitini, hali wamevikwa magunia.

4 Hao ndio ile mizeituni miwili na vile vinara viwili visimamavyo mbele za Bwana wa nchi.

5 Na mtu akitaka kuwadhuru, moto hutoka katika vinywa vyao na kuwala adui zao. Na mtu akitaka kuwadhuru, hivyo ndivyo impasavyo kuuawa.

6 Hao wana amri ya kuzifunga mbingu, ili mvua isinyeshe katika siku za unabii wao. Nao wana amri juu ya maji kuyageuza kuwa damu, na kuipiga nchi kwa kila pigo, kila watakapo”.

Unaona Mashahidi hawa wawili wataleta mapigo hayo kwa amri ya Bwana kama vile Musa alivyoleta mapigo juu ya Farao kwa Amri ya Bwana.

Na mwishoni mwa sura ya 8, tuliona pia kulikuwa na malaika (Tai) aliyeruka katika anga na kutangaza ole kwa wote wanaokaa juu ya nchi kwasababu ya sauti ya zile baragumu 3 zilizosalia, yaani baragumu la 5,6 na la 7.


Hivyo leo tunaendelea na sura ya 9 kwa Neema za Bwana..ambayo inaelezea juu ya baragumu zilizosalia isipokuwa ile ya saba tu.


Ufunuo 9: 1 “Malaika wa tano akapiga baragumu, nikaona nyota iliyotoka mbinguni, imeanguka juu ya nchi; naye akapewa ufunguo wa shimo la kuzimu.

2 Akalifungua shimo la kuzimu; moshi ukapanda kutoka mle shimoni kama moshi wa tanuru kubwa; jua na anga vikatiwa giza kwa sababu ya ule moshi wa shimoni.

3 Nzige wakatoka katika ule moshi, wakaenda juu ya nchi, wakapewa nguvu kama nguvu waliyo nayo nge wa nchi.

4 Wakaambiwa wasiyadhuru majani ya nchi, wala kitu cho chote kilicho kibichi, wala mti wo wote, ila wale watu wasio na muhuri ya Mungu katika vipaji vya nyuso zao.

5 Wakapewa amri kwamba wasiwaue, bali wateswe miezi mitano. Na maumivu yao yalikuwa kama kuumwa na nge, aumapo mwanadamu.

6 Na siku zile wanadamu watatafuta mauti, wala hawataiona kamwe. Nao watatamani kufa, nayo mauti itawakimbia.

7 Na maumbo ya hao nzige yalikuwa kama farasi waliowekwa tayari kwa vita, na juu ya vichwa vyao kama taji, mfano wa dhahabu, na nyuso zao zilikuwa kama nyuso za wanadamu.

8 Nao walikuwa na nywele kama nywele za wanawake. Na meno yao yalikuwa kama meno ya simba.

9 Nao walikuwa na dirii kifuani kama dirii za chuma. Na sauti ya mabawa yao ilikuwa kama sauti ya magari, ya farasi wengi waendao kasi vitani.

10 Nao wana mikia kama ya nge, na miiba; na nguvu yao ya kuwadhuru wanadamu miezi mitano ilikuwa katika mikia yao.

11 Na juu yao wanaye mfalme, naye ni malaika wa kuzimu, jina lake kwa Kiebrania ni Abadoni, na kwa Kiyunani analo jina lake Apolioni”.

Kama tulivyotangulia kujifunza, Nyota iliyoanguka kutoka mbinguni si kimondo bali ni ‘shetani’ na Ufunuo 12:12 inasema.. “hiyo shangilieni, enyi mbingu, nanyi mkaao humo. OLE WA NCHI NA BAHARI! Kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu.”


Na pia sehemu nyingine Bwana Yesu anasema: Akawaambia, Nilimwona Shetani, akianguka kutoka mbinguni kama umeme. (Luka10:18)


Ikiwa na maana kuwa kuanguka kwa shetani, na kutupwa chini duniani ni LAANA! Sio kitu kizuri..viumbe vyote vikaavyo baharini vitaathirika na kadhalika vikaavyo juu ya nchi…sasa wanadamu ndio wanaokaa juu ya nchi, hao ndio waathirika wakuu!.
Katika baragumu hili tunaona shetani kama nyota iliyoanguka kutoka juu…akipewa funguo za kuzimu…sasa kumbuka kuzimu zimegawanyika katika sehemu mbili. Sehemu ya kwanza ni sehemu ambapo roho za watu waliokufa katika dhambi zipo, ni sehemu ya mateso sana, roho za watu hawa zipo zikiwa katika hali ya vifungo, zikiteseka zikingoja ufufuo wa hukumu.

