"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Tuesday, February 19, 2019

MLIMA WA BWANA.


Mara nyingi tunaposoma biblia katika agano la kale Mungu alipokuwa akitaka kukutana au kusema na watu wake, aliwaita milimani, hilo tunaliona tokea mbali kabisa jinsi Mungu alivyomwita baba yetu Ibrahimu katika ule mlima Moria amtolee sadaka na kumfanyia ibada, Tunakuja kuona tena baadaye Musa akiitwa na Mungu katika milima Sinai kupewa amri zote na hukumu na sheria kwa ajili ya wana wa Israeli, tunaona tena manabii wengi jinsi Mungu alivyokuwa akisema nao katika milima, mfano nabii Eliya Mungu alizungumza naye katika mlima Karmeli, na wengine wengi mfano wa Elisha ambao ukisoma habari zao mara nyingi utakuta walikuwa wakikutana na Mungu katika milima, 
 
Hivyo hiyo ilikuwa ni kama desturi yao kupanda milimani na kukutana na Mungu..Kwasababu iliaminika hivyo na ndivyo hata alivyofanya Mungu mara nyingi alipotaka kuzungumza na watumishi wake, alifanya kuwatenga kwanza kisha kuwapandisha milimani na baadaye kuzungumza nao. (Isaya 18:7). Na kama ukichunguza vizuri utaona kuwa wote waliokuwa wanaitwa kusema na Mungu milimani waliteuliwa na Mungu mwenyewe, sio kila mtu tu alikwenda, utakuta pengine wataanza safari wengi lakini mwisho wa siku wanaofikia kule juu mlimani ni wachache, ndivyo ilivyokuwa kwa Ibrahimu, Musa na manabii.
Tunaona hata kipindi cha Bwana wetu Yesu Kristo, mara nyingi alipokusudia kusali au kwenda kuzungumza na Baba yake alikuwa na desturi ya kupanda katika mlima wa Mizeituni, na tunaona pia wakati fulani alipotaka kuonyesha utukufu wake zaidi aliwatenga kwa kuwachagua baadhi ya mitume wake,(yaani watatu tu kati ya 12) kisha akawapandisha katika mlima MREFU sio mfupi, bali mrefu na huko huko ndiko alikowabadilikia sura..tunasoma..
Mathayo 17:1 “Na baada ya siku sita Yesu akawatwaa Petro, na Yakobo, na Yohana nduguye, akawaleta juu ya mlima mrefu faraghani;
2 akageuka sura yake mbele yao; uso wake ukang'aa kama jua, mavazi yake yakawa meupe kama nuru.
3 Na tazama, wakatokewa na Musa na Eliya, wakizungumza naye”.
Sasa tukirudi kwenye kiini cha somo letu kinachosema “mlima wa Bwana”. Tunapaswa tujiulize ni kwanini Mungu alikuwa anawaita watu milimani na sio mahali pengine popote…kwanini asiwe anawaita katika mabonde azungumze nao, lakini badala yake aliwaita milimani?. Je! milima ina upako zaidi ya visiwa, au nyika?. Je! milima inakibali cha kipekee sana mbele za Mungu zaidi ya mahali pengine popote?. Kama sivyo basi ilifunua nini?

Ni wazi kuwa kila mmoja wetu alishawahi kupanda mlima na kama sio mlima basi angalau kajilima na kujionea jinsi hali ilivyo katika kuupanda..si kazi rahisi wala si kazi nyepesi, kama ilivyo katika kushuka mabondeni, au kutembea katika nchi tambarare, tunajua kabisa kupandisha mlima inachukua nguvu nyingi hivyo kama wewe ni mlegevu hutafika kileleni..Kupanda mlima ni lazima utoke jasho la kutosha, sio kama kushuka mabondeni.Wanaoweza kupanda milima mrefu sikuzote ni wachache sana na tena unapaswa uwe mtu wa mazoezi lakini kuteremka bondeni, kila mtu anaweza kufanya hivyo, tena ni raha iwe unazo nguvu au hauna hakuna asiyeweza kushuka bondeni..

