"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Saturday, October 27, 2018

MASWALI NA MAJIBU: SEHEMU YA 41

SWALI 1: Shalom,mtumishi wa BWANA!Mimi ninataka kujua je, ni halali kwa mtu wa Mungu kutumia njia za uzazi wa mpango,ikiwamo mipira?Jambo la pili,Je! taratibu za kufunga ndoa [yaani harusi] ni agizo la Mungu au ni mapokeo tu ya kibinadamu? Asante!!

JIBU: Biblia haijaeleza moja kwa moja kuhusu suala la uzazi wa mpango aidha utumike au la, kwasababu njia zinazotumika sasa hazikuwepo katikati ya watu wa kale, Lakini ni vizuri kufahamu lengo la kufanya hivyo ni nini, wapo wengine wanafanya hivyo kwasababu ya matatizo ya kiuchumi, wengine kwasababu ya mapungufu ya kimwili, wengine kwasababu ya kuzuia kuathiriwa kwa kazi yake Fulani, na pia wapo wengine ni kwasababu tu za kiasherati/zinaa n.k..

Hivyo njia nyingi za sasa zitumiwazo kwa uzazi wa mpango zinachukuliwa kwa taswira ya kiasherati kwasababu iko wazi nyingi zinatumiwa hivyo. Lakini ikiwa ni kwa wana ndoa, na dhamira zao zikiwa ni safi mbele za Mungu, na malazi yao ni masafi siku zote, na wanazo sababu za muhimu zinazowalazimu kufanya hivyo labda kwasababu za uleaji wa watoto n.k. Si dhambi wanaweza kutumia. Kwasababu kumbuka pia maandiko yanasema Katika 
1Timotheo 5: 8 Lakini mtu ye yote asiyewatunza walio wake, yaani, wale wa nyumbani mwake hasa, ameikana Imani, tena ni mbaya kuliko mtu asiyeamini.

Unaona hapo? Uzaaji wa watoto usio na mpango, hususani pale usipokuwa na uwezo wa kuwalea, ni sawa na umeikana Imani. Hivyo ni vizuri kama wewe ni mwanandoa, ukae chini katika maombi na kumuuliza Mungu, na mapatano na mwenzako, na kisha zitumike. Lakini mambo hayo hayamuhusu mtu asiye mwana-ndoa.

b) Kufunga ndoa ni agizo la Mungu, lakini Harusi ni karamu/sherehe ya Ndoa mpya. Na hizo ni desturi tu ambazo zipo katika mataifa mbalimbali kulingana na chimbuko lao. Hata taifa la Israeli walikuwa na desturi za harusi. Hivyo ikiwa ndoa mpya itaambatana na harusi kwa Mungu hakuna dhambi, wala hakuna maagizo yoyote kwenye biblia kwamba mtu akioa au akiolewa ni lazima afanyiwe harusi au asifanyiwe…Ni jinsi mtu mwenyewe atakavyopenda isipokuwa tu, tumeagizwa lolote tufanyalo kwa Neno au kwa tendo tufanye kwa jina la Yesu Kristo. Ikiwa na maana kuwa hiyo arusi isivuke vigezo vya kikristo.


SWALI 2: Ndugu zangu ni sahihi kwa Mkristo kusherekea siku ya kuzaliwa kwake[Birth day]?

JIBU: Sherehe yoyote ile iwe ni ya kuzaliwa, au mahafali, maadhimisho ya miaka ya ndoa, harusi, kumbukumbu n.k. Biblia haitatoa katazo lolote kufanyika, isipokuwa imetoa katazo tu kwa KARAMU ZA ULAFI. Tukisema karamu za ulafi tunamaanisha karamu/sherehe zozote zinazovuka mipaka ya Neno la Mungu, kwamfano sherehe zinazochanganyikana na pombe,Disco, miziki ya kidunia, uvaaji mbovu, na mambo yote yafananayo na hayo ambayo ni kunyume na Neno la Mungu, hizo zote ni karamu za ULAFI ambazo biblia imezikataza.
Ukisoma..