Na sehemu ya pili ya kuzimu, ni sehemu ambayo roho za baadhi ya malaika walioasi mbinguni zimefungiwa…Kumbuka sio mapepo yote yaliyoasi yanatenda kazi leo duniani, hapana, yapo mengine mabaya kuliko haya yaliyopo sasa, ambayo yalifungwa katika hii kuzimu ya pili, kwa makosa yaliyofanywa na hata kuna mengine yanaweza  kutupwa huko hata leo, ndio maana utaona kuna yale yaliyomsihi Bwana Yesu asiyapeleke shimoni..Huko shimoni kunakozungumziwa ni “kuzimu ya malaika walioasi’’ ni sehemu ya vifungo vya giza na mateso ambapo roho hizo zimefungwa huko mpaka siku zitakapotupwa katika ziwa la moto…ambapo tutakuja kuona katika ufunuo 20 shetani naye atakuja kutupwa huko na kufungwa kwa miaka 1000.


Sasa pia kumbuka shetani alinyanganywa funguo za mauti na kuzimu na Bwana Yesu mwenyewe, kwasababu hapo kwanza alikuwa nazo alikuwa na uwezo wa kuzileta juu roho za watu waliopo kuzimu na baadhi ya mapepo,! Ndio maana maana unaona aliweza hata kumleta Nabii Samweli juu aliyekuwa amekufa kuzungumza naye. Lakini Baada ya Bwana Yesu kuja, mamlaka yote ya wafu yakawa chini ya Yesu Kristo, hakuna kiumbe chochote hata shetani chenye mamlaka juu ya wafu au roho zilizopo kuzimu au peponi. Lakini tunaona hapa! Shetani anapewa ufunguo za kuzimu…na kama unavyoona ni ANAPEWA!! Ikiwa na maana kuwa hakuwa nazo hapo kabla…alikuwa amenyanganywa lakini hapa anapewa tena kwa muda.. sasa hapewi funguo za kuzimu mahali wanadamu walioasi walipo hapana bali anapewa funguo za kuzimu mahali malaika walioasi walipo?..hizo ni sehemu mbili tofauti.


Na kwasababu ana ghadhabu nyingi na lengo lake ni kuiharibu dunia kwasababu anajua muda wake umeisha….funguo atakazopewa atafungua kuzimu na kuyafungulia mapepo ambayo Bwana Yesu aliyafunga yasifanye kazi duniani kwa kipindi Fulani kwasababu yangeleta uharibifu mkubwa sana ambao haujawahi kuwepo!!..Ndio maana kuna umuhimu mkubwa sana wa kumshukuru Mungu kwaajili ya Yesu Kristo, maana kama si yeye sijui tungekuwa wapi leo. Shetani angetupepeta vya kutosha.


Kwahiyo shetani atapewa funguo na atayafungua hayo mapepo yaliyokuwa kifungoni, ambayo ni mabaya kuliko haya yaliyopo huru sasa duniani..Sasa biblia imeyafananisha hayo mapepo na hao nzige tunaowasoma kwenye sura hii…Kumbuka sio nzige kama nzige hawa wadudu tunaowajua watakaotoka kuzimu hapana! Bali ni maroho! Biblia imefananisha mara nyingi roho chafu na roho za wanyama au wadudu..(Kwamfano Ufunuo 16:13 unaweza ukaona jambo hilo….Inasema:  “Nikaona roho tatu za uchafu zilizofanana na vyura, zikitoka katika kinywa cha yule joka, na katika kinywa cha yule mnyama, na katika kinywa cha yule nabii wa uongo Hizo ndizo roho za mashetani, zifanyazo ishara, zitokazo na kuwaendea wafalme wa ulimwengu wote…”).


Maumivu yao ni kama ya ng’e..roho hizi zitaleta madhara makubwa katikati ya watu..pigo hili litakuwa ni kwa watu wa dunia nzima…Unajua sasahivi kila uovu Fulani unaasisiwa na roho Fulani (au pepo fulani)..Kwamfano ushoga ni mapepo Fulani ya aina hiyo yanawaingia watu na kuwapeleka kwenye ushoga…yasingekuwepo hayo watu kwa hali ya kawaida wasingeweza kuwa mashoga..kadhalika na usagaji, utafanyaji masturbation, uuaji, wizi, usengenyaji, n.k yote hayo ni mapepo.