Mambo hayo yanafunua nini katika Roho?

Sasa tukirudi katika agano jipya mambo ya mwilini yanafunua mambo yanayoendelea rohoni, Na ndio maana ukisoma mahali popote palipo na bonde utaona kuwa ni mauti inapatikana huko, BONDE LA UVULI WA MAUTI, bonde LINAFUA SHIMO LA KUZIMA, mahali makao ya shetani yalipo Na siku zote kushuka huko ni rahisi sana..Mahali Fulani Bwana alipowatoa pepo, walimsihi asiwaamuru waende shimoni, ikifunua kuwa ni sehemu ya hatari…Lakini katika vilele vya milima Mungu anapatikana, kwasababu Mungu anaketi Juu siku zote, sehemu za juu zilizoinuka.

Hivyo ndugu tukitaka leo hii kukutana na Mungu, ukitaka kuuona uso wa Mungu kwa namna nyingine na ile uliyoizoea, ukitaka Mungu aseme na wewe katika viwango vya juu sana ukitaka Mungu akufunulie njia zake kwa namna ambayo hujawahi kuona huna budi kupanda mlimani katika roho, huna budi kugharimika kuupanda mlima wa Bwana. Tena na kwa jinsi unavyopanda zaidi ndivyo utakavyofunuliwa uso wa Mungu katika viwango vya juu zaidi.

SASA TUNAPANDAJE PANDAJE MLIMA HUO, NA NI NANI ASTAHILIYE KUUPANDA MLIMA WA BWANA?

Biblia imetoa majibu yote tunaposoma kitabu cha Zaburi..
Zaburi 24:3-6 “Ni nani atakayepanda katika MLIMA WA BWANA? Ni nani atakayesimama katika patakatifu pake?
4 Mtu aliye na mikono safi na moyo mweupe, Asiyeiinua nafsi yake kwa ubatili, Wala hakuapa kwa hila.
5 Atapokea baraka kwa Bwana, Na haki kwa Mungu wa wokovu wake.
6 Hiki ndicho kizazi cha wamtafutao, Wakutafutao uso wako, Ee Mungu wa Yakobo.
Inasisitiza tena na kusema:

Zaburi 15:
1 Bwana, ni nani atakayekaa Katika hema yako? Ni nani atakayefanya maskani yake Katika KILIMA CHAKO KITAKATIFU?.
2 Ni mtu aendaye kwa ukamilifu, Na kutenda haki. Asemaye kweli kwa moyo wake,
3 Asiyesingizia kwa ulimi wake. Wala hakumtenda mwenziwe mabaya, Wala hakumsengenya jirani yake.
4 Machoni pake mtu asiyefaa hudharauliwa, Bali huwaheshimu wamchao Bwana Ingawa ameapa kwa hasara yake, Hayabadili maneno yake.
5 Hakutoa fedha yake apate kula riba, Hakutwaa rushwa amwangamize asiye na hatia. Mtu atendaye mambo hayo Hataondoshwa milele.

Unaona hapo?, vigezo vya kuuendea mlima huo?

1) Kwanza Ni mtu yule aendaye kwa ukamilifu, na kutenda haki, watu wengi wanaona shida kuishi maisha matakatifu, wanaona yatawasidia nini? watapata faida gani, kujitaabisha kujizuia na tamaa, kutokunywa pombe, kutokufanya uasherati, kutokuvaa nguo za kizinzi, watapata faida gani?..wanaona ni ngumu sana mtu kuishi kwa namna hiyo, wanaona mtu kutenda haki, kutokula rushwa ni jambo ambalo ni gumu kutolifanya, lakini hawajui hizo ndizo gharama za kuupanda mlima wa Mungu, ambapo yeye yupo huko, mahali anapopatikana.