1Petro 4: 4.3 Maana wakati wa maisha yetu uliopita watosha kwa kutenda mapenzi ya Mataifa; kuenenda katika ufisadi, na tamaa, na ulevi, na KARAMU ZA ULAFI, na vileo, na ibada ya sanamu isiyo halali;

Unaona hapo pia ukisoma …

2Petro 2: 13 Wakipatikana na madhara, ambayo ni ujira wa udhalimu wao, wakidhania kuwa ulevi wakati wa mchana ni anasa; wamekuwa ni mawaa na aibu WAKIFUATA ANASA ZISIZO KIASI KATIKA KARAMU ZAO ZA UPENDO, wafanyapo karamu pamoja nanyi;

Unaona pia hapo karamu/sherehe zenye mambo kama hayo ndani yake ni dhambi kwa mkristo kufanya, lakini ikiwa ni kwa ajili ya kuhitimu, au kuzaliwa, au ndoa, au mahadhimisho unaweza ukasheherekea upendavyo lakini hapo ndio kuzingatia lile neno linalosema Wakolosai 3: Na kila mfanyalo, kwa neno au kwa tendo, fanyeni yote katika jina la Bwana Yesu, mkimshukuru Mungu Baba kwa yeye.

Na ndio maana Bwana YESU alitushauri pale tunapojisikia kufanya karamu au kusheherekea kwa namna yoyote ile tufanye kwa manufaa ya kimbinguni zaidi, yaani kuliko kuwaalika watu wenye cheo, ni vizuri kusheherekea na watu maskini, ili thawabu yetu iwe kubwa mbinguni(Luka 4:12)..Kuliko kukata keki na ndugu zetu au na marafiki zetu tu, ni vema tukaongeza pia kukata na yatima waliokaribu nasi pamoja na wajane.. Ndio karamu yenye harufu nzuri mbele za Mungu.

 SWALI: Biblia inasema askofu anapaswa awe mume wa mke mmoja! Je! Wale wasiooa kwa ajili ya injili hawawezi kuwa maaskofu?..1 Timotheo 3 :1 "Ni neno la kuaminiwa; mtu akitaka kazi ya askofu, atamani kazi njema. Basi imempasa askofu awe mtu asiyelaumika, mume wa mke mmoja,..”

JIBU: swali zuri, na pia wengi wanachanganyikiwa kuhusu hilo, wakidhani kuwa mtu yeyote anayeitwa askofu ni lazima aoe…lakini unapaswa uelewe kuwa hapo Mtume Paulo alisema hivyo kwa mantiki ipi?, hakuwalenga wale ambao hawajaoa bado hapana, bali aliwalenga wale ambao wanao wake zaidi ya mmoja..kwamba hao ndio hawapaswi kuwa maaskofu, kwasababu ni lazima waonyeshe kielelezo kwanza wao wenyewe katika nyumba zao na ndio waje kuchunga wa nje, sasa kama mtu alikuwa na wake 6 kabla hajaamini na akaingia kwenye ukristo na ukristo unasema mtu anapaswa awe na mke mmoja, sasa unadhani wale atakaowachunga yeye kama askofu atakuwa anacho kielelezo gani?

Na ndio maana haipaswi mtu yeyote anayeitwa askofu au mchungaji awe na mke zaidi ya mmoja…Lakini haikumaanisha pale kwamba ni lazima kila anayetaka kuwa askofu awe na mke, huo ni uelewa hafifu wa maandiko.

Kumbuka mtume Paulo naye hakuwa na mke, lakini alikuwa mwangalizi wa makanisa yote, Kristo naye hakuwa na mke lakini yeye ndiye Askofu wa maaskofu. Hivyo hapo maneno hayo yaliwalenga wale ambao tayari wanao mke zaidi ya mmoja.

No comments:

Post a Comment