"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Tuesday, July 30, 2019

HATARI YA KUTOKUITAFAKARI BIBLIA VIZURI?


Shalom! Mtu wa Mungu, maandiko yanatuagiza tusiache kuonyana kila siku, maadamu iitwapo leo(Waebrani 3:13). Hivyo nakukaribisha tujifunze leo jambo moja lihusulo BIBLIA.

Nilipokuwa ninatafakari hili Neno linalosema ““Iko njia ionekanayo kuwa sawa machoni pa mtu, Lakini mwisho wake ni njia za mauti.”” Nikajiuliza hii njia ionekanayo kuwa sawa ni ipi?..Mtu akiwa mtukanaji, mtu akiwa muuaji, mtu akiwa ni fisadi n.k, njia yake haiwezi kuonekana ni sawa machoni pake, ni wazi kuwa anafahamu anapoeleka ni pabaya..Lakini njia inayoweza kuonekana ni sawa machoni pa mtu ni ipi?, ni ile inayotoka katika maandiko (BIBLIA), pale maandiko yanapomthibitishia mtu kuwa kitu hichi au kile anachokifanya kimeandikwa, basi hilo linampa amani ya kufahamu kuwa yupo katika njia sahihi.
Nataka nikuambie, biblia ni kitabu kitakatifu sana, kimekamilika na kujitosheleza kwa namna zote, hakiwezi kuongezwa wala hakiwezi kupungumzwa, lakini nataka nikuambie pia Biblia hii si ya watakatifu peke yao: Biblia si mti wenye tunda la aina moja, bali ni mti wenye matunda ya aina nyingi tofauti tofauti,. na kila mtu anachuma kinachomfaa na kuondoka kulingana na matakwa yake mwenyewe.

Na hiyo yote ni kwasababu biblia ni Neno la Mungu, na Neno la Mungu tunajua ndio lililoumba kila kitu (Yohana 1:1), halikuumba vyema tu bali hata na viovu pia, hivyo pumzi ya kila kitu inategemea hilo Neno. kwahiyo kila mtu na kila mmoja na inaweza kumnufaisha kulingana na matakwa yake mwenyewe. Shetani inamnufaisha katika lengo lake la kupoteza watu, na amefanikiwa kweli kupoteza mamilioni ya watu kwa kupitia biblia unayoisoma, hata alijaribu kuitumia hiyo hiyo kumwangusha Bwana akashindwa..

Madaktari wanaitumia hii kuwasaidia kubuni aina mbalimbali za matibabu, hata ukiangalia nembo yao kubwa maarufu inayotumiwa na Shirika la Afya ulimwenguni (WHO), utaona ni Yule nyoka wa shaba ambaye Musa aliwaagiza wana wa Israeli wamtazame ili wapone kutokana na sumu ya nyoka. Utamaduni huo ambao baadaye uligeuka kuwa wa kipagani, ulirithiwa na mataifa mengine ya kipagani kama Ugiriki wakahusisha na tiba za kienyeji na mambo hayo, na ndio huko huko mpaka ikawa maarufu katika masuala yote ya tiba duniani leo hii.

Biblia hii hii inayoisoma inatumiwa na majeshi, kubuni mbinu mpya za kupigani: Na wanafanikiwa vizuri sana. Wakati wewe unafurahia kusoma zile habari za vita vya Yoshua na waamuzi, wengine huko wanaiga mbinu za kivita. Biblia hii hii inatumiwa na wanasiasa kutengeza sera zao za kampeni na wanafanikiwa katika hilo, Msome mtu kama kwame Nkrumah raisi wa kwanza wa Ghana,si jinsi alivyoupindua utawala wa kikoloni kwa maandishi ya maandiko.

Biblia hii hii inatumiwa na wachawi na wanajimu, kuwasaidia kufanya uchawi wao: Wasingefahamu kitu kinachoitwa kafara na nguvu iliyokatika damu kama wasingesoma katika biblia..Katika Agano la kale kafara za Wanyama zilikuwa zinafanyika kwaajili ya upatanisho…Asili ya kuvaa hirizi si kutoka kwa wachawi…Wana wa Israeli waliagizwa na Mungu wazivae kwenye vipaji vya nyuso zao, ili kuwakumbusha sheria za Mungu, (vilikuwa ni viboksi vidogo vilivyokuwa vimebeba baadhi ya maneno ya kwenye Torati) lakini Baadaye shetani akaja kuiba huo utamaduni na kutengeneza za kwake kwa lengo la kulogea watu.

Wafanya-biashara na matajiri: Kanuni za kufanikiwa zote wanazitolea katika maandiko,kupanda na kuvuna. Kufanya kazi kwa bidii,n.k. zipo huko, wanazitumia na zinawaletea mafanikio makubwa sana.

Vile vile biblia hii hii inatumiwa na manabii wa Uongo, kutimiza matakwa yao: Wanasoma na kufahamu kuwa ndani ya jina la YESU, kuna uweza wa kipekee, kila kitu kinatii, hivyo hata mtu ambaye alishamkufuru Mungu siku nyingi, anaouwezo wa kulitumia hili jina ili kuamirisha chochote na kikamtii, hata kuamisha milima…hivyo anaweza kutumia fursa hiyo kujipatia mali, au kuwapoteza, kwa kisingizio cha miujiza, na anafanikiwa kabisa, na ndio maana Bwana Yesu alisema wengi watakuja siku ile wakisema Bwana Bwana…, hatukufanya unabii kwa jina lako, na kwa jina lako kutoa pepo, na kwa jina lako kufanya miujiza mingi? Ndipo nitawaambia dhahiri, Sikuwajua ninyi kamwe; ondokeni kwangu, ninyi mtendao maovu. (Mathayo 7:21).