2) Biblia inasema pia mtu asemaye kweli kwa moyo wake, utakuta mtu kuwa muwazi wakati wote kwake ni shida, na bado anajiita mkristo, biblia inaendelea kusema Asiyesingizia kwa ulimi wake. Wala hakumtenda mwenziwe mabaya, Wala HAKUMSENGENYA JIRANI YAKE.

Unaona hapo?, utakuta mtu anajiita ni mkristo, na anahudhuria ibadani, na anasali, na anafanya kazi yote ya Mungu, lakini anaona ni vigumu kuuzia ulimi wake kutokuwazungumzia wengine vibaya, kusengenya watu kwake ni kama chakula chake,. Sasa mtu kama huyu asitazamie kumkaribia Mungu kwa namna yoyote ile hata kama atakuwa anafunga kiasi gani, hata kama atakauwa anatoa sadaka kiasi gani, hata kama atakuwa anahubiri kiasi gani..Hatoweza kupanda mlima wa Bwana..

3) Biblia inasema tena mtu ambaye macho yake huwaheshimu wamchao Bwana, mtu ambaye macho yake yanamfarahia yule tu anayejitaabisha kwa Bwana, na sio watu wengine,. Sasa Hapa utakuwa mtu ni Mkristo lakini hamu na Mungu hana hata kidogo, yupo tayari kuwa mshabiki wa mipira, kuwa mfuasi wa siasa, kuwa mshabiki wa watu maarufu wa kidunia hii, muda wote anapoteza kufuatilia mambo yao, lakini tukirudi katika upande wa Mungu, ukimuuliza hata historia ya kanisa la Kristo ilianzia wapi hajui, ukimuuliza nitajie ziara za mtume Paulo zilianzia wapi na kuishia wapi? Hajui, lakini ukimuuliza ziara za maraisi wote duniani na wasanii,atakutajia na yanayokuja na kitu gani kinaendelea sasahivi katika ulimwengu wa siasa atakutajia..Sasa hiyo ni roho ya kumkinai Mungu na watu kama hao biblia inasema hawataweza kufanya maskani yao katika mlima mtakatifu wa Mungu..Watu kama hao hata waseme wao ni wakristo kiasi gani, ndani ya maisha yao wanajijua kabisa kuwa wapo mbali na ufalme wa mbinguni.

4) Biblia inandelea kusema mtu ambaye hali rushwa. Katika shughuli mkisto anazozifanya, je! Anakaa mbali na vitu kama rushwa na ukwepaji kodi?. Leo utashangaa ni mkristo lakini naye pia anatafuta njia za mkato za kukwepa kodi, mwingine anakuwa tayari kutoa rushwa ili afanyiwe jambo fulani..Sasa mambo kama hayo mtu akiwa nayo kadhalika asitarajie kumwona Mungu maishani mwake au Mungu kujifunua katika maisha yake, hata kama alibatizwa nakunena kwa lugha hiyo haijalishi, hatakaa amjue Mungu.

Hivyo Mungu kachagua sehemu ya juu iliyoinuka ili akutane na watu wake huko, sio rahisi kufika, inahitaji juhudi na bidii, kuacha usengenyaji sio rahisi kuliondoa kwa kuomba tu kama unavyodhani, inahitaji kuonyesha bidii yako binafsi kwa vitendo, mazungumzo yoyote unayoona yanakupelekea kumzunguzia mwingine kwa ubaya, ni kuyakwepa kwa namna zote, ukiudhiwa ni kuvumilia sio lazima uanze kutoa habari za mtu mwingine hadharani, unajizuia kwa nguvu, kila siku uendelee hivyo hivyo mpaka mwisho wa siku unajikuta inaumbika na kuwa ni tabia yako kutokuwazunguzia wengine vibaya..Hata na wale watu wanaokuletea hizo habari wakishakuona hauvutiwi na habari hizo, wao wenyewe watakuacha na kwenda kutafuta wanaoendana nao..Na kwa kufanya hivyo ndivyo unavyopiga hatua moja zaidi kuelekea mlima mtakatifu wa Bwana, Mungu alipo ili kusema na wale wote wamchao.

