"Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake...ufunuo 16:15"

Friday, August 2, 2019

UTALIPWA KATIKA UFUFUO WA WENYE HAKI.

Luka 14:12 “Akamwambia na yule aliyemwalika, Ufanyapo chakula cha mchana au cha jioni, usiwaite rafiki zako, wala ndugu zako, wala jamaa zako, wala jirani zako wenye mali; wao wasije wakakualika wewe ukapata malipo.
13 Bali ufanyapo karamu waite maskini, vilema, viwete, vipofu,
14 nawe utakuwa heri, kwa kuwa hao hawana cha kukulipa; kwa maana utalipwa katika ufufuo wa wenye haki”.
Katika habari hii, tunaona Bwana Yesu alialikwa na mtu mmoja mkuu sana miongoni mwa Mafarisayo ale chakula cha mchana nyumbani kwake, na bila shaka mtu huyu alikuwa ni tajiri, na katika karamu yake alialika watu wakuu, watu wa maana, na si watu wa kawaida kawaida tu, Lakini kuna kitu ambacho Bwana Yesu alikiona kimepunguka katika ukarimu wake mwema wa kuwaalika watu na wageni katika shughuli zake, kwani si wote wenye moyo kama huo.Wengine wanaweza wakawa ni matajiri na wakuu, lakini wakala vitu vyao peke yao, lakini huyu alikuwa watofauti kidogo.
Lakini pamoja na hayo, Bwana Yesu aligundua watu aliowaalika walikuwa ni matajiri tu, watu wenye uwezo kama yeye, Hivyo Bwana Yesu kwa kuliona hilo ili kumsidia kuifanya taabu yake isiwe bure, ndipo akamwambia kwa kumshauri wakati mwingine, kuwa atakapofanya sherehe awaalike watu wasiokuwa na uwezo wa kumlipa mfano wa hicho alichokifanya..Kwasababu akiwaalika watu wenye uwezo, wale watu nao watarudisha mapigo siku moja, watamwalika na yeye kwenye karamu zao na thawabu yake itakuwa imeshalipwa na wao, lakini mbinguni hatakuwa na kitu, hivyo ili taabu yake na wema wake uwe na nguvu idumuyo, siku nyingine akifanya karamu kubwa kama hiyo, asiiachie thawabu yake ilipizwe na wanadamu bali ije ilipizwe na Mungu katika siku ya ufufuo wa wenye haki, hivyo awaalike watu wasiokuwa na uwezo wa kumfanyia kama kile alichowafanyia.

Hata leo hii, yapo mambo mengi tunayafanya tukidhani tutalipwa tutakapofika mbinguni kwa ukarimu tunaoufanya..Kwa mfano leo hii labda kutokee mchango wa sherehe fulani ni rahisi kuchangia harusi ya boss wako, au mfanyakazi mwenzako kwasababu unajua kuna siku moja na wewe utahitaji wakuchangie kwenye sherehe yako, au ya ndugu yako. Lakini ukisikia yupo jirani yako ambaye ni maskini hana mbele wala nyuma kipato chake ni kidogo hata hakimtoshelezi yeye mwenyewe, halafu mwanawe anataka kuoa, hivyo anahitaji sapoti yako kidogo, Ukweli ni kwamba wengi wetu tutakuwa tayari kuingia mitini, ni kwasababu gani?, Ni kwasababu tunaona mbeleni huyu anaweza asiwe na msaada kwangu siku shughuli yangu, hivyo hata nisipomsaidia hainiathiri chochote.

Kiuhalisia Mungu hatakulaumu ulipochangia sherehe ya Yule boss wako na kuiacha hii ya huyu maskini, zaidi Mungu atakulipa, na kukulipa kwake kutakuwa ni kwa kupitia wao, na habari thawabu yako itakuwa imeishaipata hapa hapa duniani, juu mbinguni utakuwa huna kitu chochote. Ukinunua zawadi si zote uzipeleke kwa marafiki na ndugu, nyingine tenga wapelekee wasio na uwezo wa kukulipa,watu wasio na faida yoyote kwako. Unapokopesha usikopeshe wale tu ambao watakupa na Riba juu yake..Kopesha hata na Yule ambaye hawezi kukulipa na Riba juu yake mwenye uwezo wa kukurudishia kiwango kile kile ulichompa.
Luka 6:35 “Bali wapendeni adui zenu, tendeni mema, na kukopesha msitumaini kupata malipo, NA THAWABU YENU ITAKUWA NYINGI; nanyi mtakuwa wana wa Aliye juu, kwa kuwa yeye ni mwema kwa wasiomshukuru, na waovu”.
Na ndio sababu ambayo Bwana alimshauri huyu mtu aliyemwalika, nasi tupokee ushauri huo, tutafute thawabu zinazodumu milele. Ni kweli wakati mwingine unaweza kuona ni mzigo kuwa msaada kwa wasiokunufaisha Lakini thawabu yake, utaiona siku ile utakapofika mbinguni. Maana kiwango cha hazina yako ndicho kitakachofunua utajiri utakaokuwa nao mbinguni.
“Tena tusichoke katika kutenda mema; maana tutavuna kwa wakati wake, tusipozimia roho. (Wagalatia 6:9)”
Bwana akubariki.
www.wingulamashahidi.org

No comments:

Post a Comment