Ili kuelewa vizuri kama wewe ni mdadisi wa kifaa kinachoitwa computer au simu, utagundua kuwa unaponunua computer au simu inakuwa na mambo machache sana…ili kuiongezea uwezo inakubidi kudownload baadhi ya programs au softwares ili iweze kwenda kama unavyotaka wewe..utagundua kuwa ili sauti iweze kusikika vizuri, au ili uweze kuongeza milio ya simu, au uweze kuwasiliana na watu kisasa n.k inakubidi udownload applications au software kwenye simu yako au computer yako..sasa hizo applications au softwares unazoziongeza kwenye simu yako ndio mfano wa mapepo ambayo shetani anayaongeza ndani ya watu ili waweze kuwa mashoga, wauaji, wazinzi, walawiti n.k


Sasa katika siku hizo yatakapofunguliwa, zitazalika tabia duniani ambazo hazipo duniani leo…pengine utaanza kuona watu wanaanza kula nyama za watu, au utaanza kuona watu wanaanza kuwa na uwezo wa ajabu wa kipepo, ukatili wa ajabu utaongezeka ambao haujawahi kuonekana hapo kabla, pengine utaona watu wanafanya uzinzi mabarabarani bila aibu,..na kuzuka baadhi ya magonjwa ambayo ni mapya, ya mateso kushinda saratani au ukimwi,..pengine utaanza kuona na wanyama pia wanabadilika tabia, hawafugiki tena, nk n.K, siku hizo ndizo  watu watatamani kufa lakini biblia inasema mauti itawakimbia. Kila mtu ataona hakuna maana ya maisha tena, duniani hakukaliki hofu ya kila kitu.



Na kwenye ule mstari wa mwisho biblia inasema wanaye mfalme naye ni malaika wa kuzimu..jina lake kwa kiebrania ni Abadoni na kwa kiyunani ni Apolioni…Abadoni maana yake ni “MAHALI PA UHARIBIFU”. …na Apolioni maana yake ni “MUHARIBIFU”…Majina yote haya mawili yanamzungumzia ‘shetani’ ambaye ndiye mwaribifu na kila aina ya uharibifu unatoka kwake. Yeye ndiye mfalme wa kuzimu na mfalme wa hawa malaika walioachiwa kutoka kuzimu.


Na ndio maana ni vizuri kutengeneza mambo yako sasa, angali neema ya Kristo ipo, huko mbeleni ni vilio na maombolezo kwa watakaokosa unyakuo.


Tukiendelea na mistari inayofuata biblia inasema…

Ufunuo 9: 12 “Ole wa kwanza umekwisha pita. Tazama, bado ziko ole mbili, zinakuja baadaye.

13 Malaika wa sita akapiga baragumu, nikasikia sauti moja iliyotoka katika zile pembe za madhabahu ya dhahabu iliyo mbele za Mungu,

14 ikimwambia yule malaika wa sita aliyekuwa na baragumu, Wafungue nao malaika wanne waliofungwa kwenye mto mkubwa Frati.

15 Wale malaika wanne wakafunguliwa, waliokuwa wamewekwa tayari kwa ile saa na siku na mwezi na mwaka, ili kwamba waue theluthi ya wanadamu.

16 Na hesabu ya majeshi ya wapanda farasi ilikuwa elfu ishirini mara elfu kumi; nilisikia hesabu yao.

17 Hiyo ndivyo nilivyowaona hao farasi katika maono yangu, nao waliokaa juu yao, wana dirii kifuani, kama za moto, na za samawi, na za kiberiti; na vichwa vya farasi hao ni kama vichwa vya simba, na katika vinywa vyao hutoka moto na moshi na kiberiti.

18 Theluthi ya wanadamu wakauawa kwa mapigo matatu hayo, kwa moto huo na moshi huo na kiberiti hicho, yaliyotoka katika vinywa vyao.

19 Kwa maana nguvu za hao farasi ni katika vinywa vyao, na katika mikia yao; maana mikia yao ni mfano wa nyoka, ina vichwa, nao wanadhuru kwa hivyo.

20 Na wanadamu waliosalia, wasiouawa kwa mapigo hayo, hawakuzitubia zile kazi za mikono yao, hata wasiwasujudie mashetani, na sanamu za dhahabu na za fedha na za shaba na za mawe na za miti, zisizoweza kuona wala kusikia wala kuenenda.