Lakini pia biblia hii hii inatumiwa na watu wengine, na inawapa UZIMA WA MILELE.
Unaweza ukaona hapo, jinsi Biblia inavyofungua milango ya mambo mengi, hata yale maovu, lakini sio milango yote mtu akiingia kwa kupitia biblia inamletea mwisho mwema. Na ndio maana ukisoma maneno ya kwanza kabisa Bwana Yesu aliyoyahubiri ni haya, TUBUNI, KWA MAANA UFALME WA MBINGUNI UMEKARIBIA(Mathayo 4:17)..Na habari zake zote zilikuwa zinalenga ufalme wa mbinguni, kama ukitafuta mahali Bwana Yesu anakufundisha utajiri na mafanikio ya kidunia nataka nikuambie unaweza ukavunjika moyo, zaidi ya yote watu waliojaribu kumfauta kujaribu kumuuliza kuhusu mambo kama hayo aliishia kuwaambia “Uzima wa mtu haupo katika mwingi wa vitu alivyonavyo”(Luka 12:15).

Alikuwepo kwa lengo moja tu la msingi, nalo ni kumpa mtu uzima wa milele. Na wote waliomfuata waliupokea bali waliomkataa hawakaupata bali walipata sehemu ya vipengele vingine katika maandiko.,Leo hii usifurahie na kusema biblia inahimiza hichi ninachokifanya..ukadhani kuwa upo sahihi wakati wote katika hiyo njia…Unapaswa ujiulize je! matokea ya hichi ninachokifanya mwisho wake ni nini?,..Ni uzima wa milele au Mauti, au huna-uhakika?. Ikiwa ni mauti au huna-uhakika, hata kama kuna vifungu vinakusapoti, achana nacho, tafuta kilicho cha msingi kwanza, na biblia imeshaturahisishia kufahamu kilicho cha msingi, nacho ni YESU KRISTO..
Yohana 14:6 “Yesu akamwambia, Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi.”
Ni heri ukakifanya hicho, lakini huku nyuma jambo la msingi la wokovu wako na uzima wa milele lipo pamoja na wewe, hiyo haina shida kabisa,lakini unaacha mambo ya wokovu na habari za kwenda mbinguni, unasema biblia inaniambia hivi au vile …Kumbuka Yesu anasema “hapa yupo aliye mkuu zaidi ya Sulemani”.

Hivyo kwa kumalizia ni vizuri tukajua jinsi ya kuyavunja vunja maandiko na kuchagua vile vilivyo vya muhimu kwanza, ambavyo ni vya UFALME WA MBINGUNI NA HAKI YAKE NA HIVYO VINGINE VILIVYOSALIA TUTAZIDISHIWA tu Bwana ameahidi hilo, yeye si mwongo. Tunajua hizi ni nyakati za kumalizia, Kristo yupo karibuni kurudi kushinda hata sisi tunavyoweza kufikiria..Ikiwa utasikia unyakuo umepita leo na wewe umebaki utakuwa katika hali gani?. Kumbuka atakayeona uchungu zaidi sio mlevi, au jambazi, atakayeona uchungu ni Yule mkristo aliye vuguvugu ambaye aliitupilia injili za wokovu na kwenda mbinguni akageukia injili za namna nyingine za faraji, ambazo thawabu zake zinaishia hapa hapa duniani…siku hiyo huyo ndio atakayeomboleza..Kwasababu alidhani kuwa ndio njia aindeayo uzimani..Lakini mwisho wake umekupeleka kuingia katika dhiki kuu.

Utasema siku ile, Hatukupata mali kwa jina lako Bwana?, hatukufunguliwa matumbo yetu yaliyokuwa tasa kwa jina lako?, hatukufungua biashara nzuri kwa unabii wako?.nk Ni kweli mambo hayo yote uliyafanya kwa jina la Yesu lipitalo majina yote na lifungualo vifungo vyote, lakini siku ile Bwana atasema ondokeni kwangu! Kwanini? kwasababu jina hilo ulipaswa ulitumie pia kukuletea wokovu wako wa milele, si tu vitu vya ulim:wengu huu vinavyopita, jina hilo ulipaswa pia ubatiziwe kwalo, kulingana na Matendo 2:38, Matendo 8:16, Matendo 19:5 na Matendo 10:48. ili upate ondoleo la dhambi zako na upokee kipawa cha Roho Mtakatifu..Umepata fahari zote na ulimwengu mzima kwa jina hilo lakini umekosa uzima kwa jina hilo, itakufaidia nini?.

Jihadhari na njia zinazoonekana ni nzuri, zinazopendwa na kufuatwa na wengi kwa kivuli cha biblia, nyingi zinaelekea upotevuni. kumbuka njia ni nyembamba ielekeayo uzimani

Ubarikiwe sana.Tafadhali “share” ujumbe huu kwa wengine. Na Bwana atakubariki.

No comments:

Post a Comment