Kadhalika kutokufanya mambo ya ubatili, yaani uasherati, kampani mbovu zisizo na maana, kutokukaa wakati wote mitandaoni kuchati mambo yasiyo na maana, kutokwenda disco, kutofuata anasa za dunia hii, bali kinyume chake kujishughulisha na mambo ya Mungu, ni jinsi gani umpendeze yeye..Kumbuka Bwana anasema nikaribieni mimi nami nitawakaribia..Hivyo ukiwa unafanya bidii kukaa mbali na mambo maovu na kutafauta kujua habari zake, kwa kujifunza Neno, ndivyo unavyozidi kupanda kidogo kidogo mpaka kileleni alipo yeye..

Hizi ni siku za mwisho, na ndio kile kipindi ambacho Bwana Yesu alisema saa yaja ambayo waabuduo halisi watamwabudu Mungu katika roho na kweli.
Yohana 4.19 “Yule mwanamke akamwambia, Bwana, naona ya kuwa u nabii!
20 Baba zetu waliabudu katika mlima huu, nanyi husema ya kwamba huko Yerusalemu ni mahali patupasapo kuabudia.
21 Yesu akamwambia, Mama, unisadiki, saa inakuja ambayo hamtamwabudu Baba katika mlima huu, wala kule Yerusalemu…
23 Lakini saa inakuja, nayo sasa ipo, ambayo waabuduo halisi watamwabudu Baba katika roho na kweli. Kwa maana Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu”.
Ndugu unaona hiyo saa ni sasa Kristo aliyokuwa anaizungumzia, wakati huo ndio huu, Mungu anakutafuta wewe na mimi tupande tukamwabudu yeye katika MLIMA WA ROHO, huko ndiko tutakapomwabudu katika roho na kweli. Hivyo tuanze kupanda mlima huo sasa, kwa kuacha mambo hayo mabaya tuliyoyaona hapo juu bila kuchoka, bila kukata tamaa, ni kweli jasho litakutoka kidogo, lakini ili uonekane kuwa umestahili kukutana na Mungu wako uso kwa uso zaidi ya wale wengine, huna budi kupanda mlima huo wa roho kwa ukakamavu.
Tazama Neno la Mungu linavyosema..

Isaya 2:2 “Na itakuwa katika siku za mwisho, mlima wa nyumba ya Bwana utawekwa imara juu ya milima, nao utainuliwa juu ya vilima; na mataifa yote watauendea makundi makundi.
3 Na mataifa mengi watakwenda na kusema, Njoni, twende juu mlimani kwa Bwana, nyumbani kwa Mungu wa Yakobo, naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake maana katika Sayuni itatoka sheria, na neno la Bwana katika Yerusalemu.
4 Naye atafanya hukumu katika mataifa mengi, atawakemea watu wa kabila nyingi; nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.
5 Enyi wa nyumba ya Israeli, njoni, twende katika NURU YA BWANA.

Unaona siku hizi ndizo siku hizo za mwisho.

Ni maombi yangu kuwa mimi na wewe tutaanza kwenda katika nuru hii ya Neno la Mungu ili kutuongoza katika mlima huo wa Bwana.

Zaburi 43:3 “Niletewe nuru yako na kweli yako ziniongoze, Zinifikishe kwenye mlima wako mtakatifu na hata maskani yako.
4 Hivyo nitakwenda madhabahuni kwa Mungu, kwa Mungu aliye furaha yangu na shangwe yangu; Nitakusifu kwa kinubi, Ee MUNGU, Mungu wangu”.

Zaburi 123:1 “Wamtumainio Bwana ni kama mlima Sayuni, Ambao hautatikisika, wakaa milele. 2 Kama milima inavyouzunguka Yerusalemu, Ndivyo Bwana anavyowazunguka watu wake, Tangu sasa na hata milele.”

Ubarikiwe sana.

No comments:

Post a Comment