21 Wala hawakuutubia uuaji wao, wala uchawi wao, wala uasherati wao, wala wivi wao”.

Katika mstari wa 14 tunaona ikitolewa amri ya kufunguliwa kwa wale malaika wanne waliokuwa wamefungwa katika Mto Frati. Na hawa lengo la kuzuiwa katika Mto Frati ni ili wasilete madhara waliomriwa kuleta kabla ya wakati kufika, kwamba wakati ukifika waue theluthi ya wanadamu wanaoishi juu ya nchi…Ili tujue hawa malaika ni wapi…turudi nyuma kidogo kwenye ufunuo Mlango wa 7.

Ufunuo 7: 1 “Baada ya hayo nikaona malaika wanne wamesimama katika pembe nne za nchi, wakizizuia pepo nne za nchi, upepo usivume juu ya nchi, wala juu ya bahari, wala juu ya mti wo wote.

2 Nikaona malaika mwingine, akipanda kutoka maawio ya jua, mwenye muhuri ya Mungu aliye hai; akawapigia kelele kwa sauti kuu wale malaika wanne waliopewa kuidhuru nchi na bahari,

3 akisema, Msiidhuru nchi, wala bahari, wala miti, hata tutakapokwisha kuwatia muhuri watumwa wa Mungu wetu juu ya vipaji vya nyuso zao”.



Malaika hao wanne waliokuwa wamezuiwa kwenye mto Frati ndio hawa hawa ambao walionekana wamesimama kwenye pepo nne za nchi, wakizizuia pepo nne za nchi, Na pepo hizi nne ni upepo wa KI-SIASA, upepo wa KI-DINI, KI-UCHUMI na KI-JESHI. Hizo ndio pepo 4 za nchi.

Malaika hawa waliwekwa kuzuia vita vikuu vya Harmagedoni visitokee juu ya nchi.. Kwahiyo walikuwa wanazuia shughuli zozote za kipepo zisifanye kazi juu ya siasa ya dunia, uchumi wadunia, dini ya dunia wala jeshi la dunia, lakini sasa wakati huu, wataruhusu shetani aingie kuvuruga siasa ya dunia, uchumi, dini pamoja na jeshi…Yale mapepo yaliyotoka kuzimu yatawaingia wanasiasa wa dunia, sasa kuanzia wakati huu kutakuwa hakuna kuelewana duniani, kutakuwa hakuna kuvumiliana tena…mipango ya vita itawekwa, na amani itavurugika kwa kiwango kikubwa sana…Na ndio maana unajiuliza kwanini Leo mataifa makubwa yanagombana lakini hayapigani, nikwasababu malaika hawa wameamuriwa wazuie machafuko, lakini wakati utafika hakutakuwa na kuzuiwa tena, vitendo vitafuata.
 
Biblia inasema zaidi ya wanajeshi milioni 200 (elfu ishirini mara elfu kumi), watahusika katika mapambano ya vita hiyo ya Harmagedoni… “na vichwa vya farasi hao ni kama vichwa vya simba, na katika vinywa vyao hutoka moto na moshi na kiberiti.” Mstari huu unazungumzia aina za silaha zitakazotumika wakati huo, farasi anawakilisha silaha za kijeshi kama ndege za vita, vifaru, helicopter za mabomu ya atomiki n.k na kama hapo inavyosema katika midomo yao inatoka moto, moshi na kiberiti…inazungumzia mabomu, na makombora yatokayo kwenye vifaru hivyo, ndege hizo, nk na walikuwa na vichwa kama vya simba, kama vile simba angurumapo atafutapo wawindo na silaha hizi zitakuwa na mingurumo zitumiwapo.

Kwahiyo katika baragumu hili la sita ndio utakuwa mwanzo wa maandalizi ya vita ya tatu ya dunia…Vita ya Mungu mwenyezi, (Harmagedoni). Ambayo tutakuja kuisoma vizuri katika Kile kitasa cha sita katika Ufunuo ule mlango wa 16. Wakati huu machafuko ya mataifa yatakuwa mengi sana duniani. 
Kristo yupo mlangoni, umefanya uteule wako na wito wako Imara sawasawa na 2 Petro 1:10?. Kama sivyo jitazame mara mbili, kisha chagua mwisho mwema, mambo haya sio hadithi tu za zale ni mambo ambayo yatakuja kutokea dhahiri mbele ya macho ya watu wengi.
  
Bwana akubariki.

Usikose kufuatilia sura zinazofuata, pia usiache kuwashirikisha wengine habari njema baada ya kuujua ukweli huu.

Kwa mfululizo mzuri wa uchambuzi wa kitabu hichi cha Ufunuo tembelea website yetu hii   www.wingulamashahidi.org

No comments:

Post a Comment