"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Monday, June 10, 2019

RUDIA, TENA NA TENA KUMWOMBA MUNGU USIKATE TAMAA.

 
Nilipokuwa mdogo, kulikuwa na wakati kaka yetu mara nyingi alikuwa kila akitoka shule ni lazima arudi na zawadi siku nyingine alikuwa anapitia bakery anatuletea sambusa za nyama n.k., sasa alikuwa anamnunulia kila mtu ya kwake, lakini mimi na mwenzangu tulikuwa na tabia moja, alipotugawia za kwetu, tulikuwa tunazila haraka haraka, ili ziishe haraka tuanze kuwaomba wengine kabla za kwao hazijaisha…mpaka tunamrudia Yule aliyetuletea zawadi, mwanzoni anatufukuza kabisa tusimkaribie, lakini sisi tulikuwa hatuachi kumsumbua unaona kabisa amekasirika, kaudhika lakini tunazidi kumwomba tu, anatuambia tukiendelea kumsumbua sasa atatupiga, lakini tulikuwa hatuachi kumsumbua kama vile nzi, anatuonya tena, na tena kwa ukali na hasira kuwa atatupiga huku hasira zikiwa zimemjaa, lakini sisi tukiwa katika hatari ya kupigwa hatuachi kumwomba atugawie kidogo, mwisho wa siku anaona bora acheke tu, anasema haya njooni, anaigawanya sambusa mara mbili nusu anampa mmoja na nusu mwingine.

Alianza kwa hasira lakini mwisho wa siku anaishia kwa kucheka tu, anasema ngoja niwape wasizidi kunisumbua, hizi ni kanuni ambazo zipo katika maisha yetu, unapokazana kung’ang’ania kitu Fulani utakipata tu hata iweje, ndio maana hata Bwana alitoa mfano unaofanana na huo na kusema.,
Luka 18.1 "Akawaambia mfano, ya kwamba imewapasa kumwomba Mungu sikuzote, wala wasikate tamaa.
2 Akasema, Palikuwa na kadhi katika mji fulani, hamchi Mungu, wala hajali watu.
3 Na katika mji huo palikuwa na mwanamke mjane, aliyekuwa akimwendea-endea, akisema, Nipatie haki na adui wangu.
4 Naye kwa muda alikataa; halafu akasema moyoni mwake, Ijapokuwa simchi Mungu wala sijali watu,
5 lakini, kwa kuwa mjane huyu ananiudhi, nitampatia haki yake, asije akanichosha kwa kunijia daima.
6 Bwana akasema, Sikilizeni asemavyo yule kadhi dhalimu.
7 Na Mungu, je! Hatawapatia haki wateule wake wanaomlilia mchana na usiku, naye ni mvumilivu kwao?
8 Nawaambia, atawapatia haki upesi; walakini, atakapokuja Mwana wa Adamu, je! Ataiona imani duniani?"
Unaona, mfano mwingine ni huu:
Luka 11:5 "Akawaambia, Ni nani kwenu aliye na rafiki, akamwendea usiku wa manane, na kumwambia, Rafiki yangu, nikopeshe mikate mitatu,
6 kwa sababu rafiki yangu amefika kwangu, atoka safarini, nami sina kitu cha kuweka mbele yake;
7 na yule wa ndani amjibu akisema, Usinitaabishe; mlango umekwisha fungwa, nasi tumelala kitandani mimi na watoto wangu; siwezi kuondoka nikupe?
8 Nawaambia ya kwamba, ijapokuwa haondoki ampe kwa kuwa ni rafiki yake, lakini kwa vile asivyoacha kumwomba, ataondoka na kumpa kadiri ya haja yake.
9 Nami nawaambia, Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa.
10 Kwa kuwa kila aombaye hupokea; naye atafutaye huona; naye abishaye atafunguliwa."
Hivyo na wewe, leo uliyempa Kristo Maisha yako na kumwishia yeye katika Kanuni zake nataka nikuambie, usikate tamaa katika kumwomba Mungu, wala usimwekee mipaka kwa kile umwombacho..Wapo wengine wanaogopa kumwomba Mungu vitu vikubwa wakidhani kuwa Mungu hawezi kuwatendea, unavyomchukulia Mungu ndivyo atakavyojifunua kwako, yeye atakupa kwa kiwango kile kile ulichompimia yeye..Bwana alisema ombeni lolote kwa jina langu nami nitalifanya(Yohana 14:13), hakutoa masharti ya jambo hilo uliombalo maadamu lipo sawasawa na mapenzi yake..

Hata kama utaona leo wala kesho hujibiwi, usiache kuomba, hata kama itapita miezi, miaka usiache kumsumbua sumbua Mungu, kwani wakati utafika atakupa hitaji lako, kwasababu anasema kila aombaye, kila atafutaye, na kila abishaye, atafunguliwa..hiyo ni lazima, hajasema labda atapata,au labda ataona, badala yake anasema kila aombaye atapata.Kuonyesha ni kauli ya AMRI.
Yakobo 5:16 ‘’………. Kuomba kwake mwenye haki kwafaa sana, akiomba kwa bidii.
17 Eliya alikuwa mwanadamu mwenye tabia moja na sisi, akaomba kwa bidii mvua isinyeshe, na mvua haikunyesha juu ya nchi muda wa miaka mitatu na miezi sita.
18 Akaomba tena, mbingu zikatoa mvua, nayo nchi ikazaa matunda yake’’
Hivyo tumia fursa hiyo kumwomba Mungu, bila kuvunjika moyo, usije ukafika kule, ukasema laiti ningejua nilipokuwa duniani ningemwomba Mungu hiki au kile..Nafasi ipo wazi kwako sasa, mwombe Mungu KARAMA zilizo kuu yaani kipawa vyake vya rohoni, mwombe Mungu akupe ROHO WAKE MTAKATIFU kama bado hujapokea, (hilo ndio jambo kubwa ambalo mwanadamu anaweza kumwomba Mungu) maana huyo ndio chanzo cha vyote ukimpata huyo umeupata ulimwengu mzima.. mwombe bila kukata tamaa, naye atakupa kwa wakati wake. Alisema

Mathayo 11.13 "Basi, ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Baba aliye mbinguni hatazidi sana kuwapa ROHO MTAKATIFU HAO WAMWOMBAO?."

Kumbuka Roho Mtakatifu ndio muhuri wa Mungu, na Roho Mtakatifu ni zaidi ya Kunena kwa Lugha.

Ubarikiwe.

No comments:

Post a Comment